domingo, 28 de febrero de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 3 YA KWARESMA

JUMANNE WIKI YA 3 YA KWARESMA
Somo: Dan 3:25, 34-43
Zab: 25:4abc-5ab, 6-7bc, 8-9
Injili: Mt 18:21-35

Nukuu:
“Na sasa tunakufuata kwa moyo wote, tunakucha, na kuutafuta uso wako. Usitufedheheshe, bali ututendee kwa kadiri ya fadhili zako, sawasawa na wingi wa huruma zako. Utuokoe kwa kadiri ya maajabu yako, na kulitukuza jina lako, Ee Bwana.” Dan 3:40-43

“Yesu akamwambia, “Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini,” Mt 18:22

TAFAKARI: “Msamaha wa Mungu na kweli; ni kuvivaa viatu vya wale waliotusamehe na kujirudi ndani ya nafsi yako kwa wale uliowakosea.”

Wapendwa katika Kristo, leo tujikite katika tafakari yetu kwenye, “Msamaha wa Mungu na kweli; ni kuvivaa viatu vya wale waliokusamehe na waliokukosea.” Masomo yetu leo yanafunua na kufafanua kwa undani hatua za kufikia msamaha, na ulazima wa kutoa Msamaha. Ndugu yangu, Msamaha wa Mungu na kweli huridhiwa naye pale tu tunapokiri makosa yetu kwa dhati. Kukiri makosa ni kujiona kwa ndani, kuukubali ubinadamu wako katika mapungufu, kuwa tayari kuanza upya na vizuri zaidi, kuwa na matumaini na mwelekeo sahihi wa kule tuendako na kupatamani; furaha ya kweli. Somo la kwanza linaelezea hali hiyo.

Azaria anasimama na kukiri mbele ya Mungu kwa niaba ya Jamii yake kule kuishi kusikompendeza Mungu. “Na sasa tunakufuata kwa moyo wote, tunakucha, na kuutafuta uso wako. Usitufedheheshe, bali ututendee kwa kadiri ya fadhili zako, sawasawa na wingi wa huruma zako. Utuokoe kwa kadiri ya maajabu yako, na kulitukuza jina lako, Ee Bwana.” Dan 3:40-43. Hii ni hatua muhimu sana kuelekea msamaha. Je, Mungu anaitaji jambo hili ili kutusamehe? Jibu ni hapana! Kwa kufanya hivyo hatumbembelezi Mungu kwa sababu haitaji kubembelezwa. Yeye ni mkamilifu katika ukamilifu wote na haitaji cho chote kutoka kwa viumbe vyake ili vimuongozee ukamilifu wake. Ila, tunapokiri makosa yetu, tunajitambulisha kwake kwa kukubali ubinadamu wetu na kuwa sisi ni viumbe tu kwake. Tunapokaa katika nafasi yetu kadiri ya uumbaji wake, ndiyo furaha ya Mungu na uzuri wake. Kwa kufanya hivyo, tunapokea lile umbo alilotupa katika uumbaji wetu, yaani sura na mfano wake, Mwa 1:27. Ni katika hatua hii tunatambua kwamba, “rehema na msamaha ni kwa Bwana wetu, ingawa tumemwasi; wala hatukuitii sauti ya Bwana, Mungu wetu, kwa kwenda katika sheria zake, alizoziweka mbele yetu kwa kinywa cha watumishi wake, manabii,” Dan 9:9

Ndugu yangu, haya ndiyo makusudi ya kukiri makosa yetu kabla ya kwenda kuyaungama kupitia Sakramenti ya Upatanisho. Wengi wetu huwa tunakurupuka tu bila kufanya tathimini ya kina kwa yale tuliyokosea. Anayekwenda kuungama bila kufanya zoezi hili la dhamiri, ni kutokuheshimu na kuichezea sakramenti hii ya upatanisho. Hapa tunakumbushwa pia zile hatua za kupitia kabla ya kupata maondolea ya dhambi (rejea mfundisho yako kuhusu sakramenti ya kitubio/upatanishi).

Ni ukweli usiotia shaka kwamba kama Mungu angechukua hatua ya hapo kwa hapo tunapomkosea, sijua kama kuna ambaye angesalimika katika adhabu hiyo. Na ndiyo maana mzaburi anasema, “Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna MSAMAHA, ili Wewe uogopwe.” Zab 130:3-4. Kuogopwa kwa Mungu hapa hakumaanishi Mungu wetu ni katili na mwenye kutuburuza katika kufanya jambo. La hasha! Kuogopwa kwake Mungu ni pamoja na ukweli kwamba pamoja na makosa yetu kuwa mengi na yakutisha, bado anatupa nafasi ya kuyakiri na kupatanishwa naye. Kwa mantiki hii, huyu Mungu wetu niwakuogopwa kwa sisi kuwa na hofu naye.

Injili yetu leo inafafanua ulazima wa kutoa msamaha. Kipimo cha kusamehe ni kusamehe bila kipimo. “Yesu akamwambia, ‘Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini.’” Mt 18:22. Ndugu yangu, lazima tufahamu msingi wa swali la Petro. Petro anamwambia Yesu, “Bwana, ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba?” Mt 18:21. La kujiuliza ni kwamba, kwa nini Petro ajikite kwenye mara saba? Wapendwa, kadiri ya Maandiko Matakatifu, namba saba inamaanisha UKAMILIFU, YAKUTOSHA. Kwa Petro mara hizo saba za tosha na za pendeza machoni mwa Mungu.

Yesu katika hili hatengui ukamilifu na utoshelevu wa mtazamo huo alio kuwa nao Petro, bali anaupa maana zaidi na kuutimiliza, kwani Yeye mwenyewe anasema, “Msidhani ya kuwa nilikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza,” Mt 5:17. Tunapotoa msamaha yatupasa kuzama ndani katika tendo la kusamehe na kusamehewa. Ni kuvivaa viatu vya yule aliyekusamehe na wakati huo huo kujirudi ndani kwa yule  uliyemkosea. Unaposamehe kumbuka pia nawe umesamehewa mara nyingi tu.

Ni mangapi unafanya kinyume na mapenzi ya Mungu, lakini yeye amekupa muda wa kujirudi? Je, angetoa adhabu za hapo kwa hapo umengebaki salama kweli? Kwa nini wasubiri kupigiwa chetezo ndio utoe msamaha? Kwa nini tunawazungusha watu kwa kutowasamehe wanapokiri makosa yao na katika unyonge wao? Kwa nini tunaweka vikwazo na sababu nyingi ili tuwasemehe watu waliotukosea hata kama weshakiri makosa yao? Jumuiya ya wakristo, na Kanisa kwa ujumla lisilotoa msamaha ni wazi jumuiya hiyo na Kanisa hilo halimwakilishi Yesu Kristo. Mkusanyiko huo utakakuwa mkusanyiko usio na mwelekeo na mbele yake kuna giza kubwa sana!

Katika Injili ya leo Yesu anatoa simulizi la kuvivaa viatu vya wale waliotusamehe na kujirudi ndani ya nafsi zetu kwa wale tuliowakosea. Hii ndiyo namna ya uzito na ulazima wa kusamehe. Mara nyingi Yesu ameonyesha hali hiyo, na hata umauti wake kwa ajili ya dhambi zetu. Yesu alipoletewa mbele yake mwanamke yule mzizi, aliyasema haya, baada ya kulitafakari tukio hile undani akiwa anaandika chini, “Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza kumtupia jiwe,” Yoh 8:7. Wote tunajua kilichofuata baada ya maneno haya ya Yesu.

Bwana wetu Yesu Kristo ni kielelezo sahihi cha Msamaha wa Mungu. Ndugu yangu, “Mtu huyo Mungu amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe Mkuu na Mwokozi, awape Waisraeli toba na msamaha wa dhambi,” Mdo 5:31. Na nikatika “yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi; naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” Kol 1:14-15.

Ndugu yangu, msamaha ni Ukristo wetu na maisha yetu kama wafuasi wake Kristo. Msamaha ni tendo la Mungu mwenyewe na sababu ya wokovu wetu. Hakuna anayeishi kwa sababu yake mwenyewe, wala hakuna afaye kwa nafsi yake, Rum 14:7

Ndugu yangu, nani wewe usiye samehe?

Tumsifu Yesu Kristo!

“Yesu akamwambia, ‘Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini,’” Mt 18:22

Ee Yesu, nijalie Roho ya Msamaha na nifanye hivyo bila kujibakiza. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario