JUMAMOSI
WIKI YA 4 YA PASAKA
Somo:
Mdo 13:44-52
Zab:
98:1.2-3ab, 3cd-4
Injili:
Yoh 14:7-14
Nukuu:
“Paulo na Barnaba
wakanena kwa ushujaa wakasema, Ilikuwa lazima neno la Mungu linenwe kwenu
kwanza; lakini kwa kuwa mnalisukumia mbali, na kujiona nafsi zenu kuwa hamkustahili
uzima wa milele, angalieni, twawageukia Mataifa,” Mdo 13:46
“Lakini Wayahudi
wakawafitinisha wanawake watauwa wenye cheo na wakuu wa mji, wakawataharakisha
watu wawaudhi Paulo na Barnaba; wakawatoa katika mipaka yao,” Mdo 13:50
“Yesu akamwambia, Mimi nimekuwapo pamoja nanyi siku hizi
zote, wewe usinijue, Filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba; basi wewe wasemaje,
Utuonyeshe Baba?” Yoh 14:9
“Yeye
aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa
kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba,” Yoh 14:12
“Nanyi
mkiomba lo lote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana,”
Yoh 14:13
TAFAKARI:
“Jumuiya ya kwanza ya wakristo na Changamoto za uinjilishaji; Yote yawezekana
ndani na katika Kristo.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo ni jumamosi ambapo kwa namna ya pekee Mama Kanisa anatualika tutafakari
neno hili, “Jumuiya ya kwanza ya wakristo na Changamoto za uinjilishaji; Yote
yawezekana ndani na katika Kristo.” Ni ukweli usio tia shaka kwamba kukua na
kuongezeka kwa Kanisa letu kumekuwa hivyo kama kulivyo kutokana na changamoto
mbalimbali katika huinjilishaji. Tukitazama jumuiya ya kwanza ya Wakristo kama
ilivyo, walikalibiliana na upinzani mkubwa juu ya kile walichoamini sambamba na
tukio zima la ufufuko wa Yesu Kristo. Tendo hili kwa ujumla wake liliweza
kuwaunganisha watu na wakati mwingine kuwatenganisha kutokana na kile walichokuwa
wakikiamini awali juu ya maisha yao na maana halisi ya Masiha.
Kutokana na wimbi hili
la sintofahamu, jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo iliwapasa kusema juu ya Yesu
Kristo waliyemjua, waliyeishi naye, na yale aliyotenda kwa maisha yao na ufunua
mzima wa historia ya wokovu wa mwanadamu kadiri ya Maandiko Matakatifu
yalivyofumbua ukweli huu. Ni katika hali hii ya kumtangaza Kristo kadiri ya
mguso wa maisha ya kila siku ya yule waliyemwamini (Yesu Kristo) na ufunuo wa
Maandiko Matakatifu yalivyoufunua ukweli huu kupingana na ufahamu ya Wayahudi
kuhusu Masiha, Wayahudi hawa hawakuwa tayari kusikia alichokisema Mtume Paulo.
Hivyo Mtume Paulo analazimishwa kukaa kimya na Wayahudi kutokana na wingi wa
watu kuukubali ukweli juu ya Kristo. Hapa ndipo tunapoongelea kuhusu wivu wa
Wayahudi kuhusu ukweli juu ya Kristo. “Bali
Wayahudi, walipowaona makutano, wakajaa wivu, wakayakanusha maneno yaliyonenwa
na Paulo, wakibisha na kutukana,” Mdo 13:45.
Ndugu yangu
tunayesafiri sote katika tafakari hii, aliloanzisha Mungu hatuwezi kulizuia kwa
ufahamu wetu mdogo tuliokuwa nao. Tunapoukataa ukweli wa Mungu, Mungu ufikisha
ukweli huu kwa watu wengine. Licha ya kwamba Taifa la Israeli lilipendelewa
kufanya maagano na Mungu katika safari hii ya ukombozi, Mungu katika kutimiza
hazma yake hakujali kufikisha ujumbe wake wa wokovu kwa wale waliomridhia. Ni
katika namna hii wewe na mimi leo tunahesabiwa haki tunapoishi kweli hii ya
kimungu tuyafanya na kuyatimiza kwa uaminifu yale yampendezayo Mungu. Hivyo, “Paulo na Barnaba wakanena kwa ushujaa wakasema,
Ilikuwa lazima neno la Mungu linenwe kwenu kwanza; lakini kwa kuwa mnalisukumia
mbali, na kujiona nafsi zenu kuwa hamkustahili uzima wa milele, angalieni,
twawageukia Mataifa,” Mdo 13:46. Ninapotafakari hazma ya Mungu katika malengo
yake ya umilele ndani yetu, nimegundua kitu hiki; binadamu huweza tu
kuchelewesha hazma ya Mungu katika ukamilifu wake kwa wakati ufahao, ikiwa ni
subirá tu ya Kimungu kwa kujali uhuru aliokuwa nao binadamu kwa kujirudi na
kumrejea muumba wake, ila binadamu huyu hawezi kubadili mpango wa Mungu kwa
kile anachoona kinafaa kwa maisha yetu na malengo yake ambayo kwa wakati wote
na nyakati zote ni mema.
Ndugu yangu, ni kwa
namna hii lile aliloazimia Mungu linabaki kuwa na mashiko kwamba, “Mataifa waliposikia hayo wakafurahi,
wakalitukuza neno la Bwana, nao waliokuwa wamekusudiwa uzima wa milele
wakaamini,” Mdo 13:48. Mara zote ushindi kama huu hauachi kuwa na upinzani.
Unapoona umepita katika msuguano wa kiimani wa mtindo huu, yakupasa kujiandaa
vyema katika hali kinzani kwa kile ulichokisimamia. Nalisema hili si kwa
nadharia ila kwa vitendo kutokana na mang’amuzi yangu ya kichungaji kwa miaka
sita niliyokaa Parokiani kama Paroko mara tu baada ya upadirisho wangu. Kile
ulichokisimamia katika kweli na haki katika Kristo bila tuterereka, yakupasa
kujiandaa katika ukinzani wake. Jambo hili na ukweli huu unawakuta Mtume Paulo
na Barnaba. “Lakini Wayahudi
wakawafitinisha wanawake watauwa wenye cheo na wakuu wa mji, wakawataharakisha
watu wawaudhi Paulo na Barnaba; wakawatoa katika mipaka yao,” Mdo 13:50. Katika
hali ya namna hii, wewe kama mchungaji nikimaanisha mwenye dhamana kiimani
mathalani Paroko, yakupasa kusimama imara katika kweli na haki Kristo akiwa
msingi wa yote. Yatakayotokea kutokana na msuguano huu ni mapito tu. Yatakuja
kwa kasi kubwa, ila yatatoweka kama moshi wa mabua angani. Mwisho wa msuguano
huu ni ukamilifu wa kweli ya Mungu, na furaha ya kweli kwa kile ulichokisimamia
kama mpakwa mafuta. Jambo hili lilitokea pia kwa Mtume Paulo na Barnada. Roho
wa Bwana hatoacha kutufariji na kutujaza matumaini ya kulinena neno la Mungu
licha ya magumu tunayokutana nayo. “Na
wanafunzi walijaa furaha na Roho Mtakatifu,” Mdo 13:52. Kanisa leo na kama
ilivyokuwa mwanzo lapaswa daima kuishi katika ukweli huu wa Kristo ndani na
katika yeye.
Wapendwa wana wa Mungu,
msingi wa haya yote tunayoyaona kutoka jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo
yanatokana na msingi wa imani waliyokuwa nayo juu ya Yesu Kristo na yale
aliyoyafundisha. Ni ukweli usiotia shaka kwamba jumuiya hii ya kwanza ya
Wakristo waliamini barabara yule wamfuatao na kumshuhudia mbele za watu. Mtume
Filipo anapomwuliza Yesu tuonyeshe Baba nayo yatosha kumwamini, Yesu anamjibu
na kusema, “Mimi nimekuwapo pamoja nanyi siku
hizi zote, wewe usinijue, Filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba; basi wewe
wasemaje, Utuonyeshe Baba?” Yoh 14:9. Kristo
anafumbua ukweli wa kumwilishwa kwake, si tu kwa Filipo, hata kwetu pia.
Kumwilishwa huku kwa Yesu Kristo ni ukweli wa Mungu mwenyewe katika fumbo na
umbo hili la kibidamu kama sisi ila utofauti wake ni kwamba hakutenda dhambi
kama mwanadamu. Yesu Kristo anakazia ukweli huu na kusema, “Hayo maneno
niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu
huzifanya kazi zake,” Yoh 14:10b. Ufunuo huu wa Mungu kupitia Yesu Kristo ni wa
wazi na wakati mwingine wakujificha. Ila hapana shaka hata kidogo kwa umungu wa
Kristo kunakojieleza kwa yale aliyoyafanya yaani kazi zake.
Wapendwa
wana wa Mungu, Kristo analifumbua jambo hili pale tunapokuwa na shaka juu yake
kwa kusema, “La! Hamsadiki hivyo, sadikini kwa sababu ya kazi zenyewe,” Yoh
14:11b. Imani ya kweli juu ya Kristo ndiyo inayotufanya kuishi na kutenda kama
alivyofanya Yesu Kristo. Ukweli huu anausema Kristo mwenyewe, na wale wote
waliouishi ukweli huu, Kristo amefanya makuu kupitia kwao kwa mkono wake. “Yeye
aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa
kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba,” Yoh 14:12. Matendo makuu
hufanyika kwa mtu huyu aaminiye juu ya Kristo si kwa faida yake binafsi, ila
kwa kupitia mtu huyu Mungu anatukuzwe na kuabudiwa milele ndani ya Yesu Kristo
mwanaye. “Nanyi mkiomba lo lote kwa jina
langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana,” Yoh 14:13. Je,
ndugu yangu, hupendi kuwa sababu ya utukufu huu wa Mungu kupitia mwanaye Yesu
Kristo?
Wapendwa,
jibu la swali hili ndilo kiini cha Imani yetu, na maisha yetu kama Wakristo na
Wafuasi wa Kristo leo katika dunia hii tunayoishi: “KUWA SABABU YA UTUKUFU WA
MUNGU KUPITIA MWANAYE YESU KRISTO, na si vinginevyo.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Yeye aniaminiye
mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo
atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba,” Yoh 14:12
Tusali:-Ee Yesu,
tufanye kuwa sababu ya Utukufu wa Mungu kupitia kwako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario