JUMAMOSI
WIKI YA 13 YA MWAKA-C
Somo: Amo 9:11-15
Zab: 85:9, 11-12
Injili: Mt 9:14-17
Nukuu:
“Siku
hiyo nitaiinua tena maskani ya Daudi iliyoanguka, na kuziba mahali
palipobomoka; nami nitayainua magofu yake, na kuyajenga kama siku za kale; wapate kuyamiliki mabaki ya Edomu, na
mataifa yote yaitwayo kwa jina langu, asema Bwana, afanyaye hayo,” Amo 9:11-12
“Angalieni,
siku zinakuja, asema Bwana, ambazo huyo alimaye atamfikilia avunaye, na yeye
akanyagaye zabibu atamfikilia apandaye mbegu; nayo milima itadondoza divai
tamu, na vilima vyote vitayeyuka,” Amo 9:13
“Yesu akawaambia,
Walioalikwa arusini wawezaje kuomboleza, muda bwana arusi akiwapo pamoja nao?
Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga,” Mt
9:15
“Hakuna
mtu atiaye kiraka cha nguo mpya katika vazi kuukuu; maana kile kilichotiwa
huondoa kipande cha lile vazi, na pale palipotatuka huzidi,” Mt 9:16
“Wala
watu hawatii divai mpya katika viriba vikuukuu; na kama wakitia, vile viriba
hupasuka, divai ikamwagika, na viriba vikaharibika; bali hutia divai mpya
katika viriba vipya, vikahifadhika vyote,” Mt 9:17
TAFAKARI:
“Katika Kristo na ndani ya Kristo, yote yatafanywa upya. Tusife moyo huyu ni
Mungu pamoja nasi, Imanueli, Mt 1:23.”
Wapendwa wana wa Mungu, ‘unabii licha ya kubeba ujumbe wa Mungu katika
misingi ya kufundisha, kuonya na kutoa angalizo, sehemu kubwa ya ujumbe huu wa
Mungu hubeba tumaini jipya la kule tunapokutamani ambapo ndipo kusudi zima la
Mungu katika ukamilifu wake. Na wito wetu kila siku kama Yesu anavyotuamuri ni
kwamba, ‘tuwe
wakamilifu, kama Baba yetu wa mbinguni alivyo mkamilifu,’
Mt 5:48. Kuwa mkamilifu kama Mungu alivyo ni kuwa Mtakatifu. Bila utakatifu
huwezi kuwa katika himaya ya Mungu. Kuwa mwenyeji wa Mbinguni lazima uwe
mtakatifu. Na hivi ndivyo asemavyo Mtume Paulo kwamba, “tangu sasa ninyi si
wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa
nyumbani mwake Mungu,” Efe 2:19. Maneno haya ya Mtume Paulo yanatufikirisha
uwepo wetu hapa duniani. Hapa tulipo, yaani, duniani, siyo makazi yetu ya
kudumu. Tupo hapa kwa kujiandaa tu kwa uzima wa milele. “Kwa maana sisi,
wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu
Kristo; atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa
utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe
chini yake,” Flp 3:19-20
Hili
ndilo tumaini la Mungu na la kinabii kwa wale aliowaridhia kuupitisha ujumbe
wake, yaani, manabii. Nabii Amosi anafikisha ujumbe huu wa Mungu wenye
matumaini ambao ni uthibitisho wa Mungu aliye hai na mwenye kuiona historia ya
watu, na mwenye kutembea nao katika historia hiyo yenye kila aina ya dhoruba.
Dhoruba na misukosuko aipatayo mwanadamu katika historia yake na kuyakabili
katika matumaini huwa ndiyo ponya yake ya mwili na roho. Na huu ndio ujembe wa
kinabii na matumaini kwa wana wa Israeli baada ya mateso waliyoyapata ndani ya
utawala wao, na nje ya utawala wao. Na “Siku
hiyo nitaiinua tena maskani ya Daudi iliyoanguka, na kuziba mahali
palipobomoka; nami nitayainua magofu yake, na kuyajenga kama siku za kale; wapate kuyamiliki mabaki ya Edomu, na
mataifa yote yaitwayo kwa jina langu, asema Bwana, afanyaye hayo,” Amo 9:11-12.
Mungu hachoki kufanya nasi agano pale tunapomrudia katika kweli na haki.
Hata
pamoja na kufanya agano hilo la kweli na haki kama alama ya kujirudi na kufuata
njia iliyo salama, Mungu haachi kutupa angalizo ilihali akijua fika hali zetu
na ubinadamu wetu, yaani, ‘maanguko yetu.’ Naye mjumbe wa Mungu, Nabii Amosi,
anasema, “Angalieni, siku zinakuja, asema
Bwana, ambazo huyo alimaye atamfikilia avunaye, na yeye akanyagaye zabibu
atamfikilia apandaye mbegu; nayo milima itadondoza divai tamu, na vilima vyote
vitayeyuka,” Amo 9:13. Neema na baraka tuzipatazo katika maisha si kitu cha
kubeza, bali ni kitu cha kuthamini na kulindwa katika maana ya kukipigania
kisipotee. Hata hivyo, ni vyema tuelewe tunda la amani ni haki hasa pale
tunapoishi zaidi ya mtu mmoja. Na haki ni tunda la wajibu. Haki na amani huwepo
pale kila mmoja anapotimiza wajibu wake kadiri ya nafasi na wito wake.
Mungu
hatochoka kutuletea na kutukirimia yanayofaa kadiri ya mahitaji yetu pale
tunapodumisha amani ambayo ni tunda la haki, na haki ikiwa ni tunda la wajibu.
Na hivi ndivyo alivyowahaidia wana wa Israeli na kusema, “Nami
nitawarejeza tena watu wangu Israeli waliohamishwa, nao wataijenga miji
iliyoachwa maganjo, na kukaa ndani yake; nao watapanda mizabibu katika
mashamba, na kunywa divai yake; nao watafanyiza bustani, na kula matunda yake,”
Amo 9:14. Ndugu yangu, ni ndoto ya mchana kweupe kutabiri kuijenga nchi ya
maziwa na asali kwa kukanyaga haki za watu ambao kwa njia moja au nyingine wana
wajibika kwa taifa lao kadiri ya wito na nafasi zao. Huwezi kuwa na amani kama
hakuna haki. Na pasipo haki na amani hapana maendeleo. Na maendeleo
yasiyotokana na utashi wa watu hukosa thamani mbele zao hata kama machoni mwako
yatakuwa ya gharama kubwa. Na mwisho wa siku maendeleo hayo hufifia kama moshi
wa mabua kwa sababu hayakugusa maisha ya watu na hayana maana kwao. Lolote lile
lenye kugusa utashi wa watu ndilo lijengalo na kukuza maisha ya watu kwa sababu
ni zao la kile walicho.
Pamoja
na uwezo wako kama kiongozi wa kuona mbele kule wasipokuona sawa sawa wale
unaowaongoza, jaribu mara zote kutembea nao na kuwaonyesha kule unapopaona. La
siyo utafika kule utakapo ilihali wao bado hata hawajajianda kwa safari hiyo
uliyokwisha imaliza. Unapotembea hatua kwa hatua na wale unaowaongoza Mungu
anakuhakikishia hili kama kiongozi, “Nami nitawapanda katika nchi yao, wala
hawatang'olewa tena watoke katika nchi yao niliyowapa, asema Bwana, Mungu
wako,” Amo 9:15. Na hivi ndivyo uzalendo unavyojengwa. Uzalendo wa watu kamwe
haujengwi kwa shuruti za kiimla, bali uhuru na utashi uliokomaa wenye kuthamini
siyo tu kwamba hiki ni changu bali ni chetu na kina thamani kwa wote na umma.
Zaidi ya hapo ni mbwembwe tu. Na mwisho wa mbwembe ni pale sherehe inapofikia
kikomo chake. Je, maisha si zaidi ya sherehe?
Tunahitaji tafakuri ya kina. Na ndiyo maana katika maisha tunahitaji nyakati za
mafungo, yaani, kuyapitia yale tuliyokwisha yaishi (uzuri na ubaya wake), kuona
pale tulipokosea, na kuanza upya kwa nguvu ili kutokurudia makosa na kufika
pale tunapopatamani, yaani, ukamilifu ambao ndio maisha ya umilele na kusudi la
kumbwa kwetu.
Hivyo wapendwa wana wa
Mungu, kadiri ya Injili ya leo, kufunga ilikuwa moja ya mambo makuu matatu
kadiri ya Imani, mila na desturi za kiyahudu. Kufunga iliendana na kusali,
pamoja na kutoa sadaka. Haya mambo matatu yalikuwa ya msingi sana. Kitendo cha
wanafunzi wa Yesu kuonekana kutokufunga kiliwashangaza na kuwakwaza wengi, na
hasa wanafunzi wa Yohane Mbatizaji. Yesu anapoulizwa swali hili: kwa nini
wanafunzi wako hawafungi, anajibu na kusema, “Walioalikwa arusini wawezaje
kuomboleza, muda bwana arusi akiwapo pamoja nao? Lakini siku zitakuja
watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga,” Mt 9:15. Uhusiano wetu na
Kristo una sura mbili; kuna wakati wa furaha na wakati wa huzuni, itupelekayo
kwenye utukufu. Tukiwa na Yesu tu wana wa Bwana harusi na yatupasa kufurahi
naye kuliko haki.
Kwa upande wa pili wa
uhusianao wetu na Yesu unatukumbusha upo wakati wa kutoa ushuhuda wa kweli juu
ya kile tunachoamini kuhusu Yesu. Huu ndio wakati wa kuteseka na hata kufa kwa
ajili ya Kristo. Huu ndio wakati wa kufanya toba ya kweli kwa ajili ya
maaondoleo ya dhambi zetu. Huu ndiyo wakati wa kufanywa upya ndani na katika
Kristo. Na huu ndio wakati wa kutakaswa na kubeba bendera ya ushindi ya
mwanakondoo.
Nyakati hizi mbili za
mahusiano yetu na Kristo ndizo zitupazo kiini cha imani yatu. Sisi si Wakristo
wa Jumapili tu, yaani, pasaka, bali tu wafuasi wa Kristo siku zote na hasa siku
ile ya Ijumaa, yaani mateso na kufa kifo dini. Tunakufa kifo dini kwa kuIfia
kweli siku zote za maisha yetu. Yatupasa kusimama katika kweli, kufundisha
iliyo kweli, kuishi yaliyo kweli, na kushuhudia lililo kweli, hata kama
litagharimu uhai wetu. Haya ndiyo maisha ya ufuasi wa Kristo ambao tuliowengi
hatutaki kusikia.
Jambo lingine la muhimu
kujua ni hili: Yatupasa kuelewa lile lililo la zamani ambalo kwa sasa
linakamilishwa na hili jipya, mbalo tangia awali lilikuwa limejificha ndani ya
lile la zamani. “Hakuna mtu atiaye kiraka
cha nguo mpya katika vazi kuukuu; maana kile kilichotiwa huondoa kipande cha
lile vazi, na pale palipotatuka huzidi,” Mt 9:16. Maana yake nini? Ndugu yangu,
katika safari ya ukombozi wa mwanadamu, katika hatua ya mwanzo ya safari hiyo,
imebebwa katika agano la mwanzo. Agano hili kama lilivyo laelezea historia ya
mwanadamu hatua kwa hatua. Kwa lenyewe agano hili kama lilivyo lina maana ila
limekosa ukamilisho au hitimisho. Ukamilisho wa Agano la kwanza ni Upya wa
Agano jipya, ikiwa ni ufunuo wa wazi wa Mungu kwa tukio la neno kufanyika
mwili. Agano hili jipya licha ya kwamba ni ukamilisho wa agano la kale, tangu
mwanzo lilikuwa limejificha ndani ya agano la kale. Hivyo Yesu anatutaka
kulijua jambo hilo na pia kutenganisha maagano haya mawili katika “ufahamu
wake,” “umaana wake” na “nafasi zake.”
Na hii ndiyo maana ya maneno haya, “Wala
watu hawatii divai mpya katika viriba vikuukuu; na kama wakitia, vile viriba
hupasuka, divai ikamwagika, na viriba vikaharibika; bali hutia divai mpya
katika viriba vipya, vikahifadhika vyote,” Mt 9:17. Hivyo katika jambo hili
twapaswa kumfuata Kristo katika ukamilifu wote na kuachana na michanganyo. Ni
heri kuwa baridi au joto, kuliko kuwa vuguvugu katika Imani. Hili vuguvugu
kiimani ndilo litakalo pasua hekalu hili la Roho Mtakatifu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Hakuna
mtu atiaye kiraka cha nguo mpya katika vazi kuukuu; maana kile kilichotiwa
huondoa kipande cha lile vazi, na pale palipotatuka huzidi,” Mt 9:16
Tusali:-Ee Yesu na Mungu wetu, tupo
tayari kuanza yote pamoja nawe. Amina