JUMAPILI
YA 2 YA PASAKA YA MWAKA-C
Somo I: Mdo 5:12-16
Zab: 118:2-4, 13-15, 22-23
Somo II: Ufu 1:9-11a,
12-13, 17-19
Injili:
Yoh 20:19-31
Nukuu:
“Na
kwa mikono ya mitume zikafanyika ishara na maajabu mengi katika watu,” Mdo
5:12a
“hata
ikawa katika njia kuu hutoa nje wagonjwa, na kuwaweka juu ya majamvi na
magodoro, ili Petro akija, ngawa kivuli chake kimwangukie mmojawapo wao,” Mdo
5:15
“Nayo
makutano ya watu wa miji iliyoko kandokando ya Yerusalemu wakakutanika,
wakileta wagonjwa, nao walioudhiwa na pepo wachafu; nao wote wakaponywa,” Mdo
5:16
“Mimi
Yohana, ndugu yenu na mwenye kushiriki pamoja nanyi katika mateso na ufalme na
subira ya Yesu Kristo, nalikuwa katika kisiwa kiitwacho Patmo, kwa ajili ya
Neno la Mungu, na ushuhuda wa Yesu,” Ufu 1:9
Akaweka mkono wake wa
kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, na
aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele.
Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu,” Ufu 1:17b-18
“Akaja Yesu, akasimama katikati, akawaambia,
Amani iwe kwenu,” Yoh 20:19b
“akawaonyesha
mikono yake na ubavu wake. Basi wale wanafunzi wakafurahi walipomwona Bwana,” Yoh
20:20
“Akawavuvia, akawaambia, Pokeeni Roho
Mtakatifu. Wowote mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote
mtakaowafungia dhambi, wamefungiwa,” Yoh 20:22-23
“Mimi nisipoziona mikononi mwake kovu za
misumari, na kutia kidole changu katika mahali pa misumari, na kutia mkono
wangu katika ubavu wake, mimi sisadiki hata kidogo,” Yoh 20:25
“Lete hapa kidole chako; uitazame mikono
yangu; ulete na mkono wako uutie ubavuni mwangu, wala usiwe asiyeamini, bali
aaminiye,” Yoh 20:27
“Tomaso akajibu, akamwambia, Bwana wangu
na Mungu wangu!” Yoh 20:28
“Wewe, kwa kuwa umeniona, umesadiki; wa heri wale wasioona, wakasadiki,”
Yoh 20:29
“Lakini hizi zimeandikwa ili mpate kuamini
ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu; na kwa kuamini mwe na uzima kwa
jina lake,” Yoh 20:31
TAFAKARI: “Upendo wa kweli ndiyo msingi wa Ukristo wetu, ujidhihirisha
tunapoishi ndani na katika Kristo na kuwa Mashahidi wake; na ndiyo njia pekee ya
kuurithi Ufalme wa Mungu kila mmoja kadiri ya wito wake.”
Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha
Jumapili ya Pili ya Pasaka ya mwaka “C” wa Kanisa. Mama Kanisa leo anapenda
kutuongoza kwenye tafakari ya neno hili, “Upendo wa kweli ndiyo msingi wa
Ukristo wetu, ujidhihirisha tunapoishi ndani na katika Kristo na kuwa mashahidi
wake; na ndiyo njia pekee ya kuurithi Ufalme wa Mungu kila mmoja kadiri ya wito
wake.” Mafanikio na maendeleo makubwa ya Imani katika jumuiya ya kwanza ya
Wakristo yalijengeka katika msingi wa UPENDO KWA KWELI, WALIPOISHI NDANI NA
KATIKA KRISTO. Tendo hili la upendo, Kristo akiwa kielelezo cha yote,
uliwafanya wanajumuiya hawa wa kwanza kujitoa bila kujibakiza. “Na jamii ya watu walioamini walikuwa na moyo mmoja
na roho moja; wala hapana mmoja aliyesema ya kuwa kitu cho chote alicho nacho
ni mali yake mwenyewe; bali walikuwa na vitu vyote shirika,” Mdo 4:32
Ndugu yangu, hutoweza kuwa shahidi
wa Kristo na neno lake kama haupo tayari kushirikisha wengine kweli ya Kristo
iliyopo ndani yako. Kuishirikisha kweli ya Kristo ndani yako kwa wengine ni
tokeo la kulitafakari neno la uzima kwa kina kila siku ya maisha yako. Hutoweza
kusimama katika neno la Mungu kama hujalielewa na kuwa sehemu ya maisha yako.
Kama neno hili ni uzima basi yanipasa kulisoma kila siku na kulitafakari ili
liwe uzima ndani yangu. Ni vigumu pia kulitafakari neno la Mungu na kuwa sehemu
ya uzima wako kama huwezi kulisikia.
Kulisikia neno la Mungu siyo tu kwa
kupitia masikio yetu kama njia moja ya mlango wa fahamu, bali kulisikia kwa
kila kiumbe alichokiumba Mungu, na zaidi kutoka mazingira yale unayoyaishi leo
na sasa. “Ndipo akawafunulia akili zao wapate kuelewa na
maandiko. Akawaambia, Ndivyo
ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa
yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza
tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya,” Lk 24:45-48. Neno “kuanza tangu
Yerusalemu,” linaweza kutafsiriwa kuwa ni mazingira uliyopo na namna ile ulivyo
kila mmoja kadiri ya wito wake. Kuwa shahidi wa neno
hili la uzima yanipasa kuanzia pale nilipo. Neno hili lilete uzima ndani ya
ndoa yako, maisha yako ya wakfu, na katika huduma unayoitoa watu. Hali hii
ndiyo inayomkuta Mtume Petre; “hata ikawa
katika njia kuu hutoa nje wagonjwa, na kuwaweka juu ya majamvi na magodoro, ili
Petro akija, ngawa kivuli chake kimwangukie mmojawapo wao,” Mdo 5:15
Ni vigumu vile vile
kusikia neno hili la uzima kama haupo tayari kulipokea. Kulipokea Neno la Uzima
kamwe lisiwe Neno kihistoria, yaani simulizi fulani kwangu na lenye kunipa
taarifa ya mambo yaliyopita, bali Neno hilo lanihusu mimi leo na sasa na siyo
mtu mwingine. Huku ndiko kulipokea Neno la Uzima kutakapo kupelekea kulisikia,
kulitafakari, kulishirikisha, na mwisho kuwa shahidi na kufa shahidi. “Mimi
Yohana, ndugu yenu na mwenye kushiriki pamoja nanyi katika mateso na ufalme na
subira ya Yesu Kristo, nalikuwa katika kisiwa kiitwacho Patmo, kwa ajili ya
Neno la Mungu, na ushuhuda wa Yesu,” Ufu 1:9. Na huu ndio ushuhuda wa Neno
lililo hai. Ushuhuda huu wa Neno la Uzima ndio tunaoambiwa kwamba, “Na kwa mikono ya mitume zikafanyika ishara na
maajabu mengi katika watu,” Mdo 5:12a.
Wapendwa
katika Kristo, ushuhuda wa Neno la Uzima ulipelekea kujali na kutaabikiana kwa
upendo wa kweli kwa jumuiya ya kwanza ya Wakristo, na kuliweza kutatua matatizo
mengi makubwa. Hakuna miongoni mwao aliyeitaji akakosa mahitaji yake. Mt.
Augustino ambaye alichukua kielelezo hiki cha maisha ya jumuiya ya kwanza ya
Wakristo, na kufanya ndicho msingi wa jumuiya ya Kiagustino, anasema “UKIPENDA
UTAFANYA YOTE.” Ni kwa msingi huu na upendo huu wa kweli, “wala hapakuwa na mtu
mmoja miongoni mwao mwenye mahitaji; kwa sababu watu wote waliokuwa na viwanja
au nyumba waliviuza, wakaileta thamani ya vitu vile vilivyouzwa,” Mdo 4:34. Jambo la kushangaza leo katika familia
zetu, licha ya wanafamilia, yaani Baba na Mama kuunganishwa kwa Sakramenti ya
ndoa, wamekuwa wabinafsi kiasi kwamba kila mmoja wao hujifanyia mambo yake bila
kumshirikisha mwenzake.
Tatizo kubwa hapa
lipo kwa akina Baba. Utaona kila mmoja wao anasema hiki ni changu. Wakati
mwingine Baba huwa na viwanja na hata biashara kubwa ambazo mkewe hajui lolote.
Mwisho wa siku kinapotokea kifo kwa upande wa Baba, mali yote hupotea na
familia kubaki umasikini uliokithiri. Hivi nyie akina Baba, inawezekanaje
kumwamini rafiki wako wa kufikia, kuliko kumwamini mkeo na wanafamilia yako?
Marafiki hawa wa kufikia ndio wanaojua mikataba yote ya mali na biashara za
Baba huyu wa familia. Tujirekebishe! Mkeo ni zaidi ya ndugu na marafiki. Huyu
umeunganishwa naye na kuwa kitu kimoja. Unapoanza kumtenga unajipasua mwenyewe
na mwisho wake hutobaki salama.
Ndugu zangu,
tusipouishi kweli hii hasa katika ngazi ya familia, hakika bado hatujamjua
Kristo. Katika kitabu cha ufunuo
tunaona namna Yesu anavyojifunua kwa Mtume Yohane kwa njia ya maona na kusema,
“Mimi
ni wa kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na
tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za
kuzimu,” Ufu 1:17b-18. Mimi na wewe tusipo ijua kweli hii tu bado katika
giza, na tunaishi maisha ya kuigiza kwa miaka yote, kila mmoja kadiri ya wito wake. “Kila mtu aaminiye
kwamba Yesu ni Kristo amezaliwa na Mungu. Na kila mtu ampendaye mwenye kuzaa,
ampenda hata yeye aliyezaliwa na yeye,” 1Yoh 5:1. Upendo wa kweli ndiyo amri
kuu kwa kila aliyebatizwa na kumwamini Kristo. Kwa yeyote anayejiita Mkristo na
anayejitambua kuwa ni Mkristo, hakuna mbadala dhidi ya kupenda kuliko kwa
kweli. “Kwa
maana huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si
nzito,” 1Yoh 5:3. Ukipenda kweli, utafanya yote kama asemavyo Mt. Augustino.
Wepesi wa amri yeyote ni upendo katika agizo hilo na kwa kutimiza matakwa ya
hiyo amri. Jumuiya ya kwanza ya Wakristo inaishi pendo la kweli na kuwa kivutio
cha kweli katika huduma na huruma ya Mungu. Na ndivyo ilivyokuwa kwamba, “Nayo makutano ya watu wa miji iliyoko kandokando
ya Yerusalemu wakakutanika, wakileta wagonjwa, nao walioudhiwa na pepo wachafu;
nao wote wakaponywa,” Mdo 5:16
Kupenda
kuliko kweli ndiko kuzaliwa na Mungu, na kuushinda ulimwengu dhidi ya uovu.
Silaha kubwa ya kuushinda ulimwengu huu dhidi ya uovu, ni kupenda kuliko kwa
kweli. Wengi wetu ujikuta kufanya maovu kwa vile tu hawakuwahi kupendwa na mara
zote hujisikia kusalitiwa na kuhuzunishwa. “Kwa maana kila kitu kilichozaliwa
na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu,
hiyo imani yetu,” 1Yoh 5:4. Huu ndiyo msingi wa kila Mkristo mwenye Imani ya
kweli. Jambo hili la kutokupenda
kutokana na majeraha na kuumizwa kwetu, linaonekana wazi katika Injili ya leo
ambapo tunaona watu wawili (Yesu Kristo Mfufuka na Mtume Tomaso) waliojeruhiwa,
ambao mwisho wa siku mmoja wao (Yesu Kristo Mfufuka) anamponya mjeruhiwa
mwenzake (Tomaso).
Uponyaji
wa kwanza anaoutoa Yesu Kristo kwa wanafunzi wake ni kuiondoa hofu kwa salamu
yake ya upendo, “Akaja Yesu, akasimama katikati, akawaambia, Amani iwe kwenu,”
Yoh 20:19b. Tendo hili la kuwa na Amani ya kweli ndiyo mwanzo wa kuanza kupenda
kuliko kwa kweli na furaha ya kweli. Wanafunzi wa Yesu wanaonyesha furaha hii,
na kuanza kupenda tena, ingawa Mtume Tomaso hawakuwepo katika kundi. Naye Yesu
baada ya salamu ya upendo iliyojaa matumaini mapya, “akawaonyesha mikono yake
na ubavu wake. Basi wale wanafunzi wakafurahi walipomwona Bwana,” Yoh 20:20.
Furaha hii inaendana na maagizo ya kufanya anayoyatoa Kristo kwa wanafunzi
wake. Naye Kristo akawavuvia, akawaambia, “Pokeeni Roho Mtakatifu. Wowote
mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote mtakaowafungia dhambi,
wamefungiwa,” Yoh 20:22-23. Kristo hapendi furaha ya kweli aliyotupatia tubaki
nayo wenyewe. Hivyo furaha hii twapasa kuisambaza kwa wengine kila mmoja kadiri
ya wito wake, vipaji vyake, dhamana na nafasi yake katika jamii anayoishi.
Ndugu yangu ukiona hapo unapoishi hata mbwa wanakukimbia bila sababu, ujue wewe
ni shiiiiida!
Tomaso aliporejea anakokujua mwenyewe kwa
kupoteza imani yake juu ya Kristo, anapoambiwa jambo hili la kuonekana kwa
Kristo, hakuamini hata kidogo. Naye kwa ufahamu wake anatoa vigezo vya kutambua
ukweli aliousikia kutoka kwa wenzake. Naye anatoa vigezo na masharti ambavyo
lazima vizingatiwe. “Mimi nisipoziona mikononi mwake kovu za misumari, na kutia
kidole changu katika mahali pa misumari, na kutia mkono wangu katika ubavu
wake, mimi sisadiki hata kidogo,” Yoh 20:25. Kwa masharti haya na vigezo hivi
tunaweza kuona ni kwa jinsi gani Tomaso alivyo jeruhiwa na kusononeshwa kwa
tukio la kifo cha Bwana wetu Yesu Kristo.
Wapendwa,
baada ya siku nane, tunaona tukio la kukutana kwa wajeruhiwa hawa wawili, yaani
Yesu Kristo Mfufuka na Mtume Tomaso. Mjeruhiwa wa kwanza ni Yesu Kristo. Yesu
anamkuta Tomaso na kumwonyesha majeraha yake, na kusema, “Lete hapa kidole
chako; uitazame mikono yangu; ulete na mkono wako uutie ubavuni mwangu, wala
usiwe asiyeamini, bali aaminiye,” Yoh 20:27. Tendo hili la Yesu kumwonyesha
Tomaso majeraha yake na kuumizwa kwake kunatoa picha ya majivuno ya Yesu na
wakati mwingine kama kujigamba vile. Jambo hili lina ukweli wake kwa mtazamo
huu wa majeraha na makovu aliyokuwa nayo Yesu. Majereha ya Kristo na maumivu
yake hayakuwa majeraha ya kushindwa, bali majeraha ya UPENDO WA KWELI. Majeraha
ya Kristo yalikuwa majeraha ya USHINDI uliotukuka. Hayakuwa majeraha ya kuuma,
bali majeraha ya UTUKUFU. Ni majeraha ya UPENDO. Upendo ambao upo tayari
kujitoa sadaka bila kipimo na kutojibakiza. Kristo anaonyesha ubavu wake na
mikono yake ilivyotobolewa si kwa kujionyesha au kuhukumu, bali kuonyesha uzito
na undani wa upendo wake kwa Mitume na kwetu sote.
Japokuwa
Tomaso hakuwa na majereha kwenye ngozi yake, na hakuwa na kuvuja damu kutoka
mwilini mwake, majeraha yake yalikuwa ndani ya moyo wake. Haya ni maumivu ya
ndani. Moyo wake ulijeruhiwa kwa kusikishwa na kifo cha Bwana wake. Alijisikia
kudanganywa na Bwana wake Yesu Kristo. Alijisikia kushindwa baada ya kuyaweka
matumaini yote kwa Kristo kwa sababu alifikiri Yesu Kristo ni Masiha, Mfalme,
na kuhoji kwa nini Yesu afe kifo katili kama kila cha msalaba. Alifikiri Yesu
Kristo angeikomboa Israeli kutoka kwenye dola ya Kirumi. Anajiuliza hivi, kwa
nini hata yeye mwenye-Yesu ameshindwa kujinasua kutoka watesi wake? Mtume
Tomaso alisikitishwa na kusijikia kusalitiwa na Yesu. Tomaso alishawishika
kabisa kwamba alifanya uchaguzi usio sahihi kumfuata mseremala huyu wa
Galilaya. Kwa kweli Tomaso alikuwa na maumivu makubwa sana.
Wapendwa
maumivu na majeraha ya Moyo huchukua muda mrefu kupona. Majeraha haya na
maumivu ya Moyo yanachukua kuda mrefu kupona kwa sababu twaweza kuyaficha na
kujifanya hayapo. Twaweza kuongea na kutenda mambo yetu kama vile hakuna jambo
lolote baya au upungufu wowote kwetu. Wengi wetu twaweza kukaa katika hali hii
kwa miaka mingi kwa kujivisha taswira nyingine na mwonekano mwingine ambao sio
uhalisia wa kile kilicho ndani mwetu ingawa tunaendelea na mateso na maumivu
hayo. Lakini ukweli ni kwamba hatuwezi kudumu katika hali hii kwa muda wote na
nyakati zote. Mara tutaanza kujisikia vibaya na kujisikitikia na kufikiri
marafiki zetu wametutenga na wapo mbali bila kutusikiliza maumivu yetu
yanayotusonga moyoni. Mara tunajisikia kwamba hawajali na wanaubaridi kuhusu
maumivu yetu, na hivyo kuwachukia pia.
Hivyo,
katika kukutana kwa wawili hawa hasa kipindi hiki cha pasaka, mmoja wao yaani
Yesu Kristo ana majeraha ya UTUKUFU, na mwingine yaani Tomaso ana majereha ya
maumivu ya ndani. Yesu Kristo alikuwa tayari kujiponya kwa nguvu ya majeraha
yake. Tomaso alihitaji kuponywa majeraha yake lakini hapakuwa na mtu wa
kumponya. Hapa ndipo wanapokutana wajeruhiwa hawa wawili. Mjeruhiwa wa kwanza
anamponya wa pili. Uponyaji huu unajionyesha kwa maneno ya Tomaso mwenyewe
anapomjibu Kristo baada ya Kristo kumtaka kuvitia vidole vyake kwenye makovu na
majeraha yake, akisema, “Bwana wangu na Mungu wangu!” Yoh 20:28. Mwisho wa kukutana huku, kila mmoja
anapata majeraha ya UTUKUFU, na kuwa tayari kuponya wengine wenye maumivu.
Wapo maelfu ya watu
wameumizwa na kujeruhiwa miongoni mwetu. Wengine wanabeba chuki kwa usiri
mkubwa ndani ya mioyo yao kwa kusalitiwa
kulikotokana na kutokuwa na uaminifu kwa wenzi wake wa ndoa. Wengine
wanabeba chuki dhidi ya wanaofisi wenzao kwa kuwaenezea umbea na uongo mitaani.
Wengine pia wanabeba ndani ya mioyo yao chuki na manung’unika kwa milongo ya
miaka iliyopita kwa kukosa sehemu ya kuponyeshwa na kusikilizwa. Wengine
maumivu haya wanayabeba tangu kuzaliwa kwao hadi sasa kutokana na namna ya
kutungwa mimba kwao kuliko kataliwa na kwa bahati mbaya au nzuri akazaliwa.
Wengine wamesalitiwa na wapenzi wao na kuyabeba hayo hadi sasa hata kama
wanaishi maisha yao ya ndoa. Wapo wengi sana waliojeruhiwa na kuumizwa vibaya
kwa namna tofauti tofauti. Jambo hili linaweza kutokea kwa yeyote yule, iwe
mlei, mtawa na hata mtawa na mkleri.
Ndugu yangu, hata kama
tutayaficha majereha na maumivu yetu, kwa binadamu itafika wakati lazima
atayaonyesha tu wazi kwa kutafuta uponyaji. Ni njia mojawapo ya kurudisha
mizania ya ndani katika uumbaji wetu. Ukweli ni kwamba walioumizwa kweli na
kupata majeraha ya ndani hawawezi kuficha na kuvaa kinyago hicho kwa muda
mrefu. Wanaweza kuwadanganya wanaowazunguka kwa wakati tu, ila hawawezi
kujidanganya wenyewe na kuficha ukweli huu. Maumivu ya ndani ni vigumu sana
kuyavumilia.
Watu hawa wanaitaji
uponyaji. Wangepewa nafasi na uchaguzi, wote wangependa kugusa majeraha ya Kristo.
Wanapenda kujua kwa uhakika kama kuna mtu anayewapenda vya kutosha kwa
kujeruhiwa kwao na mtu huyo yupo tayari kufa kwa kuwapenda. Tatizo kubwa ni
kwamba hawawezi kumwona tena Kristo. Wanaweza tu kuwaona watu wanaojiita
Wakristo. Wakristo ambao wanajulikana kwa kujinadi kulibeba jina la Kristo na
siyo kumuishi Kristo. Swali ni hili: Je wakristo hawa wapo kweli kama Kristo?
Je, wakristo leo wameumizwa vya kutosha kwa UPENDO kiasi kwamba wanaweza
kuwaponya walioumizwa? Je, ni kweli wakristo leo wamefufuka kutoka kifo cha
kujijali wenyewe, na ubinafsi, kwamba wanaweza kuwa matumaini na kielelezo cha
kuwarudisha waliopotea kwenye kundi kwa kuumizwa kwao?
Ndugu yangu, kuurithi
ufalme wa Mungu, ni kuishi vyema wito wako na vipaji alivyo kupa Mungu. Vipaji hivyo
siyo mali yako bali viwafaidie wengine, na hasa katika kuyaponyesha majeraha na
maumivu waliyokuwa nayo. Hiki ndicho kielelezo cha maisha yetu kama Wakriso na
wafuasi wa Kristo Mfufuka. Jambo hili si katika kuangamizana, bali katika
ufaidiana na kuongozana katika umilele ambao ndiyo makusudi ya Ufalme wa Mungu.
Wapendwa ulimwengu wa leo
unamwitaji sana Kristo. Kama ulimwengu usipomwona Kristo kwa Wakristo wa leo,
waliojerehiwa watajitoa kwa Mungu, na kubeba mioyo yao inayovuja damu na
vidondo visivyoponyeka kwingine kusipo Mungu. Na wanavyojitoa huku ufikia
mahali na kuinamisha vichwa vyao na kufikiri katika akili zao: “Mungu amekufa!”
Ndugu wana wa Mungu, baada
ya miaka mingi ya kufanya biashara bila mafanikio, Mungu alitaka kumwezesha
mfanyabiasha mmoja alijulikana kwa jina la Songambele.
Alimwendea katika ndoto na
kumwambia, “omba jambo lolote nalo nitakupatia. Na utakachokiomba nitampa
mfanyabiashara wa jirani yako aliyeko upande wako wa kulia mara mbili zaidi.
Kwa mfano, ukiomba uwe na mtaji wa milioni 20, nitakupa na mwenzako nitampa
mara mbili yako yaani milioni 40.”
Mungu alimpa wiki moja
Bwana Songambele kufikiria na kisha kumpatia jibu. Baada ya wiki moja, Mungu
alimjia tena na kumwuliza, “je tayari umeshapata jibu? Songambeli alimjibu
hivi, “baada ya kufikiria kwa undani na umakini mkubwa mimi naomba niwe
chongo.”
Je, kama Songambele
ameomba awe chongo yaani jicho moja tu lake liwe na uwezo wa kuona, mwenzake
atakuwa nani?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Tomaso akajibu, akamwambia, Bwana wangu na Mungu wangu!” Yoh 20:28
Ee Yesu Mwema, tuponye majeraha na maumivu yetu ya ndani kwani
ni wewe tu unayejua ukweli wake kwa majereha na maumivu yako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario