viernes, 3 de febrero de 2017

TAFAKARI: JUMAPILI YA 5 YA MWAKA-A


JUMAPILI YA 5 YA MWAKA-A

Somo I: Isa 58:7-10

Zab: 112: 4-5, 6-7, 8-9

Somo II: 1Kor 2:1-5

Injili: Mt 5:13-16

Nukuu

"Je, Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche  na mtu mwenye damu moja nawe?" Isa 58:7

Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya yako itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde,” Isa 58:8

 “Basi, ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima,” 1Kor 2:1.

Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu,” 1Kor 2:4-5.

Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu,” Mt 5:13.

Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 5:16 

TAFAKARI: “Tu chumvi ya dunia, na nuru ya ulimwengu.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya ‘5’ ya mwaka ‘A’ wa Kanisa. Kwa namna ya pekee leo Mama Kanisa anatukumbusha kiini cha maisha yetu hata dunia kama wafuasi hai wa Bwana wetu Yesu Kristo, yaani, ‘tu chumvi ya dunia, na nuru ya ulimwengu.’ Kwa mantiki hiyo, Habari Njema ya leo, yaani, Injili, inatupa mifano miwili ya kuwa vielelezo vya Mungu aliye hai, na wakati huo huo kutoa ushuhuda wa kweli wa maisha yetu ya kila siku. Vielelezo hivyo ni kuwa chumvi na nuru. Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu,” Mt 5:13.

Chumvi kwa matumizi ya kawaida mbali na kuwa kikolezo cha kuleta ladha nzuri ya chakula, ilitumika kuvihifadhi vyakula ili vitumike kwa muda mrefu. Ili kidumu kwa muda mrefu, chakula kama nyama, samaki, na vinginevyo, vilisowekwa chumvi, na hivyo havikuweza kuharibika. Chumvi katika mantiki hii na hasa katika somo hili la Injili imetumika kama mfano halisi katika maisha ya kijamii. Mimi na wewe ili tuwe kikolezo katika kujenga ushawishi wa maisha yenye malengo, yatupasa kuchanganyika na watu. Tunaweza tu kuyajua maisha ya watu pale tunapochanganyika nao na kuwa sehemu ya maisha yao, kwa lengo la kuwasaidia kutoka katika hali zao duni na huzuni zao. Lengo hili lisipofikiwa chumvi kama chumvi haina faida yoyote, zaidi ya kutupwa nje na kukanyagwa na watu, Mt 5:13b. Chumvi ni alama ya upendo hai, na upendo hai ni hali ile ya kuwa na ufahamu wa kutosha wa uhalisia wa mambo, vitu, na watu wanao kuzunguka. Upendo bila ufahamu ni upofu. Na hali hii ya upendo ni sawa na chumvi kupoteza ladha yake.

Kielelezo cha pili katika kutoa ushuhuda wa kweli wa maisha yetu ya kila siku ni kuwa nuru ya ulimwengu.Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima,” Mt 5:14. Kimaadili yatupasa kuwa nuru. Nguvu ya kimaadili ni ushawishi mkubwa sana wa watu kutii na kufuata yale tunayowaongoza wayafanye au wayafuate. Nuru ni ushindi katika giza. Na nuru ni kinyume cha giza. Maendeleo ya watu kwa namna yoyote ile ni tokeo la ustaarabu wao. Haya ndiyo maadili ya watu katika kuona, kufikiri, kuamua, na kutenda. Pasipo ustaarabu, maadili pia huwa hovyo. Kwa maana nyingine, palipo na utaratibu hapana akili. Nuru ambayo ndiyo maadili, ustaarabu, na kielelezo cha ufahamu wa watu, yaani, akili, ni kitu cha kupewa kipaumbele. “Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani,” Mt 5:15.

Watu wengi hupatwa na mshangaa pale kunapokuwepo na msuguano kati ya kile akisemacho mtu, na ustaarabu wake yaani, maadili aliyokuwa nayo. Mwenye maadili mazuri, husukumwa na kutawala namna ya sema yake. Mtu wa mtindo huu uchagua maneno la kusema kadiri ya hadhira yake, na somo kusudiwa kwa watu husika. Kwa maana nyingine, mtu huwa na uchaguzi wa maneno ya kusema. Ni kwa maana hiyo kwamba, “Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 5:16. Nuru ya mtu ni nguvu ya maadili ya mtu, ambayo ni kama nijamu. Ni vigumu kummiliki farasi katika mwendo kama hauna nijamu. Nijamu kwa maneno mengine ndiyo nidhamu imuongozaye mtu kufikia lengo lile kusudiwa. Nijamu ndiyo saumu ile afanyayo mtu siyo tu kwa kuupa mwili wake nidhamu, bali pia kuuweka upendo katika matendo kwa ajili ya wahitaji wanao mzunguka.

Hivyo, saumu ya kweli ni pamoja na kupatazama pale ulipokosea kutokana na uovu wako, na kupigania haki za watu ikiwa ni pamoja na wale walioonewa kijamii kutokana na mifumo miovu ambayo nawe ni sehemu ya mfumo huo. Haya ndiyo matendo ya huruma yanayopaswa kuendana na Saumu ya kweli. Na hapa ni kuwa chumvi ya dunia, na mwanga wa ulimwengu.

Matendo hayo ya huruma ndiyo anayoyahoji Nabii Isaya; "Je, Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche  na mtu mwenye damu moja nawe?" Isa 58:7. Kama najinyima kwa lengo la kufunga, kile ninachojinyima kiwalenge wahitaji. Kundi hili la wahitaji tunao pande zote na siku zote. Anza hapo ulipo! Naye Yesu anatuambia ukweli huu kama alivyowaambia wale waliomnung’unikia juu ya Marhamu ambayo alimwagiwa kichwani na Mwanamke yule mkosefu, ingeuzwa ili fedha ile wapewe maskini. Naye akawajibu na kusadifu tendo lile la mwanamke yule kwa kusema, maana sikuzote mnao maskini pamoja nanyi, na kila mpendapo mwaweza kuwatendea mema; lakini mimi hamnami sikuzote,” Mk 14:7

Wapendwa katika Kristo, tunapofanya matendo haya ya huruma tunakutana na Yesu katika sura na maumbo tofauti tofauti. Ni kwa namna hii somo la kwanza kutoka nabii Isaya linalandana kabisa na ayasemayo Yesu katika Injili ya Mathayo 25:31-46. Hapa tunakutana na Yesu aliye mwenye njaa, mgonjwa, mfungwa, aliye uchi, mwenye kiu, aliye kifungoni  nk. Huku ni kukutana naye katika maisha yetu ya kawaida na ya kila siku. Mwisho wa siku Yesu anasema, "Amin nawaambia, kadiri msivyomtendea mmoja wapo wa hao walio wadogo, hamkunitendea mimi," Mt 25:45.

Ndugu yangu, hapa ndipo ilipolala hukumu yetu ya mwisho. Wenye haki watakwenda kwenye uzima wa milele, na wasio haki wataingia katika adhabu ya milele, (Mt 25:46). Bwana harusi hatunaye tena. Huu ndio wakati muhafaka wa kufunga na kufanya toba. Zoezi hili kwa Mkristo na kwa yeyote yule mwenye hofu ya Mungu ni zoezi na tendo endelevu maisha yake yote. Yesu kesha tufundisha mengi tulipokuwa naye katika makuzi yetu ya maisha ya kiroho, na sasa yatupasa kuyaishi. "Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga," Mt 9:15b. Kuyafanya haya kwa uhakika, uaminifu, na ukamilifu wake ndiyo baraka na neema kwetu. “Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya yako itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde, Ndipo utaita, na Bwana ataitika; utalia, naye atasema, Mimi hapa,” Isa 58:8-9. Amina!

Hivyo ndugu yangu ninaye safiri nawe katika tafakari hii, usisahau kamwe kundi la wahitaji katika mfungo wako na maisha yako ya kila siku. Daima uwe mtu wa kutenda haki na kuitetea pia pale inapokosekana au kukandamizwa kadiri ya nafasi yako na wito wako.

Somo la kwanza la tuonyesha, na kutufundisha namna ya kufanya toba ya kweli. Baada ya kutubu na kuondolewa dhambi, malipizi au toba yetu ya kweli ni kujifunua na kujiweka karibu na wale wote wanao itaji uwepo wetu, na kuwasaidia kadiri ya uwezo na nafasi aliyotupa Mungu. Tunapolifanya tendo hilo kuwa letu kwa moyo mkunyufu, kiwi yetu na Mungu inafanywa kama adhuhuri. "Na kama ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako, na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo nuru yako itakapopambazuka gizani; na kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri," Isa 58:10. Huu ni wito pia wa kuwa chumvi ya dunia, na mwanga wa ulimwengu.

Ndugu yangu, unapoishi hapa duniani kuna mambo mawili yanaweza kukufika. Ukiishi vizuri unakuwa muhenga. Yaani mtu aliyeishi vyema na ameacha kitu cha kuigwa na kusimuliwa kwa vizazi vyote. Usipokuwa muhenga basi uwezekano wa kuwa mzimu ni mkubwa. Mzimu ni roho ovu/mbaya. Hapa hakuna cha kuigwa wala kusimuliwa. Mtu anakosa na kupoteza historia yake. Kuishi vyema na watu kwaitaji unyenyekevu kama msingi wa fadhila zote. Unyenyekevu huu ni furaha ya Mungu. "Kumcha Bwana ni maonyo ya hekima; na kabla ya heshima hutangulia unyenyekevu," Mit 15:33

Ni unyenyekevu huu unaotusukuma tena na tena kupenda kuishi na kila mmoja wetu. Ni unyenyekevu huu unatufanya kushuka chini kabisa kwa waihitaji. "Afadhali kuwa na roho ya unyenyekevu pamoja na masikini, kuliko kugawanya nyara pamoja na wenye kiburi." Mit 16:19. Kristo ndiye kielelezo cha unyenyekevu wa kweli. Hakika huruma na neema ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu.

Tunachopaswa kuishi si maisha ya ushindani wa hoja katika majukwaa, bali zaidi ni kuishi na kutoa ushuhuda wa ukimya wa maisha ya kweli ya Ukristo wetu. Jambo hili ni muhimu sana, kwani katika utulivu Mungu yupo na kuonekana. “Na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu,” 1Fal 19:12. Huu ni wakati wa mitetemo ya Imani. Nasi tusienende kadiri ya mitetemo hiyo. Tuitafsiri hiyo mitetemo nako tutakutana na Mungu katika utulivu.

Ni wazi katika kutenda lililo la Mungu, yaani, lenye kuongozwa na upendo wa kweli, tujiandae kupata upinzani. Yule mwovu shetani hafurahii yaliyo mazuri na mema yenye kuufunua Utukufu wa Mungu. Yesu Kristo mwenyewe alipata upinzani nyumbani mwake mwenyewe. Katika hili Yesu anasema, “Amin, nawaambia ya kwamba, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe,” Lk 4:24. Je, kama hatukubaliki nyumbani kwetu na watu wanaotufahamu iwe sababu ya kutokutenda mema? Jibu ni HAPANA! Tuendelee kutenda wema na upendo kwa wote, kwa sababu asili ya upendo ni Mungu, uwepo wa upendo ni Mungu, na Upendo ni Mungu. Kuyaona haya ya Mungu ndani yetu kwahitaji unyenyekevu na kuepuka kujiinua kusiko na sifa wala siha. Hali hiyo ndani yetu itatuwezesha kusema toka moyoni maneno haya ya Mtume Paulo; “Basi, ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima,” 1Kor 2:1.

Je, mazingira yetu leo kama Taifa huru yanatuwezesha kuwa chumvi ya dunia na mwanga wa ulimwengu? Ndugu yangu, utakubaliana nami kwamba leo hekima imewekwa mfukoni, na silaha kubwa ya utendaji wetu na hasa wale waliopewa dhamana hiyo na umma, ni ile ya vitisho na kujengeana hofu. Hapana shaka kabisa baada ya miaka kumi ijayo tutakuwa taifa ya ajabu kutokea katika ulimwengu huu wa sayansi na teknolojia. Na sababu kubwa ni kutokuwa chumvi na mwanga. Tunajisikia salama zaidi kuishi katika giza, na kufanya vitu kwa usiri.

Mfumo huu wa maisha ni mfumo wa kutokujiamini ambako kumetokana na kutojitosheleza kwa kile tulichojiaminisha kuwa tunaweza. Ni vyema kuzisoma alama na nyakati, na kuzitafsiri kadiri la hitaji la wakati. Mang’amuzi ya maisha, yaani, historia ya kule tulikotoka na changamoto zake, yataendelea kuwa mwalimu wetu mzuri. Kujifanya vipofu kwa kukusudia, na kuwa viziwi kwa kuyaziba masikio kwa pamba ikiwa ni kuogopa kukosolewa, ni dalili tosha za kupoteza ladha kama chumvi, na wakati huo huo kulikumbatia giza. Anguko lake ni kubwa. Usalama wa leo na sasa kama tokeo la kuminya haki za watu na hasa kuziba midomo yao, ni janga kubwa na lenye kishindo kikubwa kesho ambayo sote tunaitamani.

Maisha ya binadamu pamoja na changamoto zake, yamejawa tumaini la kwamba ‘kesho yaweza kuwa nzuri zaidi.’ Hata mfumo wa gari una gia nne hadi tano za kusonga mbele, na moja tu ndiyo ya kurudi nyuma, tena kwa utaratibu. Kuligeuza gari kwa kuangalia ulikotoka na kupachika gia ya kurudi nyuma ukijifariji kuwa waenda mbele, litokeapo jambo mbele ya safari ni vigumu sana kustahimili kishindo chake. Ndiyo maana mara zote tunapigwa na butwaa kwa kutojianda na kutokujua chochote. Hii yote ni kumbatio la hofu tusioijua. Hofu ni ugonjwa mbaya sana. Hofu udumaza akili na ufahamu. Kwenye hofu huwezi fikiri sawa sawa. Kwenye hofu huwezi kupanga sawa sawa. Na palipo na hofu hapana ubunifu na upekee wa vitu au mambo.

Mungu ndiye anaye wezesha yote ndani yetu. “Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu,” 1Kor 2:4-5. Sifa na Utukufu ni kwa Mungu wetu. Amina

Tumsifu Yesu Kristo!

“Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 5:16

Tusali:-Ee Yesu Mwema, tujalie ujasiri wa kuwa chumvi na mwanga pale tulipo, na kuvishinda vitisho vyenye kuijenga hofu. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario