JUMATATU WIKI YA 27 YA MWAKA-C
Somo:
Gal 1:6-12
Zab/Kit: 111:1-2, 7-8, 9, 10c
Injili: Lk 10:25-37
Nukuu:
“Nastaajabu kwa kuwa
mnamwacha upesi hivi yeye aliyewaita katika neema ya Kristo, na kugeukia injili
ya namna nyingine,” Gal 1:6
“Lakini ijapokuwa sisi
au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo
tuliyowahubiri, na alaaniwe,” Gal 1:8
“Na tazama, mwana-sheria mmoja alisimama
amjaribu; akisema, Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?” Lk
10:25
“Akajibu akasema,
Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu
zako zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako,” Lk 10:27
TAFAKARI:
“Nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?
Wapendwa wana wa Mungu,
pamoja na mbwembwe zote za mwanadamu hapa duniani, ni wajibu wa kila mmoja wetu
kujiuliza swali hili la msingi alilouliza mwana-sheria mmoja wa Kiyahudi kwa
Yesu kuhusu uhai. Mwana-sheria huyu anamuuliza Yesu hivi; “Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa
milele?” Lk 10:25. Msingi wa swali hili haupo kwenye uhai tu wa leo na kesho,
bali uhai katika umilele wake. Tuelewe kwamba mwanadamu ameumbwa kuishi milele,
na hayo ndiyo makusudi ya Mungu katika uumbaji wa mwanadamu.
Tatizo kubwa la mwanadamu ni mbwembwe nyingi alizonazo
akisahau kuwa muda aliopewa hapa duniani hausimami kumsubiri. Mhubiri anatuwasa
na kusema, “mwanadamu hadumu katika heshima, bali amefanana na wanyama
wapoteao,” Zab 49:12. Fahari ya mwanadamu ni yule aliyemuumba, yaani Mungu
wake. Mengine yote ni mbwembwe tu! “Mche Bwana, Mungu
wako, umtumikie yeye; ambatana naye, na kuapa kwa jina lake. Yeye ndiye fahari yako, na yeye ndiye
Mungu wako, aliyekutendea mambo haya makubwa, ya kutisha, uliyoyaona kwa macho
yako,” Kumb 10:20-21. Ndugu unayesafiri nami katika tafakari hii, elewa kwamba
utajiri wako, ufahamu wako (kiwango cha elimu ulicho nacho), umaarufu wako, nk,
bila Mungu ni bure kabisa.
Yesu
kabla ya kumjibu vizuri mwana-sheria yule wa kiyahudi alitaka kujua uelewa wake
wa Maandiko Matakatifu (Torati) yanasema nini kuhusu uhai wa Milele.
Mwana-sheria yule akamjibu kwa staha, “Mpende
Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako
zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako,” Lk 10:27. Yesu
anaridhika na jibu hili na anamwambia hivi; “Umejibu vema; fanya hivi nawe
utaishi,” Lk 10:28. Kuishi kwetu hapa duniani ambapo kunatupelekea kuishi
milele baada ya kifo, kama wanadamu kwatuwajibisha kufanya kwa weledi mkubwa
mambo makuu mawili.
Moja, mpende Mungu wako kwa moyo wako wote, roho yako yote,
na nguvu zako zote. Kwa maana nyingine ni kutumia vyote Mungu alivyokujalia ili
umpende na ubaki kumpenda daima. Afya yako njema, akili yako ya pekee, utajiri
wako, na umaarufu wako hapa nduniani isiwe sababu ya kujitenga na upendo huu wa
Mungu. Hayo Mungu aliyokujalia kwa namna ya pekee isiwe sababu ya kuwakejeli
wenzako ambao kwa mtazamo wako wa kibinadamu waona hawastahili mema yoyote
mbele ya uso wa Mungu.
Ndugu yangu, hata yale tunayoyaona kwa macho yetu kama
udhaifu wa mtu na wengine, Mungu wakati mwingine utumia udhaifu huo kutufundisha
siri ya maisha na uhai tuliopewa na Mungu mwenyewe. Maisha na uhai tuliyonayo ni mali na zawadi yake
Mungu. Mimi na wewe tumepewa uhai huu na kuazimwa kwa muda tu hapa duniani kama
sababu ya kuutumia vyema uhai huu ili tuishi milele baada ya muda ambao kila
mmoja wetu kapewa kadiri ya mapenzi yake Mungu. “Maana siku zangu zinatoweka
kama moshi, Na mifupa yangu inateketea kama kinga,” Zab 102:3.
Pili, nimpende jirani yangu kama nafsi yangu. Jirani yangu
ni yeyote yule ninayekutana naye na wale wote wanaonizunguka, yaani, wahitaji
na wasio wahitaji. Jirani yangu ni kama kioo cha kujitazama ukamilifu wangu
mbele ya Mungu. Je, udhaifu wa jirani yangu unasema nini kuhusu maisha yangu
mimi niliyejiinua na kujiona safi na mwema kuliko wengine? Yesu, anakemea hali
hii kwa Mafarisayo na Waandishi, na kwetu pia. “Waandishi na
Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa; basi,
yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo
yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi,” Mt 23:2-3. Mtazamo huu wa
ugeugeu na kujiinua mbele za Mungu pasipo mastahili yoyote ndio sababu ya mfano
wa Msamaria mwema.
Wafarisayo
ambao kwa kiasi kikubwa walijiinua na kuwa wepesi kuwahukumu wengine, wanashindwa
kuokoa uhai ambao ni mali na zawadi ya Mungu kwa vile tu muhitaji huyu na
mhusika huyu hakuwa Myahudi. Wakati mwingine tunashindwa kusimama katika kweli
kwa vile tu mhusika siyo kutoka familia yetu, ukoo wetu, kabila letu, au kutoka
Kanda yetu. Wenye mitazamo kama hii ilihali wanajiita wafuasi wa Kristo, basi
Kristo huyo huendelea kusulubiwa kwa matendo yao. Kristo huyo siyo fahari ya
maisha yao. Mimi na wewe kama wafuasi wa Kristo hatuna kitu kingine cha
kujivunia zaidi ya Msalaba wa Kristo.
“Lakini mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu cho chote ila
msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa
kwangu, na mimi kwa ulimwengu,” Gal 6:14. Je, tusikemee maovu? La hasha!
Mkemeapo “Basi, wekeni mbali uovu wote na hila yote, na unafiki na husuda
na masingizio yote. Kwa sababu
ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia
kielelezo, mfuate nyayo zake. Yeye
alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi
kwake yeye ahukumuye kwa haki. Yeye
mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa
mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa,”
1Pet 2:1, 21, 23-24. Je, nauona udhaifu wangu ninapoutazama udhaifu wa
mwingine?
Wapendwa
wana wa Mungu, Yesu anapomwambia mwana-sheria yule afanye tathimini kati ya
wale wayahudi na yule Msamaria aliyetoa msaada kwa mhitaji yule aliyepata
kipigo na wanyang’anyi, mwana-sheria anaelewa soma lile na kumjibu Yesu, “Ni huyo aliyemwonea huruma. Yesu akamwambia, Enenda
zako, nawe ukafanye vivyo hivyo,” Lk 10:37. Wapendwa katika Kristo, yatupasa
kusimama katika kweli na haki, hivyo tutende yote kwa upendo na huruma ya
kweli. Tusipolifanya jambo hilo basi tujiandae kusutwa na dhamiri zetu katika
umiele wote.
Wapendwa
wana wa Mungu, mamlaka aliyokuwa nayo Yesu ni vita dhidi ya uovu hapa duniani.
Ni ukweli usiopingika kwa kupitia jina lake tunapata uponyaji wa kweli. “Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini
nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama
uende,” Mdo 3:6. Mamlaka
ya Yesu yamejengwa chini ya mamlaka ya Mungu.
Hivyo
hakuna jambo lolote alifanyalo Yesu Lisilo kuwa na uhusiano na Mungu, huku
jambo lile likifunua siri ya Mungu kila kukichwa. “Kwa kuwa katika yeye vitu
vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na
visivyoonekana; ikiwa ni vitu vya enzi, au usultani, au enzi, au mamlaka; vitu
vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake,” Kol 1:16. Kwa nini basi
nakuwa na mashaka juu ya utendaji wa Kristo katika maisha yangu?
Wapendwa
katika Kristo, Yesu anapotoa mfano wa vazi kuukuu na jipya, na kwa upande
mwingine divai ya zamani na kiriba kipya anataka kutufundisha jambo hili;
“kwanza kabisa lazima tujue sababu na malengo ya maisha yetu hapa duniani.
Hatupo hapa duniani kwa bahati mbaya hata kidogo. Tupo katika ulimwengu huu
kadiri ya mpango wa Mungu ambao ni dhahiri na mathubuti. Hivyo lolote lile
lililo jema mbele ya Mungu huwiishwa na kufanya upya.
Somo letu la kwanza,
linauelezea uhali wa jambo hili, yaani,
Mungu ili awe sehemu ya maisha yako na kielelezo cha yale yote
uyafanyayo, yakupasa kuushinda ubinadamu wako na matamaniyo yake. Kuushinda
ubinadamu wako, yakupasa kujipokea na kujikubali kwamba wewe ni binadamu katika
maana ya mafanikio yako na mapungufu yako. Katika uwezekano huu, ikiwa ni
mafanikio na mapungufu yake, binadamu anabaki kuwa binadamu, na Mungu anabaki
kuwa Mungu katika ukamilifu wake.
Hivyo kuwa wakamilifu
kama Mungu alivyo mkamilifu kwake Yeye mwenyewe na kwetu sisi, twahitaji
kuipokea hali yetu ya ubinadamu, na wakati huo huo kuushinda ubinadamu wetu huo
kwa kuegemea ukamilifu ule tulioitiwa na Mungu. Naye Yesu katika kweli hii
anasema, “Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa
mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48. Huu ndio wito wetu wa kila siku na
kulingana na mazingira yoyote yale tutakayokuwa, yaani, kuwa wakamilifu kama
‘Baba yetu wa mbinguni alivyo makamilifu.
Kwa
kuujua ukweli huo, Mtume Paulo analiweka jambo hili wazi kwa watu wake na
kusema, “Paulo, mtume, (si mtume
wa wanadamu, wala kutumwa na mwanadamu, bali na Yesu Kristo, na Mungu Baba
aliyemfufua kutoka kwa wafu), na ndugu wote walio pamoja nami, kwa
makanisa ya Galatia,” Gal 1:1-2. Ni wazi kabisa Mtume Paulo anataka tuwe makini
kwa jambo hili: ‘kamwe tusijifananishe na matokeo ya mafanikio yetu, bali
tuutazamie ule utukufu na ukamilifu tulioitiwa.’ Kuna anguko kubwa sana pale
tunapojifananisha na kujilinganisha na mafanikio yetu binafsi.
Mazingira hayo ndiko
kwenye chimbuko kubwa la majivuno, na penye majivuno hakuna ukuaji wa maisha ya
kiroho. Mwenye majivuno hana nafasi ya Kristo ndani ya maisha yake. Nafasi ile
ya Kristo imetawaliwa na ubinafsi wake na umimi wake. Katika hali hii kuna
anguko kubwa sana la kurudi nyuma katika imani. Mtume Paulo haoni haya kuusema
ukweli huu; “Nastaajabu kwa kuwa mnamwacha upesi hivi yeye
aliyewaita katika neema ya Kristo, na kugeukia injili ya namna nyingine,” Gal 1:6.
Ndugu yangu, yote yaliyo ya kibinadamu pasipo uhusiano na Mungu, hayana
umilele.
Wapendwa wana wa Mungu,
kilichohubiriwa na Kristo wakati ule katika historia ya wokovu wetu, na sasa
kama kielelezo cha Kanisa lililo hai, na Sakramenti ya wokovu wetu ni habari
njema ya wokovu wetu. Habari hii njema ya wokovu wetu hii hai muda wote na
katika umilele wote.
Hivyo kwenda kinyuma na
agizo hili la Yesu kabla ya kupaa kwake ili hali tunajua, ni kuipalilia ‘laana
huku tukijua.’ Agizo hilo ndilo hili, ‘kwa Kanisa kama Sakramenti ya wokovu, na
kwa Kanisa kama Mwili wa Kristo, yaani, kila aliyebatizwa na kuishi ahadi zake
za ubatizo; “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri
Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye
na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa,”’ Mk 16:15-16.
Hiki
ndicho akisemacho Mtume Paulo wa Wagalatia kuhusu mahusiano ya Habari Njema ya
wokovu na laani ipatikanayo kwa kutokuhubiri kweli iliyo katika habari njema
hivyo. Naye anasema, “Lakini
ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote
isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe,” Gal 1:8.
Kweli iliyo ndani ya
habari njema ya wokovu wetu hubaki na kuhubiriwa kama ilivyo pale tunapoushinda
ubinadamu wetu. Mtume Paulo anatutafakarisha kwa kusema, “Maana,
sasa je! Ni wanadamu ninaowashawishi, au Mungu? Au nataka kuwapendeza wanadamu?
Kama ningekuwa hata sasa nawapendeza wanadamu, singekuwa mtumwa wa Kristo,” Gal
1:10. Ndugu yangu, panapozidi ubinafsi wetu, Kristo hana nafasi.
Wapendwa wana wa Mungu,
Kristo aliye Njia, Kweli, na Uzima wetu, Yoh 14:6, anapokosa nafasi katika
maisha yetu, ni kwa namna hiyo hiyo, Mungu hana nafasi katika maisha yetu. Je,
twawezaje kumfikia Mungu bila kupita kwake Kristo aliye na mamlaka yote? Kristo
Yesu anaweka wazi ukweli huu na kusema, “Kwa
sababu hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa
amejaliwa na Baba yangu,” Yoh 6:65. Kuupata au kuufikia Ufalme wa Mbinguni bila
Kristo, ni sawa na samaki kuishi na kustawi bila maji. Je inawezekana?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kama tulivyotangulia kusema, na
sasa, nasema tena, mtu awaye yote akiwahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa
hiyo mliyoipokea, na alaaniwe,” Gal 1:9
Tusali:-Ee
Yesu, nitumie kadiri ya takwa lako, ili ujulikane pale usipojulikana. Amina