JUMANNE
WIKI YA 3 YA KWARESMA
Somo:
Dan 3:25, 34-43
Zab:
25:4abc-5ab, 6-7bc, 8-9
Injili:
Mt 18:21-35
Nukuu:
“Na sasa tunakufuata
kwa moyo wote, tunakucha, na kuutafuta uso wako. Usitufedheheshe, bali
ututendee kwa kadiri ya fadhili zako, sawasawa na wingi wa huruma zako. Utuokoe
kwa kadiri ya maajabu yako, na kulitukuza jina lako, Ee Bwana.” Dan 3:40-43
“Yesu akamwambia,
“Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini,” Mt 18:22
TAFAKARI:
“Msamaha wa Mungu na kweli; ni kuvivaa viatu vya wale waliotusamehe na kujirudi
ndani ya nafsi yako kwa wale uliowakosea.”
Wapendwa katika Kristo,
leo tujikite katika tafakari yetu kwenye, “Msamaha wa Mungu na kweli; ni
kuvivaa viatu vya wale waliokusamehe na waliokukosea.” Masomo yetu leo
yanafunua na kufafanua kwa undani hatua za kufikia msamaha, na ulazima wa kutoa
Msamaha. Ndugu yangu, Msamaha wa Mungu na kweli huridhiwa naye pale tu
tunapokiri makosa yetu kwa dhati. Kukiri makosa ni kujiona kwa ndani, kuukubali
ubinadamu wako katika mapungufu, kuwa tayari kuanza upya na vizuri zaidi, kuwa
na matumaini na mwelekeo sahihi wa kule tuendako na kupatamani; furaha ya
kweli. Somo la kwanza linaelezea hali hiyo.
Azaria anasimama na
kukiri mbele ya Mungu kwa niaba ya Jamii yake kule kuishi kusikompendeza Mungu.
“Na sasa tunakufuata kwa moyo wote, tunakucha, na kuutafuta uso wako.
Usitufedheheshe, bali ututendee kwa kadiri ya fadhili zako, sawasawa na wingi
wa huruma zako. Utuokoe kwa kadiri ya maajabu yako, na kulitukuza jina lako, Ee
Bwana.” Dan 3:40-43. Hii ni hatua muhimu sana kuelekea msamaha. Je, Mungu
anaitaji jambo hili ili kutusamehe? Jibu ni hapana! Kwa kufanya hivyo
hatumbembelezi Mungu kwa sababu haitaji kubembelezwa. Yeye ni mkamilifu katika
ukamilifu wote na haitaji cho chote kutoka kwa viumbe vyake ili vimuongozee
ukamilifu wake. Ila, tunapokiri makosa yetu, tunajitambulisha kwake kwa
kukubali ubinadamu wetu na kuwa sisi ni viumbe tu kwake. Tunapokaa katika
nafasi yetu kadiri ya uumbaji wake, ndiyo furaha ya Mungu na uzuri wake. Kwa
kufanya hivyo, tunapokea lile umbo alilotupa katika uumbaji wetu, yaani sura na
mfano wake, Mwa 1:27. Ni katika hatua hii tunatambua kwamba, “rehema na msamaha
ni kwa Bwana wetu, ingawa tumemwasi; wala hatukuitii sauti ya Bwana, Mungu
wetu, kwa kwenda katika sheria zake, alizoziweka mbele yetu kwa kinywa cha
watumishi wake, manabii,” Dan 9:9
Ndugu yangu, haya ndiyo
makusudi ya kukiri makosa yetu kabla ya kwenda kuyaungama kupitia Sakramenti ya
Upatanisho. Wengi wetu huwa tunakurupuka tu bila kufanya tathimini ya kina kwa
yale tuliyokosea. Anayekwenda kuungama bila kufanya zoezi hili la dhamiri, ni
kutokuheshimu na kuichezea sakramenti hii ya upatanisho. Hapa tunakumbushwa pia
zile hatua za kupitia kabla ya kupata maondolea ya dhambi (rejea mfundisho yako
kuhusu sakramenti ya kitubio/upatanishi).
Ni ukweli usiotia shaka
kwamba kama Mungu angechukua hatua ya hapo kwa hapo tunapomkosea, sijua kama
kuna ambaye angesalimika katika adhabu hiyo. Na ndiyo maana mzaburi anasema,
“Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako
kuna MSAMAHA, ili Wewe uogopwe.” Zab 130:3-4. Kuogopwa kwa Mungu hapa
hakumaanishi Mungu wetu ni katili na mwenye kutuburuza katika kufanya jambo. La
hasha! Kuogopwa kwake Mungu ni pamoja na ukweli kwamba pamoja na makosa yetu
kuwa mengi na yakutisha, bado anatupa nafasi ya kuyakiri na kupatanishwa naye.
Kwa mantiki hii, huyu Mungu wetu niwakuogopwa kwa sisi kuwa na hofu naye.
Injili yetu leo
inafafanua ulazima wa kutoa msamaha. Kipimo cha kusamehe ni kusamehe bila
kipimo. “Yesu akamwambia, ‘Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara
sabini.’” Mt 18:22. Ndugu yangu, lazima tufahamu msingi wa swali la Petro.
Petro anamwambia Yesu, “Bwana, ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe?
Hata mara saba?” Mt 18:21. La kujiuliza ni kwamba, kwa nini Petro ajikite
kwenye mara saba? Wapendwa, kadiri ya Maandiko Matakatifu, namba saba
inamaanisha UKAMILIFU, YAKUTOSHA. Kwa Petro mara hizo saba za tosha na za
pendeza machoni mwa Mungu.
Yesu katika hili
hatengui ukamilifu na utoshelevu wa mtazamo huo alio kuwa nao Petro, bali
anaupa maana zaidi na kuutimiliza, kwani Yeye mwenyewe anasema, “Msidhani ya
kuwa nilikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali
kutimiliza,” Mt 5:17. Tunapotoa msamaha yatupasa kuzama ndani katika tendo la
kusamehe na kusamehewa. Ni kuvivaa viatu vya yule aliyekusamehe na wakati huo
huo kujirudi ndani kwa yule uliyemkosea.
Unaposamehe kumbuka pia nawe umesamehewa mara nyingi tu.
Ni mangapi unafanya
kinyume na mapenzi ya Mungu, lakini yeye amekupa muda wa kujirudi? Je, angetoa
adhabu za hapo kwa hapo umengebaki salama kweli? Kwa nini wasubiri kupigiwa
chetezo ndio utoe msamaha? Kwa nini tunawazungusha watu kwa kutowasamehe wanapokiri
makosa yao na katika unyonge wao? Kwa nini tunaweka vikwazo na sababu nyingi
ili tuwasemehe watu waliotukosea hata kama weshakiri makosa yao? Jumuiya ya
wakristo, na Kanisa kwa ujumla lisilotoa msamaha ni wazi jumuiya hiyo na Kanisa
hilo halimwakilishi Yesu Kristo. Mkusanyiko huo utakakuwa mkusanyiko usio na
mwelekeo na mbele yake kuna giza kubwa sana!
Katika Injili ya leo
Yesu anatoa simulizi la kuvivaa viatu vya wale waliotusamehe na kujirudi ndani
ya nafsi zetu kwa wale tuliowakosea. Hii ndiyo namna ya uzito na ulazima wa
kusamehe. Mara nyingi Yesu ameonyesha hali hiyo, na hata umauti wake kwa ajili
ya dhambi zetu. Yesu alipoletewa mbele yake mwanamke yule mzizi, aliyasema
haya, baada ya kulitafakari tukio hile undani akiwa anaandika chini, “Yeye
asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza kumtupia jiwe,” Yoh 8:7. Wote
tunajua kilichofuata baada ya maneno haya ya Yesu.
Bwana wetu Yesu Kristo
ni kielelezo sahihi cha Msamaha wa Mungu. Ndugu yangu, “Mtu huyo Mungu
amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe Mkuu na Mwokozi, awape Waisraeli toba
na msamaha wa dhambi,” Mdo 5:31. Na nikatika “yeye tuna ukombozi, yaani,
msamaha wa dhambi; naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa
viumbe vyote,” Kol 1:14-15.
Ndugu yangu, msamaha ni
Ukristo wetu na maisha yetu kama wafuasi wake Kristo. Msamaha ni tendo la Mungu
mwenyewe na sababu ya wokovu wetu. Hakuna anayeishi kwa sababu yake mwenyewe,
wala hakuna afaye kwa nafsi yake, Rum 14:7
Ndugu yangu, nani wewe usiye samehe?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Yesu akamwambia, ‘Sikuambii hata
mara saba, bali hata saba mara sabini,’” Mt 18:22
Ee Yesu, nijalie
Roho ya Msamaha na nifanye hivyo bila kujibakiza. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario