martes, 2 de febrero de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 4 YA MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 4 YA MWAKA-C

Somo: 2Sam 24:2, 9-17
Zab: 32:1-2, 5-7
Injili: Mk 6:1-6
Nukuu:
“Naye Daudi akamwambia Bwana, Nimekosa sana kwa haya niliyoyafanya; lakini sasa, Ee Bwana, nakusihi uuondolee mbali uovu wa mtumishi wako; kwani nimefanya upumbavu kabisa,” 2 Sam 10b

Na Daudi alipoondoka asubuhi, neno la Bwana likamjia nabii Gadi, mwonaji wake Daudi, kusema, Nenda, ukanene na Daudi, Bwana asema hivi, Nakuwekea mambo matatu; katika haya uchague moja, nikutendee hilo,” 2Sam 24:11-12

Basi Gadi akamwendea Daudi, akamweleza, akamwambia, Basi, miaka saba ya njaa ikujie katika nchi yako? Au miezi mitatu ukimbie mbele ya adui zako, huku wakikufuatia? Au siku tatu iwe tauni katika nchi yako? Fanya shauri sasa, ufikiri, ni jawabu gani nimrudishie yeye aliyenituma,” 2 Sam 24:13

Naye Daudi akamwambia Gadi, Nimeingia katika mashaka sana; basi sasa na tuanguke katika mkono wa Bwana; kwa kuwa rehema zake ni nyingi; wala nisianguke katika mkono wa wanadamu,” 2Sam 24:14

Basi Bwana akawaletea Israeli tauni tangu asubuhi hata wakati ulioamriwa; nao wakafa watu toka Dani mpaka Beer-sheba sabini elfu.” 2Sam 24:15

Huyu si yule seremala, mwana wa Mariamu, na ndugu yao Yakobo, na Yose, na Yuda, na Simoni? Na maumbu yake hawapo hapa petu? Wakajikwaa kwake,” Mk 6:3 

Yesu akawaambia, Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani mwake,” Mk 6:4

TAFAKARI: “Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani mwake.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Yesu anatukumbusha wajibu muhimu sana, yaani, tuviheshimu na kuvienzi vilivyo vyetu. Pamoja na hayo yote, hukumu yetu iwe ya kweli na haki. Waswahili wanasema, “masikini mnyongeni, ila haki yake mpeni.” Ni wazi watu wa nyumbani mwake waliyastaajabia yale aliyoyatenda Yesu lakini hawakuutafakari Umungu wake, bali waliutazama zaidi ubinadamu wake tena katika mwono wa historia yake. Nao wanashangaa na kusema, Huyu si yule seremala, mwana wa Mariamu, na ndugu yao Yakobo, na Yose, na Yuda, na Simoni? Na maumbu yake hawapo hapa petu? Wakajikwaa kwake,” Mk 6:3. Hivyo leo ni wito kwetu kwamba tusimdharau mtu kwa vile tunaifahamu historia yake na asili yake, bali tumtazama katika upya wake.

Ni jambo la kushangaza leo kuona katika jamii yetu Tanzania baadhi yetu kuwaweka watu fulani, au makabila fulani, na hata ukanda fulani wa nchi walipotoka kama watu wasio na maana na kutokuwa na jema lolote. Bila shaka ubaguzi huu unakusudi lake kimkakati. Hata hivyo mikakati yote miovu ni chukizo kwa Mungu. Kuhusu hatari hii, Yesu anasema, “Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani mwake,” Mk 6:4. Kutokuheshimka na kupokeleka kwetu hakutoki nje ya jamii tunayoishi. Mchawi ni sisi wenyewe. Dhambi hii ya kubaguana kunakotokana na familia zetu, koo zetu, makabila yetu, na elimu zetu ni mbaya na yakuogopwa sana. Machafuko mengi ya kijamii na hata kufikia hatua ya mauaji ya kimbari huanza na chokochoko hizi. Hakuna binadamu aliye na thamani zaidi ya binadamu mwingine. Wewe ni nani na una ubora gani zaidi hata umdharau mwenzako kutokana na familia yake, ukoo wake, au kabila lake? Tuelewe kwamba mengine yote hapa duniani ni MBWEMBWE TU!

Tukubali wakati mwingine tunafanya vibaya sana hata kama jambo hilo linatumika kama utani. Utani upo kwa watani, na siyo kwa kila anayejisikia kufanya hivyo. Tuwahesimu watu na utu wao. Tofauti zao ndio uzuri wa Mungu. Hatukuumbwa ili wote tufanane kwa kila kitu. Ikiwa hivyo basi sisi si watu tena bali mitambo-“robots.” Tujifunze unyenyekevu pale tulipokosea kama alivyofanya Daudi kwa kosa la kuwahesabu watu na kutaka kujua idadi yao kinyume na atakavyo Mungu. “Naye Daudi akamwambia Bwana, Nimekosa sana kwa haya niliyoyafanya; lakini sasa, Ee Bwana, nakusihi uuondolee mbali uovu wa mtumishi wako; kwani nimefanya upumbavu kabisa,” 2 Sam 10b. Ni Daudi huyu huyu anaye omba kwa unyeyekevu na kujuta dhambi zake anapogundua ndivyo sivyo uhusiano wake na Mungu. Ee Mungu, uniumbie moyo safi, Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu Usinitenge na uso wako, Wala Roho yako Mtakatifu usiniondolee,” Zab 51:10-11. Tumuombe huyu Roho Mtakatifu akaye nasi ili tuweze kuyaona matakatifu kwa wale wote tunaoishi nao na  wanaotuzunguka.

Yote yasiyoongozwa na Roho wa Bwana yanamadhara sana katika maisha yetu. Mungu hatosita kutufundisha kwa njia nyingine ili tumrudie. Kwa kosa alilofanya Daudi anapewa mapendekezo matatu kuizuia hasira ya Mungu.Basi Gadi akamwendea Daudi, akamweleza, akamwambia, Basi, miaka saba ya njaa ikujie katika nchi yako? Au miezi mitatu ukimbie mbele ya adui zako, huku wakikufuatia? Au siku tatu iwe tauni katika nchi yako? Fanya shauri sasa, ufikiri, ni jawabu gani nimrudishie yeye aliyenituma,” 2 Sam 24:13. Hapa pia tunaona unyenyekevu wa Daudi anapoipokea adhabu hii. Daudi anapokea adhabu kwa moyo wa kushukuru. Naye Daudi akamwambia Gadi, Nimeingia katika mashaka sana; basi sasa na tuanguke katika mkono wa Bwana; kwa kuwa rehema zake ni nyingi; wala nisianguke katika mkono wa wanadamu,” 2Sam 24:14. Mungu hubaki kuwa Rehema, na Mungu wa Rehema kwetu. Pamoja na Bwana kuwaletea tauni na kufa watu elfu sabini, “Lakini huyo malaika aliponyosha mkono wake kuelekea Yerusalemu ili auharibu, Bwana akaghairi katika mabaya, akamwambia huyo malaika mwenye kuwaharibu watu, Yatosha, sasa ulegeze mkono wako,” 2Sam 24:16a. Mungu wetu hughairi adhabu yake tunapojinyenyekesha kwake kwa kufanya toba ya kweli na majuto ya dhambi.

Tumsifu Yesu Kristo


Mtu kujitenga na ugomvi ni heshima kwake; Bali kila mpumbavu ataka kugombana,” Mit 20:3

No hay comentarios:

Publicar un comentario