lunes, 13 de febrero de 2017

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 6 YA MWAKA-I


JUMATANO WIKI YA 6 YA MWAKA-I

Somo: Mwa 8:6-13, 20-22

Zab: 116:12-13, 14-15, 18-19                      

Injili: Mk 8:22-26

Nukuu:

“Ikawa baada ya siku arobaini, Nuhu akalifungua dirisha la safina, alilolifanya,” Mwa 8:6

“Akangoja na siku saba tena, akamtoa yule njiwa; naye asimrudie tena kamwe,” Mwa 8:12

“Nuhu akamjengea Bwana madhabahu; akatwaa katika kila mnyama aliye safi, na katika kila ndege aliye safi, akavitoa sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu,” Mwa 8:20

“Bwana akasikia harufu ya kumridhisha; Bwana akasema moyoni, Sitailaani nchi tena baada ya hayo kwa sababu ya wanadamu, maana mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake; wala sitapiga tena baada ya hayo kila kilicho hai kama nilivyofanya,” Mwa 8:21

“Wakafika Bethsaida, wakamletea kipofu, wakamsihi amguse,” Mk 8:22

“Ndipo akaweka tena mikono yake juu ya macho yake, naye akatazama sana; akawa mzima, akaona vyote waziwazi,” Mk 8:25

TAFAKARI: “Bwana akasema moyoni, Sitailaani nchi tena baada ya hayo kwa sababu ya wanadamu.”

Wapendwa wana wa Mungu, ukiitazama historia ya uumbaji na wokovu wa mwanadamu katika ujumla wake utagundua kwamba Mungu ana mpango mpana sana na viumbe vyake, binadamu akiwa ana nafasi kubwa katika uumbaji huo. “Maana Bwana, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine,” Isa 45:18. Hata pamoja na kweli hii, Mungu aliyemuumba binadamu huyu kwa sura na mfano wake, hakumuumba katika maana au hali ya kutenda mazuri tu bila kumpa uwezekano wa kutenda mabaya pia.

Mungu alimuumba mwanadamu huyu huru kweli kweli, katika mizania ya kwenda hata kinyume kabisa na mpango wake Mungu. Isingelikuwa hivyo basi mwanadamu huyu asingeliwajibika kwa makosa yake mwenyewe. Hapa ndipo linapokuja swala zima la nguvu ya kimaadili. Binadamu huru ni yule aliye huru kimaadili, yaani, ‘yupo huru kufanya baya, na anao uhuru pia wa kutolifanya baya hilo.’ Hivyo kwa uhuru wa kimaadili aliokuwa nao mwanadamu aweza kumwasi Muumba wake, na kwa uhuru huo huo aweza kumrudia Muumba wake.

Somo letu la kwanza laonyesha namna hiyo ya uhuru tuliojaliwa katika muono mpana wa uumbaji, na somo la Injili linatupa picha kuhusu historia nzima ya wokovu wetu. Taswira zote hizi mbili zinathibitishwa na maneno haya ya Mungu baada ya Nuhu kumtolea Mungu sadaka ya kutekekezwa kama tendo la shukrani. “Bwana akasikia harufu ya kumridhisha; Bwana akasema moyoni, Sitailaani nchi tena baada ya hayo kwa sababu ya wanadamu, maana mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake; wala sitapiga tena baada ya hayo kila kilicho hai kama nilivyofanya,” Mwa 8:21.

Ndugu yangu, hii ndiyo sababu kubwa licha ya nyakati nyingine twapigwa butwaa na kukatishwa tamaa kuona ‘kwenda sambamba baina ya Mungu (mwenye Nguvu, Uwezo, Ajuaye yote, na Mtakatifu) na uwepo wa uovu.’ Sehemu hii ya pili ya kwenda sambamba huku baina ya uwepo wa Mungu na uovu ni tendo hili la uponyaji wa mtu yule aliye kipofu katika Injili ya leo, Mk 8:22. “Ndipo akaweka tena mikono yake juu ya macho yake, naye akatazama sana; akawa mzima, akaona vyote waziwazi,” Mk 8:25. Ndani na katika uwepo wa Mungu mwanadamu aweza kutoka na kuingia kwa sababu uhuru huo anao kimaadili. Hivyo wewe na mimi hatuwezi kukwepa wajibu wala kuwajibika kwa makosa yetu wenyewe. Uovyo wa yeyote yule, na mbaya zaidi kwa yule aliyepewa dhamana na umma wa watu ni pale anapokosa nguvu ya kimaadili. Ni sawa na maneno haya ya Yesu, kwamba, “ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu,” Mt 5:13.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Ikawa baada ya siku arobaini, Nuhu akalifungua dirisha la safina, alilolifanya,” Mwa 8:6

Tusali:-Ee Yesu Mwema, mara zote tukumbushe wajibu wetu, na tutende kimaadili. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario