jueves, 21 de abril de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 4 YA PASAKA

IJUMAA WIKI YA 4 YA PASAKA
Somo: Mdo 13:26-33
Zab: 2:6-7, 8-9, 10-11ab
Injili: Yoh 14:1-6
Nukuu:
“kwetu sisi neno la wokovu huu limepelekwa,” Mdo 13:26b 

 “Na ijapokuwa hawakuona sababu ya kumfisha wakamwomba Pilato auawe,” Mdo 13:28 

Lakini Mungu akamfufua katika wafu; akaonekana siku nyingi na wale waliopanda naye kutoka Galilaya hata Yerusalemu, ambao sasa ndio walio mashahidi wake mbele ya watu,” Mdo 13:30-31

Na sisi tunawahubiri habari njema ya ahadi ile waliyopewa mababa, ya kwamba Mungu amewatimizia watoto wetu ahadi hiyo, kwa kumfufua Yesu; kama ilivyoandikwa katika Zaburi ya pili, Wewe ndiwe Mwanangu, mimi leo nimekuzaa,” Mdo 13:32-33 

Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi,” Yoh 14:1 

 “Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo,” Yoh 14:3

 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6 

TAFAKARI: “Ili nilipo mimi, nanyi mwepo. Mimi ndimi njia na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba ila kwa njia ya mimi.”

Wapendwa wana wa Mungu, ingawa upo uwezekano wa mtu yeyote kuupata wokovu na kuifikia Mbingu kutokana na msukumo wa maisha yake wenye kuongozwa na dhamiri yake njema na hofu ya Mungu hata kama hakuwahi kusikia habari njema za Kristo Yesu, wewe na mimi tuyeunganishwa na Kristo kwa Sakramenti ya Ubatizo, Kristo hubaki kuwa njia, kweli, na uzima katika usahihi wake. Kwa wale ambao bado hawajafikiwa na habari njema ya wokovu ila wanaishi kwa dhamiri zao njema, Kanisa kupitia Mamlaka yake fundishi-Magisterium, linasema hivi juu ya wokovu wao; -Mafundisho ya Kanisa hasa tunaposoma Katekisimu ya Kanisa Katoliki, namba 847 inafundisha juu ya dhamiri hai na safi ambapo hata wale wasiomjua Kristo ndiyo ponya yao. Ukweli huu pia umefafanuliwa vizuri katika mafundisho ya Mtaguso wa Pili wa Vatikano, Konstitusio ya Kichungaji juu ya Kanisa katika Ulimwengu wa leo, “Gaudium Et Spesteaches,” “Furaha na Matumaini,” inaelezea ukweli huu kama ifuatavyo; “Jambo hilo haliwahusu wakristo tu bali pia wanadamu wote wenye mapenzi mema, ambao neema ya Mungu hufanya kazi mioyoni mwao, kwa namna isiyoonekana. Maana Kristo alikufa kwa ajili ya watu wote na wito halisi wa binadamu ndio mmoja, ule wa kimungu. Kwa hiyo lazima tuwe na wazo kwamba Roho Mtakatifu anawajalia watu wote uwezekano wa kushiriki fumbo la kipasaka, kwa jinsi anayoijua Mungu,” (no. 22)

Pamoja na ukweli huo, ikiwa wewe na mimi tumeunganishwa na Kristo kwa Sakramenti ya Ubatizo na kuwa warithi wa ufalme wa mbinguni, yatupasa kuishi ndani na katika Kristo. Hivyo ni wajibu wangu leo na daima kumjua Kristo, kumpenda, kumtumikia–(kupitia wote wale walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, Mwa 1:27), na mwisho ni Yeye tu atakaye nihesabia haki mbele ya kiti chake cha uzima wa milele mbinguni. Masomo yetu ya leo yamefafanua kwa undani kweli hii.

Wapendwa wana wa Mungu, ikiwa wewe ni mfuasi wa Kristo na Mungu aliye hai, katika maana ya kuziishi vyema na kwa uaminifu ahadi zako za ubatizo, yakupasa kuelewa ukweli huu juu ya Kristo Yesu. Ukweli ni kwamba, bila Kristo hatuwezi kufanya lo lote, liwe dogo au kubwa. Kama Kristo ni Mzabibu nasi tu matawi yake, twawezaje basi kushamiri na kupata uhai pasipo shina lenyewe? Kitendawili hiki kinateguliwa na Kristo mwenyewe. Naye anasema, Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote,” Yoh 15:5. Ndugu yangu na Mbatizwa mwenzangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, kwa weledi wako na yote uliyonayo, Je, waweza kutoboa mbingu bila Kristo Yesu? Na kama vile haitoshi, Yesu anaenda mbali zaidi na kujifananisha yeye na Mlango. Ndugu yangu na Mbatizwa mwenzangu, Kristo tu ndiye Mlango wa kufikia huo upande wa pili, yaani, Mbingu. Naye Yesu anatuambia hivi, Amin, amin, nawaambieni, Mimi ndimi mlango wa kondoo. Mimi ndimi mlango; mtu akiingia kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata malisho,” Yoh 10:7, 9. Upekee wa Kristo kama ndiyo Mlango sahihi umebebwa na maneno haya mazito ya Yesu. Naye anasema hivi, “Wote walionitangulia ni wevi na wanyang'anyi; lakini kondoo hawakuwasikia,” Yoh 10:8. Maana yake ni kwamba, kama hapo-“wakati fulani” iliwezekana wachache kwa ujanja ujanja wao kupita, au waliojitangazia na hata kujiinua kwamba wao ni “milango,” hawakuwa sahihi, na hata leo kama wapo si milango au mlango sahihi. Habari Njema kwa sasa ni kwamba Yeye mwenyewe-Yesu Kristo ndiyo HABARI NJEMA HIYO, na ndiyo MLANGO SAHIHI na wa KWELI.

Kweli hii ndiyo anayoihubiri Paulo na wenzake pasipo shaka yoyote wakimjua yule wanayemuhubiri na kumtumikia, yaani Yesu Kristo. Ni kwa kumfahamu Kristo na kwa sababu yake tu, Mtume Paulo anasema, “kwetu sisi neno la wokovu huu limepelekwa,” Mdo 13:26b. Ni wazi kabisa tena pasipo shaka yoyote kama Wayahudi wangalimfahamu vizuri Kristo wasingefanya waliyofanya. Hivyo ni jukumu la kila mmoja wetu aliyepata neema ya kufikiwa na habari njema juu ya Kristo na mwokozi wetu kuwa hai na shahidi wake. Ni katika ukweli wa jambo hili Paulo Mtume anasisitiza,  Kwa maana wakaao Yerusalemu, na wakuu wao, kwa kuwa hawakumjua yeye, wala maneno ya manabii yanayosomwa kila sabato, wameyatimiza kwa kumhukumu,” Mdo 13:27. Hata pale walipokosa sababu za msingi kuuondoa uhai wa mwenye haki-Yesu Kristo, Wayahudi walitunga uongo mwingine na kulazimisha kifo chake. Hivyo, ijapokuwa hawakuona sababu ya kumfisha wakamwomba Pilato auawe,” Mdo 13:28.

Ndugu yangu, kutokuona vizuri kwa wezwa sababishwa na matatizo ya macho na hata upofu nyemelezi, na mwisho upofu wenyewe. Ila nachelea kusema kwamba upofu mbaya ni upofu wa ufahamu, yaani, upofu wa kutokuona kitu kama kilivyo, na badala yake wakiona kitu kile kama ulivyo. Hivyo kwa kufahamu udhaifu huu juu ya Wayahudi, Paulo anasema hivi juu ya Kristo, Lakini Mungu akamfufua katika wafu; akaonekana siku nyingi na wale waliopanda naye kutoka Galilaya hata Yerusalemu, ambao sasa ndio walio mashahidi wake mbele ya watu,” Mdo 13:30-31. Ndugu yangu, huwezi kumfamu Kristo na kufikiwa na habari njema hii ya wokovu ukaendelea kukaa kimya na kuyafumbia macho yaliyo kinyume na wokovu huu aliotupatia Kristo Yesu kwa gharama ya damu yake pale Msalabani.

Mimi na wewe yatupasa kufanya kitu kwa ajili ya Kristo Yesu. Yapo mengi ya kufanya kwa ajili ya Kristo, ila anza hapo hapo ulipo. Na swali elekezi ni hili; Ee Yesu na Mwakozi wangu, kwa mazingira yangu na hali yangu naweza kukufanyia nini kwa ajili ya watu wako? Yesu Kristo aliye hai atakuongoza na utamfanyia mengi mazuri. Anza na yale madogo na yaliyo chini ya uwezo wako. Haya yaliyo madogo mara nyingi si rahisi kuonekana na wengi, ila hubeba neema na baraka kubwa sana. Kwa upande wake Mtume Paulo hakukaa kimya. Alifanya kitu kwa ajili ya Yesu. Na hapa anatoa ushuhuda huo na kutuambia, Na sisi tunawahubiri habari njema ya ahadi ile waliyopewa mababa, ya kwamba Mungu amewatimizia watoto wetu ahadi hiyo, kwa kumfufua Yesu; kama ilivyoandikwa katika Zaburi ya pili, Wewe ndiwe Mwanangu, mimi leo nimekuzaa,” Mdo 13:32-33

Hapana shaka yoyote kwamba msukumo wa maisha ya Mtume Paulo ulipata msingi imara katika fundisho hili la Mtume Petro, kwamba “Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo-Yesu Kristo,” Mdo 4:12. Ufahamu huu ndio, yaani, ‘Kristo ndiye kila kitu katika maisha yetu,’ ndio unaotupeleka kuyafahamu maneno ya Yesu katika Injili ya leo. Naye Yesu anasema, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Yesu Kristo ni njia kama ulivyo Mlango pekee wa kuufikia uzima wa milele. Na njia aliyoichagua Yesu ni Msalaba. Kwa kuibeba misalaba yetu na kuchukulia kindugu katika misalaba ya wenzetu kwa uaminifu na hofu ya Mungu tunakutana naye Kristo katika hali na mazingira hayo. Yesu Kristo ni kweli halisi. Kweli hii tunakutana nayo katika neno lake hasa pale tunapokuwa tayari kulisikia neno, kulipokea neno, kulitafakari neno, kulishirikisha neno, na mwisho kuwa shahidi wa neno.

Na Yesu Kristo ni uzima halisi. Kristo ni uzima halisi tunaposhiriki Ekaristi Takatifu katika mastahili yake. Yesu anatuambia, “Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe” Yoh 6:35. Ni katika kula chakula hiki-mwili na damu yake,  Yesu anahaidi mambo mawili makuu: Moja, ni ufufuko siku ya mwisho. Naye anasema, Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:54. Na katika kula chakula hiki-mwili na damu yake, Kristo hukaa ndani yetu. Naye anasema, Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake,” Yoh 6:56. Hata hivyo Mtume Paulo anatupa angalizo la chakula hiki cha uzima. Naye anasema, Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana,” 1Kor 11:27. Yatupasa kuijongea Meza ya Bwana tukiwa na mastahili ya kufanya hivyo-usafi wa mwili na roho, yaani, pasipo hatia yoyote. Zaidi ya hapo ni kuikufuru Meza ya Bwana.

Wapendwa wana wa Mungu, kwa kupitia Sakramenti ya kitubio tunapatanishwa tena na Kristo kutoka katika hatia zote. Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu,” Isa 1:18. Hakuna sababu ya kufa moyo pale ambapo mambo huenda ndivyo sivyo. Mungu aliye Upendo na Huruma uanza upya nasi pale tunapokuwa tayari kufanya hivyo. Hivyo ndani na katika Kristo hakuna sababu ya kuwa na hofu. Tumwamini Kristo na tuziamini kazi zake na hasa kupitia Masakramenti yake. Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi,” Yoh 14:1.

Ndani na Katika Kristo kunautulivu wa kweli, naye kesha tuandalia makao ya milele. Duniani hapa ndugu yangu tunapita tu. Ulimwenguni hapa ni sehemu ya maandalizi ya huo umilele. Mbinguni ndipo kwenye nafasi ya kila mmoja wetu, na ndiyo makao ya milele. Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali,” Yoh 14:2. Lengo la Kristo ni kumpata kila mmoja wetu. Hili ndilo pia lengo msingi la Kanisa. Lilipo Kanisa katika maana ya Mwili wa Kristo nasi tukiwa viungo hai vyake, Kanisa huwa Sakramenti ya Wokovu kwa sababu Kristo yu hai mahali hapo. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo,” Yoh 14:3. Ndungu yangu, je, hu kiungo hai cha mwili wa Kristo, yaani Kanisa?

Tumsifu Yesu Kristo!

Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi,” Yoh 14:1


Tusali:-Ee Yesu Mwema na  Hai, nifanya kiungo hai cha mwili wako, ili nisiwe sababu ya kupooza kwa Kanisa pale nilipo. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario