miércoles, 22 de febrero de 2017

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 7 YA MWAKA-I


IJUMAA WIKI YA 7 YA MWAKA-I

Somo: YbS:6:5-17

Zab: 119:12, 16, 18, 27, 34, 35

Injili: Mk 10:1-12

Nukuu:

“Ukitaka kujipatia urafiki, umpate kwa kumjaribu, wala usiwe na haraka katika kumwamini; yaani, kuna rafiki wakati wa kufaa, ambaye yeye hatadumu wakti wa msiba wako,” YbS 6:7-8

 “Mcha Mungu hunyosha urafiki wake, kwa maana alivyo yeye mwenyewe ndivyo alivyo na jirani yake,” YbS 6:17.

“Lakini tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu, aliwafanya mume na mke,” Mk 10:6

“Kwa sababu hiyo mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja; hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja,” Mk 10:7-8

“Basi alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe,” Mk 10:9

Akawaambia, Kila mtu atakayemwacha mkewe na kuoa mwingine azini juu yake; na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na mtu mwingine, azini,” Mk 10:11-12

TAFAKARI: “Tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu, aliwafanya mume na mke.”

Wapendwa wana wa Mungu, hakuna hata mmoja kati yetu ambaye yupo katika ulimwengu huu kwa bahati mbaya. Ni kwa maana hiyo hiyo kwamba hakuna kati yetu aliyejipangia kuwa kama alivyo; kijinsia, kuchagua azaliwe na wazazi wa aina gani, kabila gani, au taifa gani. Tupo kama tulivyo kwa makusudi yake Mungu kwa sababu anampango mzuri na kila mmoja wetu. Je, una sababu yoyote ya kumlaumu Mungu au kumkosoa Mungu kwa kile ulicho? Angalizo: “Ndugu, msinung'unikiane, msije mkahukumiwa. Angalieni, mwamuzi amesimama mbele ya milango,” Yak 5:9. Leo kutokana na matumizi mabaya ya neno ‘uhuru,’ tumefikia hatua ya kukosoa kila kitu ambacho kimsingi ni kwenda kinyume kabisa na kusudi la uumbaji wetu.

Kwa mfano swala la jinsia Maandiko Matakatifu yanatufundisha kwamba, “tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu, aliwafanya mume na mke,” Mk 10:6. Leo walio wanaume wanataka kuwa wanawake na walio wanawake wanataka kuwa wanaume kwa kisingizio cha kutumia uhuru wao. Baadhi ya nchi za ulaya wazazi hawana tena mamlaka ya kuamua juu ya watoto wao. Mtoto akifikia umri ufaao kisheria ujiamulia jinsia aipendayo. Je, tunaenda kinyume na mpango wa Mungu? Maandiko Matakatifu yanatuambia, “Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba,” Mwa 1:27. Hii ghiliba na kasumba ya kujibadili na kuwa kitu kingine inatoka wapi? Kwa nini tunashindwa kujipokea?

Kumkosoa Mungu katika suala la uumbaji wake ni sawa na kuhasi na kuikataa ile ‘ndiyo’ iliyomo ndani mwetu. Ukosoaji huu utupelekea kuishi maisha yasiyo na malengo na mwisho wa siku tunageuka kuwa vituko. Je, unayekwenda kinyume na matakwa ya Mungu ndiyo yako ipo wapi?

Wapendwa wana wa Mungu, kwa upendo wake juu yetu, Mungu hakuishia tu kumuumba Adamu, bali aliona inafaa Adamu akawa na mwenza wake na kuifanya familia kama shina na msingi wa maisha kumwelekea Yeye mwenyewe kama ulivyo ule Utatu Mtakatifu wa umoja usiogawanyika, yaani, Mungu Mmoja na nafsi tatu; Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu. Tukirudi kwenye kusudi na hitaji la uwepo wa familia, ni kwa sababu hiyo mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja; hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja,” Mk 10:7-8. Familia itatoka wapi kama tutafuata matamanio yetu na tamaa zetu kwa kisingizio cha uhuru usio na mipaka?

Ndugu zangu, “alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe,” Mk 10:9. Leo mwanadamu amejitwalia mamlaka yasiyo yake na kujaribu kuuvaa umungu ambao pamoja na umungu huo wa kijivika, kifo hakijaacha kumwaibisha mwanadamu huyo. Hata hivyo kwa kiburi chake mwanadamu huyu hapendi kujirudi na kuwa kile kilicho kusudi la Mungu juu yake. Kusudi la Mungu la kumfanya mtu mme na mtu mke kuwa kitu kimoja ni kuufunua upendo wake kwetu, mshikamano wake, na ukaribu wake kwetu usiokoma.

Ni jukumu na wajibu wetu kuudhihirisha upendo huo wa kweli kati yetu. Hilo “pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema. Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu,” Rum 12:9-10. Tunapokosa upendo huu na umoja huu na hasa katika funganishi la Sakramenti ya Ndoa na kujishikamanisha na mwingine nje ya ndoa husika, muonekano huo hauna jina lingine zaidi ya ‘uzinifu.’ Hivyo, kila mtu atakayemwacha mkewe na kuoa mwingine azini juu yake; na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na mtu mwingine, azini,” Mk 10:11-12.

Ndugu yangu, ukubali mpango wa Mungu ndani yako. Mungu anasababu kubwa ya kukuumba kama ulivyo. Hata hivyo, pamoja na Sakaramenti hii ya ndoa kushambuliwa na maadui wengi, somo latu la kwanza kutoka kile kitabu cha Yoshua Bin Sira, anatutaka kutafakari kwa kina juu ya rafiki na urafiki wa kweli, na Injili kwa kiasi kikubwa adui wa ndoa ni wanandoa wenyewe. Ndoa nyingi leo zimekosa mwelekeo kwa sababu tu ya kuendekeza na kula amini ya usafiki usio na tija wala siha, na kukosa msimamo kati ya wanandoa wenyewe

1. MARAFIKI NA URAFIKI:

Marafiki hawapo nyuma kuharibu ndoa, hasa pale wanandoa wanaposahau fumbo la kuwa mwili mmoja. “Ukitaka kujipatia urafiki, umpate kwa kumjaribu, wala usiwe na haraka katika kumwamini; yaani, kuna rafiki wakati wa kufaa, ambaye yeye hatadumu wakti wa msiba wako,” YbS 6:7-8. Ndugu yangu, ukishafunga ndoa hakuna rafiki yeyote aliye muhimu na mkuu zaidi ya mwenzi wako. Ule mtindo wa kukaa na marafiki hadi manane ya usiku haupo tena. Huku ni kuugawa mwili wako mchana peupe pee!

Wakati mwingine mambo makubwa na ya siri kifamili tunawaamini marafiki tuliokutana nao kwenye bar na vilabu vya pombe na muziki, kuliko mwenzi wako wa Ndoa. Ndugu yangu uliye kwenye Sakramenti hii Takatifu ya Ndoa elewa ukweli huu: “Maneno matamu yatamzidishia mtu rafiki, na midomo yenye neema itamwongezea wamsalimuo,” YbS 6:5. Kuwa makini sana na marafiki wale wakuzungukao kama paka, na wakubembelezao kama mmbu kipindi cha masika.

Mfano; mikataba mbalimbali ya biashara, miradi mbalimbali tunahifadhi kwa marafiki. Kisingizio, ‘eti mwanamke hapaswi kujua kila kitu.’ Wakati fulani mama mmoja alimwuliza mume wake, tena kwa upole, "Baba Eddy, mbona lile duka la umoja famili wanasema ni lako wakati mimi sijui licha ya kuonyeshwa vielelezo vyote?" "Hivi kwa nini unapenda kunifuatilia na kufuatilia mambo yangu? Huna kitu cha kufanya? Au umekosa nini huku ndani! Kula, kuvaa, na gari nimekupa. Bado havikutoshi? Au unataka hii roho yangu? Chukua!" Mumewe alifoka na kumtolea mimacho kama kenge wa jangwa la rahara. We baba wewe, ukifa ghafla hiyo mali itakuwa ya nani? Ona ulivyo na familia kubwa na tegemezi bado.

Mara nyingi mali za familia hizi upotea kwa uficho huo huo. Kutokuambiana ukweli ni saratani mbaya sana katika Ndoa nyingi leo. Elewa, mkeo sio thamani za ndani kama sofa na vinginevyo. Huyo ni nyama na mfupa wako. Ndugu yangu, “Hakuna badala ya rafiki amini, wala uzuri wake hauna bei. Rafiki amini ni kifungu uzima; naye amchaye Mungu atampata,” YbS 6:15-16. Je, Mke wako siyo zaidi ya rafiki? Tafakari na chukua hatua.

Akina mama nao huwaamini mashoga zao kuliko hata ndugu wa familia ya mumewe. Angalizo kwenu akina Mama kwenye ndoa zenu: “Mcha Mungu hunyosha urafiki wake, kwa maana alivyo yeye mwenyewe ndivyo alivyo na jirani yake,” YbS 6:17. Kwenye kundi hili la akina Mama wenye mtindo huu wa maisha, wapo wenye miradi ya siri ambayo mwisho wake ni kifo tu. Mnashangaa nyumba inapigwa mnada wakati mmoja wa mwanandoa hajui. Inasikitisha sana. Hii ni saratani. Marafiki wamekuwa karibu na tumewakaribisha hadi chumbani. Maandiko Matakatifu leo yanatuambia hivi juu ya marafiki hawa hatarishi: “Pia kuna rafiki tena, ambaye anakula mezani pako, bali siku ya mabaya haonekani; wakati wa kufanikiwa kwako atakuwa sawa nawe, na kupiga domo juu ya watumishi wako; lakini ukipatwa na masaibu atakugeua, na kujificha mbali nawe na uso wako,” YbS 6:10-12. Ni vyema kujua mipaka ya urafiki na uhusiano wako juu ya agano lako la hiyo ndoa takatifu.

Hatuwezi kukaishi kama kisiwa, yaani, kuwaogopa jirani zetu na kutokuwa na uhusiano nao. Jambo la msingi ni kuwa na mahusiano yenye afya na yale yenye mwelekeo wa kutaabikiana katika hali zote za maisha. Hivyo, kipimo ni hiki: “Basi ujitenge na adui zako; tena ujihadhari na rafiki zako. Walakini rafiki aliye amini ndiye ngome; naye aliyempata amepata tunu,” YbS 6:13-14. Urafiki wa kuzungukana, na ule usio wa wivu wa maendeleo ni saratani hatarishi katika afya ya maisha yetu kama wanandoa, na hata maisha yoyote yale.

2. WANANDOA WENYEWE:

Ndoa inakuwa na uhai haya yakizingatiwa kadiri ya mtazamo wa Mtume Petro. "Neno la mwisho ni hili; mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikivu, wanyenyekevu; watu wasiolipa baya kwa baya, au laumu kwa laumu; bali wenye kubariki; kwa sababu hayo ndiyo mliyoitiwa ili mrithi baraka," 1Pt 3:8-9.

Ndugu yangu, maneno hayo ni mazito sana kwa wanandoa. Kwa upande wa kina mama, wapo wanaoishi kwenye ndoa bado hawana utambuzi au tofauti na usichana wao. Mama kwenye ndoa tambua kwamba kila siku yakupasa "kupungua" kwa ajili ya familia yako "iongezeke." Familia, yaani, Baba na watoto wenu waongezeke; upendo, furaha, afya, akili na mambo mengine mengi tu. Je, utapunguaje? Mtume Petro anatuambia, "kujipamba kwenu, kusiwe kujipamba kwa nje, yaani, kusuka nywele; na kujitia dhahabu, na kuvalia mavazi; bali kuwe utu wa moyoni usioonekana, katika mapambo yasiyo haribika; yaani, roho ya upole na utulivu, iliyo ya thamani kuu mbele za Mungu," 1Pt 3:3-4. Mtume Petro hapa hapingi mama usiende “salón” au kutokuvaa vizuri; bali uelewe kwamba hayo siyo vipauwa mbele katika familia.

Wengi leo katika ndoa wanatumia muda mwigi nje badala ya ndani. Vikao kila siku visivyoisha. Sema za kiroho januari hadi disemba, mikutano ya injili hadi manane ya usiku, nk. Je, saa ngapi utaijenga nyumba na ndoa yako? Huku ni kukosa busara kama tunavyoaswa, "Kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe, kadhalika mwanamke mzuri asiye na akili," Mit 11:22. Kwa maana hiyo, "kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe," Mit 14:1. Wakati mwingine unamtafuta mchawi ilhali mchawi mwenyewe ndiwe wewe.

Wanawake wengi ni wawivu kupindukia. Jua likichomoza tu utakuta mkeka upo nje. Nikujigalagaza kwenye mkeka kama dagaa wa kigoma na samaki wale “kayabo” wa kanda ya ziwa. Masikini wa Mungu labda mumewe alivutiwa na umbo lake la kushikika, baada ya nusu mwaka afadhali ya mkuyu wa handeni. Licha ndoa ni zaidi ya haya ya nje, ila nayo huleta matamanio ya kutazama kwingine kama tulipo kuna pazia na kiza. Elewa mumeo kama ameajiriwa au kujiajiri mwenyewe, awapo huko naye ameolewa na hiyo kazi yake. Awapo nyumbani anaitaji amani na utulivu.

Wanawake wengi hawana muda wa kuyasoma mapigo ya mioyo ya waume zao. Mmewe akifika nyumbani tu anadakwa mlangoni na risala ya mahitaji; utasikia yafuatayo: unajua hakuna sukari, chumvi, unga, nk. Mpe mmeo kwanza nafasi ya kupumzika. Muulize habari za huko alikotoka. Muulize angependa kupata nini kabla ya kile ulichomwandalia. Wakati mwingine kuandaa meza anafanya mfanyakazi wa ndani. Au akifanya yeye, yaani, Mama mwenye nyumba utashangaa. Ugali kaupika saa sita mchana wakati mumewe ufika nyumbani saa kumi jioni. Ugali unatoka jasho tu. Kwa nini usiandae mboga tu na wakati mumeo anapata chai ukawa unasonga ukali?

Angalia! Huko alikotoka mumeo kila mahali kuna bar na nyama choma. Na nyumba nyingi pembezoni mwa barabara kuna vibao vimeandikwa "vyumba bado vipo." Ni kwa namna hii sebule ujeuka kuwa Bar au kilabu cha pombe. Hutomwona mumeo nyumbani. Akiwa kwenye Bar au kilabuni ambapo sasa ndiyo sebule yake, hapo anahudumiwa vizuri na kwa umahiri. Huuliwa, "uncle tukusaidie nini? Anajibu, "bia, kilimanjaro." "Ya baridi "au ya moto? Mhudumu anasisitiza. Kwa vile nyumbani weshagombana na mkewe, anajibu, "ya baridi." Tazama binti huyu, hakai mbali na mteja wake. Wewe ulipomwandalia chakula mmeo ulirudi kwenye mkeka wako. Binti huyu hukaa nyuzi 45 hivi. Baba huyu akimeza fundo moja la bia ananyanyua macho anakutana na tabasam la nguvu. Kama Baba huyu alikuwa na mpango wa kunywa bia moja huongeza zadi na kufika hadi bia 5. Hapa kwishakuwa sebuleni pake. Nani wa kulaumiwa? Pamoja na udhaifu huu, wanawake wengi huwasema vibaya sana waume zao. Wengine ufikia hatua ya kuwaita waume zao "vyuma chakavu." Wapendwa katika ndoa na familia, onyaneni kindugu tena mkiwa chumbani.

Baadhi ya wanaume nao ni balaa! Kumtukana hata kumpiga mkewe mbele za watu au marafiki zake na watoto wake ni ufahari. Ona matusi hayo anavyoyafyatua kama bomu la skadi. "Mwanamke gani wewe nimekuokota bar? Bado sijaoa!" Unayasema maneno haya mbele ya watoto wako. Hata kama ni kweli hubakia maumivu makubwa kwa watoto. Mtume Petro anasema, "ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu, na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe." 1Pt 3:7.

Mke wako haitaji umnunulie ndege ili awe na furaha. Ni wewe tu kusadifu kila kitu kidogo anachokifanya nyumbani. Mmefikia hatua ya kuwaita wake zenu "magoli kipa." Mkimaanisha wao ni kudaka tu! Jambo hili halipendezi mbele ya Mungu. Nyote wawili yawapasa kusomana tabia na kupongezana kwa kila kitu mfanyacho kizuri. Mmeo akikununulia kitu kabla ya kukikosoa mpongeze na kumwambia siku nyingine ukitaka kuninunulia kitu itapendeza tukienda sote wawili. Ukweli ni kwamba, wanaume hawana uhalisi wa kuchambua uzuri kama uzuri, tupo zaidi katika idadi ya kitu au vitu. Leo niwaacha na maadui hao wawili wa ndoa.

Tumsifu Yesu Kristo!

Basi alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe,” Mk 10:9

Tusali:-Ee Yesu Mwema, tufungamanishe siku zote na kusudi la lako katika maisha yetu. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario