JUMATATU
YA WIKI YA 3 YA KWARESMA
Somo:
2 Fal 5:1-15a
Zab:42:2,
3; 42:3, 4
Injili:
Lk 4:24-30
Nukuu:
“Ndipo akashuka,
akajichovya mara saba katika Yordani, sawasawa na neno lake yule mtu wa Mungu;
nayo nyama ya mwili wake ikarudi ikawa nyamba ya mwili wa mtoto mchanga, akawa
safi,” 2Fal 5:14
“Hakuna nabii mwenye
kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe,” Lk 4:24.
TAFAKARI:
Unyenyekevu
ni msingi wa Fadhila zote; Tujinyenyekeshe na Mungu atatenda.
Wapendwa wana wa Mungu,
leo kwa pamoja tutafakari, “unyenyekevu ni msingi wa Fadhila zote;
tujinyenyekeshe na Mungu atatenda.” Masomo yote mawili leo yanatuwasa
kutafakari sana tendo hili la unyenyekevu na kujinyenyekesha. Bila shaka wote
twafahamu vizuri habari za Jemadari Naamani, na uponyaji wake kupitia Nabii Elisha.
Safari ya uponyaji wake haikuwa rahisi, kutokana na njia, na namna ya uponyaji
ule ulivyokuwa uwe kwa namna Mungu alivyopenda.
Mara nyingi hatuyapati
yale tuombayo, na hata uponyaji wa yale yatusumbuayo kutokana na mitazamo yetu
kimaisha, na namna tutakavyo Mungu kufanya huruma na upendo wake. Mtume Yakobo
anasema hivi, “hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili
mvitumie kwa tamaa zenu,” Yak 4:3. Tunapokuwa mbele ya Mungu, ni jambo la
msingi kujishusha na kujinyekesha kwani sote ni wahitaji na waja wa Mungu.
Mungu utukweza tu pale tunapojinyenyekesha kwake na kuukubali ubinadamu wetu.
Mungu daima anabaki kuwa Mungu. “Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, na
ajidhiliye atakwezwa,” Lk 14:11. Mtoza ushuru katika sala lake hekaluni,
kinyume cha Mfarisayo, sala yake ilisikika mbele ya Mungu kwa sababu
alijishusha na kusema kwa unyenyekevu na kwa uchache wa maneno kabisa, “Ee
Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi,” Lk 18:13. Kwa tendo hili la
unyenyekevu la mtoza ushuru, Yesu
anasema, “Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki
kuliko yule; (Mfarisayo) kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye
atakwezwa,” Lk 18:14
Jemadari Naamani
anapata uponyaji wa ukoma wake baada tu ya kujishusha na kufanya kadiri ya
mapenzi ya Mungu. Ndugu yangu, Mungu ana njia mbalimbali za kufikishia ujumbe
wake kwetu kadiri ya hitaji letu, na kwa kupitia jambo hilo la uponya huo liwe
somo la maisha. Naamani anashindwa kupokea njia ya uponyaji ule, yaani,
kujichovya mara saba katika mto Jordani, kwa kujitazama historia yake, na
ufahamu wake. Mpendwa, “Bwana wetu ni mkuu na mwingi wa nguvu, Akili zake
hazina mipaka,” Zab 147:5. Hatuwezi kumpangia Mungu namna ya kufanya hata kama
tukiwa na nia njema afanye yale tumwombayo na tunayotamani. Hata Yesu mwenyewe,
alimwachia Baba yake-Mungu atende kadiri ya mapenzi yake. “Akaenda mbele
kidogo, akaanguka kifulifuli, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwezekana,
kikombe hiki kiniepuke; walakini si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo
wewe,” Mt 26:39.
Naamani Jemadari,
anapojinyenyekeza na kumwachia Mungu atende kadiri ya neno lake kupitia mtu wa
Mungu Nabii Elisha, Mungu anatenda mara moja. “Ndipo akashuka, akajichovya mara
saba katika Yordani, sawasawa na neno lake yule mtu wa Mungu; nayo nyama ya mwili
wake ikarudi ikawa nyama ya mwili wa mtoto mchanga, akawa safi,” 2Fal 5:14.
Kujinyenyekesha ni kukiri makuu ya Mungu kabla na baada anapotenda mema yake
kwako. Uponyaji wa Naamani Jemadari unaibua hisia za uchaji na utambuzi wa
Mungu huyu wa Ajabu, na kusema, "Sasa tazama, najua ya kwamba hakuna Mungu
duniani mwote, ila katika Israeli,” 2Fal 5:15.
Ndugu yangu,
tunachojifunza katika maisha yetu ya sala na unyenyekevu ni kwamba tunapokuwa
mbele ya Mungu yatupasa kujua kwamba sisi ni viumbe tu, na wahitaji na waja
wake Mungu. Mungu haitaji kujua mazuri yetu kwa sababu hayatampunguzia wema,
upendo na uzuri wake. Mungu pia haitaji historia ya yale tuyafanyayo kama
alivyofanya Mfarisayo, bali tusiache kutenda mema kwani Yeye aliye mema yote na
uzuri wote ataonekana katika matendo hayo mema, hasa tunapoyatenda kwa wale
aliowaumba kwa sura na mfano wake.
Utendaji wetu uwe kama wa watoto wachanga. Watoto
wachanga ndiyo hufunuliwa mambo ya Mungu kutokana na kujiaminisha pasipo shaka
kwa wazazi wao. Katika hili Yesu anasema, “Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu
na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia
watoto wachanga,” Mt 11:25. Utendaji huu kama watoto ndio unaoturithisha ufalme
wa Mungu. “Waacheni watoto wadogo waje
kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni
wao,” Mt 19:14.
Mwisho wa siku ndugu yangu, tutahukumiwa kwa upendo
wetu. Kwa
hiyo kwa yale yote tufanyayo na tujihesabie tu kuwa tumefanya yale yampendezayo
Mungu. Ndugu yangu, Bwana wetu Yesu Krito anasema, “vivyo hivyo nanyi,
mtakapokwisha kuyafanya yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na
faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya,” Lk 17:10. Hatuna chochote za
kujivunia mbele ya Mungu zaidi ya kujinyeyekesha. Mafanikio yetu ni moja ya uzuri
wake Mungu. Mapungufu yetu ni sababu ya ubinadamu wetu. Mtume Paulo anasema,
“Lakini mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana
wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa
ulimwengu,” Gal 6:14.
Katika jambo hili ndugu
yangu, yatupasa kujua kwa uhakika kwamba Yesu Kristo ni kielelezo cha
UNYENYEKEVU. Kifo cha msalaba na cha aibu ni kwa sababu yangu na wewe. Basi,
tujivunie tu Msalaba kwani kwayo kuna utukufu. Vingine vyote ni vya kupita tu.
Mtume Paulo anatuambia makusudi ya Yesu kufanya hayo yote ni kwamba, “ambaye
yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu
ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna
ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu, tena, alipoonekana ana umbo kama
mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba,” Flp
2:6-8. Je, ndugu yangu, una cho chote cha kujivunia na kutojinyenyekesha kwa
Mungu?
Injili yetu ya leo
tunaona jinsi Yesu anavyohukumiwa kwa kujinyenyekeza. Mara nyingi tunawahukumu
watu ndivyo sivyo kutokana na kujua historia zao, maeneo ya kijeografia
walikotoka, historia za wazazi wao, mazingira ya makuzi yao, marafiki walioishi
nao, na hata mtazamo wao kimaisha. Hili ni kosa kubwa sana kufanya. Hakuna
aliyeko hapa duniani kwa bahati mbaya, au kuzaliwa kwa bahati mbaya. Sisi tu
malengo na makusudi ya Mungu. Mungu anampango na kila mmoja wetu.
Baada ya Yesu kuwaambia
ukweli Waandishi na Mafarisayo kwa kutokuamini kwao, hawapokei ujumbe ule wa
ukweli na kubadilika, bali wanatafuta njia ya kumwangamiza. Katika hili Yesu
anatujaza ujari kwa kusema, “Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake
mwenyewe,” Lk 4:24. Maana yake nini? Ukweli ni kwamba, tunaposimama katika
kweli, na kuishi kweli hiyo, ni vita twatangaza kwa wale wasioipenda kweli
hiyo. Kwa upande wa Imani ni vita, si tu ya nafsi, bali roho pia. Roho ambazo
hazimwelekei muumba wake zitakuwa kinyume na yote tusemayo na kuyaishi. Kuishi
Ukristo na kumkiri Kristo leo ni vita kubwa ya kiroho. Tulizoea kusikia hadithi
za Mashahidi wa Imani karne na nyakati za nyuma, lakini leo ni nafasi na wakati
wetu kuwa mashahidi wa Kristo. Kuna kila dalili na sababu za kuutoa ushuhuda
huo.
Tunachopaswa kuishi si
maisha ya ushindani wa hoja katika majukwaa, bali zaidi ni kuishi na kutoa
ushuhuda wa ukimya wa maisha ya kweli ya ukristo wetu. Jambo hili ni muhimu
sana, kwani katika utulivu Mungu yupo na kuonekana. “Na baada ya tetemeko la
nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto
sauti ndogo, ya utulivu,” 1Fal 19:12. Huu ni wakati wa mitetemo ya Imani. Nasi
tusienende kadiri ya mitetemo hiyo. Tuitafsiri hiyo mitetemo nako tutakutana na
Mungu katika utulivu.
Ndugu yangu, Mungu wetu
hutenda makuu katika unyenyekevu wetu. Kujinyenyekeza kwetu huku na kwa tendo
hilo, kuna faida kubwa. Faida hii siyo kuponywa tu kwa yale yanayotusumbua,
bali pia kuwa karibu naye na kujenga mahusiano mazuri na Mungu. Tujinyenyekeshe
daima!
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kumcha
Bwana ni maonyo ya hekima; Na kabla ya heshima hutangulia unyenyekevu,” Mit
15:33
Ee Yesu tujalie fadhila ya
unyenyekevu.
No hay comentarios:
Publicar un comentario