JUMAMOSI
BAADA YA JUMATANO YA MAJIVU
Somo:
Isa 58:9b-14
Zab:
86:1-6
Injili:
Lk 5:27-32
Nukuu:
"Na kama
ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako, na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo
nuru yako itakapopambazuka gizani; na kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri,"
Isa 58:10
“Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung'unikia wanafunzi
wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye
dhambi?” Lk 5:30
“Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu,
isipokuwa walio hawawezi,” Lk 5:31
"Sikuja kuwaita
wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu," Lk 5:32
TAFAKARI:
“Sikuja
kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
kipindi hiki cha kwaresma ninatutafakarisha na kutusogeza karibu zaidi na neema
na huruma ya Mungu. Kwa upande mwingine ni kuiona "furaha ya Mungu
ninapojirudi na kumrudia, pale ninapofanya toba ya kweli kama kieleleza cha
kuujenga tena uhusiano wangu na Mungu ulioathiriwa na dhambi zangu."
Pamoja na mapungufu yetu na ubinadamu wetu, bado Mungu hajakata tamaa kutupokea
kama tulivyo. Furaha yake ni kutupata hasa tunapofanya toba ya kweli. Huruma na
neema ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu.
Somo la kwanza la
tuonyesha namna ya kufanya toba hiyo. Baada ya kutubu na kuondolewa dhambi,
malipizi au toba yetu ya kweli ni kujifunua na kujiweka karibu na wale wote
wanao itaji uwepo wetu, na kuwasaidia kadiri ya uwezo na nafasi aliyotupa
Mungu. Tunapolifanya tendo hilo kuwa letu kwa moyo mkunyufu, kiwi yetu na Mungu
inafanywa kama adhuhuri. "Na kama ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako,
na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo nuru yako itakapopambazuka gizani; na
kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri," Isa 58:10
Ndugu yangu, unapoishi
hapa duniani kuna mambo mawili yanaweza kukifika. Ukiishi vizuri unakuwa
muhenga. Yaani mtu aliyeishi vyema na ameacha kitu cha kuigwa na kusimuliwa kwa
vizazi vyote. Usipokuwa muhenga basi uwezekano wa kuwa mzimu ni mkubwa. Mzimu
ni roho ovu/mbaya. Hapa hakuna cha kuigwa wala kusimuliwa. Mtu anakosa na
kupoteza historia yake. Kuishi vyema na watu kwaitaji unyenyekevu kama msingi
wa fadhila zote. Unyenyekevu huu ni
furaha ya Mungu. "Kumcha Bwana ni maonyo ya hekima; na kabla ya heshima
hutangulia unyenyekevu," Mit 15:33
Ni unyenyekevu huu
unaotusukuma tena na tena kupenda kuishi na kila mmoja wetu. Ni unyenyekevu huu
unatufanya kushuka chini kabisa kwa
waihitaji. "Afadhali kuwa na roho ya unyenyekevu pamoja na masikini,
kuliko kugawanya nyara pamoja na wenye kiburi." Mit 16:19. Kristo ndiye
kielelezo cha unyenyekevu wa kweli. Hakika huruma na neema ya Mungu ni kubwa
kuliko dhambi zetu. Tendo la Yesu la unyenyekevu na huruma linakuwa kero kwa
Mafarisayo ambao kwa kiasi fulani katika utendaji wao nasi tumo. “Ikawa Mafarisayo na waandishi wao
kuwanung'unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na
watoza ushuru na wenye dhambi?” Lk 5:30. Ni
mara ngapi wewe na mimi huendelea kuwanyooshea vidole wale waliodondoka katika
dhambi na uovu, na kutokuona tena neema na huruma ya Mungu kwa watu hao
wanapojirudi?
Injili yetu ya leo
inatupa furaha hiyo ya Mungu na toba ya mwanadamu kupitia mwanaye Yesu Kristo,
anaposema uwepo wake si kwa wenye haki, bali kwa wenye dhambi. “Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya
hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye
haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu," Lk 5:31-32. Mapaswa yetu wanadamu
ni kutambua tulipojikwaa na kumrudia Mungu. Mlango wa neema na huruma ya Mungu
upo wazi muda wote kupitia Sakramenti ya Upatanisho.
Wapendwa katika Kristo,
Maandiko Matakatifu yanatupa masimulizi mbalimbali kuonyesha furaha hii ya
Mungu-[neema na huruma yake] mja wake anapofanya toba ya kweli. Tazama furaha
ya Baba kwa mwana mpotevu, (Lk 15:11-32). Mfano wa mwanakondoo aliyepotea na
shilingi moja iliyopotea. Vinapopatikana hivi vilivyopote ni furaha kubwa sana
mbinguni. "Nawaambia, vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya
mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda
ambao hawana haja ya kutubu,"Lk 15:7.
Ndugu yangu, ni upendo
mkubwa sana kwetu kupata fursa hii na ukaribu huu na Mungu. Ni wakati mzuri wa
kupatanishwa naye. Tusisite kuijongea sakramenti ya upatanisho. Wakati ufahao ndiyo sasa.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Tena, mtu mwovu atakapoghairi, na kuuacha uovu wake
alioutenda, na kutenda yaliyo halali na haki, ataponya roho yake, nayo itakuwa
hai. Kwa sababu atafakari, na
kughairi, na kuyaacha makosa yake yote aliyoyatenda,
hakika ataishi, hatakufa,” Eze 18:27-28
No hay comentarios:
Publicar un comentario