JUMAPILI
YA 8 YA MWAKA-A
Somo I: Isa 49:14-15
Zab: 62:2-3, 6-7, 8-9ab
Somo II: 1Kor 4:1-5
Injili: Mt 6:24-34
Nukuu
“Je, mwanamke aweza
kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa
waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe,” Isa 49:15
“Mtu na atuhesabu hivi,
kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu,” 1Kor 4:1
“Hapo
tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu,” 1Kor
4:2
“Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa
maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau
huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali,” Mt 6:24
TAFAKARI: “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana
atamchukia huyu, na kumpenda huyu.”
Wapendwa wana wa Mungu, ahadi
ya Mungu kwetu ni kutokutusahau katika hali zote hata kama kibinadamu jambo
hilo linawezekana. Mungu hawezi kutusaha. “Je, mwanamke aweza kumsahau mtoto
wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza
kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe,” Isa 49:15
Maisha yetu ni mpango
wa Mungu na kwa malengo ya Mungu. Mpango huu unarahisishwa kwa uwepo wa Mwanaye
Yesu Kristo, ambaye hajifanyii mambo yake pasipo Mungu Baba aliyempeleka. “Mimi
siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo; na hukumu
yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake
aliyenipeleka,” Yoh 5:30
Ni kwa mtazamo huo,
Yesu katika Injili ya leo anatupa angalizo na kusema, “hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia
huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi
kumtumikia Mungu na mali,” Mt 6:24. Hata ukifanikiwa ni kwa muda mfupi tu. Je,
kwa nini twapaswa kumtumikia bwana mmoja? Sababu ya wazi na ya moja kwa moja ni
kuondoa ile roho iliyojigawa vipande vipande. Mfano; kama umepata mialiko
miwili ya harusi inayofanyika muda ule ule na siku ile ile, yakupasa kuchagua
moja wapo utakayokwenda hata kama zote zina uzuri au zimetofautiana. Kuchagua
huku ndiko Yesu anapotushauri kuutafuta kwanza ufalme wa Mbinguni, na kuondoa
roho ya kujigawa vipande vipande. Naye Yesu anasema, “Bali utafuteni kwanza
ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mt 6:33. Ndugu yangu, unaloneno zaidi ya ukweli huu wa
Bwana wetu Yesu Kristo?
Ni kweli isiyo shaka
kwamba ukishaingia katika mfumo huu, na mtazamo huu wa fundisho hili ya Yesu, kuutafuta
ufalme wa mbinguni kwanza, huwezi kupata “presa”-shinikizo la damu unapowaona
watu wakipigana vibega kwa kumwangaikia mfalme tumbo na utajiri wake. Kristo
anapokuwa katikati ya yote, yeye atakupatia kadiri ya mahitaji yako na kwa
wakati wake. “Basi msisumbukie ya
kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.” Mt
6:34. Hata hivyo hapa Kristo Yesu hamaanishi
tujikalie tu bila kujishughulisha na kufanya chochote kuhusu maisha yetu.
Ndugu yangu yatupasa kumuishi Kristo leo na sasa katika yale yote yampendezayo.
Mungu kamwe habariki utupu. Kumbuka ishara ile ya kwanza alioyofanya Yesu kule
Kana, Yoh 2:1-11. Ingawa kesho inasikika akilini mwetu, tuelewe kesho hiyo ipo
mikono mwa Mungu katika uhalisia wake.
Wapendwa wana wa Taifa
la Mungu, kama tunajua kwamba hakuna mtu
miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake, Rum
14:7, maisha yetu bila Kristo yatakuwa na walakini mkubwa. “Mtu
na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu,”
1Kor 4:1. Kama tu watumishi wa Kristo na mawakili wa siri za Mungu, maisha yako
hapa duniani na kadiri ya wito wako ni dhamana kubwa kwa sababu
yeshathaminishwa kwa damu ya Yesu pale Msalabani. “Nanyi mfahamu kwamba
mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka
katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya
thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,”
1Pet 1:18-19. Je, watambua thamani ya maisha yako kama mfuasi wa Kristo?
Wapendwa wana wa Mungu,
thamani ya Ukristo wako itategemea sana na namna unavyo
mwakilisha Kristo kama wakili wake katika kweli na uaminifu. Ukristo wako
usibaki katika jina tu, bali imani ya kweli ndani yako, na Kristo akiwa ndiye
kielelezo chako katika yote. Na “hapo
tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu,” 1Kor
4:2. Ni kuwa mwaminifu katika kuifuata njia yake, yaani, kuubeba msalaba wako
kwa uaminifu bila kumsaliti Kristo. Ni kuiishi kweli kadiri ya mafundisho yake
Kristo, na zaidi amri ile ya upendo.
Ukipenda kama
alivyopenda Kristo utafanya yote yampendezaye Mungu. Na mwisho ni kuuishi uzima
wa kweli kwa kushiriki Masakramenti katika hali ya usafi wa moyo, na hasa
Sakramenti ya Ekaristi Takatifu. Hali hii ya usafi wa moyo ndiyo impelekeayo
Mtume Paulo kusema kwamba, “Lakini, kwangu mimi, si kitu kabisa nihukumiwe na
ninyi, wala kwa hukumu ya kibinadamu, wala sijihukumu hata nafsi yangu,” 1Kor
4:3. Mara zote tuongozwe na dhamiri safi na yenye hofu ya Mungu. “Maana sijui sababu ya kujishitaki nafsi
yangu, lakini sihesabiwi haki kwa ajili hiyo; ila anihukumuye mimi ni Bwana,”
1Kor 4:4.
Kuujua wajibu wako na
kuutimiza kadiri ya takwa lake na kwa upendo ndiko kutakapo kuhesabia haki.
“Basi ninyi msihukumu neno kabla ya wakati wake, hata ajapo Bwana; ambaye
atayamulikisha yaliyositirika ya giza, na kuyadhihirisha mashauri ya mioyo;
ndipo kila mtu atakapoipata sifa yake kwa Mungu,” 1Kor 4:5. Ndugu yangu,
usichoke kutimiza wajibu wako kwa upendo. Hakuna aliyefilisika kwa kupenda na
kutoa kwa upendo.
Bwana na Bibi Baraka
Mfaume baada ya kutembea umbali mrefu wakiwa wametoka kuhemea, waliliona genge
upande wao wa kushoto palipokuwa wanauza machungwa. Basi Bibi Baraka alinunu
machungwa manne, yaani, mawili kwa ajili yake, na mawili kwa ajili ya mmewe. Kwa kiu na njaa ile
walioyokuwa nayo, Baba Baraka Mfaume aliyashambulia machungwa yake mawili bila
huruma huku wakiendelea na safari yao kuelekea nyumbani akewe akiwa amebeba
mkoba wake na ule wa mmewe.
Mara walipo fika
nyumbani walipokelewa kwa furaha na watoto wao John na Maria. Mara Bibi Baraka
aliomba aletwewe kisu, na mara akayatoa machungwa yake mawili kwenye mkoba
wake. Akalipasua
chungwa moja katikkati akampa kipande Maria, na kingine akampa John. Huku macho
yakiwa yanamtoka Baba Baraka kama mjusi aliyebanwa na mlango, Mkewe akapasua
chungwa la pili katikati kisha akampa mmewe kipande kimoja, naye akabaki na
kipande kilichobaki. Huu ndio upendo wa Mama wenye kujali na kuwajibika
aliousema Nabii Isaya katika somo letu la kwanza. Hata
hivyo, upendo wa Mungu kwetu ni zaidi ya mfano wa upendo huu wa Mama. Mungu
anatupenda upeo upeo, Yoh 12:24. Huyu ni Mungu asiye tusahau kamwe iwe
tunapomtegemea au kumsahau katika hali yoyote ile, Isa 49:15. Akina Baba na
wale wote wasio na upendo kama mama mpo?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Bali
utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mt 6:33
Tusali:- Ee
Yesu, uwe kitoshelezo chetu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario