JUMATATU WIKI YA 7 YA
MWAKA-I
Somo:
YbS 1:1-10
Zab:
93:1ab, 1c-2, 5
Injili:
Mk 9:13-28
Nukuu:
“Hekima yote yatoka kwa
Bwana, nayo yakaa kwake hata milele,” YbS 1:1
“Hekima iliumbwa kabla
ya vitu vyote, na ufahamu wa busara tangu milele,” YbS 1:4
“Yupo Mmoja aliye na hekima, naye yu wa
kuogopwa sana, ameketi katika kiti cha
enzi,” YbS 1:8
“Ina
wote wenye mwili kama aitoavyo, na wale wampendao amewapa kwa wingi,” YbS 1:10
“Yesu akamwambia, Ukiweza! Yote yawezekana kwake
aaminiye,” Mk 9:23
“Mara babaye yule kijana akapaza sauti, akasema,
Naamini, nisaidie kutokuamini kwangu,” Mk 9:24
TAFAKARI: “Hekima yote yatoka kwa Bwana, nayo yakaa kwake hata milele.”
Wapendwa wana wa Mungu, si jambo la ajabu leo kusikia
kila kona kelele za watu wenye hofu ya Mungu kukemea uvunjwaji wa haki za
binadamu ulio waziwazi, na wa mchana kweupe. Uvunjwaji wa haki huu unanzia pale
ulipo, familia unayoishi, tamaduni ikiwa ni pamoja na mila, desturi, na
mazingira unayoyaishi, mfumo wa siasa unaouishi au kurisishwa, uchumi
unaotawala maisha yako kila siku, na Imani unayoishi kutokana na yale
unayoyaamini. Ndugu yangu tunaye safiri sote katika tafakari hii, ni vema
ukajua kwamba huwezi kuongelea haki bila wajibu.
Haki ni tunda la wajibu
wako. Hivyo kama umewajibika vyema unayohaki na mastahili ya kile
ulichokiwajibikia. Ni kwa namna na mtazamo huu tunaongelea uvunjifu wa haki
pale mmoja wetu licha ya kuwajibika kama impasavyo haki yake inaporwa waziwazi
mchana kweupe. Uporaji wa haki hizi mara nyingi hufanywa na wale wenye “NGUVU”
katika sehemu husika. Jambo la ajabu ni hili; katika jamii yoyote ile wenye
“nguvu” hupewa dhamana hiyo na kundi hili linalohujumiwa na wenye “nguvu” hawa.
Kinachosikitisha ni kwamba, badala ya waliodhaminishwa kuwa watetesi, wao
wanakuwa wahujumu. Hawa ni wale wasiokuwa na hofu ya Mungu ndani yao, na
kipauwa mbele chao ni ubinafsi wao. Katika hali hii, amani kamwe haiwezi
ikatawala. Jamii ya mtindo huu huwa na utulivu wa kukubaliana kwa
kutokubaliana. Ni hali lenye kujionyesha kwa matumizi makubwa ya mabavu na
nguvu.
Ila jambo la kukumbuka
ni kwamba palipo na mgandamizo mkubwa wa nguvu pasipo nafasi ya kutokea, tokeo
lake ni mpasuko usiokifani. Hivyo tunahitaji amani katika maana ya kutambua utu
wa watu na tofauti zao katika kutenda na kufikiri. Tunahitaji amani kwa
kuheshimu matakwa ya wengi na yenye mwelekeo chanya wa namna watakavyo
kutawaliwa, kuwajibika, na kuuwajibisha utawala ule uliopewa dhamana na umma
wao. Ni katika amani hii tunaweza kuona matunda yake, yaani, haki ikitendeka
pasipo ghiliba. Hivyo, “tunda la haki hupandwa katika amani na wale wafanyao
amani,” Yak 3:18. Na wale waitafutao na kuifanya amani ni wale wasiyotanguliza
mbele ubinafsi wao, wala falsafa za makundi yao (vyama vya siasi), bali umoja
wa wote katika utofauti wao, wakijali uhalisi na Utaifa wao.
Wapendwa katika Kristo,
tunapopindisha kweli hii katika jamii, tuwe tayari kwa machafuko ya kila aina.
Na mwenye kujisifia katika mambo haya ni mpanda matatizo katika jamii husika na
matunda yake ni machafuko yasiyokwisha. Kweli ya kitu chochote kile haiwezwi
pindishwa kwa maslahi binafsi au ya kikundi cha walio wachache. Na kama
ikiwezekana mafanikio yake ni ya muda mfupi tu. Na hivi ndivyo Yesu asemavyo
kuhusu kweli; “tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru,” Yoh
8:32. Tunapoipindisha kweli ili tupate kuungwa mkono na wasio na ufahamu juu ya
kweli, tutayapata ya dunia hii kwa muda mfupi na kujeuka kuwa mashetani, yaani,
wapinga kweli. “Hekima
yote yatoka kwa Bwana, nayo yakaa kwake hata milele,” YbS 1:1
Hekima ishukayo kutoka
mbinguni ni kweli ile ya Neno aliyemwilishwa na kukaa kwetu, Yoh 1:14. Na huyu
ndiye Kristo. “Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli,” Yoh 8:36.
Mgandamizo wowote ule wa haki za watu
hauwezi kamwe kuzika kweli ya kile kilicho haki yao. Hivyo katika hali yoyote
ile katika mwono huu, amani haitakuwepo.
Yesu Kristo ndiyo
kielelezo cha haki kama tunda la amani. Kristo Yesu hakuja kuyatafuta yalio
yake binafsi, bali kutuweka huru katika utumwa wa dhambi. Hii ndiyo hekima
itokayo juu. “Nani awezaye kuhesabu mchanga wa bahari na mtone ya mvua na siku
za milele?” YbS 1:2. Kumbe safari kuelekea hekima ni kujua uwezo na mapungufu
yako. Huu ndio wito wa kila mmoja wetu mwenye hofu ya Mungu ambao mwisho wake
ni kuwa wakamilifu kama Baba wa Mbinguni alivyo mkamilifu. Ndugu yangu, “yupo
Mmoja aliye na hekima, naye yu wa kuogopwa sana, ameketi katika kiti cha enzi,”
YbS 1:8. Yesu anatukumbusha mwito huu na kusema, “Basi
ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt
5:48.
Ndugu
yangu, pale ulipo simama katika kweli, na kuwa mtetezi wa haki za watu wote, na
kwa namna ya pekee wanyonge kwa maana, “heri amkumbukaye mnyonge; Bwana atamwokoa
siku ya taabu,” Zab 41:1. Yote haya yanawezekana tu kama tunamwamini Yesu
Kristo, na kile alichokijia katika ulimwengu huu. Hii ndiyo hekima ya Mungu
ambayo “Bwana
ndiye aliyeiumba na kuiona na kuihesabu, na kuimwaga juu ya kazi zake zote,”
YbS 1:9. Katika kweli hii, Yesu anawakemea
wale wasiokuwa na imani naye hasa katika Injili ya leo tunapoona wanafunzi wake
wanashindwa kumtoa pepo kijana yule aliyefikwa na mkasa ule. “Akawajibu,
akasema, Enyi kizazi kisichoamini, nikae nanyi hata lini? Nichukuliane nanyi
hata lini? Mleteni kwangu,” Mk 9:19. Kumbe palipo na mashaka na pasipo njia,
tuyapeleke mahangaiko yote hayo kwa Kristo kwa Imani thabiti na ya kweli.
Katika tendo hili la
Imani Yesu anakuambia wewe na mimi kwamba, “Ukiweza! Yote yawezekana kwake aaminiye,”
Mk 9:23. Je, ukiweza nini? Ukiweza katika maana ilivyotumika hapa,
inatukumbusha kuwa na ufahamu pasipo shaka juu ya Yeye, yaani, Kristo ni nani
kwetu. Naye anasema, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila
kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Ndugu yangu, bila Kristo hatuwezi kufanya lolote
lile, liwe dogo au kubwa, “maana
pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote,” Yoh 15:5b. Je, wewe na mimi
tuna jeuri katika kweli hii? Kwa nini basi kujifanya miungu watu? Elewa jambo
hili hili juu ya hekima: “Hekima iliumbwa kabla ya vitu vyote, na
ufahamu wa busara tangu milele,” YbS 1:4. Ni vyema wewe na mimi kuiomba hekima
hii ili ituongoze kule aliko Mungu, yaani, kwenye uzima na umilele.
Wapendwa
wana wa Mungu, kwa kutambua ukweli huu, “mara babaye yule kijana
(aliyekuwa na pepo) akapaza sauti, akasema, Naamini, nisaidie kutokuamini
kwangu,” Mk 9:24. Kumbe tunapopotoka kutokana na hekima hizi za dunia,
ubinadamu, na ushetani, si vibaya tukajirudi na kutambua ubinadamu wetu
unaohitaji neema na huruma ya Mungu. Ni katika mantiki hii kwamba hekima “ina
wote wenye mwili kama aitoavyo, na wale wampendao amewapa kwa wingi,” YbS 1:10.
Kristo yupo tayari muda wote kukushika mkono unapotambua mapungufu yako
yalioyopelekea anguko lako na hasa ulipoikuza nafsi yako na kutokumpa Mungu
nafasi.
Ni kwa neema na huruma
hii ya Mungu, “Yesu akamshika mkono
akamwinua naye akasimama,” Mk 9:27. Tendo
hili linakuwa fundisho kubwa kwa wanafunzi wake Yesu. “Hata alipoingia
nyumbani, wanafunzi wake wakamwuliza kwa faragha, Mbona sisi hatukuweza
kumtoa?” Mk 9:28. Kushindwa kwa wanafunzi wa Yesu ni moja ya kuwa na Imani haba
ingawa Yesu anawaambia, “namna
hii haiwezi kutoka kwa neno lo lote, isipokuwa kwa kuomba,” Mk 9:29. Kwa namna
nyingine ni kuwa na Imani thabiti yote yawezekana.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Yupo Mmoja aliye na hekima, naye
yu wa kuogopwa sana, ameketi katika kiti
cha enzi,” YbS 1:8
Tusali:-Ee
Yesu na Jemedari wangu, nijalie hekima ya kuona uhalisi wa jambo kama ulivyo,
na siyo kuuona uhalisi huo kama nilivyo. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario