sábado, 9 de abril de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 3 YA PASAKA-C

JUMAPILI YA 3 YA PASAKA YA MWAKA-C

Somo I: Mdo 5:27b-32, 40b-41
Zab: 30:1, 3, 5, 10-12
Somo II: Ufu 5:11-14
Injili: Yoh 21:1-19 
Nukuu:
 “Petro na mitume wakajibu, wakisema, Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu. Mungu wa baba zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti,” Mdo 5:29-30

 “Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo,” Mdo 5:41

 “Baraka na heshima na utukufu na uweza una yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na yeye Mwana-Kondoo, hata milele na milele,” Ufu 5:13b

 “Akawaambia, Litupeni jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata.Basi wakatupa; wala sasa hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki,” Yoh 21:6 

 “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu,” Yoh 21:15 

Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu,” Yoh 21:16 

Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.” Yoh 21:17 

Akasema, Amin, amin, nakuambia, Wakati ulipokuwa kijana, ulikuwa ukijifunga mwenyewe na kwenda utakako; lakini utakapokuwa mzee, utainyosha mikono yako, na mwingine atakufunga na kukuchukua usikotaka,” Yoh 21:18 

Akasema neno hilo kwa kuonyesha ni kwa mauti gani atakayomtukuza Mungu. Naye akiisha kusema hayo akamwambia, Nifuate,” Yoh 21:19 

TAFAKARI: “Ndani na katika Yesu kuna Mwanga na Amani ya kweli. Kwa kumtii Yesu Kristo na kuishi ndani ya Neno lake kwa kuyafanya mapenzi yake, huyajenga upya maisha yako yaliyobomolewa na dhambi. Kwa Yesu kuna Njia ya kweli, Kweli halisi, na Uzima wa Milele.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya ‘3’ya Pasaka ya Mwaka ‘C’ wa Kanisa. Leo Mama Kanisa kwa namna ya pekee anatualika tutafakari kwa undani kiini cha Imani na Msingi kwa Kanisa-jumuiya ya kwanza ya Wakristo. Tunapotazama Kiini cha Imani na Msingi huu wa Jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo, mambo matatu ni dhahiri; Uwepo na kazi ya Nguvu ya Roho Mtakatifu, Moyo wa kupokeana {kushirikishana na kutabikiana katika hali zote bila kujibakiza}, na Nguvu ya Kimaadili. Kristo mfufuka akiwa ndiye kielelezo na sababu ya kuishi na kutenda kwao, Jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo walisimama imara kwa kila jambo hasa pale kulipotokea hujuma juu ya kweli na haki iliyolenga fumbo zima la wokovu wetu.

Hivyo kwa nguvu ya ROHO MTAKATIFU licha ya uduni wao ‘kiufahamu’ hawakusita kusema lililo kweli kwa wale walionekana kupindisha ukweli kwa manufaa yao binafsi. Tuelewe jumuiya hii  ya kwanza na hasa Mitume, hawakuwa watu wa elimu ya pekee sana. Wengi wao walikuwa na taaluma ya uvuvi tu ambayo kwa kiasi kikubwa waliipata kutokana na mazingira na makuzi yao. Roho huyu Mtakatifu aliwapa ujasiri wa ajabu na kusimama imara katika kweli na haki. Mitume wanaponyamazishwa kulinena Neno la uzima, na hasa maswahibu yaliyompata Yesu Kristo, Mtume Petro anakemea jambo hilo kwa ujasiri mkubwa na kusema, Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu. Mungu wa baba zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti,” Mdo 5:29-30. Huyu siye Petro yule aliyekuwa na woga hata kumkana Yesu mara tatu. Huyu ni Petro aliyevuviwa na Roho Mtakatifu na aliyezaliwa upya kwa Roho Mtakatifu. Kuhusu Roho Mtakatifu Petro Mtume anasema, sisi tu mashahidi wa mambo haya, pamoja na Roho Mtakatifu ambaye Mungu amewapa wote wamtiio,” Mdo 5:32. Roho Mtakatifu ni zawadi ya pekee kwa kila mmoja wetu na Kanisa kwa ujumla wake. Uwepo wa Roho Mtakatifu Katika Kanisa-Sakramenti ya wokovu, ni ukamilifu ya haya aliyoyahaidi Yesu Kristo angali na wanafunzi wake kwamba, Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu. Sitawaacha ninyi yatima; naja kwenu,” Yoh 14:16-18. Ndugu yangu, Kanisa nikimaanisha yeyote yule aliyebatizwa si mayatima. Tunaye Roho Mtakatifu atakaye tuongoza katika hali zote. Ni mimi na wewe kumpa nafasi tu. 

Umoja na nguvu ya jumuiya hii ya Wakristo wa kwanza uliimarika kwa utayari wao katika KUPOKEANA, KUCHUKULIANA, NA KUTAABIKIANA katika hali zote bila kujibakiza. Siyo kwamba matatizo hayakuwepo, bali yalipotokea yalipatiwa ufumbuzi wa haraka ili ukweli kuhusu Kristo Yesu usikwamishwe. Hapa tunaona namna ambavyo walivyolishughulikia tatizo lile la wajane katika jumuiya yao kwa kuwateua watu saba ‘mashemasi’ kutoa huduma ili neno la uzima lisikwame, Mdo 6:1-7. Hivyo, Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani,” Mdo 6:2. Moyo huu wa undugu uliounganishwa na kufungamanishwa na neno la uzima ulikuwa kiungo muhumu sana katika kuishika Imani, kuikuza Imani, na kushirikishana tunda ya Imani ya kweli, ambayo ndio Upendo na Matumaini ndani na katika Kristo Yesu Mfufuka kwa kila amuaminiye. Jumuiya hii ilipokuwa pamoja mateso yao na kutaabika kwao kulibadilika kuwa furaha kwa sababu walijua sababu ya mateso na mahangaiko yao. Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo,” Mdo 5:41.

Wapendwa katika Kristo, furaha ya kweli katika maisha ya mtindo wowote ule, iwe maisha ya wakfu au ndoa, msingi wake si mali au utajiri kama wengi wetu tunavyofikiri na kutaabika kuyatafuta hayo usiku na mchana. Furaha ya kweli kabla ya yote hujengwa katika maana na sababu ya maisha yale unayoyaishi. Utawezaje basi kupata furaha ya kweli kama unachokiishi huoni umaana wake na sababu yake? Maana na sababu ya kile unachokiishi hukupa fursa ya kuona kesho ya kile unachokiishi. Kesho ya kile unachokiishi umulika umilele wake hata kama umilele huo kwa kiasi fulani bado umefichwa kwako.

Jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo pamoja na kuongozwa na Nguvu ya Roho Mtakatifu, na umoja na mshikamano wao katika kila hali bila kujibakiza, ilikuwa imara na hasa kwa viongozi wao ambao ni Mitume kutokana na NGUVU YA KIMAADILI. Nguvu hii ya kimaadili ilikuwa mwiba kwa watesi wao na wahujumu Kanisa kwa sababu Mitume na Wakristo kwa ujumla wao waliyaishi kwa uaminifu mkubwa yale yote waliyoyasema na kuyaamini. Maisha ya hapa duniani baada ya Ufufua wa Kristo waliyaona kama jaribu, dhamana na jukumu la muda mfupi tu. Hivyo tenda yao, fikiri yao, na hata ona yao ilikuwa na mwelekeo wa mwisho wa nyakati na kwenye uzima wa milele. Hivyo kwa maono jumuiya hii iliweza kuliona Kanisa la Watakatifu waliopo mbinguni baada ya kuishinda vita hii ya imani hapa duniani. Tunaona ukweli huu kutoka somo letu la pili leo, kwamba watu wale huko mbinguni walionekana wakisema kwa sauti kuu, Astahili Mwana-Kondoo aliyechinjwa, kuupokea uweza na utajiri na hekima na nguvu na heshima na utukufu na baraka,” Ufu 5:12. Mwana-kondoo huyu ambaye ndiye Yesu Kristo ni sababu na kielelezo cha maisha na furaha ya kweli ya jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo na hata sasa kwa Kanisa kama Sakramenti ya wokovu kwa wale wote waliomridhia. “Baraka na heshima na utukufu na uweza una yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na yeye Mwana-Kondoo, hata milele na milele,” Ufu 5:13b. Hakika tuwapo hapa duniani tusisahau wosia huu wa Yesu juu ya maisha ya kila siku, kwamba, Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa,” Mt 6:33 

Tunapojaribu kuchenga ukweli huu {kuutafuta Ufalme wake na haki yake}, tunakuwa nje ya kweli mzima ya mafundisho ya Kristo na lengo zima la umilele wa maisha haya tunayoyaishi. Mara kwa mara kunakuwa na vishawisha vya kurudi nyuma na kufanya yale tuliyoyazoea. Hata Mitume hawakuweza kukwepa hali hiyo, kwani maisha yao na ukuuaji wao wa Imani ulilandana sana na maisha na mazingira yao. Hivyo Mtume Simoni Petro anawaambia wenzake, Naenda kuvua samaki. Nao wakamwambia, Sisi nasi tutakwenda nawe. Basi wakaondoka, wakapanda chomboni; ila usiku ule hawakupata kitu,” Yoh 21:3.

Wapendwa wana wa Mungu, tunapokuwa nje ya mpango mzima wa Mungu, na hasa kwa wale tuliopewa thamana hiyo {Wazazi, Wahudumu wa Kiroho, Viongozi wa Serikali, na ak}, mafanikio ya yale tuyatamaniyo huwa hewa na kutoweka kabisa. Kumhubiri Kristo na kumshuhudia kwa maneno na matendo ni kazi ya kila  aliyebatizwa na kuimarishwa. Hivyo basi, yatupasa kulifanya tendo hilo pasipo shaka. Kristo hachoki tukumbusha tunapokengeuka kuhusu ukweli huu. Kristo aweza kutumia njia mbalimbali kuwakilisha ujumbe wa kweli hii. Kwa upendo wake, Kristo mara zote anapenda kujua mahangaiko yetu, na kuturudisha katika mstari. Katika hali ya kuchoka na uchovu mwingi kwa kupigika usiku kucha bila kupata samaki, anawaambia wanafunzi wake, Wanangu, mna kitoweo? Wakamjibu, La,” Yoh 21:5. Kwa maana nyingine Yesu anataka kutuambia, Je, mnapozifuata njia zenu na kuacha maagizo yangu mnapata mafanikio?

Kuonyesha ukweli wa jambo hili, Yesu Kristo, anawafundisha njia na maagizo yake yaliyo kweli na sahihi kwa uzima wa mwili na roho. Akawaambia, Litupeni jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata. Basi wakatupa; wala sasa hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki,” Yoh 21:6.

Wapendwa katika Kristo, yawezekana ushapigana sana na maisha kiasi kwamba kila siku ni aheri ya jana. Jambo la kwanza usitafuta mchawi wala kwenda kwa waganga, au kusafisha nyota kama tunavyosikia wengi wakidanganywa. Jambo la kwanza chunguza uhusiano wako na Mungu. Je, umelitupa jarife hilo upande wa kuume wa chombo chako, yaani, maisha yake? Je, unaisha kadiri ya matakwa ya Mungu? Kama hapana, Je, unaridhika na hali hiyo? Kama siyo, Je, ni kitu gani kinachokukwamisha kurejesha uhusiano huo? Kama uhusiano wako na Mungu ni mzuri na bado unapigika sana na maisha, jambo hilo unalichukuliaje? Je, walichukulia kama kusahauliwa na Mungu, au kutokutendewa haki na Mungu? Je, unaelewaje subura ya Mungu kwa yale uyaombayo na kuyatamani?

Ndugu yangu, hakuna jambo lolote tuombalo Mungu aache kutupatia. Kama itatokea kwa hapa duniani hatukulipata basi jua umeandaliwa jambo hilo kwa umilele wake, mara baada ya maisha haya ya hapa duniani. Kamwe Mungu hamtupi mja wake. Kwa wale ambao Mungu ametukirimia zaidi na hata kupita mahitaji yetu, tunachukuliaje jambo hilo? Je, tunamtambua Mungu katika mali na utajiri wetu? Ukweli ni kwamba kamwe hatutaweza mtambua Mungu kwa yale tuliyonayo, kama hatuna upendo na Mungu. Yohane Mtume anamtambua Kristo kwa sababu alikuwa na upendo wa dhati kwa Kristo na Kristo alikuwa anampenda kwa namna ya pekee. Na hivi ndiyo Injili inavyotuambia, Basi yule mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda akamwambia Petro, Ndiye Bwana,” Yoh 21:7.

Kumtambua huku Kristo, Yohani habaki na hali hiyo mwenyewe. Anamwambia na Petro pia. Je, tunapoguswa na upendo wa Kristo na Mungu tupo tayari kuushirikisha kwa wenzetu nao wapate wokovu huo? Rejea maisha ya jumuiya ya kwanza ya Wakristo. Tunaona baada ya Petro Mtume, kusikia habari hiyo, anajitosa kwenye maji maana alikuwa uchi. “Naye Simoni Petro, aliposikia ya kwamba ni Bwana, akajifunga vazi lake, (maana alikuwa uchi), akajitupa baharini,” Yoh 21:7b. Mpendwa tunayesafari wote katika tafakari hii, Petro kuwa uchi hapa kunamaanisha kwa upande mwingine kwamba anatambua kujikwaa kwake kunakotokana na kutokuyafanya yale aliyopaswa kufanywa kama kiongozi, kama niliyoeleza hapo mwanzo.

Mara baada ya Petro kujitambua, anaingia chomboni na hapa tunaona maajabu haya. Basi Simoni Petro akapanda chomboni, akalivuta jarife pwani, limejaa samaki wakubwa, mia hamsini na watatu; na ijapokuwa ni wengi namna hiyo, jarife halikupasuka,” Yoh 21:11. Ndugu yangu, jarife hili halina tofauti na Kanisa kama chombo na Sakramenti ya wokovu wetu, ambacho kazi yake kubwa ni kuwavuta watu kwa Kristo na kuwapeleka kwake wakiwa salama. Usalamu huu ni idadi inayotolewa ya samaki hawa. Tutajulikana kwa idadi yetu mbele za Mwanakondoo. Nasi tukifika mbele ya uso wa Mungu tutajulikana kwa idadi, na wale tuliopewa kazi hiyo yatupasa tutoe hesaba ya idadi tulioifikisha mbele ya Mungu na Mwanakondo.

Hata hivyo tunasikia jarife hili-Mtego huu, haukupasuka licha ya wingi wa samaki wale. Jibu ni kwamba mtego haukupasuka kwa sababu u imara. Mtego, yaani Jarife kama Kanisa, na Sakramenti ya wokovu wetu, uimara wake unatokana na uwepo wa nguvu ya Roho Mtakatifu, ambaye uyaratibisha yote kadiri ya mahitaji ya Kanisa lake kwa nyakati zote. Tumruhusu Roho Mtakatifu huyu afanye kazi yake, na siyo Roho Mtakavitu. Roho Mtakavitu atalipasua JARIFE-KANISA. Roho Mtakavitu huyu ni: SIFA, CHEO, KUJULIKANA KULIKO BINAFSI, MAMLAKA MBELE ZA WATU, NA MBAYA ZAIDI KWA VIONGOZI WALA RUSHWA. Na kama tulivyoona katika Jumuiya ya kwanza ya Wakristo, uimara wa Kanisa leo unategemea pia kupokeana kwetu, kuchukuliana kwetu, na kutaabikiana kwetu katika hali zote bila kujibakiza. Na mwisho uimara wa Kanisa leo unategemea Nguvu ya Kimaadili kwa kila Mbatizwa na hasa kwa njia ya peke wale wote waliohesabiwa haki na Mama Kanisa kama viongozi wetu wa Kiroho. Hivyo, tusichoke kuhubiri na kuishi kwa vitendo Huruma ya Mungu kwa sababu hata hawa viongozi wala rushwa,  wote wasio na hofu ya Mungu ndani yao, na sisi sote kwa ujumla wetu kama Kanisa na wabatizwa tunahitaji huruma hiyo na wokovu wa Mungu.

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, sehemu ya mwisho ya Injili yetu ya leo, tunaona kukamilishwa kwa yale Kristo aliyoyaanzisha ndani ya  Mtume Petro hasa ule ukiri wake, “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai,” Mt 16:16, ndiyo hayo leo Yesu anataka kujua ukweli wake. Tukumbuke pia kuwa baada ya ukiri ule wa Petro Yesu alihaidi hii kwa Petro,  Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda,” Mt 16:18. Ni wazi, uwepo wa Petro kati ya Mitume wenzake na jumuiya ile ya kwanza ya Wakristo kunampatia nafasi ya pekee katika kutimiza wajibu wake na kutumika kwake. Ni wazi pia nafasi hii ya pekee kwa Petro siyo tokeo la umahiri wake, bali ni neema ya Mungu. Naye Yesu anathibitisha ukweli huu kwa kusema, Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 16:17. Mamlaka haya ya Petro kama Halifa wake Kristo ni Neema ya Mungu mwenyewe. Mbadiliko wa jina Simoni na kuwa Petro, yaani Mwamba, unathibitisha Mtu mpya mwenye jukumu Jipya. Hii ndiyo sababu pia ya Mababa watakatifu kuchagua majina mapya mara baada ya kuhesabiwa haki na Mama Kanisa.

Ni Petro huyu pamoja na ujasiri huu aliounyesha katika ukiri wake juu ya Kristo aliweza kumkana mara tatu Yesu kutokana na hofu ya kuuwawa pamoja na Kristo kifo kile cha aibu cha MSALABA. Leo Yesu anamuuliza mara tatu kama kweli anampenda kama alivyomkana mara tatu. Yesu anamuuliza, “Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu,” Yoh 21:15. Neno ‘kuliko hawa’ linabeba ujumbe mzito sana. Kwa ufupi twaweza kutafsiri hivi, ‘je wanipenda kuliko ulimwengu huu na fahari yake yote?’ Analoulizwa Petro unaulizwa wewe na mimi tuliobatizwa kwa jina lake. Huku pia ni kumkataa shetani na fahari zake zote na mambo yake yote. Msisitizo wa Yesu ni huu; ‘lisha wana-kondoo wangu,’ ‘chunga kondoo zangu,’ na ‘lisha kondoo zangu.’ Msisitizo wa kwanza ni kuwalisha wote walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, Mwa 1:27, bila kutazama utofauti wao kifamili, koo, kabila, utaifa, zangi zao, imani zao, na itikadi zao. Kwa kulitenda hili Petro ndiko kunakomrudishia nguvu yake ile ya kimaadili na kuendelea kusimama kama alama halisi ya Kristo-Upendo, Haki, Amani, Huruma, Msamaha na Unyenyekevu wa kweli. Huu ndio mwaliko wa Mahalifa wote wa Yesu Kristo toka Mtume Petro hadi leo Baba Mtakatifu wetu Fransisco. Pia huu ni wito wa kila Mbatizwa kufanana na Kristo katika kufikiri, kuona, kutenda, kusema, na kuamua. Mtume Petro kama alama halisi ya Kristo ambayo huakisi kwa wote waliomfuata baadaye, na wale wote waliohesabiwa haki katika Kanisa-Makleri, kunawataka kufanana na Kristo kwa mambo makuu matatu kama hatma ya kufika pale alipofika Kristo Yesu:

Moja, ni mwitikio wa kufanana na Kristo kama mchungaji mwema wa kondoo wote mbele ya Mungu na Kristo Mtukuka. Pili, kufanana na Kristo kama sadaka hai na yenye kupendeza katika maana ya sadaka na mtoa sadaka bila kujibakiza. Na tatu, kufanana na Kristo kulipojionyesha wazi kwa upendo wake wa kukubali kufa kifo cha aibu pale Msalabani kwa kukubali kuwa upendo wa wakosefu na wadhambi ili wawe huru. Hili la mwisho ndilo kwa msisitizo Yesu anamkumbusha Mtume Petro na kusema, “Amin, amin, nakuambia, Wakati ulipokuwa kijana, ulikuwa ukijifunga mwenyewe na kwenda utakako; lakini utakapokuwa mzee, utainyosha mikono yako, na mwingine atakufunga na kukuchukua usikotaka,” Yoh 21:18. Kama Kristo alivyojitoa sadaka pale Msalabani, ni kwa namna hiyo hiyo anavyomkumbusha Petro itakavyokuwa kwake. Akasema neno hilo kwa kuonyesha ni kwa mauti gani atakayomtukuza Mungu. Naye akiisha kusema hayo akamwambia, Nifuate,” Yoh 21:19 

Wapendwa wana wa Mungu, Ukulu huu wa Mtakatifu Petro unakipa uzito Kiti hicho katika mamlaka yake kama Yesu mwenyewe asemavyo, Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni,” Mt 16:19. Haya ndiyo mamlaka ya kiti hiki na hasa kwa swala hizi la Huruma ya Mungu kwa ondoleo la dhambi. Hii ndiyo sababu pia ya Baba Mtakatifu kuwa na uwezo na mamlaka ya kuutangaza mwaka huu wa Kanisa kuwa mwaka wa HURUMA YA MUNGU. 

Wapendwa wana wa Mungu, maswali mawili ya mwisho ya Yesu na msisitizo alioutoa Yesu {chunga kondoo zangu, na lisha kondoo zangu}, unalenga katika majukumu na mwonekano wa Ukulu huu ambao ni ule wa kutumika badala ya kutumikiwa. Na Yesu anasema, na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mt 20:27-28. Kiongozi yeyote yule aliyepewa dhamana na kuhesabiwa haki na Kanisa, yampasa kutumika na siyo kutumikiwa. Mtume Petro anasema, lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo,” I Pet 5:2. Ndugu yangu, wewe na mimi tuliye hesabiwa haki na kupewa dhamana na Mama Kanisa, hatupo hapo tulipo kwa maslahi yetu binafsi. Mimi na wewe tupo hapo tulipo kumwakilisha Kristo Yesu aliyetumika badala ya kutumikiwa. Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema,” 1Pet 5:5. Huduma yo yote ile isiyokuwa na taswira ya unyenyekevu kamwe haimwakilishi Kristo. Na kwa namna hiyo hakuna utukufu. Kristo kamwe hajidhihirishi pasipo unyenyekevu. Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka,” 1Pet 5:4. Unyenyekevu katika huduma tuzitoazo utawashangaza wengi na hasa wale ambao  mawazo yao hutanguliza nafsi zao.

Bwana na Bibi Fikiri walibahatika kupata zawadi ya watoto wanne-wawili wa kike na wawili wa mwisho wakiume. Wakiwa wanarejea nyumbani baada ya wiki moja kutokuwepo kutokana na kuwa kwenye Msiba wa Baba Mkwe wake, ambaye ndiye Baba Mzazi wa Bibi Fikiri, kila mmoja alijinunulia tunda alipendalo baada ya kupata chakula cha mchana katika  hoteli ile ambapo Mabus husimama na abiri hupata huduma hiyo.

Bibi Fikiri alinunua machungwa matatu, na Bwana Fikiri alinunua Peasi moja. Wakiwa ndani ya Bus na safari ikiendelea, Bwana Fikiria alichukua Peasi lake na kuanza kulitafuna taratibu. Baada ya masaa manne walifika nyumbani na kwa furaha watoto waliwapokea vizuri kwa sababu waliwakosa kwa muda wa wiki moja.

Basi Bibi Fikiri alimwambia mmoja wa binti yake alete sahani. Bibi Fikiri aliyachukua yale machungwa matatu aliyoyanunu na kuwagawia watoto wake wale wanne kila mmoja nusu kipande. Hivyo likabaki chungwa moja. Mama Fikiri akaagiza binti yake alete maji kwa ajili ya kumnawisha Baba yao. Hivyo Bibi Fikiri alimnawisha mikono mumewe na kulimenya chungwa lile na kumpatia.

Baada ya kula chungwa lile, Bwana Fikiri aliwaza moyoni kwa kutokujali kwake na hasa kuonyesha upendo wa kweli kwa familia na watoto wake. Yeye kama Baba alikula Peasi lake njiani na hakuwa na wazo lolote juu ya Mke wake wala watoto wake.

Bwana Fikiri alimtazama mke wake na kumwambia, “hakika tangu kuzaliwa kwangu, na miaka hii 22 ya ndoa yetu sijawahi kupata somo na fundisho zuri kama ulilonifundisha leo. Nimejiona jinsi nilivyo mtupu. Asante sana Mke wangu.” Basi kwa tabasamu, Mama Fikira alijibu, “Baba Monica nawe umeshaanza! Asante kwa kuliona hilo Mme wangu.”

-Mama Fikiri anatupa mfano mzuri wa kujali na kuwajibika kila mmoja pale alipo na nafasi aliyokuwa nayo kila mmoja kadiri ya wito wake. Huu ndio wajibu wa kila mwenye hofu ya Mungu. Amina

Tumsifu Yesu Kristo!

Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu,” Yoh 21:15


Ee Yesu Mwema na Mchungaji wetu, tukumbushe mara zote kuyaona mahitaji ya wengine na kuwa tayari kufanya chochote kadiri ya hali na nafasi tulizokuwa nazo katika jamii. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario