domingo, 19 de febrero de 2017

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 7 YA MWAKA-I


JUMANNE WIKI YA 7 YA MWAKA-I

Somo: YbS 2:1-13

Zab: 37:3-4, 18-19, 27-28, 39-40

Injili: Mk 9:29-37

Nukuu:

“Mwanangu, ukija kumtumikia Bwana, weka tayari roho yako kwa kujaribiwa,” YbS 2:1

“Ujitengeneze moyo ustahimili, wala usitaharuki siku ya kuteswa,” YbS 2:2 

“Uambatane naye wala usijitenge tena, ili mwisho wako ukuzwe,” YbS 2:3

“Kila utakalopelekewa ulipokee kwa kuchangamka moyo, uyavumilie mabadiliko ya unyonge wako,” YbS 2:4

Kwa sababu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake, akawaambia, Mwana wa Adamu yuaenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua; hata akiisha kuuawa, baada ya siku tatu atafufuka,” Mk 9:31

Akaketi chini, akawaita wale Thenashara akawaambia, Mtu atakaye kuwa wa kwanza atakuwa wa mwisho kuliko wote, na mtumishi wa wote,” Mk 9:35

“Mtu akimpokea mtoto mmoja wa namna hii kwa jina langu, anipokea mimi; na mtu akinipokea mimi, humpokea, si mimi, bali yeye aliyenituma,” Mk 9:37

TAFAKARI: “Umkabidhi Bwana njia yako, Pia umtumaini, naye atafanya.”

Wapendwa wana wa Mungu, kufanikiwa katika maisha yanayoongozwa na malengo, ni kuishi maisha yanayosukumwa au kuongozwa wakati wowote na hofu ya Mungu, sala na maombi. Maisha yenye mtazamo huu kwa ujumla wake utufikisha kwenye kusudio la maisha ya kiroho. Kuongozwa au kusukumwa na hofu ya Mungu uturejesha kwenye kusudio la uumbaji wetu, na hali yetu halisi, yaani, ubinadamu wetu. Hofu hii ya Mungu umulika na kutukumbusha kila mara kusudi la kuumbwa kwetu, yaani, tumjue Mungu, Kumb 6:5, tumpende Mungu na majirani zetu, Mt 22:29, kumtumikia Mungu na wale tuliopewa dhamana juu yao, Gal 5:13, na mwisho tuupate uzima wa milele. Hii ni hatua ya mwisho kama asemavyo Mtume Paulo katika kuvipiga vita vile vya imani hapa dunia, yaani, “mkiisha kuwekwa huru, na kuwa mbali na dhambi, na kufanywa watumwa wa Mungu, mnayo faida yenu, ndiyo kutakaswa, na mwisho wake ni uzima wa milele,” Rum 2:22. Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, hayo ndiyo maisha yanayoongozwa au kusukumwa na hofu ya Mungu.

Ndugu yangu, hatutaweza kuifikia hali hiyo kama tutabebwa na wimbi la dunia tunaloishi leo kama litakavyo. Tunaishi katika ulimwengu wa ushindani, na wakati mwingine pasipo washindani au washindaniwa. Ni ulimwengu wa vitu, na utafutaji wa  vitu kila siku hata kama havina tija leo na kwa sasa. Mtindo na mtazamo huu wa maisha huaribu na upoteza lengo na sababu ya kuumbwa kwetu. Hofu ya Mungu hutoweka, na maisha ya sala na maombi hukosa ladha yake, kama Mtume Yakobo asemavyo, Mwatamani, wala hamna kitu, mwaua na kuona wivu, wala hamwezi kupata. Mwafanya vita na kupigana, wala hamna kitu kwa kuwa hamwombi!” Yak 4:2. Maisha yenye msukumo huu kamwe mbele ya safari hayana ushindi. Ni kushindwa tu! Ni maisha yaliyokosa malengo. Ni maisha bila hitimisho ambalo kwa uhakika lipo, yaani, maisha ya umilele.

Ndugu yangu, ni kweli pasipo shaka kabisa kwamba usipo thamini umilele kama hitimisho la maisha yako, nguvu na akili zako zote zitajikita kwa haya ya leo na kesho ambayo kwa uhakika kama yalivyo hayana umilele. Katika kweli hii Yesu anakuambia wewe na mimi kwamba, “msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako,” Mt 6:19-21. Ndugu yangu, chunguza kile kinachochukua muda wako mwingi hapa duniani na ujiulize kama kina uhusiano na umilele wako mara baada ya maisha haya hapa duniani. Ndugu yangu, tukiwa na uadui na Mungu kuna kushinda kweli vita hiyo? Hakika hakuna kushinda!

Hivyo pamoja na raha na anasa zake mwisho wa siku hakuna faida yoyote. Basi kila mmoja na haihoji dhamiri yake kwa swali hili la Yesu kama anavyotuuliza, “Kwa kuwa itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake? Ama mtu atoe nini badala ya nafsi yake?” Mk 8:36-37. Ndugu yangu, pasipo shaka sindano hiyo imekuingia vizuri. Tafakari!

Wapendwa wana wa Mungu, ili tufikie lengo la maisha ya kiroho twahitaji kuishi na kukumbatia muda wote fadhila ya unyenyekevu. Unyenyekevu uturudisha katika hali ya ubinadamu wetu pale tunapotaka kujiumba na kuvaa taswira nyingine kama tokeo la majivuno yetu, mafanikio yetu kimaisha, na hata ufahamu wetu. Ndugu yangu, chochote kile kitakachojiumba kama tokeo la kujikuza zaidi na kuipoteza ile hofu ya Mungu ndani yako, mwisho wake ni kupoteza dira ya hitimisho la maisha yako, yaani, umilele wake.

Ndugu zangu, tusipokuwa na hofu hii ya Mungu hatutaweza kumtii Mungu na wala kumkaribia kwa sababu Mungu hatakuwa na nafasi ndani ya moyo wako. Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia,” Yak 4:7. Hili litawezekana tu pale tutakapokuwa tayari kujinyenyekesha na kuiishi hofu ya Mungu.

Ndugu zangu, waswahili wana msemo huu: “Maji ukishayavulia nguo huna budi kuyakoga.” Hivyo wosia kwa ye yote yule aliye tayari kuliondoa giza, yaani, uovu, na kuuleta mwanga, yaani, wema wa Mungu na kuishi kama wana Mungu, jambo hili lazima alijue kwa undani, yaani, “ukija kumtumikia Bwana, weka tayari roho yako kwa kujaribiwa,” YbS 2:1. Hutoweza kupigana vita dhidi ya uovu kama hujajiandaa vizuri kimwili na kiroho. Elewa katika vita hiyo unapambana na giza dhidi ya mwanga. Yule mwovu, yaani shetani, na mwenye kuufurahia ufalme wake, uovu ndiyo heri na furaha kwake. Hivyo maandalizi ya kimwili na kiroho ni muhimu sana. “Ujitengeneze moyo ustahimili, wala usitaharuki siku ya kuteswa,” YbS 2:2. Nguvu na silaha yako ni Muumba wako. “Uambatane naye wala usijitenge tena, ili mwisho wako ukuzwe,” YbS 2:3. Hakuna mtu ye yote aliyemtegemea Mungu akaachwa ukiwa. Itazame historia ya Kanisa letu Katoliki na ile mbegu iliyopandwa na watakatifu wafiadini. Ukweli huo wa wafiadini watufundisha kwamba, “kila utakalopelekewa ulipokee kwa kuchangamka moyo, uyavumilie mabadiliko ya unyonge wako,” YbS 2:4

Wafiadini hawa walihimarishwa kwa nguvu na neema ya Mungu kwa sababualimtegemea Mungu pasipo shaka yoyote. Wataalamu wa kufua vyuma, na hasa wale waitengenezayo dhahabu wanasema hivi, ‘kuijua dhahabu ipo tayari katika kweli yake ni pale utakapoiona sura yako kwenye dhahabu hiyo.’ Maana yake ni kwamba dhahabu hiyo haina chembe yoyote ya uchafu. Ni katika kweli hii kwamba jaribu ufananishwa na dhahabu ipitayo kwenye moto mkali. “Maana dhababu hujaribiwa motoni, na watu wateule kalibuni mwa unyonge,” YbS 2:5. Jamii yetu ya leo kuitoa hapo ilipo na kuipeleka palipo pazuri zaidi, hatuna budi kupita kwenye changamoto hii ya dhahabu.

Haya yote yanawezekana pale tu imani hai katika ufahamu wake na uamaana wake kuwa nguzo imara katika kuishi na kutenda. Hivyo “basi umwamini Yeye, naye atakusaidia; ukazinyoshe njia zako, na kulikaza taraja lako katika Yeye,” YbS 2:6. Mahangaiko na sintofahamu zake katika maisha ni swala la muda tu. Jambo la muhimu katika safari hii ya ‘mwanga dhidi ya giza,’ ‘wema dhidi ya uovu’ ni kutopoteza tumaini kwa sababu uovu katika asili yake hauna umilele. Hivyo wito ni kwamba, “enyi mnaomcha Bwana, zingojeeni rehema zake, msigeuke upande msije mkaanguka. Enyi mnaomcha Bwana, mwaaminini Yeye sana, thawabu yenu haitawapotea,” YbS 2:7-8

Ufahamu na umaana huu katika imani utupa furaha ya kweli hata katika mateso. “Enyi mnaomcha Bwana sasa tarajieni mema na furaha ya daima na rehema,” YbS 2:9. Mateso ukupa maana endapo wajua sababu ya teso hilo, ukilinganisha na furaha ile ya kweli ambayo hakuna wa kutuondolea. “Amin, amin, nawaambia, Ninyi mtalia na kuomboleza, bali ulimwengu utafurahi; ninyi mtahuzunishwa, lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha. Basi ninyi hivi sasa mna huzuni; lakini mimi nitawaona tena; na mioyo yenu itafurahi, na furaha yenu hakuna awaondoleaye,” Yoh 16:20, 22.

Historia ya maisha yetu wanadamu, na hasa mang’amuzi katika maisha, ni mwalimu mzuri sana. Wewe na mimi yatupasa kwenda kwa adabu tukijali utu wa watu kwa kusimama katika kweli na haki. Hapa ndipo ilipo pona yetu kwa wale wote tuliopewa dhamana ya uongozi na umma wa watu. “Angalieni vizazi vya kale mkaone: nani aliyemtumaini Bwana akaaibika Nani aliyekaa hali ya kumcha akaachwa? Nani aliyemwita akadharauliwa?” YbS 2:10.

Tunapodondoka katika kufikiri kwetu, kuamua kwetu, na kutenda kwetu, tusione haya kukiri mapungufu hayo kwa sababu huruma na neema ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu. Ni vyema mara zote nikajipatanisha mimi na Mungu, mimi na jirani, na mimi na mazingira yangu. Mafiga haya matatu ni muhimu sana katika ustawi wa upendo, kweli, haki, na amani katika jamii yoyote ile ya watu. Ndugu yangu, “Bwana yu mwenye huruma na rehema, husamehe dhambi na kuokoa wakati wa shida,” YbS 2:11.

Kuna anguko kubwa sana pale ninaposhindwa kujipokea, yaani, kutambua kuwa mimi ni binadamu tu na ndivyo ilivyompendeza Mungu kuniiumba kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Mungu hakufanya makosa wala kukosea kuniumba kama nilivyo. Na agizo la Mungu la mimi niwe pale alipo Yeye ni hili: “Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48. Bila ukamilifu huu, na utakaatifi huu siwezi kamwe kuwa pale alipo Mungu. Nisipo kiri hali hii na kuchukua hatua stahiki huko mbele ya safari ni giza tupu. Angalizo ni hili: “Ole wao wenye mioyo ya woga, wenye mikono iliyolegea, wakosaji waendao njia mbili. Ole wake aliye dhaifu wa moyo kwa maana amekosa imani, kwa hiyo hatahifadhiwa,” YbS 2:12-13. Unyenyekevu ndicho kivuko sahihi katika kiunzi hiki cha moyo wa woga, na mikono legelege (utoaji huduma kwa upendeleo).

Nguvu ya ufahamu, madaraka, karama, na vipaji tulivyojaliwa na Mungu nivitumie kwa Sifa na Utukufu wa Mungu. Mungu kwa kupitia hayo aliyonikirimia bila kipimo yamfanye aonekane kwa watu wote pale nilipo bila kujali itikadi zao kisiasa na kiimani, na hata historia zao nzuri au mbaya.

Wapendwa katika Kristo, maisha ya unyenyekevu na hofu ya Mungu hayatupeleki tu karibu na Mungu, bali utufanya kuwa tayari kutahabikiana katika hali zote za maisha na mahangaiko yake. Pasipo kujishusha ni vigumu kuyaona mahangaiko ya wengine na kuyabeba kama moja ya changamoto na misalaba yenye nuru ya Utukufu.

Yesu anataka tulione jambo hili vizuri ikiwa yeye ndiye kielelezo chetu. Hivyo ni “kwa sababu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake, akawaambia, Mwana wa Adamu yuaenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua; hata akiisha kuuawa, baada ya siku tatu atafufuka,” Mk 9:31. Hata hivyo Mwinjili Marko anatuambia hawakulifahamu neno lile kwa sababu walijawa na uoga na hivyo walishindwa kumuuliza Yesu, Mk 9:32

Ndugu yangu, kutokujishusha hakutakuandaa na kuwa tayari kutumika kwa ajili ya wengine. Je, kila mmoja wetu akiupenda ukubwa bila kutumika tutaepuka machafuko? Wanafunzi wa Yesu, yaani wale Thenashara, wanapatwa na ushindani huu wakiwa njiani wakipita katikati ya Galilaya na Yesu, Mk 9:34. Yesu anawaambia kiini cha ukubwa huo wanaoutamani.Akaketi chini, akawaita wale Thenashara akawaambia, Mtu atakaye kuwa wa kwanza atakuwa wa mwisho kuliko wote, na mtumishi wa wote,” Mk 9:35.

Ukubwa ni utumishi, na kutumika kweli kwa ajili ya wote pasipo kuweka mbele faida au maslahi binafsi. Huu ndio ule utumishi usio na faida kama anavyotuambia Yesu; “Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya,” Lk 17:10. Hakika sote leo tuliopewa dhamana ya uongozi katika nyanja mbalimbali katika Taifa letu- Tanzania, tungaliishi hofu hii ya Mungu na kweli katika hali ya kutumika, Kristo angeonekana kwa kila mtu.

Tusifu Yesu Kristo! 

“Mtu akimpokea mtoto mmoja wa namna hii kwa jina langu, anipokea mimi; na mtu akinipokea mimi, humpokea, si mimi, bali yeye aliyenituma,” Mk 9:37

Tusali: Ee Yesu Mwema, tujalie fadhila ya unyenyekevu, na utayari wa kutumika kwa ajili ya wengine. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario