martes, 9 de febrero de 2016

TAFAKARI: JUMATANO YA MAJIVU

JUMATANO YA MAJIVU


Soma I: Yoe 2:12-18
Zab: 50:3-4, 5-6ab, 12-14, 17
Somo II: 2Kor 5:20-6:2
Injili: Mt 6:1-6, 16-18
Nukuu:
"Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuomboleza; rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie Bwana,  Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, naye hughairi mabaya." Yoe 2:12-13

"Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye," 2Kor 5:20

"Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni," Mt 6:1

TAFAKARI: “Mwanzo wa safari ya kujitakasa Jangwani.”

Wapendwa wana wa Mungu, karibuni kwa tafakari hii tunapoanza safari yetu ya kujitakasa huko jangwani. Leo Mama Kanisa anaanza safari hiyo rasmi na wana wake kwa kujitakatifuza. Safari hii itatuchukua siku 40-"Quadragesima," ambayo hutambulika kama "Kwaresma."

Kwa nini ni siku 40?
Maana ya awali kabisa, 40 huwakilisha muda wa kutosha. Ni muda wa kutosha kwa Mungu, na kwa mwanadamu akiutumia vizuri ataufikia utakatifu wake. Namba 40 imetumika sana kuelezea "kutosha" kitu au "kikomo" cha kitu, hasa pale binadamu anapohusika kwa mwongozo wake Mungu na kumrudia baada ya maasi yasababishwayo na dhambi.

Taifa la Israel liliteseka vya kutosha jangwani kwa miaka 40. "Nami miaka arobaini nimewaongoza jangwani;  nguo zenu hazikuchakaa juu yenu, wala kiatu chako hakikuchakaa katika mguu wako," Kumb 29:5

Wakati wa Nuhu "mvua ikanyesha juu ya nchi, siku arobaini mchana na usiku," Mwa 7:12. "Musa akaingia ndani ya lile wingu, akapanda mlimani; Musa akawa humo katika ule mlima siku arobaini, mchana na usiku," Kut 24:18. Ndugu yangu katika agano la kale yapo matukio zaidi 140 yenye uhusiano wa muda wa kutosha yaani namba hiyo 40.

Ikiwa kielelezo chetu ni Yesu Kristo, Kwaresma yetu ina mwono wa mfungo wa Yesu mwenyewe jangwani kwa siku arobaini, mchana na usiku. "Akafunga siku arobaini mchana na usiku, mwisho akaona njaa," Mt 4:2.

Safari yetu leo inaanza kwa kupakwa majivu kwenye paji la uso ikiashiria mambo makuu mawili; kwanza ubinadamu wetu, ikimaanisha kuwa yatupasa kuwa wanyenyekevu. Pili, sisi tu mavumbi na mavumbini tutarudi. Ni ishara ya toba na majuto. Ni mabadiliko ya ndani yanayotuweka karibu na Mungu na baraka zake.

Somo letu la kwanza latupa picha hiyo ya mfungo. Mungu yupo tayari kuanza upya nasi pale tu, tutakapomjeukia na kuacha njia zetu mbaya. Huruma ya Mungu kwetu inategemea mabadiliko yetu kumwelekea yeye. Mungu yupo tayari kughairi adhabu yake tunapomwelekea. "Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuomboleza; rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie Bwana,  Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, naye hughairi mabaya." Yoe 2:12-13. Je, ndugu yangu upo tayari kuanza na upya na Mungu? Wakati ndiyo sasa.

Ni mambo gani ya kufanya katika safari hii?
Yapo mambo makuu matatu ya kufanya kadiri ya injili ya leo. Jambo la kwanza, kwaresma yamaanisha ni muda wa kusali na kumrudia Mungu. Kusali huku si kwa kupayuka, bali kwa kuzama zaidi ndani ya nafsi zetu. Kikomo chake isiwe tu pasaka, bali maisha yetu yote. Na mapenzi ya Mungu kwetu katika Kristo ni haya, Angalieni mtu awaye yote asimlipe mwenziwe mabaya kwa mabaya; bali siku zote lifuateni lililo jema, ninyi kwa ninyi na kwa watu wote. 16 Furahini siku zote; ombeni bila kukoma; shukuruni kwa kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu,” 1The 5:15-18 

Silaha ya mkristo yeyote ni sala. Kama kweli tunaitaji ulinzi wa Mungu, sala inapaswa kuwa tabia yetu. Kuwa mtu wa sala. Sala ya kweli na ya watakatifu ni hali ya kuomba ukiwa na imani kuwa ushapata hata kama bado.

Kusali huku pia kulenge kung'oa "dhambi Dola." Mfano: Serikali ya Tanzania inaongozwa na dola ya Chama Cha Mapinduzi-CCM. Chama hiki ndicho kilichounda serikali. CCM ndiyo dola tawala. Katika mfumo wa maisha ya kiroho, kila mmoja wetu anayo "dhambi dola," ikimaanisha dhambi tawala. Dhambi hii ni ile ambayo kila mara unajikuta ushadondoka huko na inakupelekea kuwa kero kwani kila mara unaiungama. Weka mikakati na Mungu kuiacha kwa msaada wake-"by the Will Power of God-WPG" Hili ni lengo kubwa na mojawapo ya sala hasa kipindi hiki cha Kwaresma.

Pili, ni kufunga. Kufunga hapa kwa maanisha kujinyima kwa ajili ya faida yako na wengine. Jambo hili ni kwa chochote kile utakacho amua kufanya. Yatupasa pia kulenga katika mambo yale yanayogusa mfumo wa maisha yetu ya kila siku. Mara nyingi watu wengi hulenga kujinyima kula. Si mbaya! Ila unalifanya hilo kwa makusudio ya nini? Faida ya kwanza ni kwa afya yako. Jambo la pili na la maana liwe kwa ajili ya waitaji. Usianze kuwatafuta kwa kwenda mbali. Anza na familia yako tukijua kwamba ukarimu huanza nyumbani. Itazame jumuiya yako. Wapo wahitaji wengi sana. Tazama majirani zako wasio ndani ya jumuiya yako. Na mwisho litazame Kanisa lako; iwe kigango au parokia. Naye Yesu anatuambia, Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi,” Yoh 13:35 

Tatu, Kwaresma yetu analenga katika swala zima la kutoa sadaka. Hapa yakupasa kujifunza namna ya kutoa sadaka. Kwanza si kwa kujionyesha bali kwa kutambua wajibu wako na kumtolea Mungu mastahili yake. Yote ni mali ya Mungu. 1 Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na wote wakaao ndani yake,” Zab 24:1. Na Mungu ndiye msingi wa vyote. Mbingu ni mali yako, nchi nayo ni mali yako, Ulimwengu na vyote viujazavyo Ndiwe uliyeupiga msingi wake,” Zab 89:1. Hivyo ndugu yangu,  tunamtolea Mungu kama shukrani kwa yale anayotukirimia. Sadaka yako iwe kamilifu na yenye kumpendeza Mungu. Lakini, toeni sadaka vile vya ndani, na tazama, vyote huwa safi kwenu,” Lk 11:41.  Usimtolee Mungu makapi. Hapa imaanishe sadaka halali. Ukiangalia sh 50 hadi 200 kwa mfano, hutaona maandishi haya, "fedha halali kwa malipo ya sh 50, 100, au 200." Ila kwa upande wa sh 500 hadi 10000 maandishi hayo yapo. Je, wewe unayetoa kila mara sh. 50 tu kama sadaka yako, ni pesa halali hiyo? TAFAKARI!

Ndugu yangu, tukiyafanya hayo na kuyaishi, mfungo wetu wa siku 40-Kwaresma, utakuwa na maana sana. Na pasaka yetu itamaanisha ukombozi wa kweli, wa mwili na Roho. Hiyo ndiyo maana halisi ya sadaka ya Yesu pale msalabani. Yeye aliyekubali kuchukua dhambi zetu ingawa hakuwa na dhambi. Yeye aliyekubali kuwa masikini, ili sisi tuwe matajiri. Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Ni upendo wa ajabu wa Mungu. Safarí imeanza basi tusikubali kubaki nyuma.

Tumsifu Yesu Kristo!


“Ee Yesu uliye dharauliwa kwa ajili ya dhambi zangu niwezeshe nifanye toba ya kweli. Amina”

No hay comentarios:

Publicar un comentario