ALHAMISI WIKI YA 6 YA MWAKA-I
Somo:
Mwa 9:1-13
Zab:
102:16-18, 19-21, 22-23
Injili:
Mk 8:27-33
Nukuu:
“Mungu akambariki Nuhu
na wanawe, akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi,” Mwa 9:1
“Mimi nauweka upinde wangu winguni, nao
utakuwa ni ishara ya agano kati yangu na nchi," Mwa 9:13
“Naye akawauliza, Na
ninyi mnasema ya kuwa mimi ni nani? Petro akamjibu, akamwambia, Wewe ndiwe
Kristo,” Mk 8:29
“Akawaita mkutano
pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, Mtu ye yote akitaka kunifuata na ajikane
mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate,” Mk 8:34
“Kwa kuwa mtu atakaye
kuiponya nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili
yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha,” Mk 8:25
TAFAKARI:
“Atakayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake huyo itamwagwa na mwanadamu, maana
kwa mfano wake Mungu alimfanya mwanadamu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
ni kweli isiyo shaka kwamba nafsi husalimika kwa kulipenda na kuliegemea tunda
la roho, Gal 5:22-23, na pale tu unapokuwa tayari kumfuata Kristo, kujikana
nafsi, na kujitwika msalaba wako kwa hiari bila shuruti. Yesu “akawaita mkutano
pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, Mtu ye yote akitaka kunifuata na ajikane
mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate,” Mk 8:34. Tukijua aliye mkamilifu
ni Mungu tu, basi kila mwanadamu ili aufikie ukamilifu na kumwona Mungu kama
alivyo itampasa kujisafisha kwa kile ambacho kwa tafsiri ya ndani ni ‘msalaba
wa kila mmoja wetu.’
Msalaba katika tafsiri
hii twaweza kusema ni mapungufu aliyokuwa nayo kila mmoja wetu karidi ya maisha
na wito wake. Madhaifu na mapungufu yetu huponywa pale tu tunapoyapokea ndani
na katika Kristo. Hivyo, “tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza
imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili
msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha
Mungu. Maana mtafakarini sana yeye
aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi
zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu,” Ebr 12:2-3
Ukweli wa maisha na
tafsiri ya ‘Msalaba,’ katika mwono wa Injili ya leo unatupeleka ndani zaidi
kuijua Imani yetu na yule tunayemwamini na kumfuata. Kumjua ni nani
tunayemfuata, Yesu anauliza swali la uchokozi kwa wanafunzi wake, na Petro
anatoa jibu, tena jibu lililo sahihi kabisa. “Naye akawauliza, Na ninyi mnasema
ya kuwa mimi ni nani? Petro akamjibu, akamwambia, Wewe ndiwe Kristo,” Mk 8:29.
Kristo yaani, aliyewekwa kwa sababu hiyo, yaani, wokovu wa mwanadamu. Huyu
ndiye Masiha kwa ajili ya wokovu wetu.
Imani ya kweli huwezi
itofautisha na matendo ya kweli yanayoambatana na kile mtu anachoamini. Na
wakati mwingine matendo (ya upendo na huruma) husema zaidi ya kila kilicho
ndani ya mtu yaani, Imani (yanayoonekana na yasiyoonekana). “Lakini mtu
atasema, Wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo
matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu,” Yak 2:18.
Nabii Isaya yupo tayari kupokea kadhia zote kwa sababu anayo Imani na Mungu
anayemwamini kuwa ndiye msaada na kweli katika yote. “Naliwatolea wapigao mgongo wangu, na wang'oao ndevu mashavu yangu;
sikuficha uso wangu usipate fedheha na kutemewa mate,” Isa 50:6. Nabii Isaya yupo tayari kupokea fedheha zote
akijua mwisho wa siku mateso yake si bure kwani anaye mtetezi wa kweli yaani,
Mungu. “Maana Bwana MUNGU atanisaidia; kwa sababu hiyo sikutahayari, kwa
sababu hiyo nimekaza uso wangu kama gumegume, nami najua ya kuwa sitaona haya,”
Isa 50:7.
Je,
mateso uliyonayo yanakupa mwanga zaidi kuhusu Imani yako? Tunapozungukwa na mateso na hali ya kukata tamaa
tujifunze kutoka kwa Mtume Paulo na kusema, “Lakini mimi, hasha, nisione fahari
juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo
ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu,” Gal 6:14. Mwenye Msalaba
kuna upya wa mambo, nuru, uhai, na furaha ya kweli. Naye Mtume Paulo anasema,
“Kwa
hiyo napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa
ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu,” 2Kor 12:10. Ikiwa
tafsiri ya udhaifu na mahangaiko yetu ni “Msalaba,” basi hatuna sababu ya
kukata tamaa kwa sababu, kwenye angaiko na udhaifu huo kuna upya wa mambo,
nuru, uhai, na furaha ya kweli. Je, nifanye nini?
Katika hali na
mazingira hayo napaswa kuwa na muono chanya, yaani, nikubali na kupokea kuwa
hilo ni tatizo, na kutoka hapo nichukue hatua kuelekea upya huo, nuru hiyo,
uhai huo, na furaha hiyo ya kweli. Je, kabla ya kutumia dawa kwa ajili ya
uponyaji, haitupasi kwanza kujua una sumbuliwa na ugonjwa gani? Kama hili
twalifanya, ni hivyo hivyo hata kwa maisha ya kihoro na afya yake.
Hivyo hatuna sababu ya
kujidhuru au kuendelea kuutia uhai matatani. Utajiri wako mkubwa siyo mali na
vitu ulivyonavyo vya kushikika, bali ni afya yako, uhai wako. Bila afya na uhai
ulionao, yote ulionayo ya kushikika upoteza maana yake. Na hili ndilo angalizo,
na agizo la Mungu kwetu, kwamba, “Atakayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake
huyo itamwagwa na mwanadamu, maana kwa mfano wake Mungu alimfanya mwanadamu,”
Mwa 9:6. Uhai ni mali ya Mungu, na zawadi ya Mungu kwetu. Niliye hai leo
yanipasa kuulinda uhai wangu, na wa mwenzangu hadi hapo Mungu mwenyewe
atakapoutwa.
Baada ya gharika ile,
Mungu anaurudisha uhai na ukaribu wake kwa viumbe vyake. “Mungu akambariki Nuhu
na wanawe, akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi,” Mwa 9:1. Kuzaa,
kuongezeka, na kuijaza nchi, kwa funua furaha na utukufu wa Mungu. Hakuna
chochote kilicho na kama kilivyo kisichoifunua furaha na utukufu wa Mungu.
Ndugu yangu, “hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna
afaye kwa nafsi yake,” Rum 14:7. Mungu huwasiliana na mwanadamu kila siku na
kwa njia mbalimbali. Mawasiliano haya hayakinzani na uelewa wa mwanadamu kwa
nyakati zote, licha ya maendeleo aliyo nayo. Hivyo si sahihi kusema kwamba,
“maendeleo ya sanyansi na technologia yamemfanya mwanadamu kuwa mbali
na Muumba wake.” Kinyume chake ni kwamba, mwanadamu huyu yupo mbali na
maendeleo hayo kwa kukikimbia kivuli chake. Hapa ndipo tunapoona vizuri ile
falsafa ya mbuni, yaani, “kukificha kichwa chake kwenye mbawa zake, ilhali
mwili sehemu yote ya mwili ikiwa wazi na kuonekana.”
Hatuwezi kumkimbia
Mungu kwa vigezo vya maendeleo na upya wa ufahamu wetu. Maendeleo hayo ya
kisayansi na kiteknologia yalishawekwa na Mungu mwenyewe, naye hachoki
kuyaratibisha. Naye anasema, “Mimi nauweka upinde wangu winguni, nao utakuwa ni
ishara ya agano kati yangu na nchi," Mwa 9:13. Je, katika kweli hii,
wavumbua kilicho chako katika upya na upekee wake, au wakitambulisha kile
ambacho kilikuwa bado kutambulika kwa wengine? Tafakari!
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya
nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu na
kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha,” Mk 8:25
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, tujalie neema ya kuishi fumbo zima la Msalaba kwa sababu katika huo
kuna Utukufu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario