lunes, 4 de abril de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 2 YA PASAKA

JUMANNE YA WIKI YA 2 YA PASAKA
Somo: Mdo 4:32-37
Zab: 93: 1ab, 1cd-2, 5
Injili: Yoh 3:7b-15
Nukuu:
Na jamii ya watu walioamini walikuwa na moyo mmoja na roho moja; wala hapana mmoja aliyesema ya kuwa kitu cho chote alicho nacho ni mali yake mwenyewe; bali walikuwa na vitu vyote shirika,” Mdo 4:32

Wala hapakuwa na mtu mmoja miongoni mwao mwenye mahitaji; kwa sababu watu wote waliokuwa na viwanja au nyumba waliviuza, wakaileta thamani ya vitu vile vilivyouzwa, wakaiweka miguuni pa mitume; kila mtu akagawiwa kwa kadiri ya alivyohitaji,” Mdo 4:34-35

“Amin, amin, nakuambia kwamba, Lile tulijualo twalinena, na lile tuliloliona twalishuhudia; wala ushuhuda wetu hamwukubali.” Yoh 3:11

Wala hakuna mtu aliyepaa mbinguni, ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni, yaani, Mwana wa Adamu,” Yoh 3:13

Na kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani, vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa; ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele katika yeye,” Yoh 3:14-15 

TAFAKARI: “Jumuiya yenye moyo moja na roho moja, husafiri pamoja na hutoa shuhuda iliyokweli kweli daima.”

Wapendwa wana wa Mungu, ni kweli iliyo wazi kwamba mafanikio ya jumuiya ya kwanza za Wakristo yalijijenga katika msingi wa upendo wa kindugu ulio wa wazi, na malengo yaliyo wazi na kweli kumwelekea Mungu. Jambo hili liliwafanya kushuhudia kweli kwani maisha yao yaliakisi maisha ya jumuiya yaliyo halisi.

Moyo mmoja na roho moja katika maisha ya jumuiya yoyote ile, ubebwa na mizania ya uaminifu na uwazi. Kunapokuwa na uwazi na uaminifu, hata mali aliyokuwa nayo mtu, haiwezi kuwa kikwazo katika kushirikishana. Undugu ulio wa kweli na wawazi hujengwa kwa uaminifu na upendo wa kweli. Undugu huu huwa imara kuliko ule wa kuzaliwa. Undugu wa kuzaliwa hukosa mshikamano kwa kuingiliwa na mazoea ya kujihesabia haki. Ila endapo undugu huu wa kuzaliwa ukizingatia ukweli ulio uwazi, mshikamano wa kweli, na uaminifu, undugu huu huwa imara sana. Kwa bahati mbaya uzoefu waonyesha mambo hayawi hivyo, kwa sababu tu ya kujihesabia haki kama mwanafamilia.

Umoja huu ujenga ushirika wa kudumu na wenye nia moja. “Na jamii ya watu walioamini walikuwa na moyo mmoja na roho moja; wala hapana mmoja aliyesema ya kuwa kitu cho chote alicho nacho ni mali yake mwenyewe; bali walikuwa na vitu vyote shirika,” Mdo 4:32. Ni katika mtazamo huu na uelewa huu, Mt. Augustino anaijenga jumuiya yake ya kitawa kwa mfano wa jumuiya ya kwanza ya Wakristo. Undugu huu wa Kiagustino umedumu hadi sasa.

Ndugu yangu, umoja wa moyo mmoja na roho moja, uliondoa ubinafsi wa kujilimbikizia mali kwani aliyeitaji alipata kadiri ya mahitaji yake. Na wale ambao walijiunga katika jumuiya hii yenye kushirikishana mambo ya kimwili na kiroho, walijisikia furaha na kumshuhudia Mungu wa kweli. Mungu huyu alionekana kwa kila kitu walichofanya, na kwa kila kitu walichoshirikishana. Kwa mantiki hii, wala hapakuwa na mtu mmoja miongoni mwao mwenye mahitaji; kwa sababu watu wote waliokuwa na viwanja au nyumba waliviuza, wakaileta thamani ya vitu vile vilivyouzwa, wakaiweka miguuni pa mitume; kila mtu akagawiwa kwa kadiri ya alivyohitaji,” Mdo 4:34-35.

Msimamo huu, na dira hii ya maisha, iliwafanya wanajumuiya hii kuwa kitu kimoja na hasa katika swala la ushuhuda. Hakuna aliyejibwatukia lililo lake. Kila kilichosemwa kilisemwa na kuongozwa na Roho wa Bwana. Utulivu huu na mwelekeo huu wa kimtazamo uliwafanya wanajumuiya wajue ni nani mwenye mamlaka ya kweli na wakufikika kwa urahisi. Mitume walikuwa viongozi na waelekezaji wa ushuhuda ulio kweli. Kitu hiki kilionekana wazi kwa wale waliokuwa chini yao. Hivyo vitu vyote vilikuwa chini ya uongozi na usimamizi wa mitumu, Mdo 4:35.

Wapendwa wana wa Mungu, hakuna aliyejiona bora kuliko mwingine, na wala muhimu kuliko mwingine. Kila mmoja alijitoa kwa ajili ya jumuiya na maendeleo ya jumuiya. Uzuri au ubora wa mtu ulikuwa ni ufunuo wa uzuri wa Mungu na uumbaji wake. Tunachojifunza hapa ni kwamba, uzuri, utajiri, hekima, akili, na vipaji vilionekana na ndivyo ilivyo, kwamba ni ufunuo wa Mungu na uzuri wake kwa vile alivyoviumba. Kwa maana nyingine, mali yetu halali ni dhambi zetu, ambazo mara tunapotambua udhaifu na mapungufu haya, yatupasa kupatanishwa na Mungu. Tendo hili kwa Mkristo yeyote wenye hofu ya Mungu, ni tendo la kufanya kila mara tukitambua kwamba Neema na Huruma ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu.

Wapendwa katika Kristo, kutokuishi kweli hii kama Wakristo, bado hatujamfahamu Kristo, na kama tunamfahamu kwa kuzaliwa katika familia ya wakristo, basi bado tupo kwenye mazoea na tunayo safari ndefu kiimani kweli ambayo itatuweka huru, Yoh 8:32, 36. Kwa naana hiyo hatuwezi kuyasema maneno haya ya Yesu, “Lile tulijualo twalinena, na lile tuliloliona twalishuhudia; wala ushuhuda wetu hamwukubali.” Yoh 3:11. Kama hatumjui vizuri Kristo twawezaje kumshuhudia? Yawezekana hatuna uwezo wa kuyasema kwa ufasaha, je maisha yetu yanafunua ukweli huu wa Kristo ndani yetu? Ni changamoto kubwa!

Wapendwa, tukimjua Kristo na kufuata mafundisho yake, tutafunuliwa yale ya mbinguni kwani yeye anayajua kwa sababu ametoka huko na Baba anamfunulia nyakati zote. Wala hakuna mtu aliyepaa mbinguni, ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni, yaani, Mwana wa Adamu,” Yoh 3:13. Kufahamu ukweli huu, ni tendo la kuwa tayari kila siku wanafunzi wa Kristo, yaani kujifunza kusiko kuwa na kikomo. Mtume Paulo anasema, “ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda nena moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu,” Flp 3:13-14. Kweli juu ya Kristo ni maisha mazima ya kila siku ya Mkristo, yakiambatana na tafakari juu ya yote tunayokutana nayo katika maisha ikiwa ni pamoja na majaribu yake. Kumbe hata katika majaribu yetu ya maisha tunafunuliwa ukweli ambao Mungu anataka tuujue ili nasi kesho tuwe walimu kwa wale watakao kuwa na mahangaiko na mateso kama yetu. Majaribu hutufanya kukua na kukomaa kiimani. Tusitangulize lawama na malalamiko hata mara moja; “kwa nini mimi haya yanatokea kwangu,” bali tujiulize Mungu anataka kunifundisha nini katika majaribu haya.

Tunapokubali majaribu tuyapatayo huwa tunafunuliwa kweli iliyo juu ya upeo wetu kama binadamu. Tendo hili kama binadamu utuwezesha kuinuliwa kama Kristo alivyoinuliwa msalabani na kuuvaa Utukufu uliotukuka. Na kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani, vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa; ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele katika yeye,” Yoh 3:14-15. Ndugu yangu tendo hili ni la Imani na lina uzima ndani yake. Kwa maana nyingine, tuyapokeapo majaribu yetu na mateso yetu kwa mwono wa Mungu, huwa ni furaha kwa sababu tunajua sababu ya mateso hayo. “Kwa kuwa kama vile mateso ya Kristo yanavyozidi kwetu, vivyo hivyo faraja yetu inazidi kwa njia ya Kristo,” 2Kor 1:5. Je, yale utesekayo bila kujua chanzo chake unayapa tafsiri gani katika maisha yako?

Tumsifu Yesu Kristo!

“Amin, amin, nakuambia kwamba, Lile tulijualo twalinena, na lile tuliloliona twalishuhudia; wala ushuhuda wetu hamwukubali.” Yoh 3:11


Ee Yesu Mwema, nifanye mara zote kuona maana ya mateso na mahangaiko yangu katika mtazamo wako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario