JUMAPILI
YA 3 YA KWARESMA YA MWAKA-C
Somo
I: Kut 3:1-8, 13-15
Zab:
103:1-4, 3-4, 6-7, 8, 11
Somo
II: 1Kor 10:1-6, 10-12
Injili:
Lk 13:1-9
Nukuu:
“Malaika
wa Bwana akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti;
akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea,”
Kut 3:2
“Naye
akasema, Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo
unaposimama ni nchi takatifu,” Kut 3:5
“Tena
akasema, Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na
Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu,”
Kut 3:6
“Bwana
akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia
kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao,” Kut 3:7
“Mungu
akamwambia Musa, MIMI NIKO AMBAYE NIKO; akasema, Ndivyo utakavyowaambia wana wa
Israeli; MIMI NIKO amenituma kwenu,” Kut 3:14
“wote
wakanywa kinywaji kile kile cha roho; kwa maana waliunywea mwamba wa roho
uliowafuata; na mwamba ule ulikuwa ni Kristo,” 1Kor 10:4
“Lakini
wengi sana katika wao, Mungu hakupendezwa nao; maana waliangamizwa jangwani,”
1Kor 10:5
“Basi
mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya,
kama wale nao walivyotamani,” 1Kor 10:6
“Kwa
hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke,” 1Kor 10:12
“Na
wakati uo huo walikuwapo watu waliompasha habari ya Wagalilaya wale ambao
Pilato alichanganya damu yao na dhabihu zao,” Lk 13:1
“Akawajibu
akawaambia, Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko
Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo?” Lk 13:2
“Au
wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya
kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu?” Lk 13:4
“Nawaambia,
Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo,” Lk 13:5
“Akajibu
akamwambia, Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda baadaye, vema! La,
usipozaa, ndipo uukate,” Lk 13:8-9
TAFAKARI:
“Vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi
takatifu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya tatu ya Kwaresma ya Mwaka ‘C’ wa
Kanisa. Leo kwa namna ya pekee tutafakari kwa undani maneno haya ya Mungu, “vua
viatu vyako miguuni mwake; maana mahali hapo unaposimama ni Nchi
Takatifu.”
Kwanza kabisa, maneno
haya ya Mungu ni wito maalum anaopewa Musa kwa kazi maalumu, yaani kuwatoa wana
wa Israeli utumwani Misri. Ni kieleleza cha namna ya kuwajibika na kuheshimu
wajibu huo kama tendo Takatifu. Hivyo uwepo wa Mungu unajidhihirisha kwa
kijinga cha moto chenye kuwaka bila kuteketea. “Malaika
wa Bwana akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti;
akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea,” Kut
3:2
Katika historia ya
wokovu wa mwanadamu, na kwa mapenzi yake Mungu mwenyewe, aliliteua Taifa la
wana wa Israeli kuwa kielelezo cha kusudi lake, uwepo wake, na ushirika wake.
Safari hiyo haikuwa rahisi kwani pamoja na maridhiano kati ya Mungu na Taifa
hili kwa njia ya maagano mbalimbali, wakati mwingine kulikuwa na hali ya uasi
kwa upande wa mwanadamu na kupelekea kwenda kinyume cha mpango mzima wa Mungu
kuelekea ukombozi wa kweli. Hata hivyo Mungu alibaki kuwa mwaminifu nyakati
zote, na hakuacha kuwa Huruma, Upendo, na Msamaha wa watu wake. “Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata
asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi
sitakusahau wewe. Tazama,
nimekuchora katika vitanga vya mikono yangu; kuta zako ziko mbele zangu daima,”
Isa 49:15-16. Haki, Huruma, Upendo, na Msamaha ndiyo
asili ya Mungu na ndiye Mungu ambaye kwavyo, yaani asili yake haina kipimo. Ni
kwa huruma yake Mungu anaona mateso ya watu wake huko Misri. “Bwana
akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia
kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao,” Kut 3:7.
Wewe na mimi tuliopewa dhamana ya uongozi na Mungu kwa kupitia watu wake,
yatupasa kuutazama wajibu huo wa pekee tukitumika kwa Sifa na utukufu wa Mungu
kwa ajili hiyo tu.
Pili, maneno haya
mazito ya Mungu yanatuingiza katika badiliko la ndani yenye kumpa mtu mtazamo
mpya kwa kile atarajiacho kukifanya. Mtazamo huu mpya wa kutenda si ule tena wa
mazoea, bali enenda yako iwe katika mtazamo wa Mungu, yaani mtazamo wenye kusukumwa
na HOFU ya Mungu mwenyewe. Mtu asiye na hofu ya Mungu, na hasa aliye na
madaraka ni hatari sana katika matendo yake. Hivyo katika maana hii kama
kiongozi aliye kwa ajili ya watu na Mungu, kuvivua viatu ni kuyashinda matendo
ya mwili na kushikamana na tunda la roho. Na “…tunda
la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo
hakuna sheria” Gal 5:22-23. Matendo ya mwili yasiyomtia mtu hofu ya Mungu
ni haya; “…uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui,
ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda,
ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama
nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo
hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21. Yeyote mwenye kupokea dhamana ya
uongozi na aliyetayari kutumika kwa ajili ya watu na kwa sababu ya Mungu ni
vyema akajipima vizuri katika tendo hilo la kujivua viatu vyake miguuni
mwake.
Mtazamo huu wa kujipima
unatuingiza katika tendo la kiroho na la mabadiliko, yaani, toba ya kweli. Haya
ndiyo ayasemayo Yesu katika Injili, yaani TOBA ya kweli na kwa kutokufanya
hivyo, basi yale tuyashangaayo kutokea kwa wengine basi nasi yapo mbioni. “Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote
mtaangamia vivyo hivyo,” Lk 13:5. Toba ya kweli ikulenge wewe binafsi katika
tenda yako. Usipoteze muda mwingi kuyatazama makosa au mabaya ya wengine au
yaliyowatokea kwa wengine na kujisahau kufanya mabadililiko hilo ndani mwako.
Hivyo Yesu anatoa angalizo kwa kusema, “Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao
walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? Au
wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya
kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu?” Lk 13:2, 4. Mimi na wewe yatupasa kuwa na
utayari wa kupokea huruma ya Mungu kama alivyofanya Mtoza Ushuru. Na tazama, “Lakini yule mtoza ushuru alisimama
mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga
kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi,” Lk 18:13.
Hali na utayari wa Mtoza Ushuru wa kufanya toba ya kweli na kuipokea huruma ya
Mungu ni kinyume kabisa na yule Mfarisayo aliyejihesabia haki. Naye (Mfarisayo)
alijiinua na kusali hivi, “Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine,
wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru,” Lk 18:11. Ndugu
yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, Mungu haitaji orodha ya wema na
uzuri wako. Mimi na wewe tunapaswa wema na hiyo ndiyo sifa ya wana wa Mungu. Na katika wema na uzuri huu
hatuongezi au kupunguza wema na uzuri wa Mungu. Ila kwa kutenda mema na kuwa
wema tunaudhihirisha Utukufu wa Mungu pale tulipo. Na hii ndiyo maana ya Maneno
haya ya Yesu, “Bali
maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa
yule mwovu. Basi ninyi mtakuwa
wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,”
Mt 5:37, 48. Hivyo yale yote uyafanyayo kwa ajili ya watu na Mungu, yalenge
katika utakatifu wako. Bila utakatifu kumwona Mungu ni ndoto isiyowezekana.
Tatu, maneno haya
mazito ya Mungu, “Vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama
ni Nchi Takatifu,” yanatukumbusha dhana na dhamana ya uongozi ambao kwa hakika
ni mpango wa Mungu kupitia watu wake, na kwa ajili Mungu. Uongozi ni DHAMANA.
Dhamana hii ya uongozi inatukumbusha Utakatifu wa kile uwajibikacho kama
Kiongozi na Utakatifu wa wale unaowahudumia au kuwaongoza. Viongozi wengi leo
wamesahau wajibu na kweli hii mara wapatapo madaraka. Viongozi hawa ni wale
wenye hujigeuza na kuwa miungu watu kwa yale wayasemayo na kuyaamuru kwa umma
uliowaweka madarakani. Mtume Paulo anatoa angalizo la viongozi wa mtindo huo na
kusema, “anayejidhania kuwa amesimama na
aangalie asianguke,” 1Kor 10:12. Kiongozi yeyote
aliye katika ngazi yoyote ile na taasisi yoyote ile, elewa kwamba pale ulipo
katika kutenda kwenye maana ya kutumika, ni sawa na kusimama katika Nchi
TAKATIFU kama alivyoambiwa Musa.
Historia ni mwalimu mzuri sana. Vitabu
Vitakatifu na hata historia ya mataifa mbalimbali katika ulimwengu huu,
vimeonyesha dhairi na pasipo shaka miisho ya viongozi wale ambao hawakuwa na
hofu ya Mungu, na kujijeuza wao kuwa miungu watu. Mungu anasema hivi juu ya
viongozi wenye kujifanya miungu watu, “nami
nitaikomesha fahari yao wenye kiburi; nami nitayaangusha chini majivuno yao
walio wakali,” Isa 13:11b. Mungu kamwe hapendezwa na viongozi wenye kiburi na
majivuno kwa sababu hawamwakilishi Mungu zaidi ya nafsi zao. Hivyo Mtume Paulo
anatoa angalizo, na kusema, “…wengi
sana katika wao, Mungu hakupendezwa nao; maana waliangamizwa jangwani,” 1Kor
10:5. Wapendwa wana wa Mungu, pona yako na yangu ni kusimama katika kweli na
haki, na ninapodondoka nifanya toba ya kweli kwa kuitazama neema na huruma
yangu kwangu ilivyo kubwa kuliko dhambi zangu.
Mpendwa wana wa Mungu,
tamani kila siku kutenda mema na lililo haki na kweli. “Basi
mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya,
kama wale nao walivyotamani,” 1Kor 10:6. Kila
siku Mungu anakupa nafasi ya kuwa mwema kwa sababu amekuchagua yeye ili uzae
matuma mema na yenye kudumu, Yoh 15:16. Yawezekana kwa makusudi kabisa
hujayazaa matunda hayo mema licha ya fursa nzuri uliyonayo. Kipindi hiki cha
Kwarema kiwe changamoto kubwa kujirudi na kumrudia Mungu. Na ushauri wa mwisho
ni huu: “Bwana, uuache (mtu huo,
mimi, wewe) mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda baadaye, vema! La,
usipozaa, ndipo uukate,” Lk 13:8-9. Amina.
Wapendwa katika Kristo, bila shaka sote
tunamfahamu Jogoo. Jogoo hufikiri bila kuwika mapema asubuhi hakuna
mapambazuko. Hivyo bila kuwika kwake siku haiwezi kuanza. Hii ndiyo falsafa ya
Jogoo.
Siku moja mapema asubuhi kukiwa bado na
mawingu mengi angani, Jogoo alitoka na kujilaza chali chini ya mti akiwa na
lengo la kuyazuia mawingu yasidongoke. Akiwa katika mkao huo huku miguu yake
akiielekeza juu na akiwa amezikunjua mbawa zake, katawi kidogo cha ule mti
kilikwanyuka na kushuka kwa kasi. Jogoo yule kuona vile aliruka huku akiwika
kwa hofu.
Baada ya dakika chache Jogoo yule
alijiuliza, “hili tawi limetoka ubali wa mita chache sana na limekuwa tishio
kubwa la uhai wangu. Je, nitaweza kweli kuyastahimili mawingu yale yaonekanayo
kuwa mbali? Kwa mtazamo huu, ni mimi kweli ninayeyaamza mapambazuko?”
Wapendwa wana wa Mungu Jogoo yupo kwenye
mchakato wa toba ya kweli. Je wewe na mimi tuliokirimiwa utashi na Mungu
tunasubiri nini?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nawaambia,
Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo,” Lk 13:5
Ee
Yesu, nikumbushe mara zote kuwa uongozi ni dhamana na kielelezo chake ni
kutumia kwa wote kwa hofu yako, nikitambua Utakatifu wa nafasi hiyo na Utakatifu
wa wale ninaowaongoza. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario