JUMATANO WIKI YA 5 YA PASAKA
Somo: 15:1-6
Zab: 122:1-2, 3-4ab, 4cd-5
Injili: Yoh 15:1-8
Nukuu:
“Wakashuka
watu waliotoka Uyahudi wakawafundisha wale ndugu ya kwamba, Msipotahiriwa kama
desturi ya Musa hamwezi kuokoka,” Mdo 15:1
“Lakini
baadhi ya madhehebu ya Mafarisayo walioamini wakasimama wakisema, Ni lazima
kuwatahiri na kuwaagiza kuishika torati ya Musa,” Mdo 15:5
“Mitume
na Wazee wakakusanyika wapate kulifikiri neno hilo,” Mdo 15:6
“Mimi ni mzabibu;
ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana
pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote,” Yoh 15:5
“Mtu
asipokaa ndani yangu, hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu huyakusanya na kuyatupa
motoni yakateketea,” Yoh 15:6
“Ninyi
mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote
nanyi mtatendewa,” Yoh 6:7
TAFAKARI:
“Maandalizi ya Mtaguso wa Yerusalemu; kutahiriwa kama moja ya kigezo cha kuwa
Mkristo na Mshiriki Kikanisa.”
Wapendwa
wana wa Mungu, leo tutafakari kwa undani changamoto za Kanisa la mwanzo, hasa
swala zima la kupokelewa na kushiriki huduma za kikanisa kwa wale ambao
hawakuwa Wayahudi. Tunaona Kanisa linapanuka na kuenea kila kona, ni kwa namna
hiyo hiyo linakumbwa na kasumba ya ubaguzi uliolenga mila na desturi za
Kiyahudi. Tendo la kutahiriwa kwa wayahudi lilikuwa na maana tofauti tofauti
kadiri ya walivyokuwa wanaishi na hasa maagano yao na Mungu.
Kwa
mara ya kwanza katika historia yao, tendo hili lilibeba maana ya usafi na kwa yule aliyetaka kuoa lilichukua maana ya
“Bwana harusi wa damu.” “Ndipo Sipora akashika jiwe gumu na kuikata govi ya zunga la
mwanawe, na kuibwaga miguuni pake akasema. Hakika wewe u bwana arusi wa damu
kwangu mimi. Basi akamwacha.
Ndipo huyo mkewe akanena, U bwana arusi wa damu wewe, kwa ajili ya kutahiri” Kut
4:25-26. Kutahiri kulimaanisha pia agano kati yao na Mungu hasa kwa tendo la Mungu kuwatoa utumwani
Misri, na hapa wanatairiwa kwa mara ya pili. “Wakati huo Bwana
akamwambia Yoshua, Haya, jifanyie visu vya mawe ya gumegume, watahiri tena wana
wa Israeli mara ya pili. Basi
Yoshua akajifanyia visu vya mawe ya gumegume, akawatahiri wana wa Israeli huko
Gibea-haaralothi. Na sababu ya
Yoshua kutahiri ni hii; watu wote waliotoka Misri, waliokuwa waume, hao watu
waume wote waendao vitani walikufa katika bara njiani, baada ya wao kutoka
Misri,” Yos 5:2-4. Kutahiriwa pia kulimaanisha kushika torati kikamilifu. “Basi ikiwa yeye
asiyetahiriwa huyashika maagizo ya torati, je! Kutokutahiriwa kwake
hakutahesabiwa kuwa kutahiriwa?” Rum 2:26. Pamoja na sababu nyingine zote
tulizokwisha kuziona, hii ya mwisho ndiyo iliyotumika kama kigezo cha alisiye
Myahudi kupokelewa katika jumuiya hii ya Wakristo wa kwanza ambayo kwa kiasi
kikubwa walikuwa Wayahudi. “Lakini baadhi ya madhehebu ya Mafarisayo walioamini
wakasimama wakisema, Ni lazima kuwatahiri na kuwaagiza kuishika torati ya
Musa,” Mdo 15:5. Watu wa mataifa yaani
wale ambao hawakuwa wayahudi iliwapasa kufanya tendo hili la kutahiriwa. Hivyo
Kanisa linafanya utaratibu wa kutatua tatizo hili ili upendo na amani udumu
katika kundi. “Mitume na wazee wakakusanyika wapate kulifikiri neno
hilo,” Mdo 15:6.
Mambo haya ya nje
hayapaswi kuwa sababu ya kutokuishi upendo wa Kristo katika Kanisa. “Hapo hapana Myunani
wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala mshenzi, mtumwa wala
mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote,” Kol 3:11. Injili yetu ya leo
inasema ukweli huu wa Kristo. Uzima wetu, na uhai wetu kiroho ni katika Kristo
Yesu aliye mzabibu nasi matawi yake. Kuishi katika ukweli huu ni kuzaa matunda,
yaani kuwa watu wa upendo, haki na amani
kama Kristo mwenyewe. “Kila tawi ndani
yangu lisilozaa huliondoa; na kila tawi lizaalo hulisafisha, ili lizidi kuzaa,”
Yoh 15:2
Ndugu yangu, njia
salama na amani ya kweli kama mfuasi wa Yesu ni kukaa ndani yake na kuishi
kadiri ya matakwa yake. “Kaeni ndani yangu,
nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya
mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu,” Yoh 15:4. Je, hupendi kusitawi
ndani ya Kristo? Bila Yesu Kristo katika maisha yako huku ukijiita Mkristo,
hutoweza kufanya lolote lile liwe dogo au kubwa, “maana pasipo mimi ninyi
hamwezi kufanya neno lo lote,” Yoh 15:5b. Ni katika Kristo na ndani ya Kristo
twaweza yote yawezekana katika maisha yetu kama wafuasi wake, na hasa pale
tunapoishi vyema na kwa uaminifu ahadi zetu za ubatizo. “Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani
yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa,” Yoh 6:7. Je, kinyume chake ni nini? Ndugu yangu, kinyume
chake ni KUNYAUKA KIROHO NA KIMWILI. Na mwisho wa kadhia hii ni kutokufaa kwa
chochote. “Mtu asipokaa ndani yangu,
hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu huyakusanya na kuyatupa motoni
yakateketea,” Yoh 15:6. Hakika kama mimi ni Mkristo bila Kristo katika maisha
yangu, huko mbele ya safari ni giza tupu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Ninyi
mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote
nanyi mtatendewa,” Yoh 6:7
Tusali:-
Ee Yesu, tudumishe katika upendo wako wa kweli.
No hay comentarios:
Publicar un comentario