martes, 21 de febrero de 2017

TAFAKARI: UKULU WA MTAKATIFU PETRO


UKULU WA MTAKATIFU PETRO

Februari 22

Somo: 1Pet 5:1-4

Zab: 23:1-3a, 4, 5, 6

Injili: Mt 16:13-19

Nukuu:

“lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo,” I Pet 5:2

“Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi,” 1Pet 5:3

“Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka,” 1Pet 5:4

Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema,” 1Pet 5:5 

Akawaambia, Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani?” Mt 16:15

Simoni Petro akajibu akasema, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai,” Mt 16:16

Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 16:17 

Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda,” Mt 16:18 

Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni,” Mt 16:19 

TAFAKARI:Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anafanya kumbumbuku ya Ukulu wa Mtakatifu Petro. Ukulu huu ndiyo mamlaka na Kiti chake Petro. Ukulu huu wa Mtakatifu Petro hakujitwalia mwenyewe, bali alihesabiwa haki hiyo na Kristo mwenyewe pale alipotoa ukiri wa kweli kumuhusu Kristo, yaani, aliyetengwa kwa kazi maalumu ya wokovu wetu na ndiye mwana wa Mungu.

Hivyo, moja ya jukumu la Kiti hiki ni kuifundisha na kuitetea Imani ya kweli kama kilelezo cha uwepo wa Kristo katika Kanisa. Petro kama Halifa wake Kristo, na wote waliofuata baada yake Petro, yaani, Mababa watakatifu, wana jukumu hilo kubwa katika Kanisa. Yesu alitaka kujua kama Mitume wake wanafahamu vyema yeye ni nani na ujumbe aliokuwa anausimamia. Hivyo aliwauliza wao binafsi wanafikra gani kumuhusu yeye baada ya kuwauliza watu wanasema nini juu yake. Hivyo Yesu “Akawaambia, Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani?” Mt 16:15. Jibu la swali hili ndilo linalomwesabia haki ya Ukulu wa Mtakatifu Petro na wale wote waliofuata baada yake, yaani Mababa Watakatifu. “Simoni Petro akajibu akasema, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai,” Mt 16:16. Haya ndiyo majibu sahihi ya Mtume Petro yenye kutoa picha na wajibu wa Kiti hicho-UKULU.

Yesu kwa kuridhika na jibu la Petro anauthibitisha Ukulu huo kwa kusema, “Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda,” Mt 16:18. Ni wazi, uwepo wa Petro kati ya Mitume wenzake na jumuiya ile ya kwanza ya Wakristo kunampatia nafasi ya pekee katika kutimiza wajibu wake na kutumika kwake. Ni wazi pia nafasi hii ya pekee kwa Petro siyo tokeo la umahiri wake, bali ni neema ya Mungu. Naye Yesu anathibitisha ukweli huu kwa kusema, “Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 16:17. Mamlaka haya ya Petro kama Halifa wake Kristo ni Neema ya Mungu mwenyewe. Badiliko la jina Simoni na kuwa Petro, yaani Mwamba, unathibitisha mtu mpya mwenye jukumu jipya. Hii ndiyo sababu pia ya Mababa watakatifu kuchagua majina mapya mara baada ya kuhesabiwa haki na Mama Kanisa.

Wapendwa wana wa Mungu, Ukulu huu wa Mtakatifu Petro unakipa uzito Kiti hicho katika mamlaka yake kama Yesu mwenyewe asemavyo, “Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni,” Mt 16:19. Haya ndiyo mamlaka ya kiti hiki na hasa kwa swala zima la Huruma ya Mungu kwa ondoleo la dhambi. Hii ndiyo sababu pia ya Baba Mtakatifu kuwa na uwezo na mamlaka ya kuutangaza mwaka wa Kanisa wa HURUMA YA MUNGU.

Wapendwa wana wa Mungu, majukumu na mwonekano wa Ukulu huu ni ule wa kutumika badala ya kutumikiwa. Na Yesu anasema, “na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mt 20:27-28.

Kiongozi yeyote yule aliyepewa dhamana na umma wa watu, ama kuhesabiwa haki na Mama Kanisa, yampasa kutumika na siyo kutumikiwa. Mtume Petro anasema, “lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo,” I Pet 5:2. Ndugu yangu, wewe na mimi tuliye hesabiwa haki na kupewa dhamana na Mama Kanisa, ama umma wa watu kwa mujibu wa sheria na taratibu zake, hatupo hapo tulipo kwa maslahi yetu binafsi. Mimi na wewe tulio hesabiwa haki hiyo na Mma Kanisa tupo hapo tulipo kumwakilisha Kristo Yesu aliyetumika badala ya kutumikiwa.

Nawe uliyepewa dhamana hiyo na umma wa watu kwa mujibu wa sheria na taratibu zake upo hapo ulipo kwa ajili ya umma huo wa watu waliokuweka hapo kwa kazi hiyo maalum, na siyo kuutafuta utukufu binafsi, na mwisho wa siku kujeuka na kuwa mungu mtu. Nafasi zote tuzipatazo kwa ajili ya huduma kwa jamii, yatupasa kutumikia kwa unyenyekevu, heshima, na kujali utu wa watu. “Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema,” 1Pet 5:5.

Ndugu yangu, huduma yo yote ile isiyokuwa na taswira ya unyenyekevu kamwe haimwakilishi Kristo, wala umma wa watu tunaowatumikia. Na kwa namna hiyo na katika huduma hiyo hakuna utukufu wala sifa kwa Mwenyezi Mungu. Kristo kamwe hajidhihirishi popote pale pasipo na unyenyekevu. “Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka,” 1Pet 5:4. Unyenyekevu katika huduma tuzitoazo utawashangaza wengi na hasa wale ambao  mawazo yao hutanguliza nafsi zao.

Tumsifu Yesu Kristo!

Na huku ndiko kutumika: “Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi,” 1Pet 5:3

Tusali:-Ee Yesu na Mwalimu wetu, tujalie fadhila ya unyenyekevu, ili kutumika kwetu kwa ajili ya wengine kudhihirishe uwepo wako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario