JUMAMOSI WIKI YA 6 YA MWAKA-I
Somo:
Ebr 11:1-7
Zab:
145:2-3, 4-5
Injili:
Mk 9:1-13
Nukuu:
“Basi imani ni kuwa na
hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1
“Kwa imani twafahamu ya
kuwa ulimwengu uliumbwa kwa neno la Mungu, hata vitu vinavyoonekana
havikufanywa kwa vitu vilivyo dhahiri,” Ebr 11:3
“Wakatokewa na
Eliya pamoja na Musa, nao walikuwa wakizungumza na Yesu,” Mk 9:4
“Kisha
likatokea wingu, likawatia uvuli; sauti ikatoka katika lile wingu, Huyu ni
Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye,” Mk 9:7
TAFAKARI: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye.”
Wapendwa wana wa Mungu, kuzikabili
sintofahamu za maisha kadiri ya wito na mazingira yako wangu, yanipasa kuwa na
uelewa sahihi wa imani ya kweli. Waraka huu kwa Waebrania unaelezea “imani
ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr
11:1. Kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo ni ‘kutokuwa na shaka yoyote ilhali
ukiwa umeyakabidhi yote mikono mwa Mungu katika maana ya ufahamu wa kweli wa
kile ukiaminicho, na wakati huo huo umaana wake (rationality and
significativity).’ Imani tu bila kubeba ufahamu wake na umaana wake ni
kishawishi kikubwa cha kuanguka kwenye ujinga na upumbavu. Ni kwa mantiki hii
‘imani siyo ushuhuda tu uliobebwa katika miujiza na alama nyingine kama hizo.’
Imani ni zaidi ya hayo licha kwamba kama yapo katika kweli uimarisha imani
changa. Imani ni zaidi ya ishara tuzionazo kwa sababu, Imani “ni bayana ya
mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1b.
Imani katika ufahamu na
umaana ujidhihirisha katika haya yafuatayo kadiri ya somo letu hili la leo.
Kwanza kabisa Imani huongeza na kuimarisha ufahamu wetu. Ni kwa mantiki hiyo
“kwa imani twafahamu ya kuwa ulimwengu uliumbwa kwa neno la Mungu, hata vitu
vinavyoonekana havikufanywa kwa vitu vilivyo dhahiri,” Ebr 11:3. Ni kama
afundishavyo Mtakatifu Agustino kwamba, ‘imani utupeleka katika kuelewa, na
kuelewa huimarisha imani.”
Pili, imani katika
kuyaishi na kuyatenda kiadili huwezesha mtu kuhesabiwa haki. Ila jambo la
kutofautisha hapa ni hili; utakatifu wa mtu siyo tokeo la mafanikio yake
kutokana na ‘weza yake’ ya kibinadamu, bali ni neema ya Mungu ifanyayo kazi
ndani ya mtu. Ni kwa maana hiyo, “kwa imani Habili alimtolea Mungu dhabihu iliyo
bora kuliko Kaini; kwa hiyo alishuhudiwa kuwa ana haki; Mungu akazishuhudia
sadaka zake, na kwa hiyo, ijapokuwa amekufa, angali akinena,” Ebr 11:4.
Tatu, imani utuvusha
kwa yasiyowezekana kibinadamu. Ni “kwa imani Henoko alihamishwa, asije akaona
mauti, wala hakuonekana, kwa sababu Mungu alimhamisha; maana kabla ya
kuhamishwa alikuwa ameshuhudiwa kwamba amempendeza Mungu,” Ebr 11:5. Kweli hii
inathibitishwa pia na Yesu, na kusema, “kama mngekuwa na imani kiasi cha chembe
ya haradali, mngeuambia mkuyu huu, Ng’oka, ukapandwe habarini, nao ungewatii,”
Lk 17:6.
Nne, Imani utuweka
karibu na Mungu, na umpendeza Mungu. Hivyo, “pasipo imani haiwezekani
kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na
kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao,” Ebr 11:6. Leo kati yetu bila kuona, na
kuwa na ushahidi shikika, hakuna sababu kimantiki kuamini uwepo wa Mungu. Ila
yapo mengi tu ya kimantiki ambayo hayahitaji vigezo vya kushikika wala
kuonekana ili kuamini. Mfano, huwezi kuwa mrefu zaidi yako mwenyewe.
Tano, Imani huwezesha
lisilo kimantiki kadiri ya mang’amuzi ya mwanadamu. “Kwa imani Nuhu akiisha
kuonywa na Mungu katika habari za mambo yasiyoonekana bado, kwa jinsi alivyomcha
Mungu, aliunda safina, apate kuokoa nyumba yake. Na hivyo akauhukumu makosa
ulimwengu, akawa mrithi wa haki ipatikanayo kwa imani,” Ebr 11:7. Leo wewe na
mimi tu warithi wa ufalme wa Mungu kwa sadaka ile aliyoitoa Bwana wetu Yesu
Kristo pale Msalabani.
Hivyo kwa kubadilika kwake sura Yesu Kristo kuliko ambatana
na kutokewa kwa Eliya na Musa, kunathibitisha ufunuo kamili wa Mungu kupitia
mwanaye Mpenzi Yesu Kristo, na kukamilika kwa unabii wote, yaani, Eliya, na
sheria na mamlaka yote yaani, Musa. “Wakatokewa
na Eliya pamoja na Musa, nao walikuwa wakizungumza na Yesu,” Mk 9:4. Hivyo
hapana tena ufunuo ulio wa wazi na kamili zaidi ya ufunuo huu wa Mungu kupitia
mwanaye Mpenzi. Tendo hili linathibitishwa na sauti ya Mungu mwenyewe kwa
viumbe vyote: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye,” Mk 9:7. Ndugu
yangu, Je, unafuata sauti gani katika maisha yako?
Sauti hii
kutoka mbinguni inampata Yesu Kristo heshima, mamlaka, na utukufu. “Maana
alipata kwa Mungu Baba heshima na utukufu, hapo alipoletewa sauti iliyotoka
katika utukufu mkuu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye,”
2Pet 1:17. Nasi tunapoisikia sauti hiyo na kuishi ukweli huo, tunajazwa nguvu,
heshima na utukufu kwa kuishi ndani na katika Kristo.
Wapendwa wana wa Mungu, zipo sauti
nyingi katika maisha yetu. Je, sauti hizo zinatupeleka karibu na Yesu au
zinatutenganisha na ukweli wake? Kusikia sauti hii ni kuyafanya mapenzi yake.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Basi imani ni kuwa na hakika ya
mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1
Tusali:-Ee
Yesu na Mchungaji wetu, kamwe usitutenge na sauti yako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario