JUMANNE WIKI YA 5 YA PASAKA
Somo:
Mdo 14:18-27
Zab:
145: 10-11, 12-13ab, 21
Injili:
Yoh 14:27-31a
Nukuu:
“Lakini
Wayahudi wakafika toka Antiokia na Ikonio, wakawashawishi makutano hata
wakampiga kwa mawe Paulo, wakamburuta nje ya mji, wakidhania ya kuwa amekwisha
kufa,” Mdo 14:19
“wakifanya
imara roho za wanafunzi na kuwaonya wakae katika ile Imani, na ya kwamba
imetupasa kuingia katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi,” Mdo 14:22
“Hata
walipofika wakalikutanisha Kanisa, wakawaeleza mambo yote aliyoyafanya Mungu
pamoja nao, na ya kwamba amewafungulia Mataifa mlango wa imani,” Mdo 14:27
“Amani
nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo.
Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga,” Yoh 14:27
“Mimi
sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala
hana kitu kwangu,” Yoh 14:30
TAFAKARI: “Kanisa la Mwanzo, umisionari na changamoto zake.”
Wapendwa
wana wa Mungu, tunaendelea kutafakari umisionari wa Kanisa la Mwanzo, na
changamoto zake. Mtume Paulo na mwenzake Barnaba wanakuwa mstari wa mbele
kuhakikisha neno la Bwana linafika hata kwa wale walikuwa mbali na Yerusalemu.
Kazi hii haikuwa rahisi hata kidogo. Mtume Paulo katika safari yake huko Ikonia
na Antiokia, anakutana na kikundi cha Wayahudi ambao wanawashawishi watu wa
miji hii kumpiga kwa mawe Mtume Paulo, ili kuzuia uinjilishaji huu. Hivyo, “Wayahudi wakafika toka
Antiokia na Ikonio, wakawashawishi makutano hata wakampiga kwa mawe Paulo,
wakamburuta nje ya mji, wakidhania ya kuwa amekwisha kufa,” Mdo 14:19. Hata
hivyo kunusurika huku katika kifo hakukwamishi kazi hii ya kitume.
Mtume Paulo na wenzake
walikuwa kweli majitu ya sifa. Majitu ya sifa hapa inamaanisha kwamba hawakuwa
na woga wote kulinena neno hata pale walipokatishwa tamaa. Hawakuogopa kusafiri
na kumuhubiri yule waliyekuwa wanamwamini na kumwishi kila siku ya maisha yao.
Walisafiri kila mji “wakifanya imara roho
za wanafunzi na kuwaonya wakae katika ile Imani, na ya kwamba imetupasa kuingia
katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi,” Mdo 14:22. Yesu Kristo hasa
katika fumbo zima la mateso, kifo na kufufuka kwake, ndiyo sababu ya nguvu na
msimamo wa Mitume katika safari hii ya kulihubiri na kuliishi neno la Mungu.
Walitambua wazi ni katika dhiki nyingi wataupata ufalme huo wa Mungu. Maisha na
sadaka yao ya kila siku ndio msingi wa Kanisa letu hadi leo. Je, mimi natoa
sakaka gani kuimairisha msingi huu wa Imani katika Kanisa langu?
Wapendwa wana wa Mungu,
tusianze sasa kufikiri namna ya kusafiri na kufanya umisionari wa mbali. Sinodi
ya Afrika imeweka wazi namna na mtazamo wa Kanisa letu la Afrika. Kanisa letu
la Afrika kiini chake ni familia. Kwa mtazamo huu, umisionari wetu uuanze
kwenye familia zetu. Familia zikiimarika, jumuiya zetu ndogondgo za Kikristo
nazo zitaimarika. Jumuiya hizi zikiwa imara hakika Kanisa mahalia usitawi na
hofu ya Mungu utawala ndani ya mioyo ya watu. Hivyo umisionari wetu leo kama
wabatizwa ujikite katika kuimarisha familia zetu. Hapo ndipo kwenye uhai wa
Kanisa.
Uinjilishaji huu
utafanikiwa kama kweli tutakuwa na AMANI ya kweli ndani yetu. Tunaposema amani
hatumaanishi tu amani ya kiroho, bali pia amani ya kijamii. Popote duniani leo
swala la amani limeanza kuwa kama kitendaliwi kisichoteguka. Kumekuwepo na
misuguano ya chini kwa chini na wakati mwingine misuguano ya wazi kati ya imani
moja na nyingine. Yesu Kristo anatupa angalizo juu la swala hili anaposema, “Amani nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo
mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na
woga,” Yoh 14:27. Ni wazi amani tuipatayo leo huku duniani haina uhakika. Hata
hivyo Yesu anatuambia tusiogope. Katika hali ya sintofahamu anatuhaidia Roho
wake Mtakatifu ambaye kupitia yeye Roho huyo atatupa viangalizo vyote. “Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana
yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu,” Yoh 14:30. Katika mashaka
na kutoweka kwa Amani katika ulimwengu huu, kwa wezwa rudishwa tu kwa kukubali kuongozwa na Roho Mtakatifu na
kuacha ubinafsi na maslahi binafsi.
Wapendwa
katika Kristo, kwa sasa tupo katika kipindi cha kuelekea Sikukuu ya Pentekoste.
Tuwekeze nguvu zetu zote kumwomba huyu Roho Mtakatifu atuongoze vyema katika
kipindi cha sintofaumu nyingi katika Taifa letu. Tukiikosa hiyo amani, hata
uinjilishaji wetu na umisionari wetu
kifamilia hautawezekana. Tuwaombee pia viongozi wetu wajue dhamana waliyonayo
juu ya maisha ya watu na mali zao. Tuliombee pia Kanisa liendelee kuishi katika
umoja na upendo kama Kristo mwenyewe alivyotaka liwe.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Amani
nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo.
Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga,” Yoh 14:27
Tusali:-Ee Yesu, mtume
Roho wako Mtakatifu atuangazie yaliyo haki na matakatifu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario