sábado, 23 de abril de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 5 YA PASAKA MWAKA-C

JUMAPILI YA 5 YA PASAKA YA MWAKA-C

Somo I: Mdo 14:21-27
Zab: 145:8-13
Somo II: Ufu 21:1-5a
Injili: Yoh 13:31-33a, 34-35
Nukuu:
wakifanya imara roho za wanafunzi na kuwaonya wakae katika ile Imani, na ya kwamba imetupasa kuingia katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi,” Mdo 14:22 

Na walipokwisha kuwachagulia wazee katika kila kanisa, na kuomba pamoja na kufunga, wakawaweka katika mikono ya Bwana waliyemwamini,” Mdo 14:23 

 “Hata walipofika wakalikutanisha kanisa, wakawaeleza mambo yote aliyoyafanya Mungu pamoja nao, na ya kwamba amewafungulia Mataifa mlango wa imani,” Mdo 14:27

 “Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita,” Ufu 21:4 

Na yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya,” Ufu 21:5

Enyi watoto wadogo, bado kitambo kidogo nipo pamoja nanyi” Yoh 13:33

Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo,” Yoh 13:33, 34 

Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi,” Yoh 13:35

TAFAKARI: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Naye Mungu atafuta kila chozi katika macho yenu. Mlikutanishe Kanisa mara zote na kuwaeleza mambo yote aliyoyafanya Mungu pamoja nanyi.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya tano ya Pasaka ya mwaka “C” wa Kanisa. Dominika hii ya tano ya Pasaka, masomo yetu ya leo yanatutaka kutafakari neno hili, “Amri mpya nawapa, Mpendane. Naye Mungu atafuta kila chozi katika macho yenu. Mlikutanishe Kanisa mara zote na kuwaeleza mambo yote aliyoyafanya Mungu pamoja nanyi.” Amri mpya kwa mfuasi wa Kristo na yeyote yule mwenye hofu ya  Mungu ni UPENDO. Na kama hofu ya Mungu ni kutambua kwa kina yale yote yakuzungukayo kwamba yapo kama yalivyo kwa sababu fulani, basi hakuna mwanadamu ye yote chini ya jua ambaye hata wajibika kwa amri hii mpya.

Msisitizo wa amri hii mpya-Upendo, Yesu anautoa katika saa yake ile ya mwisho, yaani muda ule na mazingira yale halisi ya kujongea kifo kile Kitukufu na kilichobeba simanzi kubwa la aibu kwetu sisi wanadamu kwa namna kilivyotendwa- kifo cha Msalaba. Lakini huu ndio upendo mkubwa wa Mungu kwetu sisi wanadamu ambao ndiyo sababu ya kifo chake kutokana na dhambi zetu. Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh 15:13. Na hili ndilo fumbo lililotanda mazingira na kifo cha yule mwenye haki-Yesu Kristo na mwokozi wetu. 

Hivyo ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, saa hii ambayo Bwana wetu Yesu Kristo anatoa agizo hili zito na muhimu la amri mpya, ni ukamilifu wa Yesu kama Mwana wa Mungu, aliyekuja kuufunua upendo wa Mungu, na upendo binafsi kwa watu wake. Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele,” Yoh 3:16. Ni kwa mtazamo huu, kifo cha Kristo kinawajengea uhusiano mpya wanafunzi wa Yesu, na Wewe na Mimi leo. Kifo hiki kinatupa uwepo wa wazi na ule wa kujificha-(fumbo) wa Mungu. Upendo huu ndiyo dira yetu na utambulisho wetu kama Wakristo na Wafuasi hai wa Kristo hadi mwisho wa nyakati. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi,” Yoh 13:35. Upendo huu kwa namna ya pekee, uwe dira ya maisha yako na utambulisho wako kila siku kadiri ya agano lako na Mungu (Mwenye hofu ya Mungu, Mlei, Mtawa, au Mtawa na Mkleri).

Upendo huu una gharama zake. Yesu kwa kutupenda upeo, kilele chake kilikuwa kifo cha Msalaba. Ndugu yangu, unaweza kutoa bila kupenda, ila hauwezi kupenda bila kutoa. Kwa kutupenda upeo, Yesu anayatoa maisha yake kwa ajili yako na yangu. Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo,” Yoh 13:33, 34. Gharama ya kwanza kufa kifo Upendo ni kuwa tayari kujinyenyekesha. Unyenyekevu ni msingi wa fadhila zote. Unyenyekevu si ujinga pale ufanyapo kitu hicho kukiwa na sababu za kufanya hivyo, na kama kadiri ya ufahamu wako kuna ukinzani kati ya tendo lile na sababu ya kufanya hivyo, tazama mafaa mapana ya kile kitarawajiwacho kwa wakati ule na ujao. Hali hii ilimkuta Yesu pale Bustanini Gestemani kama Mungu na Mwanadamu. “Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, akapiga magoti akaomba, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke,” Lk 22:41-42. Licha kuna uwezekana wa mtu kufa kwa ajili ya mwingine na katika hali ya upendo wa mashaka, ila pale tendo hilo linapoongozwa na unyenyekevu kama nilivyosema hapo awali, tendo hilo ubeba maana mpya hata kama kibinadamu kujongea au kukabiliana na jambo hilo huleta maumivu makubwa. Maumivu hayo ukoleza upendo uliopo ndani ya mtenda tendo, na mwisho maumivu hayo huwa furaha kwa sababu hutoa maana mpya ya teso katika tendo lile. Jambo hili pia linawatokea Mtume Petro na wenzake pale Gamalieli, mwalimu wa torati, mwenye kuheshimiwa na watu wote, Mdo 5:35, alipotoa ushauri kwenye baraza la Kiyahudi juu ya kukamatwa kwa Mitume isije wakawa wanapigana na Mungu. Wakakubali maneno yake; nao walipowaita mitume, wakawapiga, wakawaamuru wasinene kwa jina lake Yesu; kisha wakawaacha waende zao. Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo,” Mdo 5:40-41. Hivyo ndugu yangu, sababu ya teso huwa furaha na kikolezo cha kusonga mbele licha ya magumu katika njia hiyo. Kristo Yesu ndiye sababu ya mateso na kuaibishwa wa Mitume. Kama Kristo alikubali kufa kifo cha aibu na mateso pale Msalabani, mateso yangu na yako ni kitu gani katika kweli hii? Je, naweza kuyalinganisha na mateso yale aliyoyakabili Yesu kwa upendo mkubwa pale Msalabani? Ninapoutazama Msalaba Mtakatifu, iwe nafasi pia ya kutazama changamoto za mateso ninayokutana nayo kila siku.

Gharama ya pili ya kufa kifo Upendo ni kutii. Utii pia siyo ujinga ufanyapo utii huo kwa sababu, na mafaa mapana ya kile unachotii. Utii ni bora kuliko sadaka. Utii ni fadhili kubwa mbele ya Mungu. Utii ni kujua kwa upana kile ukifanyacho. Nabii Hosea anasema, Maana nataka fadhili wala si sadaka; na kumjua Mungu kuliko sadaka za kuteketezwa,” Hos 6:6. Kufa kifo Upendo kwa kutii ni gharama kubwa sana kwa sababu unapingana na kwenda kinyume kabisa na takwa la ufahamu wako-“will.” Hivyo ni vyema nifahamu tena kwa hofu kubwa kwamba ni kwa ajili yako na yangu kama tulivyo (katika udhaifu wetu), Kristo Yesu anakuwa mtii hadi kifo cha Msalaba ili wewe na mimi tuwe huru kutoka minyororo ya dhambi. Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba,” Flp 2:5, 8. Ndugu yangu, ni mara ngapi umeziacha neema na  baraka pale uliposhindwa kufa-kifo upendo kwa kutii? Kwa tendo hili la kufa-kifo upendo kwa kutii, Yesu anainuliwa na kutukuzwa na Baba yake wa Mbinguni kwa haya: Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba,” Flp 2:9-11

Wapendwa wana wa Mungu, kwa kujitoa nafsi yako kwa kuishi vyema na kwa uaminifu agano lako katika maisha u mtumwa wake Kristo, na kwa njia hiyo u mtumishi wa Kristo katika haki na kweli aliyoifia pale msalabani. Mtume Paulo anaamsha dhamiri zetu kwa kuhoji na kusema, Hamjui ya kuwa kwake yeye ambaye mnajitoa nafsi zenu kuwa watumwa wake katika kumtii, mmekuwa watumwa wake yule mnayemtii, kwamba ni utumishi wa dhambi uletao mauti, au kwamba ni utumishi wa utii uletao haki,” Rum 6:16. Kumbe kama mimi ni Baba katika familia yanipasa kila siku nijitahidi kupungua (kufa kifo-utii) ili mke na watoto wangu waongeze kiufahamu na kimaadili katika hofu ya Mungu. Vile vile kama mimi ni Mama katika familia yanipasa kupungua (kufa kifo-utii) ili mme wangu na watoto wangu waongezeke kiufahamu na kimaadili katika hofu ya Mungu. Na kama mimi ni mtoto katika familia yanipasa kupungua (kufa kifo-utii) ili familia yangu (mimi, ndugu zangu na wazazi wangu) waongezeke kiufahamu na kimaadili katika hofu ya Mungu. Na kama mimi ni (Mtawa, Mtawa na Mkleri, na Mkleri) yanipasa kupungua (kufa kifo-utii) ili jumuiya yangu, utume wangu, na wale wote niliopewa dhamana waongezeke kiufahamu, kimaadili, na kujawa hofu ya Mungu pale nilipo. Kupungua huku ni ile hali ya kujali na kuwajibika ipasavyo.

Kifo upendo katika utii hutupa nguvu kushinda majaribu hasa pale tunapoishi katika Kristo, ndani ya Kristo, na kwa ajili ya Kristo tukishirikishana wote na vyote kwa ukarimu yale tuliojaliwa na Mungu. Hivyo, kwa kuwa mkijaribiwa kwa utumishi huo, wanamtukuza Mungu kwa ajili ya utii wenu katika kuikiri Injili ya Kristo, na kwa ajili ya ukarimu wenu mliowashirikisha wao na watu wote,” 2Kor 9:13. Ukarimu huu ni kielelezo cha kufa kifo-Upendo katika ufukara. Ufukara ni ile hali ya kuwa na furaha kwa kuwa na machache katika maisha yako huku ukiwajali wengine. Baada ya Yohana Mbatizaji kutangaza ule ubatizo wa toba, makutano walimjia na kumuuliza katika hali ile waliyo kuwa nayo wafanye nini? Akawajibu akiwaambia, Mwenye kanzu mbili na ampe asiye na kanzu; na mwenye vyakula na afanye vivyo hivyo,” Lk 3:11. Ufukara huu unalenga kujinyima kwa ajili ya wengine, na kuwa na furaha kwa tendo hilo. Hili ndilo agizo pia ya Yesu kwa wanafunzi wake (Thenashara) anapowatumwa kutangaza ufalme wa Mungu, na kupoza wangonjwa. Akawaambia, Msichukue kitu kwa safari yenu, fimbo, wala mkoba, wala mkate, wala fedha, wala mmoja wenu asiwe na kanzu mbili,” Lk 9:3. Ndugu yangu, kadiri ya uchache wa vitu unavyokuwa navyo ndivyo kwa namna hiyo unakuwa na muda wa kutosha wa utulivu wa ndani. Bila kuwa na utulivu wa ndani mambo mengi katika maisha yako hayawezi kwenda sawa, hasa katika swala la kufanya maamuzi ya kina katika maisha-“fundamental decisions in your life.”

Mwono huu wa maisha katika maana nzima ya upendo na kufa kifo upendo (unyenyekevu, utii, na ufukara), ulikuwa msingi imara wa jumuiya ya kwanza ya Wakristo. Mateso waliyoyapata yakiambatana na dhuluma ha hujuma kwa kuteswa na hata kuuwa kwa wafuasi wa kwanza wa Kristo, tendo hilo lilikuwa na kubeba tafsiri halisi ya ‘mlango wa kuingia katika Ufalme wa Mungu.’ Mtume Paulo anawapa moyo jumuiya ya Filipi kutokana na nguvu ya  kusimama  imara katika roho moja, kwa moyo mmoja wakishindania imani ya Injili, na kusema, wala hamwaogopi adui zenu, katika neno lo lote; kwao hao ni ishara mathubuti ya kupotea, bali kwenu ninyi ni ishara ya wokovu, huo utokao kwa Mungu. Maana mmepewa kwa ajili ya Kristo, si kumwamini tu, ila na kuteswa kwa ajili yake; mkiwa na mashindano yale yale mliyoyaona kwangu, na kusikia kwamba ninayo hata sasa,” Flp 1:28-30. Kwa vyovyote vile jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo ilikuwa na mshikamano wa kweli.

Umoja na mshikamano wao (katika kweli, haki, na upendo) ndiyo pona yao. Na umoja na mshikamano wetu leo Kanisa katika kweli, haki na upendo ndiyo pona yetu. Dhambi ya usaliti waliepukana nayo kwa maneno na matendo. Kama tukistahimili, tutamiliki pamoja naye; Kama tukimkana yeye, yeye naye atatukana sisi,” 2Tim 2:12. Jumuiya hii kwa kuishi mshikamano na umoja huu, waliutazama umilele na faida zake kuliko haya ya leo na kesho. Maana mnahitaji saburi, ili kwamba mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu mpate ile ahadi,” Ebr 10:36. Saburi na utulivu wa jumuiya kwa kiasi kikubwa ulitegema uongozi ule uliowekwa na Kanisa-jumuiya mahalia na kusimikwa na Mitume, ambao uongozi huu haukutegemea maslahi binafsi bali hitaji la jumuiya husika. Viongozi hawa walikuwa wazee walioaminika na wenye hofu ya Mungu. Wote waliochaguliwa waliwakabidhi kwa nguvu ya Roho Mtakatifu kwa kuwawekea mikono Na walipokwisha kuwachagulia wazee katika kila Kanisa, na kuomba pamoja na kufunga, wakawaweka katika mikono ya Bwana waliyemwamini,” Mdo 14:23. Hata safari ya kwanza ya kimisionari kwa watu wa mataifa ilikuwa ni msukumo ya Roho Mtakatifu. Roho Mtakatifu aliwaongoza katika kila jambo. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia,” Mdo 13:2.

Mafanikio makubwa ya Jumuiya hii ya kwanza yalichochewa na maisha yao ya uwazi. Kila jambo lilisemwa katika uwazi wake, na kwa namna hiyo walitoa shukrani zao kwa Mungu kwa yote aliyowatendea. ‘Moyo usio na shukrani ukausha mema yote.’ Ni kwa namna hii ya uwazi, Hata walipofika wakalikutanisha Kanisa, wakawaeleza mambo yote aliyoyafanya Mungu pamoja nao, na ya kwamba amewafungulia Mataifa mlango wa imani,” Mdo 14:27. Jumuiya yoyote ile inayoishi kwa kujitolea kwa watu wake hasa mambo ya maendeleo yahitaji uwazi. Kadiri uwazi unavyojidhihirisha kwa watu, ndiyo kwa namna hiyo hiyo watu hujitolea kwa nguvu na mali zao kwa hitaji la Kanisa mahalia. Hivyo, tunahitaji uwazi katika matumizi na matapato katika jumuiya zetu ndogo ndogo za Kikristo, Vigango vyetu, na Parokia. Tuliopewa dhamana na kuhesabiwa haki na Mama Kanisa kwa usimamizi wa mali hizo za Kanisa mahalia, yatupasa kuwa waaminifu kwa kutoa taarifa sahihi kwa yale tuyapatayo na namna tulivyoyatumia kwa wakati ufaao. La sivyo mbele huko ni giza tupu. Tuelewe kwamba tu wakili na wazimamizi wa mambo yote yale yampendezayo Mungu.

Namna hii ya utendaji ndiyo njia sahihi ndani na katika Kristo, na kupata ushindi dhidi ya uovu na maovu. Hii ndiyo Yerusalemu Mpya. Maana, tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni,” Isa 65:17. Kutenda kwetu kunakosababisha ulimwenguni hapa kuwe sahemu salama ya kuishi ndiyo baraka na neema tuzipataza. Tendo hilo pia huufunua Uzuri na Utukufu wa Mungu. Kama vile mbingu mpya na nchi mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema Bwana, ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa,” Isa 66:22. Mungu kamwe hawezi kutuacha tukaangamia katika janga lolote lile tunaposimama katika kweli, haki na upendo. Mungu hatoacha kuyafuta machozi yetu tuyafanyapo yote kwa ajili yake na Utukufu wake. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita,” Ufu 21:4. Mungu ni ngome imara kwa wale wote wanaomlilia na kumwelekea. Na katika shida na mateso hayo kwa sababu ya kweli, haki na upendo, hatutakosa faraja kutoka kwake. Na yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya,” Ufu 21:5. Ndugu yangu, tukiwa tumefika mwisho wa safari ya tafakari, bila shaka umegundua ni kitu fulani si sawa sawa katika maisha yako. Linalowezekana kufanyika leo lifanye na wala lisingoje kesho.

Wapendwa katika Kristo, Frank Kisoli alijulikana sana kwa fani yake ya ufundi viatu, na zaidi kurekebisa soli za viatu. Umaarufu huu ndio ulimpa jina lake la pili yaani, “Kisoli.” Frank Kisoli alifahamika na kila mtu na marika tofauti kwa huduma hii ya kurekebisa viatu. Alikuwa na uwezo mkubwa sana wa kukaa muda mrefu kwenye huduma hiyo ya kushona viatu, na hasa kurekebisha soli.

Pamoja na huduma hiyo, alikuwa mcheshi sana na alipokeleka na wote. Mara mteja ajiapo viatu vyake humuuliza swali hili, “wavitambua tena viatu vyako na visigino vyake? Huyu ndiye Frank Kisoli mrekebishaji. Karibu sana.” Basi kwa maneno haya ilikuwa furaha sana kwa wateja wake. Hivyo kila wakati huwezi kumkosa mtu kwenye kibaraza kile cha nyumba yake. Kutokana na kazi hii, aliweza kujipatia mahitaji yake ya kila siku, na kuwasomesha vizuri watoto wake.

Lakini jambo la ajabu ni hili, licha ya mafanikio mengi aliyoyapata kuwa na nyumba nzuri, kuvaa vizuri yeye na familia yake, watoto wake kusoma na kuwa na maisha mazuri, Frank Kisoli hakuacha kazi yake ile. Siku moja mteja na rafiki yake alimuuliza, “hivi kwa nini pamoja na maendeleo vyote uliyokuwa nayo kwa nini usiache kazi hii na kufanya kazi nyingine zenye hadhi, au basi ufungue kiwanda kikubwa?” Frank Kisoli alimjibu hivi, “kwa vile watu wanaendelea kuvaa viatu na siyo wote wenye uwezo wa kununua viatu vipya kila mara, naona sitawatendea haki watu hao kama nikiacha kazi hii. Najisikia furaha kuifanya licha ya changamoto zake kwa mfano vipo viatu vingine huwa vinanuka sana,” wote (Frank Kisoli na rafiki yake) waliangua kicheke! “Basi na iwe hivyo,” rafiki yake alimjibu.

Ndugu yangu, yapo mengi ya kutafakari na kujifunza kutoka kwa Frank Kisoli. Ila haya ni dhahiri:

-Hakuna kazi yenye heshima au isiyo na heshima. Jambo la msingi ni utayari wa hutuma ile uitowayo, na furaha ile uipatayo kwa kile ukifanyacho. Je unawafikia wahitaji wako kila mmoja na uzito wa shida yake ile katika huduma uitowayo? Kwa hili Frank Kisoli alifanikiwa sana.

-Kwa vile tunaishi na tunatembea hapa na pale, na kukutana na hili na lile ndiyo kwa namna hiyo tunadondoka hapa na pale. Hali hii ni sawa na soli ya kiatu. Tunamwitaji Frank Kisoli, yaani Sakramenti ya utapanisho. Hapa tunapatanishwa tena na Kristo na kuwa wapya. Kumbuka swali la Frank Kisoli kwa mteja ajiaye viatu vyake, na jibu alilolitoa kwa rafiki yake yule aliyemshauri kuacha kazi yake ya ushonaji na viatu.

-Mama Kanisa kama alivyo Frank Kisoli, ataendelea kufanya kazi yake kama Sakramenti ya Wokovu kwa watu wote katika kweli, haki, na upendo akitambua kuwa familia yake ni familia ya wakosefu (wadhambi) na watakatifu. Kazi hii ya wokovu watu Mama Kanisa ataifanya hadi mwisho wa nyakati.

Tumsifu Yesu Kristo!

 “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi,” Yoh 13:35


Tusali:-Ee Yesu Mwema, bila wewe hatuwezi kufanya lolote. Tujalie nguvu ya kuyafanya yote ya kupendezayo na tukuone kwa wote tunao wahudumia kila mmoja wetu kadiri ya wito na nafasi yake. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario