viernes, 26 de febrero de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 3 YA KWARESMA MWAKA-C

JUMAPILI YA 3 YA KWARESMA YA MWAKA-C
Somo I: Kut 3:1-8, 13-15
Zab: 103:1-4, 3-4, 6-7, 8, 11
Somo II: 1Kor 10:1-6, 10-12
Injili: Lk 13:1-9
Nukuu:
Malaika wa Bwana akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti; akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea,” Kut 3:2

Naye akasema, Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu,” Kut 3:5 

Tena akasema, Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu,” Kut 3:6

Bwana akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao,” Kut 3:7

Mungu akamwambia Musa, MIMI NIKO AMBAYE NIKO; akasema, Ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli; MIMI NIKO amenituma kwenu,” Kut 3:14

wote wakanywa kinywaji kile kile cha roho; kwa maana waliunywea mwamba wa roho uliowafuata; na mwamba ule ulikuwa ni Kristo,” 1Kor 10:4

Lakini wengi sana katika wao, Mungu hakupendezwa nao; maana waliangamizwa jangwani,” 1Kor 10:5

Basi mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya, kama wale nao walivyotamani,” 1Kor 10:6 

Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke,” 1Kor 10:12 

Na wakati uo huo walikuwapo watu waliompasha habari ya Wagalilaya wale ambao Pilato alichanganya damu yao na dhabihu zao,” Lk 13:1 

Akawajibu akawaambia, Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo?” Lk 13:2 

Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu?” Lk 13:4

Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo,” Lk 13:5

Akajibu akamwambia, Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda baadaye, vema! La, usipozaa, ndipo uukate,” Lk 13:8-9 

TAFAKARI: “Vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya tatu ya Kwaresma ya Mwaka ‘C’ wa Kanisa. Leo kwa namna ya pekee tutafakari kwa undani maneno haya ya Mungu, “vua viatu vyako miguuni mwake; maana mahali hapo unaposimama ni Nchi Takatifu.” 

Kwanza kabisa, maneno haya ya Mungu ni wito maalum anaopewa Musa kwa kazi maalumu, yaani kuwatoa wana wa Israeli utumwani Misri. Ni kieleleza cha namna ya kuwajibika na kuheshimu wajibu huo kama tendo Takatifu. Hivyo uwepo wa Mungu unajidhihirisha kwa kijinga cha moto chenye kuwaka bila kuteketea. Malaika wa Bwana akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti; akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea,” Kut 3:2

Katika historia ya wokovu wa mwanadamu, na kwa mapenzi yake Mungu mwenyewe, aliliteua Taifa la wana wa Israeli kuwa kielelezo cha kusudi lake, uwepo wake, na ushirika wake. Safari hiyo haikuwa rahisi kwani pamoja na maridhiano kati ya Mungu na Taifa hili kwa njia ya maagano mbalimbali, wakati mwingine kulikuwa na hali ya uasi kwa upande wa mwanadamu na kupelekea kwenda kinyume cha mpango mzima wa Mungu kuelekea ukombozi wa kweli. Hata hivyo Mungu alibaki kuwa mwaminifu nyakati zote, na hakuacha kuwa Huruma, Upendo, na Msamaha wa watu wake. Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe. Tazama, nimekuchora katika vitanga vya mikono yangu; kuta zako ziko mbele zangu daima,” Isa 49:15-16.  Haki, Huruma, Upendo, na Msamaha ndiyo asili ya Mungu na ndiye Mungu ambaye kwavyo, yaani asili yake haina kipimo. Ni kwa huruma yake Mungu anaona mateso ya watu wake huko Misri. Bwana akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao,” Kut 3:7. Wewe na mimi tuliopewa dhamana ya uongozi na Mungu kwa kupitia watu wake, yatupasa kuutazama wajibu huo wa pekee tukitumika kwa Sifa na utukufu wa Mungu kwa ajili hiyo tu.

Pili, maneno haya mazito ya Mungu yanatuingiza katika badiliko la ndani yenye kumpa mtu mtazamo mpya kwa kile atarajiacho kukifanya. Mtazamo huu mpya wa kutenda si ule tena wa mazoea, bali enenda yako iwe katika mtazamo wa Mungu, yaani mtazamo wenye kusukumwa na HOFU ya Mungu mwenyewe. Mtu asiye na hofu ya Mungu, na hasa aliye na madaraka ni hatari sana katika matendo yake. Hivyo katika maana hii kama kiongozi aliye kwa ajili ya watu na Mungu, kuvivua viatu ni kuyashinda matendo ya mwili na kushikamana na tunda la roho. Na  “…tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria” Gal 5:22-23. Matendo ya mwili yasiyomtia mtu hofu ya Mungu ni haya; “…uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21. Yeyote mwenye kupokea dhamana ya uongozi na aliyetayari kutumika kwa ajili ya watu na kwa sababu ya Mungu ni vyema akajipima vizuri katika tendo hilo la kujivua viatu vyake miguuni mwake. 

Mtazamo huu wa kujipima unatuingiza katika tendo la kiroho na la mabadiliko, yaani, toba ya kweli. Haya ndiyo ayasemayo Yesu katika Injili, yaani TOBA ya kweli na kwa kutokufanya hivyo, basi yale tuyashangaayo kutokea kwa wengine basi nasi yapo mbioni. Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo,” Lk 13:5. Toba ya kweli ikulenge wewe binafsi katika tenda yako. Usipoteze muda mwingi kuyatazama makosa au mabaya ya wengine au yaliyowatokea kwa wengine na kujisahau kufanya mabadililiko hilo ndani mwako. Hivyo Yesu anatoa angalizo kwa kusema, “Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu?” Lk 13:2, 4. Mimi na wewe yatupasa kuwa na utayari wa kupokea huruma ya Mungu kama alivyofanya Mtoza Ushuru. Na tazama, Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi,” Lk 18:13.  Hali na utayari wa Mtoza Ushuru wa kufanya toba ya kweli na kuipokea huruma ya Mungu ni kinyume kabisa na yule Mfarisayo aliyejihesabia haki. Naye (Mfarisayo) alijiinua na kusali hivi, Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru,” Lk 18:11. Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, Mungu haitaji orodha ya wema na uzuri wako. Mimi na wewe tunapaswa wema na hiyo ndiyo sifa ya  wana wa Mungu. Na katika wema na uzuri huu hatuongezi au kupunguza wema na uzuri wa Mungu. Ila kwa kutenda mema na kuwa wema tunaudhihirisha Utukufu wa Mungu pale tulipo. Na hii ndiyo maana ya Maneno haya ya Yesu, Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu. Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:37, 48. Hivyo yale yote uyafanyayo kwa ajili ya watu na Mungu, yalenge katika utakatifu wako. Bila utakatifu kumwona Mungu ni ndoto isiyowezekana.

Tatu, maneno haya mazito ya Mungu, “Vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni Nchi Takatifu,” yanatukumbusha dhana na dhamana ya uongozi ambao kwa hakika ni mpango wa Mungu kupitia watu wake, na kwa ajili Mungu. Uongozi ni DHAMANA. Dhamana hii ya uongozi inatukumbusha Utakatifu wa kile uwajibikacho kama Kiongozi na Utakatifu wa wale unaowahudumia au kuwaongoza. Viongozi wengi leo wamesahau wajibu na kweli hii mara wapatapo madaraka. Viongozi hawa ni wale wenye hujigeuza na kuwa miungu watu kwa yale wayasemayo na kuyaamuru kwa umma uliowaweka madarakani. Mtume Paulo anatoa angalizo la viongozi wa mtindo huo na kusema, anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke,” 1Kor 10:12. Kiongozi yeyote aliye katika ngazi yoyote ile na taasisi yoyote ile, elewa kwamba pale ulipo katika kutenda kwenye maana ya kutumika, ni sawa na kusimama katika Nchi TAKATIFU kama alivyoambiwa Musa.

Historia ni mwalimu mzuri sana. Vitabu Vitakatifu na hata historia ya mataifa mbalimbali katika ulimwengu huu, vimeonyesha dhairi na pasipo shaka miisho ya viongozi wale ambao hawakuwa na hofu ya Mungu, na kujijeuza wao kuwa miungu watu. Mungu anasema hivi juu ya viongozi wenye kujifanya miungu watu, “nami nitaikomesha fahari yao wenye kiburi; nami nitayaangusha chini majivuno yao walio wakali,” Isa 13:11b. Mungu kamwe hapendezwa na viongozi wenye kiburi na majivuno kwa sababu hawamwakilishi Mungu zaidi ya nafsi zao. Hivyo Mtume Paulo anatoa angalizo, na kusema, …wengi sana katika wao, Mungu hakupendezwa nao; maana waliangamizwa jangwani,” 1Kor 10:5. Wapendwa wana wa Mungu, pona yako na yangu ni kusimama katika kweli na haki, na ninapodondoka nifanya toba ya kweli kwa kuitazama neema na huruma yangu kwangu ilivyo kubwa kuliko dhambi zangu.

Mpendwa wana wa Mungu, tamani kila siku kutenda mema na lililo haki na kweli. Basi mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya, kama wale nao walivyotamani,” 1Kor 10:6. Kila siku Mungu anakupa nafasi ya kuwa mwema kwa sababu amekuchagua yeye ili uzae matuma mema na yenye kudumu, Yoh 15:16. Yawezekana kwa makusudi kabisa hujayazaa matunda hayo mema licha ya fursa nzuri uliyonayo. Kipindi hiki cha Kwarema kiwe changamoto kubwa kujirudi na kumrudia Mungu. Na ushauri wa mwisho ni huu: Bwana, uuache (mtu huo, mimi, wewe) mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda baadaye, vema! La, usipozaa, ndipo uukate,” Lk 13:8-9. Amina. 

Wapendwa katika Kristo, bila shaka sote tunamfahamu Jogoo. Jogoo hufikiri bila kuwika mapema asubuhi hakuna mapambazuko. Hivyo bila kuwika kwake siku haiwezi kuanza. Hii ndiyo falsafa ya Jogoo.

Siku moja mapema asubuhi kukiwa bado na mawingu mengi angani, Jogoo alitoka na kujilaza chali chini ya mti akiwa na lengo la kuyazuia mawingu yasidongoke. Akiwa katika mkao huo huku miguu yake akiielekeza juu na akiwa amezikunjua mbawa zake, katawi kidogo cha ule mti kilikwanyuka na kushuka kwa kasi. Jogoo yule kuona vile aliruka huku akiwika kwa hofu.

Baada ya dakika chache Jogoo yule alijiuliza, “hili tawi limetoka ubali wa mita chache sana na limekuwa tishio kubwa la uhai wangu. Je, nitaweza kweli kuyastahimili mawingu yale yaonekanayo kuwa mbali? Kwa mtazamo huu, ni mimi kweli ninayeyaamza mapambazuko?”

Wapendwa wana wa Mungu Jogoo yupo kwenye mchakato wa toba ya kweli. Je wewe na mimi tuliokirimiwa utashi na Mungu tunasubiri nini?

Tumsifu Yesu Kristo!

Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo,” Lk 13:5


Ee Yesu, nikumbushe mara zote kuwa uongozi ni dhamana na kielelezo chake ni kutumia kwa wote kwa hofu yako, nikitambua Utakatifu wa nafasi hiyo na Utakatifu wa wale ninaowaongoza. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario