JUMAPILI
YA 1 YA KWARESMA YA MWAKA-C
Somo
I: Kumb 26:4-10
Zab:
91:1-2, 10-15
Somo
II. Rum 10:8-13
Injili:
Lk 4:1-13
Nukuu:
“Wamisri
wakatuonea, wakatutesa, wakatutumikisha utumwa mzito,” Kumb 26:6
“Tukamlilia
Bwana, Mungu wa baba zetu; Bwana akasikia sauti yetu, akaona na taabu yetu, na
kazi yetu, na kuonewa kwetu,” Kumb 26:7
“Bwana
akatutoa kutoka Misri kwa mkono wa nguvu, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa
utisho mwingi, na kwa ishara, na kwa maajabu; naye
ametuingiza mahali hapa, na kutupa nchi hii, nchi ijaayo maziwa na asali,” Kumb 26:8-9
“Na
sasa, tazama, nimeleta malimbuko ya mazao ya ardhi uliyonipa, Ee Bwana. Kisha
ukiweke chini mbele za Bwana, Mungu wako, ukasujudu mbele za Bwana, Mungu
wako,” Kumb 26:10
“Kwa
sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni
mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka,” Rum 10:9
“Kwa
maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata
wokovu,” Rum 10:10
“Kwa
maana andiko lanena, Kila amwaminiye hatatahayarika,” Rum 10:11
“Kwa maana hakuna tofauti ya Myahudi na Myunani; maana yeye yule ni Bwana wa wote, mwenye utajiri kwa wote wamwitao; kwa kuwa, Kila atakayeliitia Jina la Bwana ataokoka,” Rum 10:12-13
“Ibilisi
akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, liambie jiwe hili liwe mkate,” Lk 4:3
“Yesu
akamjibu, Imeandikwa ya kwamba mtu hataishi kwa mkate tu,” Lk 4:4
“Ibilisi
akamwambia, Nitakupa wewe enzi hii yote, na fahari yake, kwa kuwa imo mikononi
mwangu, nami humpa ye yote kama nipendavyo,” Lk 4:6
“Basi,
wewe ukisujudu mbele yangu yote yatakuwa yako,” Lk 4:7
“Yesu
akajibu akamwambia, Imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke
yake,” Lk 4:8
“Akamwongoza
mpaka Yerusalemu, akamweka juu ya kinara cha hekalu, akamwambia, Ukiwa ndiwe
Mwana wa Mungu, jitupe chini; kwa
maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake wakulinde; na ya kwamba,mikononi mwao
watakuchukua, Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe,” Lk 4:9-11
“Yesu
akajibu akamwambia, Imenenwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako,” Lk 4:12
“Basi
alipomaliza kila jaribu, Ibilisi akamwacha akaenda zake kwa muda,” Lk 4:13
TAFAKARI:
“Ibilisi akamwacha akaenda zake kwa muda.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya kwanza ya Kwaresma mwaka “C.” Masomo
yetu yote matatu yanatualika tusimame katika Imani ya kweli, na hasa katika
matendo. Pili, yatupasa kuwa imara hata baada ya kuyashinda majaribu katika vita
hivi vya Imani, kwa sababu yule mwovu shetani kushindwa kwake siyo mwisho wake
wa kutujaribu. Basi Yesu “alipomaliza kila
jaribu, Ibilisi akamwacha akaenda zake kwa muda,” Lk 4:13.
Ni kwa namna hiyo kwamba Imani kwa
Waisraeli haikuwa ni kitu cha kufikirika au kuwazika kwa mbali, bali matendo
halisi. Pale walipogundua yote yamefanyika kwa mkono wa Mungu hawakuacha
kuonyesha kwa matendo Imani yao. “Tukamlilia
Bwana, Mungu wa baba zetu; Bwana akasikia sauti yetu, akaona na taabu yetu, na
kazi yetu, na kuonewa kwetu,” Kumb 26:7. Kilio cha wana wa Israeli ni juu ya
mateso waliyoyapata huko Misri. “Wamisri
wakatuonea, wakatutesa, wakatutumikisha utumwa mzito,” Kumb 26:6. Kwa tendo
hili na mkono huu wa Mungu kuwaondoa katika mateso yao, na hasa kuwapatia ardhi
kwao hakikuwa kitu cha kawaidasi kitu hata kidogo. Ni zaidi ya miaka mia nne
walikuwa utumwani. “Bwana akatutoa kutoka
Misri kwa mkono wa nguvu, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa utisho mwingi, na
kwa ishara, na kwa maajabu; naye
ametuingiza mahali hapa, na kutupa nchi hii, nchi ijaayo maziwa na asali,” Kumb 26:8-9.
Maisha ya Kiyahudi yalionekana kutiliwa mkazo kwenye mambo
makuu matatu; moja, umuhimu wa Hekalu Takatifu kama sehemu pekee ya kuabudu na
kumtokea Mungu shukrani zao na sadaka za kuteketezwa. Pili, Maandiko
Matakatifu, yaani Torati. Na mwisho milki ikiwa ni ardhi pamoja na uongozi
madhubuti uliowekwa na Mungu mwenyewe. Hivyo kile walichokipata kutoka ardhi
walikitoa kwa Mungu wakitambua ni kwa namna gani alivyowatendea. “Na sasa, tazama,
nimeleta malimbuko ya mazao ya ardhi uliyonipa, Ee Bwana. Kisha ukiweke chini
mbele za Bwana, Mungu wako, ukasujudu mbele za Bwana, Mungu wako,” Kumb 26:10.
Imani na matendo halisi vilikwenda pamoja. “Umheshimu Bwana kwa jicho la
ukarimu, wala usimtolee malimbuko ya kazi za mikono yako kwa ubahili. Kwa kila
kitolewacho uonyeshe ukunjufu wa uso, hata sehemu ya kumi uiweke wakfu kwa
changamko. Mpe Mungu kama alivyokupa wewe, na kama mkono wako ulivyopata, utoe
kwa ukarimu,” Ybs 35: 7-9. Jambo hili litakupa wajibu wako mbele ya Mungu. Na
utawajibika kumrudishia Mungu kilicho chake. Mara nyingi tunamrudishia Mungu
mabaki ya kazi za mikono yetu. Elewa vitu vyote ni mali yake MUNGU.
Wapendwa wana wa Mungu,
Biblia Takatifu siyo kitabu cha katekesi wala tafiti ya kiteolojia, bali ni
historia ya wokovu yenye kuonyesha mwingiliano wa matendo ya wokovu ya Mungu
kwa watu wake. Uhusiano wa Mungu na watu wake haukuwa wa kufikirika, bali wa
kuchangamana na matendo makuu ya Mungu. Uhusiano huu wa Imani na Muumba wetu
unaoendana na matendo yetu, Mtume Paulo anauzungumzia katika ukiri wa Neno la
Mungu, na Bwana, yaani Yesu Kristo. “Kwa
sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni
mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka,” Rum 10:9. Kulikiri jina Yesu
ni kutambua mambo makuu manne katika ibada yenye kumpendeza Mungu, yaani
kuabudu kuliko sahihi, halisi, kutafakari, na matendo. Kama haya mambo manne
hayapo na hayafanyiki katika kuabudu kwetu, basi huo sio ukiri bali ni ibada ya
‘kupayukapayuka.’ Na katika kulifanya jambo hili la ukiri lililo sahihi,
halisi, la tafakari, na matendo, “hakuna tofauti ya Myahudi na Myunani; maana
yeye yule ni Bwana wa wote, mwenye utajiri kwa wote wamwitao; kwa kuwa, Kila atakayeliitia Jina la
Bwana ataokoka,” Rum 10:12-13. Kuliita jina hili la Bwana siyo kwa kupayuka,
wala kusukumwa kwa hisia zetu.
Hakika Yesu angezifuata
hisia zake, hasingeweza kuyashinda majaribu kule jangwani. Yesu hakuziruhusu
hisia zake zimtawale kwa sababu alimruhusu Roho wa Mungu ayatawale maisha yake.
Na Yesu, hali amejaa Roho Mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho
muda wa siku arobaini nyikani, akijaribiwa
na Ibilisi. Ni Roho huyu aliyeyasukuma yote aliyoyafanya na hasa pale
alipotangaza rasmi mapambano ya kweli na haki katika lile lililo ovu na
kumkomboa mwanadamu. “Roho wa Bwana yu juu
yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma
kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha
huru waliosetwa,” Lk 4:18. Na ni Roho huyu huyu
aliyemwezesha kuyaona yote kwa mwelekeo wa Mungu Baba. “Saa ile ile alishangilia kwa Roho Mtakatifu,
akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya
umewaficha wenye hekima na akili; umewafunulia watoto wachanga; Naam, Baba, kwa
kuwa ndivyo ilivyokupendeza,” Lk 10:2.
Huyu
ndiye Roho aliyemwezesha kuyashinda yale majaribu jangwa juu ya Sifa, Mamlaka,
Utajiri, na Umaarufu, [Lk 4:4, 6, 8, 9-11]. Baada ya ushindi huu wa Yesu,
Ibilisi alimwacha kwa muda. “Basi
alipomaliza kila jaribu, Ibilisi akamwacha akaenda zake kwa muda,” Lk 4:13.
Unaposhinda majaribu katika maisha yako usije ukajisahu na kubweteka kana
kwamba vita hiyo ishafikia ukomo. Yakupasa kuwa macho muda wote kama asemavyo
Mtume Petro, “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi,
kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze,” 1Pet 5:8.
Kila
mmoja wetu anajangwa lake ambalo ukitaka uzima wa milele utaupata na ukitaka ya
hapa duniani utayapata pia. Ila ni vigumu sana kuyapata ya milele kama utabobea
kwa haya ya leo na kesho, yaani ya hapa duniani. Ukiyachuchumilia ya umilele,
kuna uhakika wa kuyapata yote ya duniani kwa amani na furaha. Basi “utafuteni ufalme wa Mungu, na hayo mtaongezewa,” Lk 12:31.
Maisha yangu kama Mtawa na Padre ni yanipasa kuyaisha kwa uaminifu huku
nikiyashinda majaribu yangu ya kila siku kwa nguvu ya sala na uwezo wa Roho
Mtakatifu. Nawe ule mlei na kadiri ya wito wako, ni vyema ukajua yakupasayo
kuishi na hasa uaminifu kwa kile ulichoitiwa. Kipindi hiki cha kwaresma
tunapata nafasi ya kuzama ndani ya nyoyo zetu kwa lengo la kujitakasa na
kumrudia Mungu katika kumwabudu kuliko sahihi, halisi, tafakari, na kwa matendo
hai. Ibilisi utuacha tu kwa muda ila hajaghairi nia yake ya kutudondosha. Basi tukeshe
tukiomba na kushikamana na Kristo aliyeyashinda majaribu yake jangwani.
Daudi
Kibobo alidumu zaidi ya miaka mitatu akimwomba Mungu ampatie kwa namna yoyote
ile mtaji wa kufanya biashara, kutokana na vibarua vigumu alivyokuwa anafanya
kila siku. Siku mmoja mvua zilinyesha siku nzima. Hivyo hapakuwa na kibarua cha
kufanya. Ilipofika jioni ya saa kumi na moja hivi huku kukiwa bado na manyunyu
ya mvua, aliwaza aende shambani angalau alime matuta matatu ya viazi vitamu.
Akiwa
njiani kuelekea shambani mwake, alikuta gari dogo limekwama barabarani. Alifaka
pale na kumkuta Bwana mmoja akiwa hajui cha kufanya. Kwa kujua tatizo lile,
Daudi Kibobo alilivamia pori na kukata fito za kutosha. Alizitandaza kwa ujuzi
kwenye lile tope na kumwamuru mwenye gari awashe gari na kuondoka. Kweli gari
ile ndogo ilitoka kwenye tope. Yule Bwana alimwita Kibobo na kumwambia, ndugu
asante sana kwa msaada wako. Ningependa kukufahamu zaidi. Kibobo akamwambia
jina lake na yule Bwana akajitambulisha kama Yonathani Nyare. Nyare alimtaka
Kibobo akutane naye kesho ofisini kwake. Mapema asubuhi Kibobo aliwasili na kwa
bahati nzuri alikutana na Bwana Nyare. “Hii ndiyo asante yangu,” Nyare
alimkabidhi bahasha na ndani yake kulikuwa na milioni moja. Kabla Kibobo
hajasema neno, Nyare alimwambia, “Bwana Daudi Kibobo, jana ungekuwa mtu mbaya
ungeweza kuwa tajiri mkubwa leo. Kwenye gari yangu nilikuwa na milioni mia
tatu. Nasema tena, asante sana.” Kibobo hakuamini macho yake. Alitoa shukrani
zake na aliondoka.
Njiani
Kibobo alipanga mipango yake vizuri kuhusu biashara atakayoifanya na kufikia
muhafaka wa kufanya biashara ya kuuza mazao na hasa mahindi. Vile vile aliweka
ahadi kwa Mungu kwamba kila atakapouza mazao yake, atamtolea Mungu asilimia
kumi ya faida ile.
Kibobo
alianza kazi ile mara moja. Mauzo ya kwanza alipata faida milioni moja, na kwa
asilimia kumi alitoa laki moja kama shukrani kwa Mungu. Mzigo wa pili alipata
faida laki tisa, na kwa asilimia kumi alimtolea Mungu shukrani ya elfu tisini.
Alifanya zoezi hili kwa mwaka mzima na mambo yalikuwa vizuri sana. Akiwa mwaka
wa pili wa biashara yake, mara moja alipata faida ya milioni 100, na kwa
asilimia kumi ilimpasa amtolee Mungu milioni kumi. Akiwa analiwaza hilo ofisini
mwake, akaja Bwana mmoja akiwa na lengo la kuuza gari yake ya mzigo aina
ya Fuso Mpya kwa milioni 10, kwani
alikuwa tatizo kubwa sana katika familia
yake.
Basi, kwa
uzuri wa gari lile la mizigo na hitaji alilokuwa nalo Kibobo alilinunua kwa
fedha ile ambayo alishaitenga kwa kutoa shukrani kwa Mungu akiahidi kwamba
mwezi ujao atamtolea Mungu milioni kumi na tano. Akiwa amejiridhisha na dhamiri
yake, Kibobo aliondoka na dereva wake kufuata mzigo wa mahindi. Akiwa njiani
wakati wa kurudi na akiwa na mzigo wa mahindi, gari ile ilipinduka na
kuharibika kabisa, naye akavunjika mguu. Pesa aliyokuwa ameweka kwenye mfuko,
kwa ajili ya kununulia mchele yote ilipotea. Ni jana tu alitoka Benki kutoa
pesa yote na kubakiza milioni moja.
Kibobo
alibaki na milioni yake moja aliyoanza nayo miaka mitano iliyopita. Leo milioni
hiyo haitoshi hata kwa kumgharamia matibabu yake. Ndugu yangu, tuwe waaminifu
kwa ahadi zetu tutoazo kwa Mungu, na tubaki kwenye imani ya kweli hata pale
tunapopata majaribu.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Basi
alipomaliza kila jaribu, Ibilisi akamwacha akaenda zake kwa muda,” Lk 4:13
No hay comentarios:
Publicar un comentario