ALHAMISI WIKI YA 5 YA MWAKA-I
Somo:
Mwa 2:18-25
Zab:
128:1-2, 3, 4-5
Injili:
Mk 7:24-30
Nukuu:
"Bwana Mungu
akasema, si vema huyu mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana
naye." Mwa 2:18
“Adamu akawapa majina
yao kila mnyama wa kufugwa, na ndege wa angani, na kila mnyama wa mwituni;
lakini hakuonekana wa kumsaidia Adamu aliyefanana naye,” Mwa 2:20
“Bwana Mungu akamletea
Adamu usingizi mzito, naye akalala; kisha akatwaa ubavu wake mmoja, akafunika
nyama mahali pake, na ule ubavu alioutwaa katika Adamu Bwana Mungu akaufanya
mwanamke, akamleta kwa Adamu,” Mwa 2:21-22
“Adamu akasema, Sasa
huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa
mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume,” Mwa 2:23
“Kwa hiyo mwanamume
atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili
mmoja,” Mwa 2:24
"Akamwambia,
Waache watoto washibe kwanza; maana si vizuri kukitwaa chakula cha watoto, na
kuwatupia mbwa," Mt 7:27.
“Naye akajibu,
akamwambia, Naam, Bwana, lakini hata mbwa walio chini ya meza hula makombo ya
watoto,” Mk 7:28
“Akamwambia, Kwa sababu
ya neno hilo, enenda zako, pepo amemtoka binti yako,” Mk 7:29.
TAFAKARI:
“Hata mbwa walio chini ya meza hula makombo ya watoto.”
Wapendwa taifa la wana
wa Mungu, masomo yetu leo yanatualika kutafakari UPENDO na HURUMA ya MUNGU
kwetu. Somo la kwanza linazidi kuonyesha upendo huo kwa kumpatia Adam mwenzi
wake na kumwondolea huzuni zake kwa kuishi upweke. Pia kwa tendo hilo la
kimungu tunafundishwa maisha ya pamoja ni maisha ya kimungu kama ulivyo
uhusiano wa UTATU MTAKATIFU; Mungu Baba, Mwana na Roho mtakatifu.Tendo hilo pia
la tufundisha kwamba tupo hapa duniani kwa ajili ya wenzetu pia kwa sababu tuna
huo mfanano wa sura na mfano wa Mungu.
Kwa upande wa Adamu,
msaidizi wake Eva, siyo mjakazi wala mtumwa wake; bali mwenzi wake na ‘msafiri
twaliwa’ mwenzake katika uzima na umilele, yaani, utakatifu. Adamu bila Eva
hajakamilika, na Eva bila Adamu kadhalika. Hapa kuna tendo la kimungu la
UKAMILISHANO. Tendo hili ndilo taswira halisi ya ndoa na umaana wake. Ni agano
na siyo mkataba. Katika agano hili kuna kupoteza kwa ajili ya mwingine. Hesabu
ya Mungu hapa ni ya pekee. Kwa kawaida 1+1=2. Kwa upende wa hesabu ya Mungu,
1+1=1. Maana ya jibu la Mungu ni hii, "kwa hiyo mwanamke atamwacha baba
yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili MMOJA,"
Mwa 2:24.
Adamu anaonyesha furaha
ya tendo hili la UPENDO wa Mungu kwa namna hii ya ajabu, akisema, "sasa
huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa
mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanaume," Mwa 2:23. Hakujawahi
tokea dunia mtunzi aliye onyesha ya
moyoni na mguso wa furaha ya kimungu kama Adamu kwa tenzi hii ya pekee, Mwa 2:
23.
Ndugu yangu, mbona
wamfanya mwenzi wako wa ndoa kama kigaragosi fulani hivi? Huo sio mpango na
upendo wa Mungu. Je, mnaokimbilia kupeana talaka kwa sababu nyepenyepesi
mwataka kuvunja mpango wa Mungu? Yesu ananena hivi kuhusu talaka, "Lakini
tangu mwanzo wa kuumba ulimwengu, alifanya mume na mke. Kwa sababu hiyo mtu
atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili
mmoja; hata wamekuwa si mwili tena, bali mwili mmoja," Mk 10:6-8. Hapa tunapewa
tena hesabu ya kimungu na Yesu, 1+1=1. Ndugu yangu unayesoma habari hii,
"Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana
waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu," Ebr 13:4.
Somo la Injili la
tuonyesha pia HURUMA na UPENDO wa Mungu. “Waache watoto washibe kwanza; maana
si vizuri kukitwaa chakula cha watoto, na kuwatupia mbwa," Mt 7:27. Nini
maana ya maneno haya? Ni kweli pasipo
shaka kabisa kwamba katika mpango mzima wa wokovu wetu wanadamu, ilimpasa Mungu
aanze na kundi fulani la watu, na kwa Upendo na upendeleo wake wa kimungu Taifa
la wana wa Israeli walipewa upendeleo huo wa kwanza.
Pili, yatupasa kujua
vizuri lugha aliyotumia Yesu kumjibu mama huyu asiye Myahudi aliyemwendea kwa
shida ya uponyaji wa mwanaye. Ni lugha iliyokwisha zoeleka katika jamii ile
wakati ule kati ya Wayahudi na majirani zao. "Watoto" hapa yamaanisha
wana wa Israeli, "mbwa" ni wale wasio Waisraeli, ikimaanisha watu wa
mataifa. Na "mkate," ikimaanisha huduma ya uinjilishaji wa habari
njema ya wokovu. Kwa mantiki hiyo Yesu alitumwa kwanza kwa taifa hili la
kiyahudi. "Sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israelí,"
Mt 15:24. Hii ndiyo sababu hasa ya Yesu kuyasema hayo yote. Ila kwa jibu lake
anaonyesha HURUMA kwetu pia, yaani, nasi tupo katika mpango wa wokovu wa Mungu
baada ya wana wa Israeli kushiba. Jibu la mama huyu ni mwelekeo wa sisi sote
tunapokuwa mbele ya Mungu tukijua wote ni wadhambi na waitaji pia. Ni tendo la
unyenyekevu. Anajibu na kusema, "Naam, Bwana, lakini hata mbwa walio chini
ya meza hula makombo ya watoto," Mk 7:28.
Swali ni kwamba, kama
Yesu alitumwa kwanza kwa wana wa Israeli, mbona walimkataa? Mtume Paulo anatupa
jibu lake, anaposema, "Basi nasema, Je, Wamejikwaa hata waanguke kabisa?
Hasha! Lakini kwa kosa lao wokovu umewafikia Mataifa, ili wao wenyewe watiwe
wivu," Rum 11:11.
Ndugu yangu, tazama
maajabu ya Mungu wetu! Mipango yake ni ya ajabu machoni mwetu, UPENDO na HURUMA
vya ufunua UKUU wake na UHASILI wake. Yatupasa sote wenye ufahamu na utambuzi
huu kujibu UPENDO na HURUMA ya Mungu kwa KUJINYENYEKEZA kwake kama tendo pekee
la uhitaji wetu sisi wanadamu. Tendo hili litakuwa FURAHA ya Mungu na kwetu
pia.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Bwana, lakini hata mbwa walio
chini ya meza hula makombo ya watoto,” Mk 7:28
Tusali:-Bwana
wewe ndiwe mwenye haki. Utazame udogo wangu, nijalie ufahamu wako, utambuzi wa
Upendo, Huruma yako, na daima nijinyenyekeze kwako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario