IJUMAA
WIKI YA 2 YA PASAKA
Somo:
Mdo 5:34-42
Zab:
27:, 4, 13-14
Injili:
Yoh 6:1-15
Nukuu:
“Lakini
mtu mmoja, Farisayo, jina lake Gamalieli, mwalimu wa torati, mwenye kuheshimiwa
na watu wote, akasimama katika baraza, akawaambia, Enyi waume wa Israeli,
jihadharini jinsi mtakavyowatenda watu hawa,” Mdo 5:34a-35.
“Basi
sasa nawaambia, Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi
hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjwa, lakini
ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na
Mungu,” Mdo 5:38-39
“Nao walipowaita mitume, wakawapiga,
wakawaamuru wasinene kwa jina lake Yesu; kisha wakawaacha waende zao,” Mdo
5:40b
“Nao
wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili
kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo,” Mdo 5:41
“Na
kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri
habari njema za Yesu kwamba ni Kristo,” Mdo 5:42
“Na
mkutano mkuu wakamfuata, kwa sababu waliziona ishara alizowafanyia wagonjwa,”
Yoh 6:2
“Yesu
akasema, Waketisheni watu. Basi watu waume wakaketi, wapata elfu tano jumla
yao,” Yoh 6: 10a-10c
“Basi
Yesu akaitwaa ile mikate, akashukuru, akawagawia walioketi; na kadhalika katika
wale samaki kwa kadiri walivyotaka,” Yoh 6:11
“Kusanyeni vipande vilivyobaki,
kisipotee cho chote,” Yoh 6:12b
“Hakika huyu ni nabii yule ajaye
ulimwenguni,” Yoh 6:14b
“Akajitenga, akaenda tena mlimani yeye
peke yake,” Yoh 6:15b
TAFAKARI:
“Nguvu ya Maadili na Unyenyekevu hutuhesabia haki na kweli kama wafuasi wa
Kristo. Mwono huu wa maisha utuweka karibu na Kristo nyakati zote.”
Wapendwa
wana Mungu, kwa pamoja tutafakari masomo ya leo na hasa nini maana ya nguvu ya
kimaadili na unyenyekevu kwa kile tunachoishi kama wafuasi wa Kristo. Matokeo
ya ukweli huu ndiyo ushuhuda wa kweli kwa jamii inayotuzunguka. Hapana shaka
yoyote kwamba, jumuiya ya kwanza ya Wakristo walipata nguvu ya kulinena jina la
Kristo, na hivyo kugeuka kuwa mwiba mkali kwa watesi wao, kutokana na nguvu yao
kimaadili na unyenyekevu waliokuwa nao.
Mamlaka haya ya
kimaadili hujijenga kwanza kabisa kwa KUJITAMBUA. Kujitambua huku ni pamoja na
kujua nini shabaha ya kile unachokiishi, na malengo yake. Kwa upande mwingine
ni kujua malengo ya maisha yako. Maisha ya aina yoyote ile huongozwa na
malengo. Maisha yanapokuwa na malengo, maisha hayo huwa na mwono tofauti
kabisa, kwani rasilimali muda hutumika vizuri. Maisha yasipoongozwa na malengo
ni sawa na wingi wa miaka usio na maana.
Haina maana yoyote
kujitapa kwa kuwa na miaka 50 au 90-(yaani kuishi kwa ‘bonus’), bila kutafakari
umaana wa miaka hiyo na uhusiano wako na Mungu. Ni ukweli pia idadi ya miaka
kwa Mungu haina maana. Umaana wa idadi ya miaka huja pale tu, unapoanza
kujiuliza na kufanya tafiti moyo ya “ulichofanya na idadi hiyo ya miaka
uliyopewa kama zawadi.”
Ndugu yangu tunaye
safiri wote katika tafakari hii, ukishajitambua katika maana niliyokwisha isema
hapo juu, hatua ya pili itakuvuta KUJISHUSHA. Na hii ndiyo maana halisi ya kujinyenyekesha
kwa kile ulichodhani mwanzoni ulikuwa kumbe sivyo, ili uwe kile ulicho katika
uhalisia wako na yale unayotaka kuyafanya ili ufikie malengo halisi ya maisha
yako. Jambo hili kulifikia si hatua ya mara moja kama kulala na kuamka.
Kinachotukwamisha mara nyingi ni pale tunapovaa kinyago “mask” kwa kuficha
ukweli wetu halisi ambao mara nyingi hatupendi kuugusa wala kuuzungumzia popote
pale. Hakuna filamu nzuri ya maisha zaidi ya maisha yako mwenyewe. Kuitazama
filamu hii ni kujinyenyekesha kuliko kwa ndani kabisa. Ukiweza fanya hivyo, ni
mwanzo wa safari ya maisha yenye malengo.
Mambo haya mawili
muhimu; kujitambua na kujishusha ambayo matokeo yake ni kuwa na nguvu kimaadili
na unyenyekevu. Hii ndiyo silaha pekee ya kumjua Kristo na maagizo yake kadiri
ya mafundisho yake. Jambo hili ndiyo sababu ya kuogopwa kwa jumuiya ya kwanza
ya wakristo na kuwafanya tofauti na waliowatangulia kama akina Theuda na Yuda
Mgalilaya ambao walipata umaarufu na mara wakatoweka, Mdo 5:37-37.
Jambo hili kwa Kanisa
la Mwanzo lilikuwa na faida kuu tatu; kwanza kabisa waliumega mkate-kwa
kutambua mahitaji yao ya kila siku “basic needs.” Pili waliumega Mkate kama
adhimisho la Ekaristi Takatifu-ikiwa ndicho kiungo pekee cha umoja wao
kijumuiya. Yesu Kristo hapa alikuwa kiunganishi cha umoja huo hadi leo. Jumuiya
yeyote ile ya Kikristo kwa mfumo wowote ule wa maisha bila Yesu wa Ekaristi
kuwa kiungo cha maisha hayo, jumuiya hiyo hubakia kuwa kama kikundi cha
waigizaji wasicho kijua wakiigizacho, Yoh 15:5. Na tatu waliumega mkate kwa
kulisikiliza, kulifundisha, na kulinena neno la uzima, yaani Maandiko
Matakatifu.
Wapendwa, ni katika
maana hii tunaona mtu maarufu kama Gamalieli akisimama na kutoa angalizo kwa mafarisayo
wenzake kuhusu dhuluma wanayoifanya dhidi ya wafuasi hawa wa Kristo. “Lakini mtu mmoja, Farisayo, jina lake Gamalieli,
mwalimu wa torati, mwenye kuheshimiwa na watu wote, akasimama katika baraza,
akawaambia, Enyi waume wa Israeli, jihadharini jinsi mtakavyowatenda watu
hawa,” Mdo 5:34a-35. Mambo wayafanyayo Wakristo hawa msingi wake ni Kristo, na
utendaji wake ni nguvu ya Kimaadili na Unyenyekevu.
Wakati mwingine tusipo
lijua jambo hili, hubaki kupingana na nguvu tusiyoijua. Gamalieli anawakumbusha
uwepo wa Mungu na uweza wake juu ya lililo haki. Kamwe hatuwezi kushinda dhidi
ya haki ya Mungu. Vita hii na msuguano huu dhidi ya Mungu ni angamizo kubwa
kwetu binafsi. Gamalieli anasema, “basi
sasa nawaambia, Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi
hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjwa, lakini
ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na
Mungu,” Mdo 5:38-39. Leo mimi binafsi najiuliza ‘nini sababu ya mfululizo wa
ajili za magari katika Taifa letu, na majanga mengine ambayo kwa kiasi kikubwa
ni huzini na majonzi katika jamii.’
Wapendwa, nina Imani
pasipo shaka kwamba, yawezekana wakati fulani mahali fulani, na watu fulani
hatukutenda iliyo haki. Ni ukweli pia katika jamii yetu, licha ya maovu mengi
tunayotenda mbele za Mungu, jambo hili ni wazi kabisa hatujachukua hatua za utosha.
Kumekuwepo na dhuluma za muda mrefu katika jamii yetu, na kubwa zaidi ni
dhulumu dhidi ya uhai. Ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi-Maalbino wamekuwa
wakiwindwa na kuuwa kama vile si binadamu na hawana haki ya kuishi. Vyombo vya
usalama ikiwa ndala yenyewe, haijafanya vya kutosha kunusuru maisha haya ambayo
ni zawadi ya Mungu kwa kila mwenye pumzi. Uhai ukiwa ndiyo uwepo wa Mungu
mwenyewe, kuukatiza au kuuchukua bila mamlaka yake Mungu ni kupingana na Mungu
mwenyewe. Je katika jambo hili tupo na
tutakuwa salama?
Jambo lingine ambalo ni laana pia kwa
taifa hili, ni kufumbia macho haki za wanyonge, na kuzipora haki hizo bila woga
wowote. Leo usipojulikana na mbaya zaidi kama huna fedha, huwezi patiwa haki
yako. Jambo hili limeshakuwa la kawaida kabisa hata pale unapotakiwa kupata
haki zako za kijamii kadiri ya katiba, kama vile matibabu, elimu na mengineyo.
Rushwa na Ufisadi ndiyo virusi hatari kabisa katika jamii yetu leo. Je, na hili
tupo na bado tutakuwa salama? Ni Mungu gani amabaye hatajitokeza na kusimama
katika uovu huu?
Wakristo wetu wa kwanza wanahesabiwa
haki kwa nguvu yao ya kimaadili na unyenyekevu pale wapoishi yale wayasemayo na
kuyashuhudia dhidi ya dhuluma ya watesi wao, na uovu wao juu ya mwenye haki
Yesu Kristo waliomwondosha katika ulimwengu huu kwa ukatili mkubwa kushuhudiwa
na binadamu. Wanapopigwa na kuteswa Wafuasi wa Yesu hawaachi kusimama katika
kweli na haki. Wanapokatazwa kulisema jina hili lenye nguvu ya ajabu-Yesu
Kristo hawaachi kuwa na furaha. Baada ya kipigo na mateso, “nao wakatoka katika ile
baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa
ajili ya Jina hilo,” Mdo 5:41.
Ndugu yangu, ni mara
ngapi wafurahi kwa kuaibishwa kwa ajili ya Jina hili kuu ya Yesu Kristo
Mnazareti? Ni mara ngapi twataka kusafishwa majina yetu kwa vile tu hayakutendewa
haki? Ni mara ngapi tunapenda kutambulika tulivyo zaidi ya kumtambulisha Kristo
aliye mfalme wa amani, haki, upendo na unyenyekevu? Ni ukweli usiotia shaka
kwamba Kristo anapoinuliwa kwa yale tuyafanyayo ni kwa namna hiyo hiyo nasi
tunanyanyuliwa. Kinyume chake ni balaa kubwa, na maanguko yake hayana mfano. Kristo asipokuwa kielelezo cha maisha yetu,
hatutaweza kumshuhudia hata majumbani mwetu, majirani zetu na jamii
inayotuzunguka. “Na kila siku, ndani
ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za
Yesu kwamba ni Kristo,” Mdo 5:42. Bila nguvu ya kimaadili na unyenyekevu bado
hatutaweza kufikia hatua hii ya Kanisa la mwanzo.
Bila shaka kila mmoja
wetu anayo sababu kubwa kabisa ya kuwa hapo alipo sasa. Jambo la kujiuliza ni
hili; Je, sababu hiyo imebeba ukweli wa kile ninachokichuchumilia kila siku ya
maisha yangu? Injili ya leo inatupa angalizo kuhusu changamoto hii muhimu ya
maisha. Ni kweli kila aliyemwona Yesu na kumfuata alikuwa na sababu yake.
Injili ya leo inatupa mbili ya sababu za kumfuata Kristo kadiri ya kundi lile
siku ile na wakati ule. “Na mkutano
mkuu wakamfuata, kwa sababu waliziona ishara alizowafanyia wagonjwa,” Yoh 6:2.
Je, kutakuwa na sababu yeyote ya kumfuata Yesu Kristo kama akiwaponya wangonjwa
wote tulikuwa nao leo? Ndugu yangu ishara tu ya kitu fulani katika ufuasi wa
Kristo hauakisi Imani ya kwetu juu ya Kristo licha kwamba ni moja ya kutupa
uhakika wa nguvu na uwezo wa Kristo.
Tunachopaswa kufanya
kama wafuasi wa kweli wa Kristo ni kufundisha ukweli juu ya Kristo na nafasi
yake katika maisha yetu ya kila siku. Huku ni kuwaketisha chini wanaotaka
kumjua. Yesu akasema, Waketisheni watu. Basi watu waume wakaketi, wapata elfu
tano jumla yao,” Yoh 6: 10a-10c. Kuwaketisha watu chini wenye shahuku ya kumjua
Kristo ni kutoa mafundisho ya kweli, ili kuziponya mwili, nafsi na roho zao
kutoka katika mahangaiko ya kila siku. Leo katika tukio hili, Kristo anawaponya
hangaiko hilo la mwili kwa kuwalisha mikate na samaki. Tendo hili ni moja ya
yale mambo makuu matatu waliyoyafanya mitume na wafuasi wengine wa Kristo baada
ya ufufuko wake.
Tendo hilo la kuwalisha
kimwili katika mahitaji yao, linatanguliwa na shukrani kwa yale
aliyowashirikisha, ambayo leo tunapata taswira halisi ya adhimisho la Ekaristi
Takatifu. Adhimisho hili ni karamu ya Kristo na shukrani kwa Mungu. “Basi Yesu akaitwaa ile mikate, akashukuru,
akawagawia walioketi; na kadhalika katika wale samaki kwa kadiri walivyotaka,”
Yoh 6:11. Ndugu yangu, moyo usio na shukrani hukausha mema yote machoni mwa
Mungu. Ni kwa moyo huu wa shukrani wanakula na kusaza na kukusanya mabaki
yaliyoyajaza makapu kumi na mbili. Makapu haya kumi na mbili ni idadi ya
makabila kumi na mbili ya Israeli. Kwa maana nyingine kilichobaki likiweza
kuwalisha taifa zima. Kwa maana hii, muujiza huu wa Yesu siyo tu kwa watu wale
elfu tano waliokula na kusaza. Kristo katika jambo hili la shukrani
anatukumbusha wajibu muhimu sana. Kwa vile yote tulivyonavyo tumepewa kwa
upendo wa huruma ya Mungu. Hivyo ili tuendelee kupata neema hizo, yatupasa
kuhifadhi yale yaliyobaki kwa sababu hatuna uhakika wa kesho. Yesu anasema,
“Kusanyeni vipande vilivyobaki, kisipotee cho chote,” Yoh 6:12b. Ni mara ngapi
unatumia hovyo aliyokukirimia Mungu kwa upendo ili hali jirani yako analala na
njaa kila siku? Je na baada ya kula na kushiba, bado unaona sababu ya kumfuata
Kristo kwa karibu?
Ndugu yangu, kula na
kunywa vikiongozwa na ishara mbalimbali, siyo sababu msingi wa imani yetu
kumfuata Kristo, na imani yetu haijajengwa katika mambo hayo. Tunaona baada ya
watu hawa kula na kushiba walitaka
kumfanya Yesu kuwa mfalme wa Mikate. Kwa maana nyingine tunamgeuza Kristo kama
“Supermarket” ambayo tunauhakika wa kupata kila kitu, na pale tu tunapokuwa na
hitaji hilo. Tunapokuwa na mwono huu, Kristo ujitenga nasi kwa sababu bado hatujamjua
vizuri, na hatujui nafasi na lengo lake katika maisha yetu ya kila siku.
“Akajitenga, akaenda tena mlimani yeye peke yake,” Yoh 6:15b. Kwa mantiki hii,
inawezekana sala zetu hazijibiwa kadiri tuombavyo kwa sababu tunamchukulia
Kristo kama sehemu ya kuyapata tu yale tuyamataniyo hata kama siyo ya muhimu
katika maisha yetu. Na ndiyo maana Mtume Yakobo anatupa angalizo kwa kutuwasa,
“Hata mwomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa
zenu.” Yak 4:3
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nao
wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili
kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo,” Mdo 5:41
Ee Yesu na Mchungaji wetu Mwema,
lisimamie Kanisa lako leo katika nguvu ya kimaadili na Unyenyekevu kwa Viongozi
wako na Wakristo wote kwa ujumla wao. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario