miércoles, 27 de abril de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 5 YA PASAKA

IJUMAA WIKI YA 5 YA PASAKA
Somo: Mdo 15:22-31
Zab: 57:8-9, 10, 12
Injili: Yoh 15:12-17
Nukuu:
sisi tumeona vema, hali tumepatana kwa moyo mmoja, kuwachagua watu na kuwapeleka kwenu pamoja na wapendwa wetu Barnaba na Paulo,” Mdo 15:25

watu waliohatirisha maisha yao kwa ajili ya jina la Bwana wetu Yesu Kristo,” Mdo 15:26

Basi tumewatuma Yuda na Sila, watakaowaambia wenyewe maneno yayo hayo kwa vinywa vyao,” Mdo 15:27 

Kwa maana ilimpendeza Roho Mtakatifu na sisi, tusiwatwike mzigo ila hayo yaliyo lazima,” Mdo 15:28

yaani, mjiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na nyama zilizosongolewa, na uasherati. Mkijizuia na hayo, mtafanya vema. Wasalamu,” Mdo 15:29

Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi,” Yoh 15:12

Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki,” Yoh 15:13

Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni,” Mdo 15:16

TAFAKARI: Maamuzi na wakaraka wa Mtaguso wa Yerusalemu: “Sisi sote tuna mastahili sawa mbele ya Kristo, yeye ndiye aliyetuchagua bila mastahili yetu ili tuzae matunda ya kudumu.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, “sisi sote tuna mastahili sawa mbele ya Kristo, yeye ndiye aliyetuchagua bila mastahili yetu ili tuzae matunda ya kudumu.” Yakiwa haya ndiyo majumuisho ya Mtaguso wa Yerusalemu, Kristo anatupenda kama tulivyo na kutuhesabia haki mbele zake na mbele ya Mungu Baba bila kujali familia tulizozaliwa, koo tulizotoka, kabila tulizotoka, na hata mataifa tuliyotoka. Hakika, ingekuwa haya niliyoyataja kuwa gizezo cha kuwa Mkristo na hata kuwa Mtumishi katika Kanisa lake KRISTO, bila shaka ingekuwa ndoto leo mimi kuwa kama nilivyo. Ni katika msingi huu nilioutaja (Kristo ametuchagua bila ya mastahili yetu), Mtaguso wa Yerusalema wanaafikiana vyema kuhusu swala la watu wa mataifa waliolipokea neno na kuunda ujumuiya ya Kikristo. Ukristo wetu hautokani na hayo matabaka niliyoyasema hapo juu. Ukristo wetu unatokana na kuhesabiwa haki na Kristo mwenyewe, kulikotokana na kutupenda upeo. Hivyo Mtaguso wa Yerusalemu unatoka tamko lifuatalo, sisi tumeona vema, hali tumepatana kwa moyo mmoja, kuwachagua watu na kuwapeleka kwenu pamoja na wapendwa wetu Barnaba na Paulo,” Mdo 15:25. Mtume Paulo na Barnaba wanachaguliwa kwa vigezo vya maisha yao kupeleka ujume huu kwa wale waliolipokea neno. Ni watu waliohatirisha maisha yao kwa ajili ya jina la Bwana wetu Yesu Kristo,” Mdo 15:26.

Hata hivyo Yuda na Sila ndio watakaosema kwa vinywa vyao juu ya ujembe huo. Basi tumewatuma Yuda na Sila, watakaowaambia wenyewe maneno yayo hayo kwa vinywa vyao,” Mdo 15:27. Yuda na Sila bila shaka ni watu waliokuwa karibu sana na jumuiya hiyo mpya ya Antiokia. Uwakilishi huu ni njia mojawapo ya kuboresha ukaribu wao na jumuiya ya Yerusalemu, na kuanza kuishirikisha jumuiya hii mpya ya Antiokia yale yote yamuhusuyo Kristo. Ukaribu na umoja huu si wakubebeshana mizigo, bali ni fursa ya kuyatafakari makuu ya Mungu na upendo wake kwa kila mmoja aliyeridhia upendo na umoja huo wa Kristo. Roho Mtakatifu ndiye mleta umoja huo. Kwa maana ilimpendeza Roho Mtakatifu na sisi, tusiwatwike mzigo ila hayo yaliyo lazima,” Mdo 15:28.

Hivyo basi, ili kuendelea na umoja huu na upendo huu ndani na katika Kristo, iliwapasa kujitengana na yale ambayo hayakuwa na mwelekeo wa Kimungu. Ni ukweli kwamba kama tunataka kuishi katika Kristo, yatupasa kujikana wenyewe na kumfuata. Yatupasa kuacha yale ya zamani na kuyachuchumilia yale yampendezayo Kristo. Hivyo basi, jumuiya hii mpya ya Antiokia, inapaswa kufanya haya yafuatayo; yaani, mjiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na nyama zilizosongolewa, na uasherati. Mkijizuia na hayo, mtafanya vema. Wasalamu,” Mdo 15:29. Tunapoachana na makandokando haya ya maisha ndipo tunapokuwa karibu na upendo wa Kristo na kutimiza mapenzi yake. Huu ndio upendo anaotutaka Kristo tuuishi kama familia yenye hofu ya Mungu na kuwajibika. Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi,” Yoh 15:12. Ndugu yangu, jambo hili si rahisi! Mimi na wewe leo tupo hiki tulicho kama tokeo la historia yetu tangu kuzaliwa, makuzi yetu ambayo yameathiriwa na mila na desturi zetu, ufahamu wetu ambao umeathiriwa pia na mfumo mzima wa elimu tuliokuwa nao. Katika mazingira hayo ya makuzi, lengo ni kuuona ukweli kama ulivyo, na siyo kuuona ukweli kama tulivyo. Hapa ndipo penye tofauti kubwa ya kusoma na kuelimika. Wote walioelimika wamesoma, ila siyo wote waliosoma wameelimika. Hapa kusoma simaanishi kwenda darasani kama ilivyo ada, bali kuyaelewa vizuri mazingira yanayokuzunguka, ambayo kwa kiasi kukubwa si lazima kwenda darasani kadiri ya mfumo unavyotutaka. Hivyo kwa mazingira ya Kanisa la mwanzo, na changamoto iliyowakabili, Mtaguso ule uliwalazimu kuyaona yote katika upendo wa Kristo na hatma ya upendo huo ambao ni kifo kile cha Msalaba.

Upendo huu miongoni mwetu wenye taswira ya Kristo mwenyewe, ni upendo unaoitaji kujitoa sadaka kwa wengine. Kupenda kama Kristo alivyotupenda kunatudai kujitoa sadaka kwa wale tunaoishi nao kila siku. Upendo usiojitoa sadaka bado hujafikia ukomavu wake. Yanipasa kujisikia furaha tena na tena ninapojitoa sadaka kwenye familia yangu, jumuiya yangu ya kitawa, jumuiya yangu ndogo ndogo ya Kikristo, na hata Kanisa langu ninaposali na kumsifu Mungu. Yesu anatuambia, Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki,” Yoh 15:13. Hili Yesu kalifanya kwa vitendo. Hatua hii ya upendo ni ukomavu katika maisha ya Kiroho. Mimi na wewe iwe changamoto yetu ya kudumu.

Ndugu yangu, tunayafanya haya yote si kwa vile sisi ni mashujaa wa kufanya hivyo. La hasha! Tunafanya hayo yote kwa sababu  yupo ambaye kabla ya sisi kuyafanya hayo kesha yafanya na anaendela kuyafanya ndani mwetu kwa  nguvu na neema zake. Mtu huyu ni Kristo mwenyewe. Unapoona unatenda jambo jema na watu wakaliitikia kwa moyo wa upendo, elewa jambo hilo linamkono wa Kristo ndani yake. Wewe na mimi katika tendo hili tutakuwa tumetumika vizuri kama watumishi waliofanya vyema yale waliopaswa kuyafanya. Hivyo katika kweli hii, Yesu natuambia, Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni,” Mdo 15:16. Hakika matunda yanayotokana na kutumika vyema kwa nguvu na neema za Mungu, hudumu daima hata kama kwa wakati ule sisi hatutakuwepo kushuhudia ukweli huo. Hivyo mara zote tujione hivi: Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya,” Lk 17:10 

Ndugu yangu usiache kutenda mema hata kama kwa hali ya ubinadamu wako unakatishwa tamaa kufanya hivyo. Uhalisi wa wema huo ni Mungu mwenyewe.

Tumsifu Yesu Kristo.

Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni,” Mdo 15:16


Tusali:- Ee Yesu wangu na yote kwangu, nitumie vyema kama chombo chako kisicho na faida. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario