miércoles, 3 de febrero de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 4 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 4 YA MWAKA-C

Somo: 1Fal 2:1-4, 10-12
Zab: 1Nya 29:10, 11ab, 11d-12, 12acd
Injili: Mk 6:7-13
Nukuu:
Mimi naenda njia ya ulimwengu wote; basi uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamume,” 1Fal 2:2 

uyashike mausia ya Bwana, Mungu wako, uende katika njia zake, uzishike sheria zake, na amri zake, na hukumu zake, na shuhuda zake, sawasawa na ilivyoandikwa katika torati ya Musa, upate kufanikiwa katika kila ufanyalo, na kila utazamako,” 1Fal 1:3

ili Bwana afanye imara neno lake alilonena kwa habari yangu, akisema, Ikiwa watoto wako wataiangalia njia yao, wakienda mbele zangu kwa kweli, kwa moyo wao wote, na kwa roho yao yote, (akasema), hutakosa mtu katika kiti cha enzi cha Israeli,” 1Fal 2:4 

Basi Sulemani akaketi katika kiti cha enzi cha Daudi baba yake; na ufalme wake ukawa imara sana,” 1Fal 2:12 

akawakataza wasichukue kitu cha njiani isipokuwa fimbo tu; wala mkate, wala mkoba, wala pesa za bindoni; lakini wajifungie viatu; akasema, Msivae kanzu mbili,” Mk 6:8-9 

Akawaambia, Mahali po pote mtakapoingia katika nyumba, kaeni humo hata mtakapotoka mahali pale,” Mk 6:10 

Na mahali po pote wasipowakaribisha ninyi wala kuwasikia, mtokapo huko, yakung'uteni mavumbi yaliyo chini ya miguu yenu, kuwa ushuhuda kwao,” Mk 6:11

Wakatoka, wakahubiri kwamba watu watubu,” Mk 6:12

Wakatoa pepo wengi, wakapaka mafuta watu wengi waliokuwa wagonjwa, wakawapoza,” Mk 6:13 

TAFAKARI: “Kama Mzazi unawaachia urithi gani watoto wako?”

Wapendwa wana wa Mungu, nachelea kusema kwamba leo malezi wayapatayo watoto wetu kutoka kwa wazazi wao yamekuwa kama yale ya kuku huria, kujitafutia wenyewe. Malezi haya ni hatari sana kama ilivyo kwa kuku hawa huria yalivyo hatarishi kwa ugonjwa wa kideri.  Hatari ya kwanza ni kwamba wazazi wanakosa nguvu ya kimaadili katika kuonya, kukemea, kuagiza na kuongoza. Wazazi hawawezi tena kuwa kwenye nafasi zao kwa sababu wanapigana vikumbo huko mitaani na watoto wao katika ile hali ya kujiokotezea kama kuku huria.

Hatari ya pili ni aina ya viongozi tunao wapata kutoka  katika jamii yetu leo. Si jambo la kushangaza leo kuwaona viongozi tena wenye nafasi kubwa katika jambii wasiojishemu, na wasio na akiba ya maneno midomoni mwao. Viongozi hao ni zao au tokeo la familia hizi huria. Na ninapoongelea viongozi ninamaanisha pande zote, iwe taasisi za serikali au za kidini. Si jambo la kushangaza kumwona kijana mdogo kabisa tena wa umri akimnasa makofu Babu au mzazi wake wa kumzaa kwa vile tu nafasi na ofisi yake inaruhusu. Ulewi wa madaraka na matumizi mabaya ya madaraka. Hiki ni kizazi cha nyoka! Je, tufanye nini? Yatupasa kila mmoja wetu kadiri ya nafasi na wito wake kwenda kwenye kiini cha tatizo, yaani, FAMILIA, na kuangali ni wapi tulipokosea au potoka.

Leo kwa namna ya pekee Mama Kanisa anatutaka tujifunze kwa Mfalme Daudi na kwa Yesu mwenyewe. Wakati wa siku zake za mwisho ulipotimia, Mfalme Daudi alimwita mtoto wake Sulemani na kumwachia urithi wa kudumu. Kwanza, Daudi  anatambua uwezo wa mtoto wake na yale yatayomkabili huko mbele ya maisha. Daudi anamwambia mwanaye, Mimi naenda njia ya ulimwengu wote; basi uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamume,” 1Fal 2:2. Leo wazazi wetu wanafanya yale ya kawaida sana na ya mzunguko wa kawaida. Wakati mwingine ni mtindo wa kuiga tu. Mfano, wajibu mkubwa wa mzazi leo: Mtoto ameenda shule, amekula, amelala, na amevaa, basi. Hakuna muda wa kukaa na watoto wetu na kujadili yale ambayo hatuyasemi kwa kuwahofia. Haya ambayo hatuyasemi ndiyo wanayookoteza huko mitaani na mwisho wanaishia kwenye gonjwa la kideri kama kuku huria.

Mfalme Daudi anamwambia mtoto wake Sulemani, “uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamume.” Haya maneno ni mazito sana. Hii ndiyo jando ya watoto wa kiume. Je, wewe Baba unajua wajibu huu muhimu kwa watoto wako wa kiume. Leo kuwaona watoto wa kiume kutoboa masikio, kuvaa hereni, kusuka nywele, na kuvaa milegezo ni jambo la kawaida na jambo la kusikitisha wapo wazazi wanao furahia hali hii na hata kuwashawishi watoto wao kuwa hivyo. Ajabu na robo! Je, na wewe Mama una nafasi ya kukaa na mtoto wako wa kike na kumwambia, “uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamke?” Hii ndiyo unyago kwa watoto wa kike. Leo si jambo la ajabu kuwaona mabinti zetu kuiga tabia za kiume na kutaka kuwa hivyo. Hivi Mungu alikosea kutuumba kama tulivyo? La hasha! Wazazi wetu wapo likizo isiyo na ukomo.

Wapendwa wana wa Mungu, shule ya kwanza na ya muhimu ni FAMILIA. Tukikosea hapa hatuna mtu katika ukamilifu wake. Malezi ya mwili ni muhimu sana. Hili la mwili linaendana pili na la kiroho. Wazazi na walezi mnawajibu wa kuwafundisha watoto wenu kuishi na hofu ya Mungu. Nasi katika taasisi za kidini na serikali tunawajibu huo kadiri ya nafasi na karisma ya taasisi. Hili nalo Mfalme Daudi analifanya kwa mtoto wake Sulemani. Naye Daudi anamwambia Sulemani, uyashike mausia ya Bwana, Mungu wako, uende katika njia zake, uzishike sheria zake, na amri zake, na hukumu zake, na shuhuda zake, sawasawa na ilivyoandikwa katika torati ya Musa, upate kufanikiwa katika kila ufanyalo, na kila utazamako,” 1Fal 1:3

Jamii isiyokuwa na hofu ya Mungu ni hatari sana. Leo kuona watu wanachinjwa kama kuku katika matukia tofauti tofauti ni matukio ambayo yanaanza kuzoeleka. Mbaya zaidi ni pale unapoona jamii kutoshitushwa na haya yanapotokea. Leo mtu kukwapua hela za umma kwa kiasi kukubwa awezacho kinaonekana kama sifa na mafanikio. Tusiporudi kwenye kiini cha tatizo yaani, FAMILIA, hata kama tukianzisha mahakama za mafisadi kila mtaa haitakuwa tiba kwa tatizo la ufisadi kwa sababu hata hao mahakimu tunaotegemea wasimamie sheria na kutenda haki wana Upungufu wa Kinga ya Maadili-“UKIMA.” Huu UKIMA ni tatizo kubwa sana leo katika Familia zetu, Taasisi zetu za kidini na hasa taasisi za kiserikali, na Taifa kwa ujumla wake.

Pasipo na hofu ya Mungu, haki za wanyonge huporwa mchana kweupe. Pasipo na hofu ya Mungu, waliopewa dhamana na umma huzikanyaka haki za watu bila kujali. Pasipo na hofu ya Mungu, katiba ya nchi kama sheria mama uvunjwa bila kujali kila kukichwa. Kinachoangaliwa hapa ni maslahi binafsi na ya kichama. Je, haya hamuyaoni?

Kwenye malezi mazuri ya mwili na roho maisha yajayo huwa na matumaini. Kwenye malezi mazuri ya mwili na roho, kuna urithishwaji mzuri wa maadili kutoka kizazi kimoja kwenda kingine. Leo walio wengi ukimuuliza kesho itakuaje hana jibu, zaidi ya ubabaishaji tu. Kila mmoja anaishi kwa ujanja ujanja tu. Kila mmoja yupo kumuwahi mwingine, tena kwa kumdhuru. Leo wote tunaishi kama tupo kwenye vituo vya treni, yaani, kila mmoja anaushikilia mzigo wake akifikiri aliye jirani yake ni mwizi. Ajabu na roho! Mfalme Daudi anamwachia mtoto wake Sulemani urithi wa maadili mema akijua kuna matumaini hapo kesho. Naye anasema, ili Bwana afanye imara neno lake alilonena kwa habari yangu, akisema, Ikiwa watoto wako wataiangalia njia yao, wakienda mbele zangu kwa kweli, kwa moyo wao wote, na kwa roho yao yote, (akasema), hutakosa mtu katika kiti cha enzi cha Israeli,” 1Fal 2:4. Wapendwa wazazi, walezi, na wale wote walio kwenye taasisi za kidini, na kiserikali tuna kazi ya zaida kulitoa Taifa hapa lilipo na kulipeleka hapo kesho kwenye mwanga wa kweli. Tuache mtindo wa kuishi kama vile kesho haipo. La sivyo mbele huko ni giza tupu!

Matokeo ya malezi mazuri ya mwili na roho aliyoyatoa Daudi kwa mtoto wake, ni kile alichokuwa Mfalme Sulemani. Basi Sulemani akaketi katika kiti cha enzi cha Daudi baba yake; na ufalme wake ukawa imara sana,” 1Fal 2:12. Je, tunaacha uhenga gani kwa watoto wetu na familia zetu mara tuuachapo ulimwengu huu?

 Alilolifanya Mfalme Daudi kwa mwanaye Sulemani, ndilo analolifanya Yesu kwa wanafunzi wake ‘Thenashara,’ yaani, wale kumi na mbili, anapowatuma wawili wawili. Fundisho la kwanza ni kwamba Yesu anawafundisha mitume wake mshikamano akijua ‘umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu.’ Jambo la pili, Yesu anawapa angalizo la namna ya kuuendea ulimwengu ili wafanikishe lengo la msingi ambalo lipo mbele yao, yaani, “wakahubiri kwamba watu watubu,” Mk 6:12. Ili lengo hili lifikiwe, yawapasa, “wasichukue kitu cha njiani isipokuwa fimbo tu; wala mkate, wala mkoba, wala pesa za bindoni; lakini wajifungie viatu; akasema, Msivae kanzu mbili,” Mk 6:8-9. Ukweli ni kwamba kadiri watakavyo jitenga na malimwengu haya ndiyo watakavyokuwa huru kulifikia lengo hili Msingi, “kuhubiri habari njema, na kufanya toba ya kweli.”

Malezi hayo ayatoayo Yesu kwa hao Thenashara yana lenga hasa mwili na ndiyo jando yao. Huwezi kuyafikia malengo yako kama hautakuwa na kiasi katika maisha yako. Hili Yesu analiona vizuri sana. Yesu anazidi kulikazia hili na kuwaambia, “Mahali po pote mtakapoingia katika nyumba, kaeni humo hata mtakapotoka mahali pale,” Mk 6:10. Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, ili kuyafikia malengo yako katika maisha unahitaji utulivu wa mwili na roho. Na hata pale unapofanikiwa unahitaji utulivu wa mwili na roho kuyachambua kwa kina mafanikio hayo. Huku ndiko Yesu anakokuita kwenda faraghani. Basi wale mitume waliporudi walimweleza mambo yote waliyoyatenda; akawachukua, akaenda nao faraghani mpaka mji mmoja uitwao Bethsaida,” Lk 9:10.  Maisha ya kutangatanga bila tafakari ya kina kwa kile utakacho kukifanya ni vigumu kukifikia. Hili nalo Yesu analiona. 

Kwa upande wa kiroho, Yesu hakuacha kuwafundisha wanafunzi wake ili walifikie lile lengo. Naye anawaambia wanafunzi wake, Na mahali po pote wasipowakaribisha ninyi wala kuwasikia, mtokapo huko, yakung'uteni mavumbi yaliyo chini ya miguu yenu, kuwa ushuhuda kwao,” Mk 6:11. Anachokisema Yesu hapa ni hiki; ‘wanafunzi wake wasipoteze muda kwa kujihesabia haki hata kama watathihakiwa kuliko wazi na kwa makusudi.’ Watu hawana uwezo wa kuwahesabia haki isipokuwa Mungu mwenyewe. Hayo yakitokea yawapasa kuondoka wakiwa na moyo mweupe bila kuchua lolote kutoka kwao. Ni Mungu tu mwenye kutuhesabia haki na mastahii yetu, ndiye atakaye tenda haki hiyo. Hakuna sababu ya kuwabeba watu vichwani mwao na mioyoni kwao kwa vile tu hawakutendewa haki kwa kukaribishwa kwa heshima. Jambo la muhimu ni kulenga kwenye lengo msingi lilio mbele yao. Muda kamwe hautawasubiri.

Matokeo ya mafundisho haya ya Yesu kwa     Mitume wake, Thenashara, Wakatoa pepo wengi, wakapaka mafuta watu wengi waliokuwa wagonjwa, wakawapoza,” Mk 6:13. Na huu ndio mpango kazi wa Yesu, Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19. Mpango kazi huu, Mitume wake na wapelekwa wake Yesu wanaanza kuutekeleza. Na kauli mbiu ya mpango kazi huu ni hii: “Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili,” Mk 1:15. Ndugu yangu kwa kifupi hiki ndicho mimi na wewe tupaswacho kukijua kuhusu siri ya wokovu wetu ambao kama tulivyo mwili na roho hatutaweza kulifikia lengo hili kama tusipoyafanya yote hayo mawili katika ukamilifu wake, na hatutaweza pia kulifikia lengo letu hili kama tutadhara moja ya hayo mawili, yaani mwili na roho. Huu ndio urithi tunaopaswa kuwarithisha watoto wetu leo. Maisha yetu ya umilele yanategemea sana maandalizi mazuri leo hapa duniani.

Tumsifu Yesu Kristo!

Mtu mwema huwaachia wana wa wanawe urithi; Na mali ya mkosaji huwa akiba kwa mwenye haki,” Mit 13:22
NA

Bwana anazijua siku za wakamilifu, Na urithi wao utakuwa wa milele.” Zab 37:18

No hay comentarios:

Publicar un comentario