IJUMAA WIKI YA 6 YA MWAKA-I
Somo:
Mwa 11:1-9
Zab:
33:10-11, 12-13, 14-15
Injili:
Mk 8:34-9:1
Nukuu:
“Nchi yote ilikuwa na
lugha moja na usemi mmoja,” Mwa 11:1
“Wakasema, Haya, na
tujijengee mji, na mnara, na kilele chake kifike mbinguni, tujifanyie jina; ili
tusipate kutawanyika usoni pa nchi yote,” Mwa 11:4
“Bwana akasema, Tazama,
watu hawa ni taifa moja, na lugha yao ni moja; na haya ndiyo wanayoanza
kuyafanya, wala sasa hawatazuiliwa neno wanalokusudia kulifanya,” Mwa 11:6
“Kwa sababu hiyo jina
lake likaitwa Babeli; maana hapo ndipo Bwana alipoichafua lugha ya dunia yote;
na kutoka huko Bwana akawatawanya waende usoni pa nchi yote,” Mwa 11:9
“Mtu ye yote akitaka
kunifuata na ajikane mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate,” Mk 8:34b
“Kwa kuwa mtu atakaye
kuiponya nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili
yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha,” Mk 8:35
TAFAKARI:
“Msalaba Mtakatifu ni Utukufu, na Baraka.”
Wapendwa wana wa Mungu,
mitikiso katika maisha na hasa nyakati zile ambazo tulizozoea utulivu, mitikiso
hiyo ulenga katika ukamilifu wa kile kilichokusudiwa ingawa si rahisi kuelewa
kweli hiyo katika mazingira na nyakati hizo za misukosuko. Nyakati hizo za
utulivu ni kama zinavyoelezewa kutoka somo letu la kwanza, yaani, “Nchi yote
ilikuwa na lugha moja na usemi mmoja,” Mwa 11:1. Hizi ndizo zile nyakati ambazo
mimi na wewe ujiwekea mipango mingi na kuwa na hamu ya kufanya hiki na kile. Na
hivi ndivyo ilivyokuwa, “Haya, na tujijengee mji, na mnara, na kilele chake
kifike mbinguni, tujifanyie jina; ili tusipate kutawanyika usoni pa nchi yote,”
Mwa 11:4. Haya yote na katika uzuri wake ni mawazo ya kibinadamu tu, ila Mungu
anampango wa kila mmoja wetu na kila alichokiumba, “maanamawazo yangu si mawazo
yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana,” Isa 55:8.
Hivyo, “Bwana akashuka
ili auone mji na mnara waliokuwa wakiujenga wanadamu,” Mwa 11:5. Hapa ndipo
tunapoona mpango wa Mungu unavyojidhirisha na kwenda kinyume kabisa na mpango
wa mwanadamu na matamanio yake. “Bwana akasema, Tazama, watu hawa ni taifa
moja, na lugha yao ni moja; na haya ndiyo wanayoanza kuyafanya, wala sasa
hawatazuiliwa neno wanalokusudia kulifanya,” Mwa 11:6. Ila alitendalo Mungu au
kuliamuru ulenga katika ukamilifu licha ya kwamba linaweza kupita katika mateso
na sintofahumu nyingi. “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana,
ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za
mwisho,” Yer 29:11.
Hili ndilo lililokuwa
lengo la Mungu katika sintofahamu hii ya babeli, yaani, “Kwa sababu hiyo jina
lake likaitwa Babeli; maana hapo ndipo Bwana alipoichafua lugha ya dunia yote;
na kutoka huko Bwana akawatawanya waende usoni pa nchi yote,” Mwa 11:9. Embu
tazama uzuri wa tendo lile la mvurugano wa lugha hapo Babeli, na hivi leo
ulimwengu umeshehena wingi wa lugha mbalimbali. Tendo hili licha ya kuwa teso
na msalaba kwa mwanadamu kutokufikia lengo lake la kuujenga mnara ule wa Babeli
linaufunua uzuru, furaha, na utukufu wa Mungu.
Wapendwa wana wa Mungu,
licha ya Msalaba kuwa kitambulisho, kielelezo na uthibitisho wetu Wakristo, kwa
wengi ni makwazo na aibu. Kwa kifupi hao ni adui wa Msalaba. "Maana wengi
huenenda, ambao nimewaambieni mara nyingi habari zao, na sasa nawaambia hata
kwa machozi, kuwa ni adui za msalaba wa Kristo." Flp 3:18. Ndugu yangu,
licha kwa mwono wa kibinadamu Msalaba una taswira ya mateso, ndiyo njia pekee,
halisi na uhai wa Mkristo kama mfuasi wa Yesu Kristo. "Mtu yeyote
asiyechukua Msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi
wangu," Lk 14:27.
Je, yatosha tu
kuuchukua Msalaba na kumfuata Kristo? La hasha! Kuuchukua Msalaba kwa maanisha
mambo makuu yafuatayo; Kujikana nafsi, Kujitwika/kuhiari kwa ukunjufu, na
kumfuata Yesu kama kielelezo sahihi cha Msalaba. "Wakati huo Yesu
aliwaambia wanafunzi wake, Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike
msalaba wake, anifuate," Mk 8:34. Maana yake ni nini? Ndugu yangu,
kujikana kuna lenga haswa nafsi na matamanio yake. Siyo yote nafsi ipendayo
yana njia, kielelezo na uhai wetu kwa maisha ya umilele. Yesu anatutakia maisha
ya umilele. Hapa duniani tupo tu kwa muda mfupi na tunajiandaa tu kwa maisha
halisi ya umilele.
Yesu anagusia jambo
hilo kwa kusema, "Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na
kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake?" Mt
16:26. Tunapoizuia nafsi kupata kila kitu kiipendacho ni kuiokoa nafsi hiyo kwa
ajili ya umilele, "kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na
mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona," Mt 16:24. Je, upo
tayari kuachilia fahari kwa uliyoshikamana nayo?
Jambo hili wakati
mwingine litakuitaji uyafumua maisha yako yote na kuanza kuyasuka tena. Huku ni
kuzaliwa upya katika roho! Yesu analiongelea jambo hili kwa Nikodemo, na
kusema, "Amin, amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi
kuuona ufalme wa Mungu," Yoh 3:4. Kwa maana, "kilichozaliwa kwa mwili
ni mwili; na kilichozaliwa kwa roho ni roho," Yoh 3:6. Kuikana nafsi ni
kuanza mfumo mpya na Kristo. Tatizo kubwa la wengi nikufikiri bado muda upo na
kwa hiyo hakuna haraka.
Kujitwika Msalaba kwa
maanisha mambo mawili. Kwanza ni jambo la hiari na huru. Hatupaswi kuona aibu
hasa pale tunapotaka kujenga mahusiano na Kristo. Yawezekana wakati fulani
katika maisha yako uliheshimika sana kutokana na nafasi uliyokuwa nayo na
huduma uliyokuwa unatoa; iwe kwenye familia, kuajiriwa au utawani. Leo huna
nafasi hiyo na hujulikani tena. Kujenga mahusiano na Kristo katika kujitwika
msalaba ni kuanza upya pale ulipo. Tatizo letu hupenda kuishi kindotondoto na
kihistoriahiria. Huko haupo tena. Kama gitaa lako limebakia na nyuzi nne badala
ya sita, zipige hizo hizo hadi mwisho. Ni kuubeba Msalaba hadi mwisho na
kuwabwa juu yake. "Akatoka, hali akichukua Msalaba wake, mpaka mahali
paitwapo Fuvu la kichwa, au kwa kiebrania, Golgotha. Wakamsulubisha huko, na
wengine wawili pamoja naye, huku na mmoja huku, na Yesu katikati" Yoh
19:17-18. Wengi huwa tunafika Golgotha, ila ikifikia kuwabwa tunatoweka. Ndugu
yangu, licha ya Yesu kusaidiwa na Simoni Mkirene, hatimaye alikubali kuwabwa.
Hapa ndipo kwenye taji la ushindi. Hapa ndipo kwenye FURAHA ya kweli katika
mateso. Je, huamini nisemayo?
Haya hapa maneno ya
Yesu mwenyewe, "Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila
neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa
thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii
waliokuwa kabla yenu," Mt 5:11-12.
Jambo la pili,
kujitwika huku kunaweza kukawa si jambo la hiari yako, bali mshangao unaolenga
baraka na ushirikishwaji wa utukufu wa Mungu na kuwa sehemu ya utukufu huo.
Jambo hili linamtokea Simoni Mkirene. "Na walipokuwa wakimwondoa
walimkamata mtu mmoja, Simoni Mkirene, aliyekuwa ametoka shamba, wakamtwika
Msalaba, auchukue nyuma yake Yesu." Lk 23:36. Ndugu yangu, yaliyotokea kwa
Mkirene huyu yawezekana kabisa yametokea kwako au yakatokea kwako. Kuna nyakati
nyingine hatujua sababu haswa ya kuingizwa katika mateso ya wengine.
Tunawajibika kubeba lawama za wengine hata pale ukweli unapojulikana kwamba
hatuhusiki.
Umefikia hata kutengwa
na ndugu kwa sababu usizozifahamu. Ndugu yangu, lichukulie jambo hilo kama
Mkirene. Ni mshangao wenye neema na utukufu ndani yake. Kwenye Msalaba pana
mateso, na penye mateso pana baraka na Utukufu. Kwa mantiki hii, hakuna utukufu
pasibo Msalaba; na hakuna Msalaba usio na utukufu tunapoubeba na Kristo
aliyeshinda mateso ya Msalaba. Acha kulalamika! Mtazame Yesu. Mpendwa, Msalaba
ni fahari kwetu wakristo hasa tunatafakari maneno haya ya siku ya ijumaa kuu
kabla ya kutoa heshima kwa Msalaba Mtakatifu. Maneno hayo Padre au Shemasi
huyasema akiwa anaufunua Msalaba uliofunikwa kitambaa, na kusema, "Huu
ndiyo Mti wa Msalaba, ambao wakovu wetu umetundikwa juu yake. Njoni njoni
tuuabudu." Msalaba ni FAHARI kwetu kwa sababu wokovu wetu umetundwa juu
yake. Mtume Paulo analiongelea jambo hili kwa kusema, "lakini mimi, hasha,
nisione fahari juu ya kitu cho chote ila Msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo,
ambaye kwa huo ulimwengu umesulubishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu," Gal
6:14.
Msalaba ni UNYENYEKEVU.
Msalaba wa Kristo watufunza unyenyekevu halisi. Msalaba unaturudisha kwenye
uhasili wetu kama wanadamu. Tunakumbushwa katika mateso na mahangaiko yetu kuwa
na kubaki kama mwanadamu. Tunapojaribu kujikweza na kuwa kama Mungu au kitu
kingine, tunabakia kuwa shetani ambaye alitamani hivyo. Mtume Paulo anasema, "tena,
alipoonekana ana umbo kama mwanadamu,
alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya Msalaba," Flp
2:8. Unyenyekevu ni msingi wa fadhila zote. Unyenyekevu utufunza. Ni darasa la
maisha muda wote hadi kufa. Yesu analithibitisha hilo kwa kifo chake. Kwenye
ulimwengu huu wa ushindani ni vigumu kunielewa. Ila ukitaka kupata maarifa ya
kimungu jinyenyekeze kwa kujua umaana wake, "kwa sababu neno la Msalaba
kwao wanaopotea ni upuuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya
Mungu," 1Kor 1:18. Ndugu yangu, ni nini zaidi ya nguvu ya Mungu katika
maisha yako? Je, ni sifa, kufahamika, pesa, umaarufu, cheo, ufahamu (akili),
unavyoving'ang'ania kwa nguvu zote? Je, tunaitaji hayo kufuzu maisha ya
umilele? Ndugu yangu unayesoma habari hii jipange sawa sawa!
Msalaba ni UPATANISHO.
Tumepatanishwa na Mungu kwa mateso na kifo cha Bwana wetu Yesu Kristo pale
msalaba. "Akawapatanisha wote wawili katika mwili mmoja, kwa njia ya
msalaba, akiisha kuufisha ule uadui kwa huo msalaba, " Efe 2:16. Kwanza
kabisa kwa kuupokea msalaba katika maisha yako ya kila siku unapata nafasi ya
kujikusanya na kuzama zaidi katika makusudio ya mahangaiko na mateso yako, na
siyo jibu lake. Mahangaiko na mateso mengine katika maisha hubakia kuwa fumbo,
na kama ni fumbo halina jibu kwa sababu si tatizo. Matatizo yana majibu, fumbo
halina jibu. Tunalielewa tu kwa kujikusanya na kuzama katika tafakari, ikilenga
katika umaana wa fumbo hilo (mateso na mahangaiko).
Mfano: mmeishi miaka
zaidi 10 bila kupata mtoto. Mnampata mnajawa FURAHA. Mnamsomesha na anapata
kazi nzuri. Mnafurahi. Anampata mchumba mwema na mwaminifu. Mnafurahi. Siku
moja kabla ya ndoa yao, mtoto wenu huyo anapata ajali anafariki. Mkitazama umri
wenu umefikia saa 12 jioni. Nyumbani kwenu mlitegemea mjukuu mnajikuta mpo na
paka na mbwa tu. Ni majonzi makubwa. Ila mtazame Mungu. Yesu Kristo ni Mtoto
pekee wa Mungu. Lakini Mungu kamtoa sadaka kwa ajili ya wokovu wetu. Katika
hili watazame Ibrahimu na Mama María. "Na penye msalaba wake Yesu walikuwa
wamesimama mamaye, na umbu la mamaye, Mariamu wa Klopa, na Mariamu
Magdalene," Yoh 19:25. Hapa tunaonja uchungu na Faraja. Ni uchungu kwa
namna ya kifo hicho na matazamo wetu kibinadamu. Ni Faraja kwa sababu yametimia
makusudio ya Mungu kwa upendo wake
kwetu sisi wanadamu. "Basi
Yesu alipokwisha kuipokea ile siki, alisema, Imekwisha. Akainama kichwa,
akaisalimu roho yake," Yoh 19:30.
Ndugu yangu, hakuna
UTUKUFU kwa yeyote ajiitaye mkristo pasipo MSALABA. Msalaba ni Bendera yetu na
twapasa kuipeperusha hadi mwisho wa safarí. Ni kweli njiani tunakutana na
tufani zito la upepo na vimbunga vya hapa na pale. Shikilia vyema mlingoti huo
uliobeba BENDERA. Hapo tutapata NEEMA, BARAKA na UTUKUFU. Ni hapo tu twaweza
kulichagua na kukaa mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Basi ndugu
yangu, "ukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu;
ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na
kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu, "
Ebr 12:2.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mtu ye yote akitaka kunifuata na
ajikane mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate,” Mk 8:34b
Tusali:-Ee
Yesu uliye shujaa na mshindi wa mateso, kifo na msalaba, tujalie kila mmoja
wetu kuona fahari juu ya Msalaba na changamoto za maisha ya kila siku, kadiri
ya wito ulotujalia na huduma tuitoayo. Kamwe tusiupige kisogo msalaba wako
Mtakatifu. Tutakatifuze na Msalaba wako wenye ushindi na Utukufu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario