JUMAMOSI
WIKI YA 5 YA PASAKA
Somo: Mdo 16:1-10
Zab: 100:1b-2, 3, 5
Injili: Yoh 15:18-21
Nukuu:
“Basi akafika Derbe na Listra, na hapo palikuwa na
mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa mwanamke Myahudi aliyeamini;
lakini babaye alikuwa Myunani,” Mdo 16:1
“Paulo
akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa akamtahiri kwa ajili ya Wayahudi
waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye ni Myunani,” Mdo
16:3
“Basi
walipokuwa wakipita kati ya miji ile, wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume
na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike,” Mdo 16:4
“Makanisa
yakatiwa nguvu katika ile Imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku,” Mdo 16:5
“Iwapo
ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia
ninyi,” Yoh 15:18
“Kama
mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi
si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu
huwachukia,” Yoh 15:19
“Lakini
haya yote watawatenda kwa ajili ya jina langu, kwa kuwa hawamjui yeye
aliyenipeleka,” Yoh 15:21
TAFAKARI:
““Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya
kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi,” Yoh 15:18
Wapendwa wana wa Taifa
la Mungu, leo kwa namna ya pekee tutafakari changamoto za uinjilishaji za
Kanisa la mwanzo na changamoto tunazokumbana nazo leo katika utume wetu kama
wabatizwa na wahudumu katika Kanisa. Bila shaka wiki nzima hii tumekuwa
tukitafakari changamoto hizi na hatua waliyochukuwa Mitume kukabiliana nazo,
hasa kwa kuitisha Mtaguso wa Yerusalemu.
Matokea ya Mtaguso huu
ulikuwa: “Wajiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu,
na damu, na nyama zilizosongolewa, na uasherati. Mkijizuia na hayo, mtafanya
vema. Wasalamu,” Mdo 15:29. Hata hivyo Kanisa bado linakumbana na changamoto za
mila na desturi za Kiyahudi. Hivyo ili Timotheo afuatane na Mtume Paulo,
inampasa kutahiriwa. “Basi akafika
Derbe na Listra, na hapo palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana
wa mwanamke Myahudi aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani,” Mdo 16:1. Je kwa tendo hili Paulo atakuwa ameenda kinyume
na maamuzi ya Mtaguso wa Yerusalemu? Ndugu yangu tunayesafiri wote katika
tafakari hii, ni vyema tuelewe jambo hili. Licha ya kwamba Kanisa ni la
kiulimwengu, na hili limethibitishwa katika mitaguso mbalimbali, maamuzi ya
mitaguso hiyo hayaondoi upekee wa changamoto ya Kanisa mahalia, mfano Kanisa la
Tanzania. Hapa ndipo tunapozungumzia busara za kichungaji kuenenda na mazingira
husika bila kuwakwaza watu. Hivyo, tukio hili la kutahiriwa kwa Timotheo
linaendana na mazingira maalumu bila kuwakwaza watu, ili kuweza kupenyeza
ujumbe ule waliokuwa wameubeba au kusudiwa, na hapa ikiwa ni maamuzi ya Mtaguso
wa Yerusalemu.
Mtume Paulo anatupa
sababu ya kufanya hivyo ikiwa ndiyo busara ya kichungaji. “Paulo akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa akamtahiri kwa
ajili ya Wayahudi waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye
ni Myunani,” Mdo 16:3. Je, Paulo alilifanya jambo hili kutowakwaza Wayahudi?
Bila shaka Paulo analifanya jambo hili kwa malengo hayo, kama anavyosema
Kristo, “Akawaambia wanafunzi wake, Makwazo
hayana budi kuja, lakini ole wake mtu yule ambaye yaja kwa sababu yake! Ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia
lifungwe shingoni mwake, akatupwe baharini, kuliko kumkosesha mmojawapo wa
wadogo hawa,” Lk 17:1-2. Ni vizuri kutowakwaza wale tunaotaka waufahamu ukweli
wa Mungu. Kwa upande wa kichunguaji, ni rahisi sana kumhubiri Kristo kwa kwale
wasiomjua bado, kuliko kuwarudisha wale waliokatishwa tamaa hasa pale
tunapowakwaza.
Kwa
mambo yale ambayo hayaendi kinyume na imani yetu, yanapotokea bila kujua au
kujiandaa, ni vyema tukayapa muda ili tuyaelewe na kutumia mbinu ya
kuwaelimisha wale wayafanyayo, hasa tukilenga katika kutaka kujua ‘kwa nini
wanafanya kama wanavyofanya.’ Hivyo kwa kulitambua jambo hilo, inakuwa rahisi
kufikisha ujumbe ule uliokusudiwa. “Basi
walipokuwa wakipita kati ya miji ile, wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume
na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike,” Mdo 16:4. Mambo haya huwa
tunakutana nayo mara nyingi hasa pale tunapoanza utume mpya katika mazingira
mageni kinyume na mila na desturi zetu tulizokulia na kuzizoea. Jambo la msingi
ni kushikilia mafundisho sahihi ya Kanisa (katika kuyafundisha kwa lugha
nyepesi na mifano hai ili yaeleweke kwa waamini) na yenye mwelekeo wa wokovu,
na maisha ya umilele.
Ni
dhahiri kwa Kanisa la mwanzo mengi yalifundishwa na yenye kuleta umoja kindugu
na Kikanisa kwa ujula wake, ila haya manne yapo wazi, ususani tendo la
kutahiriwa kuonekana kama kigezo cha kuchangamana pamoja; Kwanza, mafundisho
yalisisitiza kuzishika amri za Mungu. “Kutahiriwa si kitu, na
kutokutahiriwa si kitu bali kuzihifadhi amri za Mungu,” 1Kor 7:19.
Pili, kuishi maisha ya
Ufufuko ndani na Katika Kristo Yesu, na hapa yakilenga haswa mila na desturi
zetu zilizopotofu na zisizo na mwelekeo wa wokovu na maisha ya umilele. Msalaba
wa Kristo ndiyo kielelezo cha huo Utukufu wenyewe. “Lakini
mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu
Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa
ulimwengu. Kwa sababu kutahiriwa
si kitu, wala kutokutahiriwa, bali kiumbe kipya,” Gal 6:14-15. Hapa
tunakumbushwa pia hakuna Utukufu pasipo Msalaba kwa ye yote yule aliye mfusi
mwaminifu wa Yesu Kristo.
Tatu, mafundisho ya
Kanisa la mwanzo yalijikita kwenye kweli ya kuwa yote katika yote na Kristo
Yesu. Kujitoa bila kujibakiza katika hali ya kusahau tofauti zetu zisizo na
mwelekeo wa wokovu na maisha ya umilele. Hivyo “hapo
hapana Myunani wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala
mshenzi, mtumwa wala mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote,” Kol 3.11.
Nne, yote yapo kama
yalivyo kwa neema ya Mungu. Hakuna kati yetu mwenye kujihesabia haki mwenyewe.
Zipo sehemu nyingi katika Maandiko Matakatifu, na hasa Agano Jipya
zinazoonyesha kweli hii. Hivyo ndugu yangu, “kujisifu kwetu ni huku,
ushuhuda wa dhamiri yetu, ya kwamba kwa utakatifu na weupe wa moyo utokao kwa Mungu;
si kwa hekima ya mwili, bali kwa neema ya Mungu; tulienenda katika dunia, na
hasa kwenu ninyi,” 2Kor 1.12
Hivyo
wapendwa wana wa Mungu, wewe na mimi yatupasa kujua kweli hii, kwamba,
utamaduni wa mahali fulani ni sehemu ya Maisha yao, na hivyo ni Utakatifu wao.
Kwa maana hiyo, tuwapo katika mazingira hayo ni kufanya kama alivyoambiwa Musa
na Mungu, “Bwana alipoona ya kuwa amegeuka ili atazame, Mungu
akamwita kutoka katikati ya kile kijiti, akasema, Musa! Musa! Akasema, Mimi
hapa. Naye akasema, Usikaribie
hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi
takatifu,” Kut 3:4-5. Yatupasa kuvivua viatu vyetu, ili kujua utakatifu wa
mahali pale. Yatupana kuwa tayari kuona upya na watu wa mahali pale ili kujua
ukweli halisi ya maisha yao. Uinjilishaji wetu na umisionari kwa ujumla wake
unapokosa dhana hii ya kuona upya yale tunayokutana nayo, ukiambatana na upole wa kujifunza, mwisho wa siku tunaishia
kutokuwaelewa watu husika na kuwa na sintofahamu kubwa. Mtihani huu Mtume Paulo
anaufaulu vizuri, na matokea yake ni kwamba, “Makanisa
yakatiwa nguvu katika ile Imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku,” Mdo 16:5. Ukiona kila unayekutana naye anakukimbia ujue
kunatatizo kubwa katika mahusiano yako na wale unaokutana nao. Kabla ya kumtafuta
mchawi, zama kwanza ndani yako na jipekue vizuri namna yako ya kufanya mambo,
na namna ya kufikisha kwao kile ulichotarajia-ujumbe.
Wakati mwingine
yawezekana kabisa ukakumbana na pingamizi kubwa kutokana na mazoea yao ambayo yamekuwa
sehemu ya tabia yao. Unapotenda jambo jema kwa watu na mapokeo yao yakawa
mabaya, wala usikate tamaa. Tumia njia njingine ili ujumbe ule ule uwafike
vyema. Na zaidi ya hayo Yesu anatuimarisha kwa kutupa moyo na kusema, “Iwapo ulimwengu
ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi,” Yoh
15:18. Kama ulimwengu huo ulishamchukia yule kwa wakati huu unayemtumikia,
hakika huyo huyo ndiye atakaye kupa njia na namna ya kufanya pale ukutanapo na
mkwamo. Yesu anasema hivi kuhusu hali hii mara inapotoka: “Na
watakapowachukua ninyi, na kuwasaliti, msitafakari kwanza mtakayosema, lakini
lo lote mtakalopewa saa ile, lisemeni; kwa maana si ninyi msemao, bali ni Roho
Mtakatifu,” Mk 13:11. Kwa vile ujumbe uusemao na kuusimamia si wetu binafsi,
kwa wakati huo Roho Mtakatifu atatusaidia kuyasema yale yatupasaya kuyasema kwa
sifa na utukufu wa Mungu.
Ukweli ni kwamba yeyote
anayekuwa ndani na katika Kristo, ujitenga na mwelekeo na mtazama wa yale
tunayoyaishi na kukutana nayo kila siku. Mtu huyu huyaona mambo yote katika
mtazamo mwingine. Unapokuwa na maisha yenye malengo, na hasa maisha katika
ufuasi wa Kristo, utayaona yote katika umilele. Kukiona kitu katika umilele
wake, ukweli huu hupingana na dhana ya leo na sasa. Tupo katika ulimwengu wa ‘ponda
mali kifo chaja.’ Hivyo Yesu Kristo anatuambia kuhusu ukweli huu, kwamba, “Kama
mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi
si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo
ulimwengu huwachukia,” Yoh 15:19. Hufanyapo kila kitu na kupigiwa makofu,
jaribu kuchunguza makofi hayo. Wakati mwingine makofi hayo huashiria kejeri.
Mwisho tuwe tayari
kutendwa vibaya kama Kristo alivyotendwa kwa sababu watesi hawa hawamjua yule
aliyempeleka Kristo. “Lakini haya yote
watawatenda kwa ajili ya jina langu, kwa kuwa hawamjui yeye aliyenipeleka,” Yoh
15:21. Tusisahau pia matatizo na magumu katika utume wetu, yanatufanya kukua na
kukomaa kiroho.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lakini
haya yote watawatenda kwa ajili ya jina langu, kwa kuwa hawamjui yeye
aliyenipeleka,” Yoh 15:21
Tusali:-Ee
Yesu, uliyeshinda uovu kwa wema, tujalie uvumilivu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario