JUMAPILI
YA 4 YA PASAKA YA MWAKA-C
MCHUNGAJI
MWEMA
Somo
I: Mdo 13:14, 43-52
Zab:
100:1-2, 3, 5
Somo
II: Ufu7:9, 14b-17
Injili:
Yoh 10:27-30
Nukuu:
“Sinagogi
ilipofumukana, Wayahudi na waongofu watauwa wengi wakashikamana na Paulo na
Barnaba; ambao, wakisema nao, wakawatia moyo kudumu katika neema ya Mungu,” Mdo
13:43
“Bali
Wayahudi, walipowaona makutano, wakajaa wivu, wakayakanusha maneno yaliyonenwa na
Paulo, wakibisha na kutukana,” Mdo 13:45
“Baada ya hayo
nikaona, na tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu,
watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile
kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya
mitende mikononi mwao,” Ufu 7:9
“Kwa maana huyo
Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kiti cha enzi, atawachunga, naye atawaongoza
kwenye chemchemi za maji yenye uhai, na Mungu atayafuta machozi yote katika
macho yao,” Ufu 7:17
“Kondoo
wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata,” Yoh 10:27
“Nami
nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya
katika mkono wangu,” Yoh 10:28
TAFAKARI:
“Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa
uzima wa milele.”
Wapendwa
wana wa Mungu, leo Mama Kanisa
anaadhimisha Dominika ya nne ya Pasaka ya Mwaka “C” wa Kanisa. Dominika hii ya
nne kadiri ya Mpango wa Kiliturjia, na inavyojionyesha yenyewe katika tafakari
nzima ya masomo ya leo, hujulikana kama “Dominika ya Mchungaji Mwema.” Yesu
Kristo ndiye Mchungaji wetu Mwema kwani ni kwake tu kunaweza kuupata Uzima huo
na kuufikia Umilele huo kama anavyosema, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila
kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Hivyo kwa ukweli huu, sisi wenyewe bila Kristo
Yesu hataweza kufanya lolote. Yesu anaweka bayana kweli hii anapojifananisha na
Mzabibu. Naye anasema, “Mimi
ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa
sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote,” Yoh 15:5. Hivyo
tunapoadhimisha Dominika hii ya Mchungaji mwema ni vyema kuelewa kweli hiyo
kuhusu Yesu Kristo.
Yesu
Kristo Mchungaji Mwema na Baba mwenye ukamilifu wa Ubaba wa Mungu Baba, ni
kwake tu tunapoweza kupata ukamilifu wa Tumaini la kweli, Imani dhabiti, na
Upendo wa kweli. Kwa mafundisho yake, kuishi kwake, na kuutoa uhai wake kwaajili
yako na yangu angali hapa duniani, amethibitisha pasipo shaka yoyote hayo mambo
makuu matatu: Imani, Tumaini, na Upendo. Mimi na wewe kila mmoja kadiri ya wito
wake, vipaji vyake, na nafasi yake katika jamii husika anayoishi ni wajibu
wangu kama Mkristo na Mfuasi wa Kristo kuishi kweli hii; “Kuwa Mchungaji Mwema
kama alivyokuwa Kristo Yesu.” Kuwa kama Kristo-Mchungaji Mwema ni kuishi
ukilenga Utukufu ukijua wazi kabla ya taji hilo la Utukufu kuna Msalaba. Huu
ndio mwito wa somo letu la kwanza na la pili.
Wapendwa
wana wa Mungu, kinachowatokea Paulo na Barnaba huko Perge hakina tofauti na
kile kilichomtokea Yesu huko Nazareti
siku ya Sabato katika sinagogi alipopewa chuo cha Nabii Isaya na kulisoma neno
ambalo ndilo lililokuwa mpango kazi wake hapa duniani, Lk 4:16-21. Yesu
alitangaza mpango kazi waka na kusema, “Roho
wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari
njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona
tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na
kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa. Akaanza
kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:18-19, 21. Neno hili halikupokelewa kwa furaha, na hasa
kwa Wayahudi waliokuwa na msimamo makali juu ya Masiha yule waliyekuwa
wakimngoja. Fikra na mategemeo yao ilikuwa kuja kwa Masiha ambaye kwa kiasi
kikubwa alibeba taswira ya kisiasa-kuwatoa katika utawala ule wa Kirumi. Hivyo baada ya Yesu kuutoa mpango kazi wake,
“Akakifunga chuo, akamrudishia mtumishi, akaketi; na watu wote waliokuwamo
katika sinagogi wakamkazia macho,” Lk 4:20. Kumkazia macho huku Yesu
kulidhihirisha wazi hawakuwa tayari kuupokea ujumbe ule.
Mtume Paulo na Barnaba
huko Perge wanapatwa na maswahiba hayo hayo wakiwa kwenye sinagogi. Licha ya
kwamba sinagogi lilifurika watu na kupokelewa vizuri na wenyeji (Mchanganyiko
wa Wayahudi na wasio wayahudi), Wayahudi hawakufurahiswa na habari njema ile
waliyoitangaza, Mdo 13:43. “Bali Wayahudi,
walipowaona makutano, wakajaa wivu, wakayakanusha maneno yaliyonenwa na Paulo,
wakibisha na kutukana,” Mdo 13:45. Licha ya vurugu na vitisho hivi vya
Wayahudi, Paulo na Barnaba waliutazama Utukufu uliokuwa mbele yao ilhali
wakijua pia kuna Msalaba kama alama ya Ushindi. Ni kwa mantiki hii, “Paulo
na Barnaba wakanena kwa ushujaa wakasema, Ilikuwa lazima neno la Mungu linenwe
kwenu kwanza; lakini kwa kuwa mnalisukumia mbali, na kujiona nafsi zenu kuwa
hamkustahili uzima wa milele, angalieni, twawageukia Mataifa,” Mdo 13:46. Kwa
tendo hili la Paulo na Barnaba wanatambua ni wajibu wao kufuata njia ile ya
Mchungaji wetu Mwema-Yesu Kristo.
Kutokuupokea ujumbe huu
wa habari njema kwa Wayahudi haikuwa sababu ya wao (Paulo na Barnaba) kukaa
kimya. Hapa Paulo na Barnaba wanakumbuka na kutukumbusha pia mafundisho ya Yesu aliposema, “Na
mtu asipowakaribisha wala kuyasikiliza maneno yenu, mtokapo katika nyumba ile,
au mji ule, kung'uteni mavumbi ya miguuni mwenu. Amin, nawaambia, itakuwa rahisi nchi
ya Sodoma na Gomora kustahimili adhabu ya siku ya hukumu, kuliko mji ule,” Mt
10:14-15. Na hiki ndicho kilichotokea baada ya Wayahudi wa Perge kukataa habari
njema ya wokovu na kuleta ufitini juu ya Paulo na Barnaba: “Lakini Wayahudi wakawafitinisha wanawake watauwa
wenye cheo na wakuu wa mji, wakawataharakisha watu wawaudhi Paulo na Barnaba;
wakawatoa katika mipaka yao. Nao wakawakung'utia mavumbi ya miguu yao, wakaenda
Ikonio,” Mdo 13:50-5. Hakika kumpiga
teke chura siyo kukatiza safari yake bali kumwongezea mwendo! Na mti wenye
matunda ndio upigwao mawe!
Hujuma wanazozipata Paulo na Barnaba
zinakuwa chachu ya kusonga mbele na kulihubiri Neno la Uzima. “Kwa sababu ndivyo
tulivyoamriwa na Bwana, Nimekuweka uwe nuru ya Mataifa, Upate kuwa wokovu hata
mwisho wa dunia,” Mdo 13:47. Agizo hili
la kufikisha habari njema hata mwisho wa dunia ni kwa kila Mbatizwa. Na hii
ndiyo ajenda mzito na mahususi Yesu aliyowaachia wanafunzi na Kanisa kwa upana
wake kabla ya kupaa mbinguni akisema, “Enendeni
ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka;
asiyeamini, atahukumiwa,” Mk 16:15-16. Ujumbe huu mahususi wa Ufalme wa Mungu, unaambatana
na hukumu kwa Yule asiyeamini. Wajibu wangu na wako, yaani wewe uliyebatizwa,
na Kanisa kwa ujumla wake, ni kulihubiri na kuliishi neno la Mungu bila kukoma.
Mwijili Mathayo kalihusisha tendo hili la
kuhubiri neno na ufalme wa Mungu na Sakramenti ya Ubatizo. Maana yake, siyo tu
kulihubiri neno la Mungu, bali na kuwavuta watu kwa Mungu na kuuonja upendo na
furaha hiyo. "Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa
wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na
kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi" Mt 28:19-20. Paulo na
Barnaba wanaitendea haki ajenda hii nzito na muhimu.
Wapendwa katika Kristo,
“uzuri ni gharama, na penye utaratibu kuna akili.” Mimi na Wewe leo kwa
kumwamini Kristo na kumfuata kila siku itukumbushe kuwa tumekombolewa kwa
gharama kubwa sana-Damu ya Mwanakondoo, Yesu Kristo. “Nanyi mfahamu
kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate
kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya
thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,”
1Pet 1:18-19. Ndugu yangu tunayesafari sote katika tafakari hii, ni wazi kwamba
usichokijua thamani yake wakati mwingine ni vigumu kukithamini. Ni heshima
kubwa sana tuliyopewa Mimi na Wewe kwa tendo la Yesu Kutufia pale Msalabani. Ni
upendo mkubwa sana kwetu. Tendo hili kubwa na la upendo limeusadifu mwenendo
mzima wa Yesu Mchungaji Mwema. Hivyo kuwa Mchungaji Mwema ni kwenda ndani
kabisa ya maisha ya Kondoo zako kwa lengo la kuwainua na kuiona nuru ile
uliyonayo. Kweli hii kaifanya Kristo Yesu pasipo shaka yoyote. “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo,
jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba
ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Hii ndiyo taswira ya
Mchungaji Mwema ambaye kila Mbatizwa kadiri ya wito na maisha yake apaswa
kuishi pale alipo.
Mimi na Wewe tunapoishi
hapa duniani kama sehemu ya maandalizi ya maisha ya umilele, na kuufia ukweli
huu kama Kristo, tu mashahidi mbele ya Mwanakondoo katika maisha ya umilele
naye Mbinguni. Huu ndio ufunuo wa Yohana kadiri ya somo letu la pili leo. “Baada ya hayo nikaona, na tazama, mkutano mkubwa
sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na
jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za
Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao,”
Ufu 7:9. Hawa ndio wale watakao fahamika kwa
mavazi yao meupe, yaani, utakatifu wao. Ni katika dhiki na taabu bila kupoteza
Imani, Matumaini, na Upendo kwa ajili ya Kristo-Mwanakondoo aliye hai tunaoshwa
kwa damu yake Takatifu na kuhesabiwa haki kama wateule wake na warithi wake.
Yohana anaambiwa katika maono yale kwamba, “Hao
ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya
meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” Ufu 7:14b
Tunayo kazi moja tuu
mara ya kuushinda ulimwengu huu, yaani, kumtumikia Mungu mchana na usiku katika
hekalu lake. Hawa ndio wale watakao hesabiwa haki baada ya kuushinda ulimwengu
huu. “Kwa hiyo wako mbele ya kiti cha enzi
cha Mungu, nao wanamtumikia mchana na usiku katika hekalu lake, na yeye aketiye
katika kiti cha enzi atatanda hema yake juu yao,” Ufu 7:15. Hali yetu ya
kuchoka hatutakua nayo tena kwa sababu tutakuwa na miili tukuka na takatifuzwa.
Hivyo walio na miili hiyo “Hawataona njaa tena, wala hawataona kiu tena,
wala jua halitawapiga, wala hari iliyo yote,” Ufu 7:16. Mchungaji wa kundi hili
la watukuka na watakatifuzwa ni Mwana-Kondoo katika kiti chake cha enzi na cha
Utukufu. “Kwa maana huyo Mwana-Kondoo,
aliye katikati ya kiti cha enzi, atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi
za maji yenye uhai, na Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao,” Ufu 7:17.
Ni raha iliyoje kuwa ndani na katika Kristo nyakati na majira yote licha ya
taabu na dhiki tunazokutana nazo kila siku?
Wapendwa wana wa Mungu,
furaha tunayoitegemea kutoka kwa Kristo ni tokeo la kuisikia sauti yake. Zipo
sauti nyingi sana tuzisikiazo kila mmoja kadiri ya wito na mazingira yake. Ni
mara ngapi umekatishwa tamaa hapo ulipo kwa kusikiliza sauti nyingine na siyo
ya Kristo Mchunguji wetu Mwema? Yesu anakuambia leo wewe na mimi, kwamba, “Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua,
nao wanifuata,” Yoh 10:27. Je, unaiheshimu sauti yako ya ndani, yaani, dhamiri
yako njema? Dhamiri njema ndiyo mwito wa Yesu pia ndani yako. Dhamiri hii njema
utuongoza kwa yaliyomema (kuyatenda) ili kuifikia ile mede ya dhahabu-uzima wa
milele katika Kristo Yesu, Flp 3:14. Hivyo, Kristo tu ndiye mwenye uwezo wa
kutupatia uzima huo wa milele. Naye anasema, “Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea
kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu,” Yoh 10:28. Bila
Kristo usalama wetu upo matatani. Ila ndani na katika Kristo tunauhakika wa
kila kitu na hatuna cha kupoteza.
Ndugu yangu, yale yote
yanayokupa matumaini hapa duniani kwayo bila Kristo hayana umilele. Yesu anatupa hakikisho la matumaini ya
kweli na kusema, “Baba yangu aliyenipa hao
ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba
yangu. Mimi na Baba tu umoja,” Yoh 10:29-30.
Ndugu yangu, vyote uvionavyo na usivyoviona kwa macho haya ya kibinadamu vipo
kama vilivyo kwa sababu ya Neno, yaani Yesu Kristo. “Hapo mwanzo
kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo
mwanzo alikuwako kwa Mungu.Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye
hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:1-3. Ndugu yangu, kilicho chako na
mali yako ni kipi zaidi ya dhambi zako?
Padre Joseph Nalia na
Mungu baada ya upadirisho wake alitumwa na Askofu wake uchungaji eneo la
wafugaji. Mazingira ya eneo lile yalikuwa makame sana. Mifugo ilikuwa mingi
ukilinganisha na idadi ya watu. Hata hivyo watu walionekana wanyonge na
wadhaifu sana licha ya wingi wa ng’ombe, kondoo na mbuzi walikuwa nao.
Padre Nalia na Mungu
Joseph, alihuzunishwa sana na hali za waamini wake, na hasa kutokufika Kanisani
kusali na kupata Katekesi ya kina. Alipofanya tafakari kwa nini waamini wake
wapo kama walivyo, lilimjia wazo la kuwatembelea na kujua hali zao. Padre
Joseph alianza kutembelea kaya baada ya kaya. Baada ya mwaka mmoja kutokana na
ukubwa wa Parokia ile alifanikiwa kuwatembelea waamini wake wote.
Padre Joseph Nalia na
Mungu alijifunza mambo mengi sana. Baadhi ya mambo hayo ni kama haya yafuatayo:
Moja, wengi wa waamini
wake wanakosa muda wa kufika Kanisani kwa katekesi na Misa kutokana na kutumia
muda mwingi kutafuta malisho ya mifungo yao.
Pili, aligundua familia
nyingi ni dhaifu kiafya kutokana na kutokula mlo kamili, na mara nyingine kula
mlo mmoja tu kwa siku.
Tatu, Padre Nalia na
Mungu aligundua ukame ule kwa kiasi kikubwa ulisababishwa na wingi wa mifugo.
Nne, wingi wa mifugo
ile haukuweza kubadili hali za maisha ya waamini wake: Kimwili na Kiroho. Ili
kuwa ni sehemu ya sifa tu kwa mtu kuwa na ng’ombe nyingi na kumfanya kuwa na
uwezo wa kuoa wanawake wengi.
Na tano, Padre Joseph
aligundua kwamba karibia asilimia 96 ya waamini wake ni washirikina na wenye
kuamini imani potofu.
Kwa kutambua matatizo
hayo Padre Joseph alifanya yafuatayo: Kwanza aliongea na viongozi wa vijiji vyote
vya Parokia ile na kuwaomba wawakutanishe watu wao wote siku ya jumamosi kwani
kutakuwa na mganga maarufu. Kwa vile waliamini sana ushirikina hakuna aliyekosa
kikao kile.
Wakiwa wamekwisha
kupanga yote na Mseminari aliyekuja Parokiani pale kwa uchungaji namna
watakavyofanya, Mseminari yule alijitambulisha kwenye kikao kile kama yeye
ndiye Mganga Mashuhuri-“Mti Mkavu.” Lengo la ujio wake ni kutengeneza mvua ili
kusiwe tena na tatizo la majani kwa ajili ya mifungo.
Basi Mseminari yule akiwa
amevalia mavazi ya kutisha na sasa kama Mganga Mti Mkavu, alitabiri huku akitoa
sauti ya kutisha, “vijiji hivi vinamatatizo sana kwa sababu mmekwenda kinyume
na mizimu ya Mababu zenu. Kurudisha amani katika vijiji hivi kuanzia sana kila
familia lazima itoe ng’ombe wasiopungua 10, na mbuzi wasiopungua 15. Ng’ombe na
mbuzi hawa watakuwa wanachinjwa kutokana na mahitaji ya kila kijiji. Ngozi za
wanyama hao zitawambwa na kutengeneza wigo kubwa ili kupunguza kasi ya upepo
kwa sababu kwenye upepo huo ndiko kwenye mizumu hiyo inayoleta fujo.”
Watu wote walikaa kimya
kwa hofu juu ya utabiri ule. Hivyo siku iliyofuata ng’ombe na mbuzi waliletwa
parokiani pale kwa wingi. Kila kijiji kiliteua wazee watano kwa ajili ya
kuchinja na kugawa nyama kwa kila kaya. Baada ya miezi mitatu afya za watu
zilibadilika. Na baada ya miezi mitatu baadaye, idadi kubwa ya mifugo ilipungua
na kuwafanya wakazi wale kutumia muda mwingine kwa kazi za kilimo kilichozunguka
maeneo yao. Kwa vile ilikuwa kipindi cha kilimo, mvua zilianza kunyesha na hali
ilibadilika.
Watoto na baadhi ya
watu wazima walipata muda wa kwenda mafundisho na hata kuudhuria misa kila
jumapili kwa sababu kila familia ilikuwa
na mifugo michache. Padre Joseph aliwaleta wataalam wa kilimo na kutoa
elimu kuhusu kilimo cha kisasa na ufugaji wa kisasa. Baada ya miaka mitatu
mambo yalibadilika kabisa. Afya za watu zilikua nzuri, na wengi waliachana na
Imani potofu kwa katekesi ile aliyoitoa Padre Nalia na Mungu ya nyumba kwa
nyumba.
Ndugu yangu, tujifunze
kwa Padre Joseph Nalia na Mungu. Nawe pia ni Mchungaji mwema pale ulipo kadiri
ya wito wako na mazingira yako ya kazi.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nami
nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya
katika mkono wangu,” Yoh 10:28
Tusali:-Ee Yesu Mchungaji wetu Mwema, tujalie Neema
ya kutumika bila kujibakiza kila mmoja kadiri ya wito wake ili Wewe uonekane
kwa kila tutakaye muhudumia kama Baba na Mchungaji mwema ukiwa Wewe ndiye
kielelezo chetu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario