ALHAMISI BAADA YA JUMATANO YA MAJIVU
Somo:
Kumb 30:15-20
Zab:
1:1-4, 6
Injili:
Lk 9:22-25
“Nazishuhudiza
mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimekuwekea mbele yako uzima na mauti,
baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako,” Kumb 30:19.
“kumpenda Bwana,
Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uzima
wako, na wingi wa siku zako; upate kukaa katika nchi Bwana aliyowaapia baba
zako, Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, kuwa atawapa,” Kumb 30:20
“Akawaambia wote, Mtu
ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila
siku, anifuate,” Lk 9:23
“Kwa kuwa mtu
atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake
kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha,” Lk 9:24.
“Kwa kuwa yamfaa
nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akijiangamiza, au kujipoteza mwenyewe?”
Lk 9:25
TAFAKARI:
“Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila
siku, anifuate.”
Wapendwa wana wa Mungu,
maelekezo ya Mungu juu ya maagizo yake iwe amri au sheria, hayana lengo la
kuukandamiza uhuru wetu, bali endapo tutakuwa ndani ya mwongozo huo hapo ndipo
ulipo uhai na umilele wetu. Kwa maana nyingine, Mungu wetu siyo mfano wa Jitu
katili ambalo lengo na kiini cha utendaji wake ni kwa ajili ya ubinafsi wake.
Mungu alipenda na kupendezwa kumuumba mwanadamu kwa sura na mfano wake si kwa
kujifaidia mwenyewe, bali kwa sifa na utukufu wake. Uwepo wetu haumpunguzi wala
kumwongezea Mungu chochote na hasa katika utukufu wake. Ila kuishi kadiri ya
maagizo ya Mungu kuna faida kwetu ikiwa ni kuishi katika Amani ya kweli, na
mwisho wa maisha haya hapa duniani tuwe na maisha ya milele pamoja naye.
Hata pamoja na nia
njema hii, Mungu hatushurutishi kumtii ili tufaidike na utukufu wake, ila kwa
kumfuata kwa hiari bila kuburuzwa ni njia mojawapo ya kufunuliwa utukufu wake.
Hivyo leo ni hiari yako na yangu kuchagua uzima au umauti. “Angalia,
nimekuwekea leo mbele yako uzima na mema, na mauti na mabaya; kwa hivi nikuagizavyo leo kumpenda Bwana,
Mungu wako, kuenenda katika njia zake, na kushika maagizo yake, na amri zake,
na hukumu zake, upate kuwa hai na kuongezeka; Bwana, Mungu wako, apate
kukubarikia katika nchi uingiayo kuimiliki,” Kumb 30:15-16. Ndugu yangu, Mungu tu ndiye apaswa kuabudiwa
kuliko kwa kweli na haki. Kinyume cha hapo ni balaa tupu, Kumb 30:18. Ni
katika ukweli huu kwamba “kujisalimisha” kwa Mungu ndiyo njia pekee na sahihi
ya kumjua, kumpenda, kumtumikia na mwisho kurudi kwake mbinguni. Kujisalimisha
huku kwa hiari ndiko Yesu anakosema “kuikana nafsi.” “Kwa kuwa mtu atakaye
kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili
yangu ndiye atakayeisalimisha,” Lk 9:24.
Ingawa uhai na umauti kuwa sehemu ya ubinadamu wetu, ipo nafasi kubwa ya
umilele kama wewe na mimi tutaamua vyema hatma ya maisha yetu kwa kujisalimisha
huko kuliko kwa hiari. Naye Mungu anasema, “Nazishuhudiza mbingu na nchi juu
yenu hivi leo, kuwa nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana;
basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako,” Kumb 30:19.
Wapendwa wana wa Mungu, uzima wetu upo
pale tunapozishika amri za Mungu siyo kwa woga mbali kwa kuzipenda kwani mwisho
wake ni umilele. “Kumpenda Bwana, Mungu wako, kuitii sauti
yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uzima wako, na wingi wa siku zako;
upate kukaa katika nchi Bwana aliyowaapia baba zako, Ibrahimu, na Isaka, na
Yakobo, kuwa atawapa,” Kumb 30:20. Hivyo tafsiri ya sheria ya Bwana siyo teso
bali ni njia ya kuyajua mapenzi yake kwako. “Heri
walio kamili njia zao, Waendao katika sheria ya Bwana,” Zab 119:1
Kwa
maana hiyo, ni lazima nichague kumtii Mungu katika Imani. Kila wakati
unapoamini hekima ya Mungu na kufanya kila analosema, hata pale unapokuwa
huelewi, unakuza urafiki wako na Mungu. Mara nyingi hatufikiri utii kama sifa
ya urafiki na Mungu wa sababu ya mausiano yasiyo ya afya kati yetu na mzazi,
mkubwa wa kazi, na hata majirani zetu. Lakini Yesu aliweka wazi kwamba utii ni
kigezo cha uhusiano na Mungu. “Ninyi mmekuwa rafiki zangu,
mkitenda niwaamuruyo,” Yoh 15:14. Sisi ni marafiki na Mungu, lakini siyo sawa
na Yeye. Yeye ni kiongozi wetu atupendaye, na tunamfuata. Tunamtii Mungu, si
kama wajibu au kwa hofu au kwa kushurutishwa, bali kwa sababu tunampenda na
tunaamini kwamba anajua kile kilicho bora kwetu. Tunataka kumfuata Kristo kwa
shukrani kwa yote aliyotufanyia, na tunapomfuata kwa karibu, ndipo urafiki wetu
naye unakuwa wa kina zaidi.
Wasioamini mara nyingi
hudhani kwamba Wakristo hutii kwa sababu ni wajibu, au kuogopa lawama, au
kuogopa hukumu, lakini ukweli ni kinyume cha hayo. Kwa sababu tumesamehewa na
kuwekwa huru, tunatii kwa upendo, na utii wetu hutuletea furaha kubwa! Yesu
anasema, “Kama vile Baba alivyonipenda mimi, nami nilivyowapenda ninyi, kaeni
katika pendo langu. Mkizishika amri
zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba
yangu na kukaa katika pendo lake. Hayo
nimewaambia, ili furaha yangu iwe ndani yenu, na furaha yenu itimizwe,” Yoh
15:9-11.
Angalia jinsi ambavyo
Yesu anatutazamia kufanya yale tu aliyotenda kwa Baba yake. Uhusiano wake na
Baba yake ni kielelezo cha uhusiano wetu naye. Yesu alifanya chochote Baba
alichomwagiza kufanya, kwa upendo. Urafiki wa kweli si wa kukaa tu, bali ni wa
vitendo. Yesu anapotuagiza kuwapenda wengine, kusaidia wahitaji, kuwagawia
wengine mali zetu, kuwa na maisha safi, kusamehe, na kuwaleta wengine kwake,
upendo hutuchochea kutii mara moja. Mara nyingi tunapewa changamoto ya
kumfanyia Mungu “mambo makubwa.” Ni dhahiri kwamba Mungu anafurahishwa zaidi
tunapotenda mambo madogo madogo kwa ajili yake kutokana na utii wa upendo.
Yawezekana huwa hayaonekani kwa wengine, lakini Mungu anayaona na kuyahesabu
kuwa matendo ya kuabudu.
Nafasi kubwa inaweza
kutokea mara moja katika maisha, lakini nafasi ndogo ndogo zinatuzunguka kila
siku. Hata katika matendo madogo kama vile kusema kweli, kuonyesha wema,
kuwatia moyo wengine, tunaleta tabasamu katika uso wa Mungu. Mungu anathamini
matendo rahisi tu ya utii kuliko sala zetu, sifa na sadaka. “Naye Samweli akasema, je! Bwana huzipenda sadaka za
kuteketezwa na dhabihu Sawasawa na kuitii sauti ya Bwana? Angalia, kutii ni
bora kuliko dhabihu, Na kusikia kuliko mafuta ya beberu,” 1Sam 15:22.
Yesu
alianza huduma yake ya hadharani katika umri wa miaka thelathini kwa kubatizwa
na Yohane. Katika tukio hilo Mungu alizungumza kuto mbinguni; “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye,” Mt
3:17. Je, Yesu alikuwa anafanya nini kwa miaka thelathini ambacho
kilimfurahisha Mungu? Maandiko Matakatifu hayasemi kitu kuhusu miaka hiyo
iliyojificha, isipokuwa kwa maneno machache kutoka Mwinjili Luka, kwamba “Akashuka
pamoja nao mpaka Nazareti, naye alikuwa akiwatii; na mamaye aliyaweka hayo yote
moyoni mwake,” Lk 2:51. Miaka thelathini ya kumpendeza Mungu ilijumlishwa
katika maneno: “naye alikuwa akiwatii.”
Hivyo wapendwa katika
Kristo, kama tuonavyo masomo yetu ya leo yanatuelekeza kufanya maamuzi ya kweli
kuhusu maisha yetu na kumfuata Kristo. Je, Yesu anasema nini juu ya AMRI? Yesu
yupo wazi kabisa kuhusu amri na mahusiano yake na umilele. Amri ni ‘Upendo’
ambao kwa kupitia Yeye, yaani Kristo, upendo wa Mungu Baba ni dhahiri kwetu. “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda
ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo,” Yoh 13:34. Hivyo kumpenda Kristo na Mungu
Baba ni kuishika amri hii ya Mapendo. “Mkinipenda, mtazishika amri zangu,” Yoh
14:15. Hivyo mara zote yanipasa mimi na wewe nimwone Kristo kwa yeyote yule
nitakaye kutana naye bila kujali itikadi zetu za maisha, familia zetu, koo
zetu, makabila yetu na utaifa wetu.
Wapendwa
wana wa Mungu, kumtambua Kristo katika maana ya kuwa na amri zake Kristo na
kuzishika ni kumpenda Kristo na huko ndiko kupendwa na Mungu Baba. Hili ndilo
dhihirisho la Kristo kwetu, yaani, kuishi ndani na katika Kristo Yesu. Naye
Yesu anasema, “Yeye aliye na amri zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye;
naye anipendaye atapendwa na Baba yangu; nami nitampenda na kujidhihirisha
kwake,” Yoh 14:21. Ndugu yangu, wewe na mimi tu wafuasi wa Kristo kwa kuzishika
amri zake na huko ndiko kukaa katika pendo la Kristo.
“Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi
nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake,” Yoh 15:10. Licha
kwamba hapa Yesu katumia muda mwingi kuelezea amri, ukweli ni huu anaousema
kuhusu amri; “Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi,” Yoh
15:12. Sadaka ya Yesu pale msalabani yanipasa ihakisi na isadifiwe na kutukuzwa
daima kwa kupendana sisi kwa sisi. Tusipofanya hivyo, ni kwamba tunaendelea
kumsulubisha Yesu pale msalabani.
Kati ya mtihani mgumu
wa maisha ni kuamua kuacha jambo fulani ulilolizoea na kuanza njia nyingine.
Hapa ndipo wengi hushindwa. Mara nyingi tunajawa hofu ya sintofahamu ya mambo
yajayo na tusiyo yajua. Ila kama kweli tunataka kuwa karibu na Mungu, na kuokoa
nafsi zetu yatupasa kufanya maamuzi. Maamuzi ye yote yale katika maisha yana
gharama zake. Na uamuzi utakaochukua lazima utapimwa. Wengi watakushangaa na
hata kukucheka. Wala usihofu kwa sababu duniani hapa ni mahali tu pa kujiandaa
kwa ajili ya umilele.
Somo la kwanza kwa
mantiki hiyo, linatupa angalisho; kuchagua kati ya kifo au uhai. Uzuri na utamu
wa maisha haya ya leo na sasa unatutia upofu wa kuona uzuri wa maisha ya
umilele. Jambo hilo Yesu analiongelea katika mfumo wa msalaba. Tusipokuwa
tayari kujikana, kuchukua misalaba yetu, na kumfuata, hatufai kuwa wanafunzi
wake. “Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba
wake kila siku, anifuate,” Lk 9:23.
Jambo
hili la maanisha nini?
Kuikana nafsi ni tendo
la kuvua mwelekeo na mvuto wa yale uyapendayo na yasiyo na tija ukilinganisha na
maisha ya umilele. Na maisha yasiyo na tija ni pamoja na "ponda mali kifo chaja." Ni
maisha ya kutokuwa na hofu ya Mungu. Ni maisha ya kujipenda kupita kiasi na
kujihurumia. Ni maisha ya kuukataa ubinadamu wako na mipaka yake na kujiona
mungu mtu. Huku ni kutoikana nafsi.
Kuubeba msalaba ni
kukubali kuongozwa. Ni kukubali mapungufu yako kama binadamu ili iwe changamoto
kwako kuelekea ukamilifu. Ni kujipokea. Ni hali ya uitaji wa neema ya Mungu. Ni
hatua muhimu ya awali kuanza kukua kiroho. Ni kukubali kujiachia mikononi mwa
Mungu na kumtegemea yeye tu. Ni kuwa na imani juu ya Mungu ingawa mapungufu
yapo kama binadamu.
Kumfuata Yesu, ni
kumfanya Yesu kuwa njia, na ukweli, na ulizi, Yoh 14:6. Yesu ni njia kuelekea
uzima wa milele. Hakuna njia nyingine ndugu yangu. Na njia aliyochagua Yesu ni
msalaba. Nasi kama wafuasi wake, msalaba haukwepeki. Yesu ni ukweli. Ukweli huu
ndio utakao tuweka huru, Yoh 8:32. Yesu Kristo ndiyo uzima wetu. Mwili na damu
yake Yesu ni uzima na uhai kwetu, Yoh 6:54.
Ndugu yangu, wakati wa
kukata shauri ni sasa na kumrudia Mungu. Kishawishi kikubwa ni kudhani kuwa
muda bado upo. Linalowezekana leo, lisingoje kesho.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kwa maana Kristo ni mwisho wa
sheria, ili kila aaminiye ahesabiwe haki. Kwa
maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata
wokovu,” Rum 10:4, 10
Tusali:-Ee
Yesu na Ngome yangu, nijalie neema ili niweza kujinasua katika vifungo vyangu
vya kimwili na kiroho. Amina