ALHAMISI
WIKI 5 YA PASAKA
Somo:
Mdo 15:7-21
Zab:
96:1-2a, 2b-3, 10
Injili:
Yoh 15:9-11
Nukuu:
“Na
baada ya hoja nyingi Petro akasimama, akawaambia, Ndugu zangu, ninyi mnajua ya
kuwa tangu siku za kwanza Mungu alichagua miongoni mwenu ya kwamba Mataifa
walisikie neno la Injili kwa kinywa changu, na kuliamini,” Mdo 15:7
“Bali
twaamini kwamba tutaokoka kwa neema ya Bwana Yesu vile vile kama wao,” Mdo
15:11
“Kwa
sababu hiyo mimi naamua hivi; Tusiwataabishe wale waliomgeukia Mungu katika
Mataifa; bali tuwaandikie kwamba
wajiepushe na unajisi wa sanamu, na uasherati, na nyama zilizosongolewa, na
damu,” Mdo 15:19-20
“Mkizishika
amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za
Baba yangu na kukaa katika pendo lake,” Yoh 15:10
TAFAKARI:
“Tutaokoka kwa neema ya Bwana Yesu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
ni siku nyingine tena kwa neema ya Mungu tunapata fursa ya kulitafakari neno
lake. Leo kwa namna ya pekee tulitafakari hili neno, “Tutaokoka kwa neema ya Bwana Yesu.” Hakika kile tulicho mbele ya Mungu
si kile tunachokipigania sana na kutupotezea muda mwingi hapa duniani, ikiwa
kitu hicho kinalenga tu ubinafsi wetu. Njia ya Mungu ni ya ajabu sana. Ni
ukweli usiotia shaka kwamba leo katika mazingira yetu bila ya kufahamika
hutambuliki. Kufahamika huku hakujalishi tu kujuana na mtu. La hasha! Naposema
kufahamika ni pamoja na utaratibu tuliojiwekea katika jamii tunayoishi. Mfano:
Viwango vya kufaulu kwa wale waliopata bahati ya kusoma. Bila kupita viwango na
masharti hayo, maisha yako huko mbeleni ni utata mtupu. Viwango vya kimadaraja
kutokana na kufaulu kwako na kukufanya kuwa pale ulipo leo, navyo ututofautisha
na wengine na wakati mwingine hutufanya kujisahau na kujiona huo ndio mwisho wa
yote.
Maisha
ya hapa duniani yanakikomo chake. Na tena ni kwa muda mfupi tu. Maisha
anayotutaka Mungu tuishi ni ya umilele. Hivyo kuwa kwetu salama na kupata mastahili
mbele ya Mungu ni kwa njia ya NEEMA YA BWANA WETU YESU KRISTO. Je, hii inamaana
kwamba tusijishughulishe na haya tunayoyaishi leo na utaratibu wake? La hasha!
Ukweli ni kwamba Mungu anatupenda kama tulivyo na atatuokoa kama tulivyo, ili
hali tu, yale tunayoyaishi yaakisi Umungu wake. Niwe tajiri au masikini, mwenye
elimu ya pekee au kawaida, mwenye cheo au kabwela, kwa maisha yangu niishiyo
kama hayaakisi Umungu wake ni kama moshi unaotoweka mara.
Mtazamo
huu wa Kimungu ndiyo msingi wa Mtaguso wa Yerusalemu kuhusu uhalali wetu mbele
ya Mungu na wokovu wetu. Uhalali huu si mastahili yetu, bali ni wema na upendo
wa Mungu aliyekuwa wa kwanza kutupenda. Je, kuna sababu ya kujichukia? Huna
sababu yoyote ya kujichukia. Yupo anayekupenda zaidi ya vyote vyenye thamani
katika dunia hii. Mtu huyu akupendi tu, bali anakutakia maisha ya umilele. Huyu
ndiye Yesu Kristo aliyekufa kwa ajili yako na kila siku anakufa kwa ajili yako
unapomwelekea, ili mwisho wa siku uurithi ufalme wa Baba na kuishi naye milele yote.
Ufahamu
huu ndiyo unaomfanya Mtume Petro kusimama na kuuambia mkusanyiko ule wa Mitume
juu ya wale waliolikubali neno la Mungu na kuokolewa nalo. “Na
baada ya hoja nyingi Petro akasimama, akawaambia, Ndugu zangu, ninyi mnajua ya
kuwa tangu siku za kwanza Mungu alichagua miongoni mwenu ya kwamba Mataifa
walisikie neno la Injili kwa kinywa changu, na kuliamini,” Mdo 15:7. Mtume
Petro anavunja ukimya. Mara nyingi katika maisha yetu tunashindwa kuuona ukweli
kama ulivyo tunaposafiri na kuishi katika nukuu za mila na desturi zetu ambazo
nyingi zina mapungufu makubwa.
Ni
kweli kwamba tupo kile tulicho kutokana na matokea ya historia yetu. Ni ukweli
pia, tusipotoka katika mfuko huu kifikra ni vigumu kuuona ukweli kama ulivyo,
na badala yake kuuona ukweli huo kama tulivyo. Wayahudi waliithamini na
kuilinda sana historia yao, bila kujua kwamba Mungu hakuacha kujifunua kwao na
wale waliowazunguka. Kama ilivyo kweli kwamba hakuna binadamu yeyote aliye hai
kwa sababu yake mwenyewe bila Mungu, ni kwa namna hiyo uwepo wetu hauwezi kuwa
na maana bila Mungu mwenyewe. Hivyo kwa namna ya pekee na mpango wa Mungu kama
ulivyo, “twaamini kwamba tutaokoka kwa
neema ya Bwana Yesu vile vile kama wao,” Mdo 15:11. Mungu huyu hana ubaguzi kwa
kile alichokiumba kwa sura na mfano wake. Kufanya hivyo ni kujibagua Yeye
mwenyewe, na hivyo kuufifisha Umungu wake kwa vile alivyoviumba.
Wapendwa
wana wa Mungu, ni ukweli huu unaomfanya Mtume Yakobo aliyekuwa Askofu wa
Yerusalemu wakati ule wa Mtaguso huu kusimama na kutoa neno la mwisho kuhusu
tatizo lile juu ya watu wa Mataifa waliomgeukia Mungu na wokovu wake. Naye
anasema, “Kwa sababu hiyo mimi naamua hivi;
Tusiwataabishe wale waliomgeukia Mungu katika Mataifa; bali tuwaandikie kwamba wajiepushe na
unajisi wa sanamu, na uasherati, na nyama zilizosongolewa, na damu,” Mdo
15:19-20. Matendo haya ya kipagani hayana nafasi mbele ya Mungu aliye yote
katika yote. Mungu ufurahi pale tunapozishika amri zake kwa uaminifu na haki.
Na sheria yake ni UPENDO. Tujipende kama tulivyo na kuumbwa kwetu, na tuwapende
wenzetu kama walivyoumbwa kwani wanaufunua uzuri wa Mungu, na tumpende Mungu
kwani ndiye uzima wetu na yetu yote, umilele wote.
Ndugu
yangu, neno UPENDO si geni kwako, na wala kwangu. Hii ndiyo amri
anayotusisitiza Bwana wetu Yesu Kristo
anaposema, “Mkizishika
amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za
Baba yangu na kukaa katika pendo lake,” Yoh 15:10. Ni furaha kubwa sana kuishi
bila hatia. Kuishi bila hatia ni kuishi katika upendo wa Kristo. Kristo ni
mwalimu wetu na mfano wetu halisi wa Upendo. Kama hujui fani ya Kristo katika
somo la upendo, “utazame msalaba wake.”
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mkizishika
amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za
Baba yangu na kukaa katika pendo lake,” Yoh 15:10
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, usituache. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario