viernes, 19 de febrero de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 2 YA KWARESMA MWAKA-C

JUMAPILI YA 2 YA KWARESMA YA MWAKA-C

Somo I: Mwa 15:5-12, 17-18
Zab: 27:1, 7-8, 8-9, 13-14
Somo II. Flp 3:17-4:1
Injili: Lk 9:28b-36
Nukuu:
Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako. Akamwamini Bwana, naye akamhesabia jambo hili kuwa haki,” Mwa 15:5-6 

Akamwambia, Unipatie ndama wa miaka mitatu, na mbuzi mke wa miaka mitatu, na kondoo mume wa miaka mitatu, na hua, na mwana njiwa.” Mwa 15:9

Ikawa, jua lilipokuchwa likawa giza, tazama, tanuru ya moshi na mwenge unaowaka ulipita kati ya vile vipande vya nyama,” Mwa 15:17 

Maana wengi huenenda, ambao nimewaambieni mara nyingi habari zao, na sasa nawaambia hata kwa machozi, kuwa ni adui za msalaba wa Kristo,” Flp 3:18 

mwisho wao ni uharibifu, mungu wao ni tumbo, utukufu wao u katika fedheha yao, waniao mambo ya duniani,” Flp 3:19 

Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo,” Flp 3:20 

atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake,” Flp 3:21

Basi, ndugu zangu, wapendwa wangu, ninaowaonea shauku, furaha yangu, na taji yangu, hivyo simameni imara katika Bwana, wapenzi wangu,” Flp 4:1 

Ikawa katika kusali kwake sura ya uso wake ikageuka, mavazi yake yakawa meupe, yakimeta-meta,” Lk 9:29 

Na tazama, watu wawili walikuwa wakizungumza naye, nao ni Musa na Eliya; walioonekana katika utukufu, wakanena habari za kufariki kwake atakakotimiza Yerusalemu,” Lk 9:30-31 

Petro na wale waliokuwa pamoja naye walikuwa wamelemewa na usingizi; lakini walipokwisha amka waliuona utukufu wake, na wale wawili waliosimama pamoja naye,” Lk 9:32 

Ikawa hao walipokuwa wakijitenga naye, Petro alimwambia Yesu, Bwana mkubwa, ni vizuri sisi kuwapo hapa; na tufanye vibanda vitatu; kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya; hali hajui asemalo,” Lk 9:33 

Sauti ikatoka katika wingu, ikisema, Huyu ni Mwanangu, mteule wangu, msikieni yeye,” Lk 9:35

TAFAKARI: “Na hili ndilo agano letu la milele, ‘Huyu ni Mwanangu, mteule wangu, msikieni yeye.”

Wapendwa wana wa Mungu, Mama Kanisa leo anaadhimisha Dominika ya pili ya kwaresma ya mwaka “C” wa Kanisa. Masomo yetu yote matatu ya leo yanatuelekeza ni wapi lilipo agano letu la milele, na mapaswa yake kama kweli twataka kulifikia agano hilo, yaani, maisha hayo ya umilele.

Ndugu yangu tunayesafiri wote katika tafakari hii, elewa kwamba uwepo wako katika ulimwengu huu, na haya yote katika ulimwengu huu yanaufunua uwepo wa Mungu, ikiwa ni pamoja na fumbo zima la wokovu wetu. Hivyo uwepo wako si bahati mbaya hata kidogo! Wewe ni kusudi la pekee la Mungu ambalo mwisho wake ni umilele wa maisha yako. Ukweli huu unajidhihirisha katika historia ya wokovu wa mwanadamu. Huu ni mpango mahususi wa Mungu ambao tunaweza kuuona katika maeneo makuu manne; Uumbaji wa ulimwengu, Uumbaji wa mwanadamu, Maagano ya Mungu na watu wake, na mwisho tendo la kumwilishwa.

Uumbaji wa ulimwengu unathibitisha na kujionyesha kama sababu ya maandalizi ya uumbaji wa mwanadamu. Mwanadamu anaandaliwa sehemu ya kuishi ili amjue Muumba wake, ampende, amtumikie, na mwisho arudi kwake alipoandaliwa, yaani uzima wa milele. Hivyo, Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi,” Mwa 1:1. Mbingu na nchi hizi hazikuumbwa tu bila malengo. Maana Bwana, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine,” Isa 45:18. Huu ndio mpango wa Mungu juu ya mwanadamu. Hakika ni mpango wa pekee sana. Uwepo wako leo si bahati mbaya.

Na alivyoyaona yote yanafaa na kupendeza, ndipo ilipompendeza Mungu kumuumba mwanadamu kwa sura na mfano wake. Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba,” Mwa 1:27. Na kwa sababu hii mwanadamu anaowajibu huu mbele ya Mungu; kumjue, kumpenda, kumtumia, na kurudi kwake alipomwandalia, yaani, uzima wa milele. Hata pamoja na wajibu huu msingi, uwepo wako na wangu katika ulimwengu huu lazima uwe wa kuzaa matunda mena kila tunapopata fursa ya kuvuta pumzi aliyotupa Mungu. Naye Yesu anatuambia hivi, Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni,” Yoh 15:16. Kristo ndiye aliyetuchangua sisi kwa sababu pasipo yeye hakikufanyika cho chote lilichofanyika. Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu. Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:1-3. Ndugu yangu ona ulivyo tokeo na mpango maalumu wa Mungu!

Pamoja na uumbaji huu wa pekee wa mwanadamu, Mungu hakumwaacha ajiendee peke yake. Kwa nyakati mbalimbali Mungu amefanya maagano na watu wake ili kuwa nao karibu na wao walifikie lengo la kuumbwa kwao, yaani maisha ya milele. Somo letu la kwanza linazungumzia mpango na ukaribu huu wa Mungu kwa watu wake. Naye Mungu akamleta nje Abramu “akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako. Akamwamini Bwana, naye akamhesabia jambo hili kuwa haki,” Mwa 15:5-6. Mungu anamuhesabia haki Abramu kwa sababu ya hofu ya Mungu iliyokuwa ndani mwake.

Hata pamoja na hakikisho hilo la haki, Abramu anataka kujua ukweli na uhakika wa jambo hilo. Naye Mungu anajidhihirisha hivi katika agano lile, Akamwambia, Unipatie ndama wa miaka mitatu, na mbuzi mke wa miaka mitatu, na kondoo mume wa miaka mitatu, na hua, na mwana njiwa.” Mwa 15:9. Kielelezo hiki tambulishi cha Mungu kinaendana na kipimo cha utii wa Abramu. Abramu anafanya kama Mungu alivyomwamuru na haya ndiyo matokeo yake. Ikawa, jua lilipokuchwa likawa giza, tazama, tanuru ya moshi na mwenge unaowaka ulipita kati ya vile vipande vya nyama,” Mwa 15:17. Mungu anajidhihirisha katika hali ya tanuru ya moshi na mwenge unaowaka. Licha ya maagano kama haya kati ya Mungu na watu wake, Mungu huyu ameendelea kuwa karibu na watu wake kupitia Manabii na Waamuzi.

Wapendwa wana wa Mungu, kwa upendo usio na kipimo, wakati ulipotimia, (Ebr 1:1-2), katika historia hii ya wokovu, Mungu mwenyewe amejimwilisha na kukaa nasi. Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli,” Yoh 1:14. Hivyo wapendwa katika Kristo, lnjili ya leo inauweka sawa ukweli huu kwa mambo makuu matatu; Dira yetu ya kufuata kama Wakristo, Utumilifu wa nyakati, na Hatma yetu iliyojengeka katika agano la umilele. Haya yote yanafanyika katika tukio hili la kugeuka sura kwa Bwana wetu Yesu Kristo kadiri ya simulizi la Injili ya leo.

Kwanza, Dira yetu ya kufuata kama Wakristo. Heshima na cheo chako kama Mkristo ni utakatifu wako. Hivyo maisha yetu kama Wakristo kuelekea umilele yatafikika na kuwezekana kama ni tokeo la utakatifu wetu kwa kuyaona maisha kama ni jukumu la muda fupi hapa duniani na kama pia sehemu pekee ya maandalizi. Udhihirisho wa utakatifu huu kama dira yetu ya maisha ni tendo lile la kubadilika sura Kristo Yesu. Ikawa katika kusali kwake sura ya uso wake ikageuka, mavazi yake yakawa meupe, yakimeta-meta,” Lk 9:29. Kristo anavikwa Utukufu wake ambao ataunyakua rasmi mara baada ya mateso, kifo na ufufuko huko Yerusalemu. Hivyo Utukufu wa Kristo hautenganishwa na msalaba/mateso. Kwa maana nyingine hakuna Utukufu pasipo msalaba. Kama Kristo ndiye njia, kweli na uzima, Yoh 14:6, nasi wafuasi wake itatupasa kupita njia hiyo hii ya msalaba, ukweli huu anaotufundisha, ili tuufikie uzima ule, yaani maisha ya milele.

Pili, ukamilifu wa nyakati. Katika tendo hili la kugeuka sura, tunaelezwa tokeo la watu wawili, yaani Musa na Eliya katika mazungumzano na Yesu. Na tazama, watu wawili walikuwa wakizungumza naye, nao ni Musa na Eliya; walioonekana katika utukufu, wakanena habari za kufariki kwake atakakotimiza Yerusalemu,” Lk 9:30-31. Katika tendo hili, Musa anawakilisha Torati, na Eliya Unabii. Hivyo leo Yesu anaikamilisha Torati. Naye Yesu anatuambia, “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin, nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaoondoka, hata yote yatimie,” Mt 5:17-18. Torati inatimilizwa kwa amri ya upendo kwa Mungu na jirani.Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii,” Mt 7:12. Ni ndani na katika Kristo tu tunapata neema na kweli kwa mkono wake.  Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo,” Yoh 1:17. Na huku ndiko kutimilika kwa sheria na kutamalaki kwa upendo, kweli, na neema.

Leo pia unabii wote ulionenwa juu ya Kristo na historia nzima ya wokovu wetu unakamilika. Unabii huu unafika ukomo wake kwa uwepo wa Kristo ambaye ni UPENDO WA MUNGU kwetu. Mtume Paulo anasema, Upendo haupungui neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika,” 1Kor 13:8. Huyu ndiye Kristo Yesu! 

Tatu, hatma yetu iliyojengeka katika agano la milele. Kristo ndiye kielelezo chetu na wokovu wetu. Leo Mungu Baba anauweka ukweli huu hadharani na kusema, “Huyu ni Mwanangu, mteule wangu, msikieni yeye,” Lk 9:35. Hili ndilo agano la milele kati yetu na Mungu, na Kristo akiwa ndiye daraja na mlango halisi wa sisi kupitia kwani ni kwake tu tutakuwa salama kama njia, ni kwa Kristo tu tunalishwa kweli katika kweli, na Kristo tu ndiye uzima halisi.

Wapendwa wana wa Mungu, pasipo shaka yoyote tutaelewa sasa vizuri somo letu la pili hasa pale Mtume Paulo anaposema sisi wenyeji wetu upo mbinguni. Tumeumbwa ili tuishi milele. Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo,” Flp 3:20. Hivyo ndugu yangu lazima utambue kwamba maisha yako hapa duniani ni jukumu la muda mfupi. Kuishi maisha yanayoongozwa na malengo kunatusukuma kuelewa ukweli huu, yaani uzima wa milele. Hivyo wale wote wanaoishi bila lengo hili la umilele  mwisho wao ni uharibifu, mungu wao ni tumbo, utukufu wao u katika fedheha yao, waniao mambo ya duniani,” Flp 3:19. Duniani hapa ni sehemu ya maandalizi ya umilele, na kupita tu. Haya siyo makazi yetu ya kudumu. Mungu hajakusudia jambo katika uumbaji wako. Na unapolazimisha jambo hili, yaani kushikamana na ulimwengu huu basi unakuwa adui wa msalaba wa Kristo, na sadaka yake pale msalaba haisemi chochote kuhusu ukombozi wako, Flp 3:18. Hivyo ndugu yangu, ni Kristo tu atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake,” Flp 3:21. Kwa maana nyingine, kwa nguvu zako bila Kristo ni bure. Utajiri wako bila Kristo ni bure, na vipaji na karama zako bila Kristo ni bure pia. Na katika ukweli huu wapendwa katika Kristo, ninaowaonea shauku, furaha yangu, na taji yangu, hivyo simameni imara katika Bwana, wapenzi wangu,” Flp 4:1. Kwa Kristo kuna furaha ya kweli. Amina

 Mzee Mbute Mabiti alifahamika sana kwa utajiri wake usihesabika. Alijali sana shughuli zake na hivyo kuchangamana kidogo sana wa watu. Alipenda sana kusafiri mwenyewe safari fupi na za mbali. Ilikuwa ni marufuku kumpakiza mtu kwenye gari yake ‘Toyota Landcruzer V 8.’ Umuombapo ‘lift’ na ikiwa amekuonea huruma usimamisha gari yake na kukupa nauli ya uko uendako na kusema, “komaa uwe na lako,” huku akikutolea macho kama mjusi aliyebanwa kwenye mlango. Hakika alikuwa Mzee Mabiti kama jina lake.

Siku moja akiwa anasafiri na kupita katikati ya mbuga moja ya wanyama alikutana na wamasai wawili, mume na mke. Baba huyu Mmasai aliomba ‘lift’ kwani hali ya mke wake haikuwa nzuri kwa sababu alikuwa karibu na kujifungua. Mzee Mabiti alisimamaisha gari yake kama kawaida. “Kulikoni? Mnashida gani, na niwasaidie nini?” aliwauliza Bwana na Bibi wale Wamasai kwa jeuri. “Baba lai, tunaomba lifuti,” Bwana yule mmasai alimjibu kwa unyonge. “Siwezi kuwapa ‘lift’ kwenye gari yangu, na sijawahi fanya hivyo kwa yeyote yule. Chukueni elfu kumi hii itawasaidia,” Mzee Mabiti alijibu kwa hasira. “Asante Baba lai, ila baki na hela yako kwa maana hapa mbugani haitatusaidia zaidi ya msaada wa lift,” yule Bwana alimshukuru Mzee Mabiti.

Basi, Mzee Mabiti alipandisha kioo cha gari yake, na kuondoka mwendo wa mashindano ya magari. Akiwa umbali wa kama kilometa mbili hivi, Mzee Mabiti alipata mpasuko wa tairi moja ya nyuma, upende wa kushoto wa gari yake na kuserereka pembeni ya njia. Haja kaa sawa, akaliona kundi la simba wanne wanakuja kulielekea gari lake. Mzee Mabiti hakuweza kutoka nje ya gari yake kwa lengo la kuvisha tairi nyingine aendelee na safari yake.

Baada ya nusu saa hivi wale Wamasai mtu na mke wake wakawa wamefika katika eneo la tukio huku simba wakiwa wananing’inia kwenye vioo wa gari ile. Wale Wamasai wakawafukuza simba wale kiasi cha kilomita moja hivi, na kurudi kumjulia hali Mzee Mabiti. Mzee Mabiti hakuwa na  biti tena. Alijawa na upole wa aibu kubwa. Alitoka ndani ya gari yake na kuomba msamaha ile familia. Bwana yule Mmasai akamsaidia kubadili lile tairi, na bila kusema neno Mzee Mabiti akawafungulia mlango mwenyewe na kuanza safari. “Leo nimejifunza mambo mengi kutoka kwenu ndugu zangu. Na hiki ndicho nilichojifunza: mali, ufahari, fedha siyo kitu kama hauna upendo wa kweli na kuwajali watu wengine. Nisameheni bure kwa kile kitendo kisicho cha utu nilichokifanya kwetu. Mzee Mabiti aliyasema maneno yale huku machozi yakimtoka. “Sisi Baba lai ameshakusamehe yooote. Asante sana kwa msaada yako,” Walimjibu kwa moyo wa shukrani.

Tumsifu Yesu Kristo.

Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo,” Flp 3:20


Ee Yesu, nijalie jicho la upendo wa kweli ili niweze kukuona kwa kila nitakayekutana naye katika maisha yangu na huduma nitakayokuwa naitoa kwa ajili ya watu wako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario