lunes, 11 de abril de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 3 YA PASAKA

JUMATANO WIKI YA 3 YA PASAKA
Somo: Mdo 8:1-8
Zab: 66:1-3a, 4-5, 6-7a
Injili: Yoh 6:35-40
Nukuu:
Siku ile kukatukia adha kuu ya kanisa lililokuwa katika Yerusalemu; wote wakatawanyika katika nchi ya Uyahudi na Samaria, isipokuwa hao mitume,” Mdo 8:1

Lakini wale waliotawanyika wakaenda huko na huko wakilihubiri neno,” Mdo 8:4 

Kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete, wakaponywa,” Mdo 8:7

Lakini naliwaambia ya kwamba mmeniona wala hamwamini,” Yoh 6:36 

Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe,” Yoh 6:37 

Na mapenzi yake aliyenipeleka ni haya, ya kwamba katika wote alionipa nisimpoteze hata mmoja, bali nimfufue siku ya mwisho,” Yoh 6:39

TAFAKARI: “Kwa Yesu Kristo kuna uzima na ufufuo siku ya mwisho; Je, umewekeza wapi maisha yako?”

Wapendwa wana wa Mungu, ni kweli pasipo shaka yoyote kwamba kila mmoja wetu kuna kitu ambacho kinaongoza na kuyasukuma maisha yake. Kitu hicho ndiyo dira na sababu ya mtu kufanya afanyavyo na kuishi aishivyo. Msukumo huo ndiyo unaotufanya kama tulivyo. Msukumo huyo ndio unaotupa furaha na matumaini kwa yale tunayoyatarajia. Msukumo huo wa maisha ndio unaotupa moyo wa kuendelea kufanya tunayoyafanya. Na kwa upende mwingine, msukumo huo wa maisha huwa sababu ya huzuni yetu ya kudumu.

Hivyo ndugu yangu tunayesafiri pamoja katika tafakari hii, kwa namna ya pekee leo tulitafakari neno hili, “Kwa Yesu Kristo kuna uzima na ufufuo siku ya mwisho; Je, umewekeza wapi maisha yako?” Mtume Paulo anasema jambo hili kuonyesha kile kinachosukuma maisha yake. “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1. Huu ndiyo msukumo sahihi wa maisha yetu ya ufufuko, maisha mapya na Kristo. Ni maisha ya kuutafuta ufalmwe wa Mungu kwa yale yote tuyafanyayo. Ni kumwona Kristo kwa kila unayekutana naye, ishi naye, na kuwajibika kwako kwao kadiri ya wito wako, nafasi yako, na vipaji na uwezo aliokujalia Mungu.

Wapendwa wana wa Mungu, msukumo huu wa maisha ndiyo sababu ya kifo dini na shahidi cha Stefano. Jumuiya ya kwanza ya Wakristo inahujumiwa na Sauli na kutawanyika. Mitume wakisukumwa na Kristo aliye sababu ya maisha yao, na Roho Mtakatifu, wanabaki Yerusalemu wakitoa ushuhuda wa Kristo hadi toni la mwisho licha ya machafuko yaliyotokea kwa sababu ya kifo cha Shahidi Stefano. Siku ile kukatukia adha kuu ya Kanisa lililokuwa katika Yerusalemu; wote wakatawanyika katika nchi ya Uyahudi na Samaria, isipokuwa hao Mitume,” Mdo 8:1. Hata wale waliotawanyika kutokana na hujuma hii, hawakukoma kulitangaza na kulihubiri jina hili lililopita majina yote, Yesu Kristo Mnazareti. Lakini wale waliotawanyika wakaenda huko na huko wakilihubiri neno,” Mdo 8:4. Miongoni mwa watu hawa ni Filipo.

Filipo analihubiri Jina la Yesu na wengi wanaona mwanga, kweli, na uzima kwa kuponywa na kuwa huru. Kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete, wakaponywa,” Mdo 8:7. Haya ndiyo mambo makuu ya Mungu kwa wale wanao mwamini na kumtegemea. Haya ndiyo mambo makuu Mungu huyafanya kwa wale wasiokuwa na shaka naye na uwezo wake. Mungu huyatenda makuu hayo kwa wale wasiokatishwa tamaa na vipingamizi dhidi ya kile wanachoamini.

Wapendwa katika Kristo, ndani na katika Kristo kuna uzima na ufufuo siku ya mwisho. Maisha ya kweli na Kristo, ndiyo njia sahihi ya kuufikia umilele ambao ndiyo makusudi ya uumbaji wetu. Kazi kubwa ya Kristo ni kuhakikisha walio mridhia hawapotei hata mmoja. Ulizi ndani ya Kristo ni salama kuliko linzi nyingine zote unazoweza kufikiria. Ni ulinzi, si tu katika usalama wa miili yetu na mali zetu, ila roho zetu katika hali ya ufufuo na uzima wa milele. Naye Yesu anatuhakikishia jambo hili na kusema, Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe,” Yoh 6:37. Ndugu yangu maisha yako umeyawekeza kwa nani? Je, kwenye utajiri wako? Je, kwa marafiki zako? Je, akili na ujanja wako? Je, katika maisha yako ya kijanja kijanja? Je, kwenye kadi zako za benk ya “life security?” Yote hayo utayaacha na kuondoka na Roho yako tu. Je, mbele ya Mungu utajitetea na nini? Njia salama ni kuwekeza kwa Kristo kupitia Benk yake-“ROHO YAKO”

Mpendwa tuliyeanza safari hii ya tafakari pamoja upoooo? Hivi unajua mapenzi ya Mungu kupitia mwanaye Yesu Kristo? Ndugu yangu, mapenzi yake Mungu kwako kupitia mwanaye Mpenzi ni kukupatia uzima wa milele na ufufuo siku ya mwisho bure. Nasema bure kwa sababu huitajiki kuununu ila kuuridhia kila siku ya maisha yako. Naye Yesu anasema, Na mapenzi yake aliyenipeleka ni haya, ya kwamba katika wote alionipa nisimpoteze hata mmoja, bali nimfufue siku ya mwisho,” Yoh 6:39.

Ndugu yangu kabla sijakuacha, jaribu kuchunguza jambo hili. Je, ni kitu gani kwa siku kinachukua muda mwingi kwako? Kitu hicho ndicho kinachochukua uhai wako, na mwisho wa siku ndicho kitakachokuwa hatima ya maisha yako. Kitu hicho ndicho kibebacho Imani yako mbele ya Mungu. Swali la kujiuliza ni hili; Je, kitu hicho kinauhusiano wowote wa karibu na Kristo? Kama hakina, umejipanga vipi kujibu maswali haya mawili mbele ya Mungu: Swali la kwanza:-Umefanya nini na upendo wa Mwanangu Mpenzi Yesu Kristo aliyekufa kifo cha aibu pale Msalabani kwa ajili yako? Na swali la pili na la mwisho: Umefanya nini na vipaji nilivyokupa bure? Yesu Kristo anasema hivi, “Kwa kuwa mapenzi yake Baba yangu ni haya, ya kwamba kila amtazamaye Mwana na kumwamini yeye, awe na uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho,”Yoh 6:40. Kristo keshafanya nafasi yake, wewe na mimi je?

Tumsifu Yesu Kristo!

Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe,” Yoh 6:37

Ee Yesu uliye yote katika yote, yatengeneze maisha yangu kadiri ya msukumo wako kila siku kwa kila nifanyacho. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario