JUMAPILI YA 6 YA
MWAKA-A
Somo I: YbS 15:15-20
Zab: 119: 1-2, 4-5, 17-18, 33-34
Somo II: 1Kor 2:6-10
Injili: Mt 5:17-37
Nukuu
“Ukipenda,
utazishika amri zake, na kutenda amini ni shauri lako,” Ybs 15:15
“Mbele
ya mwanadamu upo uzima na mauti, naye atapewa apendavyo,” YbS 15:17
“Walakini
iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu; ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao
wanaoitawala dunia hii, wanaobatilika,” 1Kor 2:6
“Mambo
ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, (Wala hayakuingia katika
moyo wa mwanadamu) Mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao,” 1Kor 2:9
“Msidhani
ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali
kutimiliza,” Mt 5:17
“Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele
mmoja kuwa mweupe au mweusi,” Mt 5:36
TAFAKARI:
“Ukipenda, utazishika amri zake, na kutenda amini ni shauri lako.”
Wapendwa wana wa Mungu,
Sheria ya Bwana ni utaratibu wa kuyaishi yale yampendezayo Mungu, na kuwa na
mahusiano mazuri naye kwani Yeye ndiye uhai na uzima wetu. “Ameweka mbele yako moto na maji; utanyosha mkono
wako uchaguavyo,” YbS 15:16 Wana wa Israeli walipewa sheria kama
mwongozo wa kutenda na kuwa na mahusiano mazuri na Mungu. “Bwana akamwambia
Musa, Njoo huku juu kwangu mlimani, uwe huku; nami nitakupa mbao za mawe na ile
sheria na hiyo amri niliyoiandika ili uwafundishe,” Kut 24:12. Sheria hizi
zilipaswa kufuatwa kiaminifu, upendo kwa jirani, na bila kuzichakachua. “Ukipenda, utazishika amri zake, na kutenda amini ni
shauri lako,” Ybs 15:15
Ukamilifu na uaminifu
wa mtu ulipatikana katika kuzishika sheria za Bwana. Kwa sababu, “sheria ya
Bwana ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa Bwana ni amini, Humtia
mjinga hekima.” Zab 19:7. Hivi ndivyo ilivyopaswa kuzishika sheria za Bwana. Na
hilo ndilo lililokuwa kusudi la sheria. Jambo la kushangaza wakati wa Yesu,
Wayahudi hawakuwa wanafuata Torati kama iliyokuwa mwanzo, yaani, nyakati za
Musa. Wayahudi walikuwa wanafuata tafsiri ya Torati ambayo iliendana na
matamanio yao na siyo ya Mungu. Huu ndio ugomvi uliokuwepo kati ya Yesu na
Waandishi na Mafarisayo.
Matamanio haya ya
Mafarisayo na Waandishi katika ubinadamu wao ambayo yalienda kinyume na tamanio
la Mungu juu ya sheria nyakati zile za
Yesu, ndiyo hayo yaliyojitokeza pia nyakati zile za Nabii Eliya na wale wafuasi
wa miungu ya Baali. Kuwarudisha kwenye mstari wa kweli na haki, ikiwa ni
kumfuata na Mungu wa kweli na wakuabudiwa, Nabii Eliya anawaasi na kusema, “Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini?
Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni
yeye. Wale watu hawakumjibu neno,” 1Fal 18:21.
Ndugu yangu
tunayesafiri sote katika tafakari hii, kwa hiki kilichotokea, Wayahudi
hawakupaswa kukengeuka katika imani yao. Ila kadiri tusomapo historia ya Taifa
hili la Israeli na kutafakari, tunaona mambo hayakuwa kama yalivyopaswa kuwa. Hali ya uvuguvugu wa imani ya kweli ilikuwa hivyo hata
nyakati za Yesu hata pamoja na kupewa torati kama mwongozo wa kufuata na kuwa
karibu na mapenzi ya Mungu.
Jambo muhimu sana la
kujua ni kwamba kipindi cha Yesu, Wayahudi na hasa mafarisayo na waandishi
hawakuwa wanaifuata Torati kama iliyokuwa, ila tafsiri yake (maisha ya dini na
matendo yake kupitia masimulizi), iliyojulikana kwa ujumla kama TALMUD. Talmud
ilibeba mambo mawili: MIDRASH (tafsiri ya mambo mbalimbali toka Torati), na
MISHNAH (marudio/waliyorudia au mafundisho)
Kwa mantiki hiyo hapo
juu ya TALMUD, vitabu vile vitano vya Torati vingewezwa kuandikwa kwa kurasa
350 tu; wakati TALMUD ilichukuwa hadi vitabu 523; vilivyo rudufiwa (printed)
katika mabando (volumes) 22. Haya ndiyo yanayonukuliwa na mafarisayo na
waandishi kama mapokeo ya wazee. Sehemu nyingi za mafundisho ya Yesu anapinga
jambo hili la kufuata mapokeo ambayo ni tafsiri kutoka Torati, (Mt 15:2-3, 6;
Mk 7:3, 5, 8, 9, 13). Naye Yesu anawaambia, “Ninyi mwaiacha amri ya Mungu, na
kuyashika mapokeo ya wanadamu,” Mk 7:8. Kwa maneno mengine ni sawa na kuchagua
mauti na kuacha uhai. “Mbele ya mwanadamu upo
uzima na mauti, naye atapewa apendavyo,” YbS 15:17
Mapokea haya ni ukweli
wa Mungu uliopotoshwa. Mtume Paulo baada ya kuongoka na kuujua ukweli kuhusu
sheria ya Bwana anawaambia Wakolosai, “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa
elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa
jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo,” Kol
2:8. Ukweli ni kwamba, Mtume Paulo kama Mfarisayo kabla ya kuongoka kwake
aliyafuata mapokeo haya ya wazee ambayo yalikuwa ni ‘ukweli wa Mungu
uliopotoshwa.’ Paulo anakiri jambo hili na kusema, “Nami naliendelea
katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu,
nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu,” Gal 1:14.
Kwenye jambo hili,
yaani kweli ya Sheria ya Bwana, Yesu anawakemea Mafarisayo na Waandishi na
kusema, “Msidhani ya kuwa nilikuja kuitangua Torati au Manabii; la, sikuja
kutangua, bali kutimiza,” Mt 5:17. Hapa Yesu akubaliani nao kwa swala la
kuichakachua Torati kama walivyokwisha kufanya. Yesu anarudisha mpango mzima wa
Mungu katika safari nzima ya ukombozi wa mwanadamu. Yesu anatoa zaidi maana ya
sheria na ushikaji wa sheria hiyo. Yesu anawakosoa Mafarisayo kwa unafiki wao
katika sheria na kusema, “Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa
mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria,
yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine
msiyaache,” Mt 23:23
Utimilifu wa sheria
kadiri ya mpango mzima na mtazamo wa Yesu umebebwa katika upendo. Hii ndiyo
amri mpya. “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi
mpendane vivyo hivyo,” Yoh 13:34. Mtakatifu Agustino anatuambia kwamba,
“ukipenda utafanya yote.” Ni katika mantiki hii kwamba, “mkipenda, mtazishika
amri zangu,” Yoh 14:15. Je, leo hatushangai kuona baadhi ya viongozi
wakiichakachua Katiba ya nchi zao kwa ajili ya matamanio yao na uchu wao wa
madaraka? Jambo hili limekuwa chanzo kikubwa cha machafuko mengi duniani na
hasa kwenye bara letu la Afrika. Ni ukweli usiopingika kwamba, vikundi vingi
vya kigaidi vimejitokeza pale sauti ya wengi katika mkondo sahihi, yaani,
demokrasia ilipokanyagwa, kuporwa, kubezwa, na hata kubakwa kwa manufaa wa watu
wachache tu katika kundi zima la walio wengi. Tanzania yetu leo haipo mbali na
ukweli huu. “Hekima ya Bwana yatosha, mkuu
mwenye uweza hutazama vyote,” YbS 15:18. Ni vyema tukasoma alama za
nyakati. Nguvu ya madaraka aliyopewa kiongozi na umma wa watu, siyo fimbo ya
kuwachapa, bali kuwaongoza katika kweli na haki.
Leo jamii yetu
imeingiwa na hofu na ubaridi wa ajabu kwa sababu, ‘mwenye nguvu apaswa
kupishwa.’ Wengi waanza kujisiri kuwa kuzuizini ilhali wapo huru. Hapa hakuna
tena hekima ya Mungu. Leo tunatumia nguvu nyingi sana kujenga mnara wa hekima
ya kibinadamu, na mwisho wa siku ni kama yale yaliyotokea kule Babeli, Mwa 11:3-9.
“Walakini iko hekima tusemayo kati ya
wakamilifu; ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao wanaoitawala dunia hii,
wanaobatilika,” 1Kor 2:6. Leo baadhi ya viongozi waliopewa dhamana ya uongozi
na umma wanasahau kuwa wao ni binadamu, tena wenye mifupa na nyama, na kinyume
chake wanajifananisha na Mungu. Katika mazingira haya hakuna “hekima ya Mungu
katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa
utukufu wetu,” 1Kor 2:7. Na mtego wa wengi, hasa upofu wa madaraka hawaijui
hekima hii “hata mmoja; maana kama wangaliijua, wasingalimsulibisha Bwana wa
utukufu,” 1Kor 2:8. Unapotumia madaraka yako vibaya na kuwaumiza watu,
kuwanyong’onyesha watu, na hata kuwatia hofu watu, ujue waendelea kumsulubisha
Kristo aliyekufa kwa ajili yako na hao usiowatendea haki na kweli. Kristo
alikuwa kwa ajili yako na yangu ili sote tuwe huru mwili na roho. Ndugu yangu
pasipo na unyenyekevu hapana uwepo wa Mungu. Hivyo hivyo pasipo upendo, kweli,
na haki twaukataa uwepo wa Mungu. Hivyo, “Mambo ambayo jicho halikuyaona wala
sikio halikuyasikia, (Wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu,) Mambo ambayo
Mungu aliwaandalia wampendao,” 1Kor 2:9. Na hayo ndiyo yafanywayo na
wanyenyekevu wa Mungu, yaani, wenye hofu ya Mungu.
Wapendwa katika Kristo,
Injili yetu ya leo yatutaka tuyapime matendo yetu vyema hasa katika mizania ya
kusamehe na kusamehewa. Yesu katika hili anatoa angalizo kubwa na kusema,
"haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia
kamwe katika ufalme wa mbinguni," Mt 5:20. Mafarisayo na waandishi
walijihesabia haki kuwa ni watu wema, na ndiyo kipimo cha kweli. Ndugu yangu,
Mungu pekee ndiye hutuhesabia haki, tena si kwa matakwa yetu, bali kwa matakwa
yake kwa sababu Yeye tu ndiye HAKI. Sisi binadamu tunashiriki tu ukamilifu wa Mungu
kwa kuwezeshwa naye. Kwa mantiki hiyo, Mungu “hakumwamuru
mtu yeyote awe asi, wala kumruhusu atende dhambi,” YbS 15:20. Ila kila mmoja
wetu kawezeshwa kuwa mkamilifu kama Baba yetu wa mbinguni alivyo mkamilifu, Mt
5:48. Hata hivyo katika kweli hii kila mmoja yupo huru kuchagua uzima au
umauti, YbS 15:17.
Mafarisayo na waandishi
walijihesabia haki na kuwa miungu watu. Huu ni upofu uliopitiliza. Kuwajua
vizuri Mafarisayo na Waandishi nakualika usome sura yote ya 23 ya mwinjili
Mathayo. Ni kwa sababu hiyo Yesu anatoa angalizo kwanza kama kweli tunataka
uponyaji, lazima kusamehe kama hatua muhimu na mizania ya kusamehewa.
Kusamehe ni amri kama
kweli na sisi tunataka kusamehewa. Sala ya ‘Baba yetu’ imeliweka jambo hili
wazi kama sharti la upatanisho na Mungu. Cha ajabu sala hii tunaisali wengine
kila siku na kila mara kwa siku, ila bado kusamehe ni shiiida! Je, utaponywaje
kama tatizo lako ni kuvunjika mguu, ila "P.O.P" umefunga shingoni?
Mbona kila siku unatibu ugonjwa usioumwa kwa dawa tofauti? Kwa nini inakuwiya
vigumu kusamehe na kupatana na ndugu yako? Je, wewe ni mkamilifu sana?
Unatofauti gani na mafarisayo na waandishi wanachukuwa nafasi ya Mungu kwa
kujihesabia haki?
Wapendwa
wana wa Mungu, ukitaka sala yako, na maombi yako yapate kibali mbele ya Mungu,
jipatanishe wewe mwenyewe, wewe na uliyekosana naye, na pia wewe na Mungu.
Hivyo “basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu
yako ana neno juu yako, iache
sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha
urudi uitoe sadaka yako,” Mt 5:23. Wengi na hasa wale tuliokosewa hupenda
kuyarefusha mambo sana, na wakati mwingine tungependa tunyunyuziwe ubani kwa
cheteso cha dhahabu ili tuwe tayari kwa kuyaongelea yale yaliyotutatiza.
Ila
baraka na neema hutujia pale tunapokuwa na uhusiano mzuri na wenzetu,
mazingira, na Mungu Muumba wetu.
Furaha ya Mungu kwetu ni kuuishi upendo wa kweli na kuwa na mahusiano mazuri
kati yetu na viumbe vyake vingine. Mahusiano haya mazuri huufunua utukufu wake
Mungu. Maisha kama safari, yatupasa kuulinda uhusiano huo na ndugu zetu,
mazingira na Mungu kadiri tunavyosafiri hadi mwisho wa safari yetu hapa
duniani. Haya ni maisha yanayoongozwa na Roho wa Mungu ambaye utupa
hofu hiyo ya Mungu ndani yetu. “Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho. Maana
Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu,” 1Kor 2:10
Ni kwa mantiki hiyo
agizo la Yesu lakutaka wewe na mimi, "patana na ndugu yako uwapo naye
njiani," Mt 5:25. Maana yake ni nini? Kupatana
na ndugu yako mngali njiani ni kufanya juu chini kupatana na ndugu yako angali
yu hai. Msivute muda pasipo sababu. Kengele ikishagongwa hakuna tena pa
kujitetea. Maapizo na laana hazikusaidii chochote. Unazidi jizibia riziki zako
bure na baraka kutoka kwake mwenyezi Mungu. Unaposamehe unajiponya na kumponya
mwenzako pia. "Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi
wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi," Yoh 13:35.
Wapendwa wana wa Mungu,
ibada na sadaka zetu kwa Mungu huwa safi na za kumpendeza Mungu pale tunapokuwa
na amani ya kweli ndani mwetu, na ndugu zetu, mazingira yetu, na Muumba wetu. “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku
ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya
madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka
yako,” Mt 5:23-24. Amani hii ni pale unapokuwa tayari kupatana na kusamehe bila
kipimo.
Wengi
tumeshuhudia watu hawapendi kupatana na kuishia kuapizana pasipo sababu. Wapo
wengine hata baada ya kuzidiwa wakiwa kitandani karibu ya kufa wanapoomba
upatanisho na ndugu yake kunakuwa na mkwamo bila mwitikio wowote na mwisho mtu
huyo hufariki katika hali ya majonzi
makubwa. Hivi unajisikiaje ndugu yako kufa akikuomba upatane naye nawe kwa
kiburi chako hukusikia na hatimaye ndugu yako anafariki? Ndugu yangu, “Patana
na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije
akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani,” Mt
5:25. Je, kwa kutokupatana na ndugu yako angali hai, utajibu nini mbele ya
Kadhi-Mungu mwisho wa siku?
Wapendwa wana wa Mungu, hapa ndipo tunapoweza kuona udogo wa kitu
unavyokuwa na kufikia ukubwa wake ambao unatuwia vigumu kujinasua. Huu ndio
mtazamo wa dhambi kadiri ya Injili ya leo. Kumbe kadiri ya Injili
ya leo dhambi haihesabiki tu kwa kufanya tendo halisi, bali hata kwa kuwaza na
kuvutwa kwa hisia ya kufanya dhambi hiyo. Mizania ya dhambi ipo sawa kwa
kufanya au kutokufanya ili hali tu tamaa ile ya kufanya jambo hilo ipo ndani
yako. Kilichokosekana hapo ni mazingira halisi ya kulitenda jambo hilo, ila
uzito wa dhambi ni ule ule. Tafsiri hii ya dhambi inatupeleka mbali zaidi na
kututoa katika mtazamo wa kizamani ya kusema kuna dhambi ndogo na kubwa. Yesu
anatupa angalizo katika jambo hili: “Mmesikia
kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi
nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye
moyoni mwake,” Mt 5:27-28. Je, si yale yamtokayo mtu moyoni mwake ndiyo
yamtiayo unajisi? Je, si ndani ya moyo wa mtu ndipo kwenye vyanzo vya yale yote
yamjazayo mtu na kumfanya kile alicho? Pasipo utulivu wa ndani viongoza
matamanio yako ya nje (jicho, au mkono, Mt 5:29-30) hukosa mwelekeo. Nuru ile
ya ndani inapofifishwa yote ya nje huenda mrama.
Wapendwa
wana wa Mungu, “Hamjafahamu bado ya kuwa kila kiingiacho
kinywani hupita tumboni, kikatupwa chooni? Bali
vitokavyo kinywani vyatoka moyoni; navyo ndivyo vimtiavyo mtu unajisi,” Mt
15:17-18. Utulivu wa ndani ndiyo taswira halisi ya mtu.
Wapendwa wana wa Mungu,
‘ujumbe mchanganyo’ ni maoteo ya kilicho kiovu. ‘Nataka sitaki’ imewaponza
wengi sana katika maamuzi yao na mwisho walijikuta katika janga ambalo
hawakutarajia. Mfano: Kesi nyingi za ‘kubakwa’ na hata kufanyiwa vitendo vibaya
nje ya ridhaa ya mtu, vimetokea kwa sababu ya ujumbe mchanganyo. Kujiepusha na
hali na mazingira hayo maovu, Yesu anatuambia,
“maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa
yule mwovu,” Mt 5:37. Maneno yako yapaswa kunyooka kama kiapo chako. Kwa upande
mwingine kiapo chochote kile kinachochukuliwa au ‘kuliwa’ bila hitaji la
‘kiapo’ kama kiapo, na kuchukuliwa kama maongezi tu ya kawaida, kiapo hicho
kama kilivyo ujeuka kuwa kufuru. Amri ya pili ya Mungu inakataza jambo hilo
kama isemavyo, “usilitaje bure jina la Mungu wako,” Misale ya Waamini, Toleo la
1993, uk. 1077.
Mkristo
wa kweli na mwenye kuishi vyema Ukristo wake, haitaji viapo kumfanya aamini au
kuwaaminisha wengine ukweli wa kitu. Na ndiyo maana Yesu anasema, “lakini mimi
nawaambia, Usiape kabisa; hata kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha
Mungu; wala kwa nchi, kwa maana ndiyo
pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mkuu,”
Mt 5:34-35. Mara nyingi anaye apa kwa vitu ni kielelezo cha wazi kwamba kile
akisemacho hakina ukweli. Je, tunapokula viapo mbalimbali twafanya makosa? La
hasha! Hatufanyi makosa katika maana ya kujengeana uaminifu na utayari wetu wa
kutimiza kile tulichokubaliana kwa sifa na utukufu wake Mungu, hasa pale
linapojitokeza swala ya huduma kwa watu au umma. Hatufanyi jambo hili kama
maongezi yetu ya kawaida, bali kwa wakati na kusudi maalum.
Wapendwa
wana wa Mungu, yatupasa pia kutofautisha kitu kimoja hapa na cha muhimu sana.
Kiapo akifanyacho mtu kama nilivyokwisha kusema hapo juu, hakibebwi katika
ishara zile na alama zile tuzifanyazo kwa sababu hata uwepo wa ishara na alama
hizo tuzitumiazo hatujui uhasili wake katika maana ya ‘kwa nini zipo kama
zilivyo.’ Tofauti hii Yesu anaisema kwa mfano huu, kwamba, “Wala
usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele mmoja kuwa mweupe au
mweusi,” Mt 5:36. Kwa maelezo haya twajifunza
mambo mawili. Kwanza, ‘kiapo’ siyo kitu cha kawaida katika maana ya kucheza
nacho. Pili, kiapo siyo hitimisho la kila kitu kama tunakichukulia ‘kiapo’
katika maongezi ya kawaida. Kwa kufanya hivyo twayapalilia maoteo ya uovu na
yule mwovu-shetani.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Lakini Mungu
ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu,”
1Kor 2:10
Tusali:-Ee Yesu
Mwema, tujalie hekima, unyenyevu, na moyo wa msamaha. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario