JUMATANO WIKI YA 5 YA MWAKA-I
Somo:
Mwa 2:4b-9, 15-17
Zab:
104:1-2a, 27-28, 29bc-30
Injili:
Mk 7:14-23
Nukuu:
"Bwana
akamwagiza huyo mtu, akisema, Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula,
walakini matunda ya mti wa ujuzi wa wema na mabaya usile, kwa maana siku
utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika," Mwa 2:16-17
“Hakuna kitu kilicho nje ya mtu ambacho
kikimwingia chaweza kumtia unajisi, bali vile vimtokavyo, ndivyo vimtiavyo
unajisi yule mtu,” Mk 7:15
“kwa sababu hakimwingii
moyoni, ila tumboni tu; kisha chatoka kwenda chooni? Kwa kusema hivi
alivitakasa vyakula vyote,” Mk 7:19
“Akasema, Kimtokacho
mtu ndicho kimtiacho unajisi,” Mk 7:20
“Kwa maana ndani ya
mioyo ya watu hutoka mawazo mabaya, uasherati, wivi, uuaji, uzinzi, tamaa
mbaya, ukorofi, hila, ufisadi, kijicho, matukano, kiburi, upumbavu,” Mk 7:21
“Haya yote yaliyo maovu
yatoka ndani, nayo yamtia mtu unajisi,” Mk 7:23
TAFAKARI:
“Yote
yaliyo maovu yatoka ndani, nayo yamtia mtu unajisi.”
Mungu ni Upendo na
kwake yote huyafanya kwa sababu ya upendo. Wazazi wetu wa mwanzo wanapewa
upendeleo ukiambana na utaratibu wa kuishi kwenye hii bustani. Bustani ina
mambo makuu matatu; a) Aina zote za miti ya matunda, b) Matunda ya mti wa uzima,
na c) Matunda ya mti wa ujuzi wa wema na
mabaya.
Pamoja na kupewa ruksa
ya kula matunda yote, waliwe pia angalizo la kutokula matunda ya mti wa ujuzi
wa wema na mabaya, Mwa 2:17. Tendo la kwenda kinyume na agizo hili ni KIFO. Cha
kujifunza leo ni kwamba tangu mwanza kifo hakikuwa katika mpango wa Mungu. Mungu
anatutakia uzima wa milele.
Madhara ya kutokufuata
maangalizo na utaratibu fulani iwe ni kazi au aina yeyote ya stadi za maisha
yapo mengi. Tazama milipuko ya magonjwa mengi sugu na yasiyoponyeka! Yote yametokana
na kutumia utashi wetu vibaya. Mara nyingi binadamu twapenda kujua kwa bidii
sana kile kilicho jificha nyuma ya "pazia." Je, haitoshi kuyajua haya
yaliyomahitaji yetu na yale tu yenye uzima ndani yake? Ni vizuri tukatumia
udadisi wetu kumjua Mungu, kuboresha maisha yetu kuelekea utakatifu, na
kuifanya dunia hii kuwa sehemu nzuri zaidi ya kuishi licha ya kwamba ni sehemu
ya kujiandaa kwa maisha ya umilele.
Ndugu yangu tunaye
safiri sote katika tafakari hii, ni vyema tukazama ndani kidogo kwenye fumbo
hili la mtu kama alivyo, ili tuweze kujua ujumbe wa Injili ya leo. Mtu kamili
anakuwa katika sehemu kuu tatu:-Nafsi, Roho, na Mwili. “Mungu wa amani mwenyewe
awatakase kabisa; nanyi Nafsi zenu na Roho zenu na Miili yenu mhifadhiwe mwe
kamili, bila lawama, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.” I The 5:23
Katika hili Roho na
Nafsi huwa pamoja na ndizo wewe mwenyewe. Mwili ni nyumba ya roho na nafsi.
Katika uumbaji Mungu aliumba mwili kwa udongo halafu akapulizia pumzi puani
ambayo ni roho yake ndipo mtu huyo akawa nafsi iliyo hai. “Bwana Mungu
akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa
nafsi hai.” Mwa. 2:7. Miili tuliyonayo ni nyumba ya Nafsi na Roho. Kwa hali hii
sisi binadamu ni wawili. Kuna mtu wa ndani na mtu wa nje. Mtu wa ndani ni Nafsi
na Roho, na mtu wa nje ni Mwili lakini watu hawa wapo pamoja hatuwezi
kuwatenganisha wala kumwona kwa macho ya nyama huyu mtu wa ndani, ila yupo.
Kwa mantiki hii ya
fumbo hili la uumbaji wetu na utu wetu, ni muhimu sana mtu atawale hisia zake.
Nafsi ikiegemea rohoni huleta matunda mzuri. “Lakini tunda la Roho ni upendo,
furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya
mambo kama hayo hakuna sheria.” Gal. 5:22-23. Kwa maana nyingine, “hakuna kitu
kilicho nje ya mtu ambacho kikimwingia chaweza kumtia unajisi, Mk 7:15a.
Ila nafsi inapoingia
katika Mwili mambo huwa mabaya kwani ufanya matendo ya mwili kama tusomavyo
katika maandiko matakatifu, “basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya:
uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu,
hasira, fitina, faraka, uzushi husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na
hayo; katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba
watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” Gal.5:19-21.
Kwa maneno mengine ni kwamba, “ndani ya mioyo ya watu hutoka mawazo mabaya,
uasherati, wivi, uuaji, uzinzi, tamaa mbaya, ukorofi, hila, ufisadi, kijicho,
matukano, kiburi, upumbavu,” Mk 7:21. Na haya kadiri ya Injili yetu ya leo
ndiyo yamtiayo mtu najisi. “Kimtokacho mtu ndicho kimtiacho unajisi,” Mk 7:20.
Ni vizuri kujua nafsi
yako imeegemea wapi. Ikiegemea rohoni utaenda Mbinguni. Ikiegemea mwilini
utaenda motoni. Na “haya yote yaliyo maovu yatoka ndani, nayo yamtia mtu
unajisi,” Mk 7:23. Hali na mazingira haya ndiyo mauti yetu ya pili
tuilazimishayo kwa uhuru na utashi wetu, licha ya sadaka kubwa aliyoitoa Bwana
wetu Yesu Kristo pale Msalabani kwa ajili ya dhambi zako na zangu.
Tumasifu Yesu Kristo!
“Hakuna kitu kilicho nje ya mtu
ambacho kikimwingia chaweza kumtia unajisi, bali vile vimtokavyo, ndivyo
vimtiavyo unajisi yule mtu,” Mk 7:15
Tusali:-Ee
Yesu na Mwalimu wangu, nifundishe, niamshe kila mara, na niimarishe ili nafsi
yangu iegemee roho. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario