viernes, 5 de febrero de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 5 YA MWAKA-C

JUMAPILI  YA 5 YA MWAKA-C
7/2/2016
Somo I: Isa 6:1-2a, 3-8
Zab: 138:1-2, 2-3, 4-5, 7-8
Somo II: 1Kor 15:1-11
Injili: Lk 5:1-11
Nukuu:
Ndipo niliposema, Ole wangu! Kwa maana nimepotea; kwa sababu mimi ni mtu mwenye midomo michafu, nami ninakaa kati ya watu wenye midomo michafu; na macho yangu yamemwona Mfalme, Bwana wa majeshi,” Isa 6:5

Kisha mmoja wa maserafi wale akaruka akanikaribia; naye alikuwa na kaa la moto mkononi mwake, ambalo alikuwa amelitwaa kwa makoleo toka juu ya madhabahu; akanigusa kinywa changu kwa kaa hilo, akaniambia, Tazama, hili limekugusa midomo yako, na uovu wako umeondolewa, na dhambi yako imefunikwa,” Isa 6:6-7

Kisha nikaisikia sauti ya Bwana, akisema, Nimtume nani, naye ni nani atakayekwenda kwa ajili yetu? Ndipo niliposema, Mimi hapa, nitume mimi,” Isa 6:8

Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mitume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu,” 1Kor 15:9 

Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami,” 1Kor 15:10 

Basi, kama ni mimi, kama ni wale, ndivyo tuhubirivyo, na ndivyo mlivyoamini,” 1Kor 15:11 

Hata alipokwisha kunena, alimwambia Simoni, Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki,” Lk 5:4

Simoni akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu,” Lk 5:5

Basi, walipofanya hivyo walipata samaki wengi mno, nyavu zao zikaanza kukatika; wakawapungia mikono washirika wao waliokuwa katika chombo cha pili, waje kuwasaidia; wakaja, wakavijaza vyombo vyote viwili, hata vikataka kuzama,” Lk 5:6-7 

Simoni Petro alipoona hayo, alianguka magotini pa Yesu, akisema, Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana,” Lk 5:8 

“Yesu akamwambia Simoni, Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu,” Lk 5:10b 

TAFAKARI:Tweka mpaka kilindini.”   
                                                                             
Wapendwa wana Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya ‘5’ ya mwaka ‘C’ wa Kanisa. Wazo kuu la masomo yetu yote matatu linatoka katika Injili ya leo kwa maneno haya ya Yesu aliyomwambia Simoni, “Tweka mpaka kilindini.” Maneno haya ya Yesu yanaamsha hari mpya ndani ya tumaini lile ambalo lishapotea kutokana na kukata tamaa, na wakati mwingine kutojipokea kutokana na historia zetu na mazingira yetu ya ukuaji yaliyo mabaya. Mara zote tunapopata nafasi ya kukutana na Mungu anatualika kuanza upya naye, Mungu wetu aliye UPENDO, HURUMA, MSAMAHA, HAKI, na UPOLE.

Wito wa Nabii Isaya unaonyesha mtazamo wa Mungu na jinsi tunavyojitazama kama watu tusiostahili kwa yale Mungu anayotufikiria. Hakika upendo, huruma, msamaha, haki, na upole wa Mungu hatuwezi kuufananisha na kitu chochote. Mungu atabaki kuwa Mungu kwa milele yote! Isaya anapotazama mwaliko wa Mungu na kile alicho anaona ni vitu viwili tofauti. Naye anasema, “Ole wangu! Kwa maana nimepotea; kwa sababu mimi ni mtu mwenye midomo michafu, nami ninakaa kati ya watu wenye midomo michafu; na macho yangu yamemwona Mfalme, Bwana wa majeshi,” Isa 6:5. Pamoja na historia zetu zilizombaya, kushindwa kwetu katika maisha, na kudharauliwa kwetu, bado Mungu anasema, “tweka mpaka kilindini.” Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, ‘kutweka mpaka kilindini’ kuna maanisha hivi; pamoja na shindwa yako bado una kitu cha kufanya na kubadili historia yako mbaya. Hivyo kitumie kitu hicho katika ukamilifu wake na hadi mwisho wake, na yote yatakuwa mapya.” Huu ndiyo ujumbe mahususi.

Mpendwa katika Kristo, unapojiachia kwa Mungu bila kujibakiza katika maana ya kuyatweka yote mpaka kilindini, ndipo utakaso unapokujilia na kufanywa upya mbele ya Mungu, na kuhesabiwa haki kwa mastahili ya Mungu mwenyewe. Isaya anayaendea mabadiliko haya katika maisha yake kwa sababu Mungu kesha pendezwa naye. Kisha mmoja wa maserafi wale akaruka akanikaribia; naye alikuwa na kaa la moto mkononi mwake, ambalo alikuwa amelitwaa kwa makoleo toka juu ya madhabahu; akanigusa kinywa changu kwa kaa hilo, akaniambia, Tazama, hili limekugusa midomo yako, na uovu wako umeondolewa, na dhambi yako imefunikwa,” Isa 6:6-7. Ni mara ngapi tunajiona watu tusiofaa mbele za watu na kujipoteza kabisa? Ndugu yangu, hata kama ulimwengu wote utakuchukia, Mungu hubaki na upendo wake kwako wa ajabu. Embu itazame mikono ya Yesu pale msalabani. Yesu anakuambia, ‘tazama nimeyakubali haya yote na hata kufa kifo cha aibu msalabani kwa sababu nakupenda kupita vyote.’ Hakika Mungu anatupenda upeo!

Wapendwa wana wa Mungu, utaisikia sauti ya Mungu ndani yako unapo utafakari upendo huu wa Mungu ulio wa ajabu. Isaya anaisikia sauti ya Mungu ndani yake, na kusema, Kisha nikaisikia sauti ya Bwana, akisema, Nimtume nani, naye ni nani atakayekwenda kwa ajili yetu? Ndipo niliposema, Mimi hapa, nitume mimi,” Isa 6:8. Isaya anazaliwa upya mwili na roho na sasa yupo tayari kuyafanya mapenzi ya Mungu. Huwezi kukutana na Mungu katika maisha yako naye akakuacha kama ulivyokuwa mwanzo.

Kwa uzoefu aliokuwa nao Simoni kama mvuvi wa samaki, isingekuwa rahisi kuuchukua ushauri wa Yesu wa kurudi tena ndani ya maji na kuvua samaki. Elewa kwamba usiku kucha Simoni na wenzake walikesha wakivua bila kupata chochote. Usiku ndio muda muhafaka wa kuvua samaki. Leo kwa namna ya kushangaza Yesu anamwambia Simoni azitupe nyavu zake ndani ya maji, na kwenda kinyume kabisa na utaratibu wa uvuvi. Hata alipokwisha kunena, alimwambia Simoni, Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki,” Lk 5:4. Simoni akitambua alichokifanya usiku kucha bila kupata chochote, akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu,” Lk 5:5. Maneno haya ya Simoni “lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu,” yanaonyesha kujisalimisha kwa Simoni pasipo shaka mbele ya Yesu. Maneno hayo ya Simoni yenye kuonyesha kujisalimisha kwake, ndiyo roho na uzima. Katika hili Yesu anasema, Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima,” Yoh 6:63. Na neno lile Yesu alilomwambia Simoni “tweka mpaka kilindini,” ndiyo uzima na ponya yake Simoni.

Na tazama huu ndio uzima juu ya neno lile la Yesu na kujisalimisha kule kwa Simoni: Basi, walipofanya hivyo walipata samaki wengi mno, nyavu zao zikaanza kukatika; wakawapungia mikono washirika wao waliokuwa katika chombo cha pili, waje kuwasaidia; wakaja, wakavijaza vyombo vyote viwili, hata vikataka kuzama,” Lk 5:6-7. Ndugu yangu, yawezekana umekata tamaa katika maisha yako kutokana na jambo fulani ambalo kwa uelewa wako na uzoefu wako hakuna pa kutokea. Leo Yesu anakuambia neno hili, “‘tweka mpaka kilindili,’ yaani jaribu tena kile kilichobaki katika ukamilifu wake, na hadi mwisho wake kabisa, nawe utaona uwezo wangu.”

Matokeo ya nguvu na uwezo wa Yesu katika muujiza huu, kinamfanya  Simoni kuyaona maisha yake ya ndani. Simoni Petro alipoona hayo, alianguka magotini pa Yesu, akisema, Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana,” Lk 5:8. Ndugu yangu, hutoweza kujiona ulivyo kama hutojiachia ndani na katika Kristo Yesu. Kuiona vizuri chunusi iliyoko kwenye paji la uso wako, yakupasa kusimama mbele ya kioo. Kumbe kujiachia mbele ya kioo kunakuwezesha kujiona vizuri. Yesu ni kioo kwetu, na ndivyo Simoni alivyojigundua kuwa yu mdhambi. Pamoja na udhaifu ule aliokuwa nao Simoni bado Mungu anampango na maisha yake. Tena mpangu mahususi kabisa. Naye “Yesu akamwambia Simoni, Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu,” Lk 5:10b. Yesu anaifanya njia katika maisha ya Simoni. Huyu ndiye baadaye aliyejulikana kama Simoni Petro, na juu yake ndipo lilipo jengwa Kanisa. Mtume Paulo anatuambia, Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili,” 1Kor 10:13

Wapendwa wana wa Mungu, ukiyatazama maisha yako na jinsi Mungu alivyoendelea kuwa upendo na huruma kwako, hakika yote ndani yetu ni kwa neema ya Mungu. Hakika, “Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” Zab 130:3. Hivyo ni pamoja na historia mbaya aliyokuwa naya Sauli wa Tarso, leo kwa neema ya Mungu anajulikana kama Mtume Paulo. Paulo anatoa ushuhuda wa maisha yake na kusema, Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mitume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu,” 1Kor 15:9. Hata pamoja na ukweli huo, huruma na neema ya Mungu ni kubwa zaidi ya uovu wako kama utajisalimisha kwake. Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami,” 1Kor 15:10. Mungu yupo tayari kuanza upya nawe endapo tu kama upo tayari. Hizi ni neema za Mungu zinazotuzunguka kila wakati. Na kwa namna ya pekee mwaka huu wa Kanisa wa huruama ya Mungu ni wakati wa kutumia fursa hiyo vizuri. Ndugu yangu, tweka mpaka kilindini!

Ngesha Biloko alijulikana sana kwa upigaji wa gitaa la nyuzi sita. Hakuna aliyeweza kushindana naye katika ujuzi huu wa uchezaji gitaa. Hivyo liliandaliwa tamasha kubwa sana, na walialikwa wachezaji maarufu wa gitaa ulimwengu mzima.

Siku moja kabla ya shindano lile, Ngesha Biloko aliwasili katika jiji lile yalipokuwa yameandaliwa mashindano yale akiwa na gitaa lake. Biloko alipokelewa vizuri na kuonyeshwa chumba chake. Kesho yake kama kawaida alifanya mazoezi chumbani mwake na kujiridhisha.

Jioni ilifika mashindano yalianza. Biloko alikwa mtu wa kumi katika orodha ile ya wacheza gitaa 15 maarufu duniani. Ilipofika wakati wake alipokelewa kwa mbwembwe jukwani kwa sababu wengi waliyajua makali yake. Akiwa jukwani, na watu wote kwenye ukumbi ule wakisubiri kusikia uchezaji wake, Biloko alipikwa na butwaa alipoona gitaa lake likiwa na nyuzi tatu tu. Hakujua kilichotokea kuhusu gitaa lake.

Hata hivyo hakuwa na njia nyingine zaidi ya kuzicheza nyuzi zile tatu zilizobaki. Alijitia ujasiri na kulicharaza gitaa lile. Baada ya kumaliza dakika zake tano kama ilivyokuwa imepangwa, ukumbi mzima ulirindima kwa kelele za shangwe na vifijo. Msema chochote-MC, katika ukumbi ule alisema hivi, “tumekuwa tukisikia uchezaji wako wa gitaa kwa kuda mrefu sasa, ila leo umekuja na kitu kipya kabisa ambacho hakijawahi kusikika masikioni mwetu. Viva Biloko, Viva!!”

Ndugu yangu, Biloko alitweka mpaka kilindini.

Tumsifu Yesu Kristo.

Lakini tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka kwetu,” 2Kor 4:7

No hay comentarios:

Publicar un comentario