JUMANNE
WIKI YA 4 YA PASAKA
Somo: Mdo 11:19-26
Zab: 87:1b-3, 4-5, 6-7
Injili: Yoh 10:22-30
Nukuu:
“Basi
wale waliotawanyika kwa sababu ya ile dhiki iliyotukia kwa habari ya Stefano,
wakasafiri hata Foinike na Kipro na Antiokia, wasilihubiri lile neno ila kwa
Wayahudi peke yao,” Mdo 11:19
“Mkono
wa Bwana ukawa pamoja nao, watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana,” Mdo 11:21
“Habari
hizo za watu hao zikafika masikioni mwa Kanisa lililokuwako katika Yerusalemu;
wakamtuma Barnaba, aende hata Antiokia,” Mdo 11:22
“Na wanafunzi waliitwa
Wakristo kwanza hapo Antiokia,” Mdo 11:26b
“Basi
Wayahudi walimzunguka, wakamwambia, Hata lini utatuhangaisha nafsi zetu? Kama
wewe ndiwe Kristo, utuambie waziwazi,” Yoh 10:24
“Yesu
akawajibu, Naliwaambia, lakini ninyi hamsadiki. Kazi hizi ninazozifanya kwa
jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia,” Yoh 10:25.
“Lakini
ninyi hamsadiki, kwa sababu hammo miongoni mwa kondoo wangu,” Yoh 10:26
“Kondoo
wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata,” Yoh 10:27.
“Nami
nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu
atakayewapokonya katika mkono wangu,” Yoh 10:28
TAFAKARI:
“Matendo mema ndani ya Kristo na katika Kristo, umtambulisha Kristo pale
tulipo; wote tumeitwa kuwa wamisionari.”
Wapendwa wana wa Mungu,
kutawanyika kwa jumuiya ya kwanza ya Wakristo, kulitokana na kuhujumiwa kwa
jumuiya hiyo, na hasa kile kifo cha Shahidi Stefano. Kwa upande mwingine,
kupitia mateso haya, habari njema zinafika kila kona na wengi wanamwamini
Mungu. “Basi wale waliotawanyika kwa sababu
ya ile dhiki iliyotukia kwa habari ya Stefano, wakasafiri hata Foinike na Kipro
na Antiokia, wasilihubiri lile neno ila kwa Wayahudi peke yao,” Mdo 11:19.
Kutawanyika huku kwa jumuiya hizi za Wakristo tukienda mbali zaidi tunaona ni
kutokana na sadaka ile ya pekee aliyoitoa Yesu pale msalabani. Ni kwa kupitia
sadaka hiyo hiyo-kwa kila mmoja wetu, Kanisa linakua na kuenea popote duniani.
Wapendwa, tunapokuwa na
Kristo katika nia na matendo yetu tunabarikiwa kwa sababu tuyafanyayo ni
mwendelezo wa kazi yake ya kuikomboa dunia. “Mkono
wa Bwana ukawa pamoja nao, watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana,” Mdo 11:21.
Hapa tunaona safari ya uinjilishaji ndiyo inaanza, na Kanisa katika maana ya
kila Mbatizwa linakuwa Kanisa la Kimisionari. “Habari
hizo za watu hao zikafika masikioni mwa kanisa lililokuwako katika Yerusalemu;
wakamtuma Barnaba, aende hata Antiokia,” Mdo 11:22. Kazi hizi za kimisionari
ndizo zinazolifanya Kanisa likue na kuenea kila mahali. Kazi hizi pia ndizo
zinazo watambulisha wale wazifanyazo. Ni hapa Antiokia kwa mara ya kwanza
wanafunzi wa Yesu wanaitwa Wakristo. “Na wanafunzi waliitwa Wakristo kwanza
hapo Antiokia,” Mdo 11:26b. Kuitwa kwao huku ni kutokana na matendo yao
kuendana na kile walichokuwa wakikiamini na kukihubiri-Yesu Kristo Mwana wa
Mungu aliye hai, kufanya toba ya kweli, na kukaribia kwa Ufalme wa Mungu.
Wapendwa katika Kristo,
mtindo huu wa kimisionari unaitajika sana nyakati zetu. Matendo mema ndani ya
Kristo na katika Kristo, umtambulisha Kristo pale tulipo; na kwa namna hiyo wote
tumeitwa kuwa wamisionari. Umisionari wa kutembea na vipasa sauti kwa sasa
hauna nafasi sana. Tunaitaji umisionari wa matendo mema kwa watu wote. Kristo alishaanza
kulifanya hili pale ambapo Wayahudi walitaka kupata uhakika kama kweli yeye
ndiye Kristo mwenyewe. “Yesu akawajibu,
Naliwaambia, lakini ninyi hamsadiki. Kazi hizi ninazozifanya kwa jina la Baba
yangu ndizo zinazonishuhudia,” Yoh 10:25. Kazi azifanyazo Yesu ndizo
zinazomthibitisha. Ni kwa namna hiyo hiyo kwamba kazi tuzifanyazo kama Wabatizwa
na Kanisa kwa ujumla wake zitamtambulisha Kristo pale tulipo.
Wapendwa, asiyesadiki
matendo hayo mema ni wazi hamsadiki hata Kristo pia. Je, tuache kutenda mema?
Jibu ni HAPANA. Tusiache kutenda mema kwa vile tu wapo watu ambao hawayaoni
mema tuyatendayo, na wala hawamsadiki Kristo. Yesu anasema, “Lakini
ninyi hamsadiki, kwa sababu hammo miongoni mwa kondoo wangu,” Yoh 10:26. Ni
Kristo mwenyewe anayejua hatma ya wale wasiomsadiki. Kazi yetu ni kusambaza
upendo wa Kristo kila kona. Ni Kristo mwenyewe atakaye wabadilisha mioyo yao
wasiomsadiki kadiri atakavyoona yeye na wakati ufaao. Naye anasema, “Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua,
nao wanifuata,” Yoh 10:27. Kondoo walio
mbali na sauti ya Kristo ipo siku watavutwa karibu kwa matendo yetu mema kama
wafuasi wake Kristo. Ni Kristo mwenyewe atawapa uzima na kuwahifadhi katika
mikono yake.Yesu anasema, “Nami
nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu
atakayewapokonya katika mkono wangu,” Yoh 10:28. Mimi na wewe kama wabatizwa
tutimize vyema ahadi zetu za ubatizo.
Tumsifu Yesu Kristo.
“Mkono
wa Bwana ukawa pamoja nao, watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana,” Mdo 11:21
Tusali:-Ee
Yesu Kristo na Mchungaji wetu Mwema, tujalie neema ya kutenda matendo mema kila
wakati. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario