JUMATATU WIKI YA 6 YA MWAKA-I
Somo:
Mwa 4:1-15, 25
Zab:
50:1, 8, 16bc-17, 20-21
Injili:
Mk 8:11-13
Nukuu:
"Kama ukitenda
vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo
inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde." Mwa 4:7
“Kaini akamwambia Habili nduguye, [Twende
uwandani] Ikawa walipokuwapo uwandani, Kaini akamwinukia Habili nduguye,
akamwua,” Mwa 4:8
“Wakatokea Mafarisayo,
wakaanza kuhojiana naye; wakitafuta kwake ishara itokayo mbinguni;
wakimjaribu." Mk 8:11
“Akawaacha, akapanda
tena chomboni, akaenda zake hata ng'ambo,” Mk 8:13
TAFAKARI:
“Ubaya wa kutokuona mema kwa wenzetu.”
Wapendwa wana wa Taifa la
Mungu, masomo yetu ya leo yanatualika kutafakari juu ya ubaya wa kutokuona
mazuri kwa wenzetu. Kwa maneno mengine twaalikwa kushinda hisia na wivu hasi
kwa yale mazuri kutoka kwa wenzetu.
Katika somo la kwanza
bila shaka wote tunajua simulizi la Habili/Abeli na Kaini. Hawa ni ndugu wa
damu kabisa. Habili alijulikana kwa shughuli za ufugaji kondoo, na nduguye kama
mkulima.
Wivu wa Kaini unatokana
na kutokupata kibali mbele ya uso wa Mungu kwa shukrani ya mazao yake kama
sadaka. Ilimpasa kujifunza kutoka kwa nduguye namna ya kufanya ili naye sadaka
yake ipate kibali (Mwa 4:7). Badala yake anaamua kuitoa roho nduguye ili
asipate upinzani.
Dhambi hii wengi
miongoni mwetu twaifanya sana; kwa kujua au kutokujua. Haijalishi umetoa roho
ya mtu au la! Ukiwa na wivu wowote ule usio wa kujenga, huna tofauti na kosa la
Kaini.
Kwa nini Ndugu yangu
wajisikia vibaya mwenzako akifanya vizuri? Kwa nini unakosa raha mwenzako
akiendelea? Hali hii haijalishi mahali ulipo, wito ulio nao, au ofisi uliyo
kabidhiwa na umma au jumuiya yoyote ile. Kwa nini unashindwa kumshukuru Mungu
kupitia mazuri ya ndugu yako kifamilia, mtawa mwenzako, mfanyakazi mwenzako,
mfanyabiashara mwenzako?
Tatizo kubwa tulilo
nalo wengi ni kutaka kufanana na mwingine tukisahau kwamba kila mmoja wetu kaumbwa
pekee na tofauti ikiwa ndiyo taswira halisi ya uzuri na utukufu wa Mungu. Kwa
nini unapoteza asili yako na kutaka kuwa kivuli cha mwenzako? Ndugu yangu, hayo
siyo malengo ya Mungu ya uumbaji wako.
Unachotakiwa kufanya
ndugu yangu ni kugundua vipaji na uwezo wako. Utaweza tu kufikia hatua hii
ikiwa; kwanza, kwa kujipokea ulivyo. Pili, kwa kutambua mapungufu yako. Tatu,
weka bidii kwa kile Mungu alichokupa cha pekee (vipaji vyako). Kupoteza muda
kwa kubeza kazi na mazuri ya wengine hakuta kusaidia kamwe. Utaishia tu katika
mfadhaiko wa moyo na kuwa na shinikizo la damu la kupanda na kushuka kila mara,
na pasipo tiba. Kushinda na kupoteza muda na fedha kwa waganga hakutakusaidia.
Eti unaenda kusafisha nyota! Hakika wajinga
ndiyo waliwao!
Katika injili, Yesu
anakutana na kundi hilohilo lenye wivu. Mafarisayo hawaoni wala kuamini yote
ayatendayo Yesu. Bado wanadai ishara zaidi.
Ndugu yangu, ukiukubali
wivu hasi/usio wa kujenga, hakika hautakuwa tofauti na kipofu, tena kipofu wa
macho na roho. Jipokee ndugu yangu na fanya mabadiliko ya kweli utaona
yaliyojificha ndani yako. Wengi tunaishi na hata kufikia kufa bila kutumia
vipaji alivyotupa Mungu. Sababu kubwa tunatumia muda mwingi kujishughulisha na
mambo yasiyo yetu na wafanyayo wenzetu. Na tunayafanya hayo aidha kwa
kuyaharibu au kuyabeza. Wivu ni hatari sana. Wivu ufifisha akili na roho zetu.
Bwama wetu Yesu Kristo
hapendi kupoteza muda na yule anayebeza kazi zake. Kwa busara, "akawaacha,
akapanda tena chomboni, akaenda zake hata ng'ambo," Mk 8:13. Yesu anatufundisha
kutokupoteza muda kushindana na mwenye wivu. Mwache tu kwani mwisho wa wivu na
ubaya ni AIBU! Ufufuko wa Yesu ulikuwa zaidi ya ishara waliyotaka na imekuwa
AIBU yao milele. Je, na wewe unataka kuingia mkumbo huo?
Ndugu yangu, jiulize
kwa nini unakosa raha kwa mazuri ya mwenzako? Elewa dhambi hii ya wivu ikikua
uzaa mauti!(Mwa 4:8)
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kwani hasira humwua mtu mpumbavu,
Nao wivu humwua mjinga,” Ayu 5:2
Tusali:-Ee
Yesu, nipe nguvu na neema ya kutenda mema nyakati zote za uhai wangu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario