martes, 19 de abril de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 4 YA PASAKA

ALHAMISI WIKI YA 4 YA PASAKA

Somo: Mdo 13:13-25
Zab: 89:2-3, 21-22, 25, 27
Injili: Yoh 13:16-20
Nukuu:
Katika uzao wake mtu huyo Mungu amewaletea Israeli Mwokozi, yaani, Yesu, kama alivyoahidi,” Mdo 13:23

“Lakini, angalieni, anakuja mmoja nyuma yangu ambaye mimi sistahili kumlegezea viatu vya miguu yake,” Mdo 13:25b 

Sisemi habari za ninyi nyote; nawajua wale niliowachagua; lakini andiko lipate kutimizwa, Aliyekula chakula changu Ameniinulia kisigino chake,” Yoh 13:18

Tangu sasa nawaambia kabla hayajatukia, ili yatakapotukia mpate kuamini ya kuwa mimi,” Yoh 13:19

TAFAKARI: “Wokovu wetu ni katika Kristo; na hukumu yetu itatokana na mahusiano yetu na Kristo”

Wapendwa wana wa Mungu, kama kweli tu wafuasi wa Kristo, ukweli huu ni ni bayana na sehemu muhimu sana ya maisha yetu kama wafuasi wake KRISTO: “Wokovu wetu ni katika Kristo; na hukumu yetu itatokana na mahusiano yetu na Kristo.” Hatuwezi kuongelea wokovu wa Mkristo pasipo Kristo, na ni kwa namna hiyo hiyo hatuwezi kuongelea hukumu ya mwisho pasipo uhusiano wetu na Kristo. Je, Mkristo ni nani? Kwanza kabisa Mkristo ni yule aliyebatizwa katika Mungu mmoja nafsi tatu kadiri ya kanuni ya ubatizo ilivyo: “Nakubatiza kwa jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu.” Kwa kanuni hii tu haitashi wewe kuwa Mkristo.

Hatua ya pili ya Mkristo kamili ni ufuasi wake katika Kristo katika fumbo zima la kifo, mateso, na ufufuko wake Kristo. Ni katika fumbo hili tunazifia dhambi zetu pamoja naye, na kufufuka naye katika hali ya upya pamoja naye. Upya huu wa maisha katika Kristo na ndani ya Kristo unamapaswa yake. Mapaswa yake ni kuisha kama Kristo mfufuka, yaani maisha safi na yasiyo na hatia yoyote. Tunapoisha katika hatia tunaendeleza mateso ndani na katika Kristo. Kristo Mfufuka ni mshindi dhidi ya dhambi na kifo. Kufurahia na kuisha katika hali ya dhambi ni kuendeleza mateso ya Kristo Mfufuka, na kutothamini sadaka hii kubwa ya Kristo kwa maisha yetu kama wafuasi wake. Ni katika mateso, kifo na ufufuko wake Kristo, ndipo kwenye kilele kizima cha historia ya wokovu wetu. Kristo ndiye mkamilisho wa kilele hiki.

Jambo hili muhimu katika maisha ya Mkristo, ndilo ambalo Mtume Paulo katika safari yake ya umisionari huko Pafo na Perge analiwekea msingi. Mtume Paulo anasema, Katika uzao wake mtu huyo Mungu amewaletea Israeli Mwokozi, yaani, Yesu, kama alivyoahidi,” Mdo 13:23. Ndugu yangu, wakovu wako pasipo Kristo ni sawa na maisha ya samaki jangwani. Je, inawezekana? Ndugu yangu, usipolielewa jambo hii muhumu katika maisha yako kama Mkristo, kuruka ruka kwako kutoka kikundi kimoja cha kitume kwenda kingine ndani ya Kanisa hakuna maana yoyote. Kuhama kwako dhehebu moja la Kikristo kwenda likingine hakuna maana yoyote. Kubadili dini yako ndani ya Kristo kwenda dini nyingine hakuna maana yoyote. Kusimama leo mbele ya kadamnasi na kusema umeokoka hakuna maana yoyote.

Ukweli wa Yesu Kristo na nafasi yake katika historia nzima ya wokovu wetu, unasemwa na Yohane Mbatizaji, ambaye leo katika somo letu la kwanza Mtume Paulo ananukuhu ukweli huo na kusema, “Lakini, angalieni, anakuja mmoja nyuma yangu ambaye mimi sistahili kumlegezea viatu vya miguu yake,” Mdo 13:25b. Maneno haya yanatafsiri hii: “HAKUNA WA KULINGANISHWA NA YESU KRISTO KATIKA HISTORIA NZIMA YA WOKOFU WETU.” Kulegeza kamba za viatu vya Yesu kungemaanisha uwezekano wa mbadala wa Yesu Kristo, kitu ambacho kadiri ya mpango huu wa wokovu hakipo. Hapa ndipo penye fumbo zima la UFUNUO WA MUNGU KWA MWANADAMU. Tunapoona baadhi ya binadamu wenzetu wanajiinua na kujitanua kuwa wao ndio kweli na uzima, ni kichekesho na mshangao mkubwa. Umepata wapi mamlaka hayo ndugu yangu? Kanisa kama chombo elekezi cha wokovu wetu-Sakramenti ya wokovu, na uzima wetu kuelekea umilele, ni mwili wa Kristo mwenyewe ambao sisi wabatizwa na waishio mapaswa ya ubatizo huo tu viungo vyake. Ni makosa makubwa sana, leo tunaposikia mtu anajiinua na kusema nakwenda kusali katika “KANISA LA EDGAR.” Kanisa ni la Kristo; ndani na katika Kristo.

Kuujua ukweli huu na kutokuuishi ni usaliti mkubwa mbele ya Kristo aliyekufa kwa sababu yako. Yesu katika injili ya leo anasema, Sisemi habari za ninyi nyote; nawajua wale niliowachagua; lakini andiko lipate kutimizwa, Aliyekula chakula changu Ameniinulia kisigino chake,” Yoh 13:18. Aliyewachagua Kristo ni pamoja na sisi tunaohesabiwa haki hiyo na Mama Kanisa kwa Sakramenti ya Ubatizo. Mama Kanisa anafanya kazi hiyo leo kwa niaba ya Kristo mwenyewe. Kwa tendo hili la Sakramenti ya ubatizo, tumeshiriki na kula chakula chake, yaani kuwa warithi wa ufalme wa Mbingu ambao tayari umeanza katika ubatizo wetu ila bado kukamilishwa. Fumbo hili tunalisema sana hasa wakati wa maziko ya Mkristo. Padre huyasema maneno haya anapomnyunyuzia maiti (akiwemo kaburi) maji ya baraka: “Katika maji ya ulibatizwa Mungu akamilishe ndani mwako aliyoanzisha katika ubatizo.” Kumgeuzia kisigino Kristo ni kutokutambua ukweli huu.

Wakristo wengi leo ni wamajina tu na matukio, nikimaanisha; katika ukweli wake wa nje yaani usio wa kisakramenti. Ukweli huu wa kimatukio ni pamoja na Ubatizo, Sakramenti ya Ekaristi, Kipaimara na Ndoa kwa wenye bahati. Leo wengi wanaishi tu bila Sakramenti hii ya Ndoa na kujihalalishia. Sakramenti ya Kipaimara au kuimarishwa leo imekuwa kama Sakramenti ya kuliaga Kanisa, “The send off Sacrament.” Mkristo huyu ataonekana tena Kanisani akiwa mfu. Maisha katika ufufuko hayapaswi kuwa ya mtindo huu. Yesu Kristo anatupa angalisho la mtindo huu ya maisha bila yeye, na kusema, Tangu sasa nawaambia kabla hayajatukia, ili yatakapotukia mpate kuamini ya kuwa mimi,” Yoh 13:19. Angalisho hili ya Yesu leo linatutaka tufahamu kiini cha maisha yetu na Imani yetu kipo wapi. Ndugu yangu, hauna wakati mwingine wa kujipanga zaidi ya wakati huu na sasa. Usomapo habari hii, usiutafute ukweli huu pengine zaidi ya kwenda ndani ya moyo wako na uguse pale ambapo mara nyingi hupendi kupagusa na umepafunika licha ya kwamba ukweli wa kilicho ndani yake unakijua. Hapo usipopataka kupagusa na kupaongelea ndiyo wewe mwenyewe, na ndipo kwenye ufunguo wa kwenda pale alipo Kristo.

Tumsifu Yesu Kristo!

Tangu sasa nawaambia kabla hayajatukia, ili yatakapotukia mpate kuamini ya kuwa mimi,” Yoh 13:19


Tusali:-Ee Yesu, najua sasa hakuna wokovu pasipo wewe. Niwezeshe kila siku ya maisha yangu kuishi kweli hii. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario