jueves, 4 de febrero de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 4 YA MWAKA-C

IJUMAA WIKI YA 4 YA MWAKA-C
Somo: YbS 47:2-13
Zab: 18:31, 47, 50-51
Injili: Mk 6:14-29
Nukuu:
“Naye Bwana akamwondolea dhambi zake, akaiinua pembe yake hata milele; akampa agano la ufalme, na kiti kitakatifu cha enzi katika Israeli,” YbS 47:11

“Na kwa ajili yake akainuliwa mwanawe, mtu wa ufahamu aliyekaa salama. Sulemani alimiliki katika siku za kufanikiwa, naye Mungu akampa raha kumzunguka pande zote, ili alijengee jina lake nyumba, na kumwekea tayari patakatifu pa milele,” YbS 47:12-13

Maana Herode alimwogopa Yohana; akimjua kuwa ni mtu wa haki, mtakatifu, akamlinda; na alipokwisha kumsikiliza alifadhaika sana; naye alikuwa akimsikiliza kwa furaha,” Mk 6:20

Akamwapia, Lo lote utakaloniomba nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu,” Mk 6:23

Basi akatoka, akamwuliza mamaye, Niombe nini? Naye akasema, Kichwa cha Yohana Mbatizaji,” Mk 6:24 

Mara akaingia kwa haraka mbele ya mfalme, akaomba akisema, Nataka unipe sasa hivi katika kombe kichwa cha Yohana Mbatizaji,” Mk 6:25 

Mfalme akafanya huzuni sana, lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya hao walioketi karamuni, hakutaka kumkatalia,” Mk 6:26 

Mara mfalme akatuma askari, akaamuru kuleta kichwa chake. Basi akaenda, akamkata kichwa mle gerezani,” Mk 6:27 

akakileta kichwa chake katika kombe, akampa yule kijana, naye yule kijana akampa mamaye,” Mk 6:28

Wanafunzi wake waliposikia habari, walikwenda, wakauchukua mwili wake, wakauzika kaburini,” Mk 6:29

TAFAKARI: “Lo lote utakaloniomba nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu.”

Wapendwa wana wa Mungu, sifa na kutaka umaarufu umewaponza wengi. Ni jambo la busara kujua uwezo na mipaka yako hasa pale unapotakiwa kutoa maamuzi kwa nafasi uliyo nayo. Ni mara ngapi kwenye vikao mbalimbali vya maandalizi ya matukio mbalimbali kama vile; harusi, jenzi mbalimbali, unatoa ahadi ambazo kwa kiasi fulani zipo nje ya uwezo wako. Waswahili wanasema hivi, “mbuzi hula umbali wa kamba yake.” Leo tunaona katika Injili tukio la ajabu sana. Mfalme Herode anajiweka kitanzi mwenyewe kwa kutaka sifa na umaarufu.

Ikiwa ni siku ya kuzaliwa kwake, Herodi anatoa ahadi kwa Binti yake ambaye aliufurahisha ukumbi kwa kucheza vizuri. Wakati mwingine yakupasa kuwa na hakiba ya maneno hata kama hali ya kusema chochote inakuruhusu. Naye Herode akamwapia binti yake, Lo lote utakaloniomba nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu,” Mk 6:23. Maneno haya yalikuwa mazito sana kwa binti huyu. Hivyo kwa hali ile alihitaji ushauri wa haraka. Basi akatoka, akamwuliza mamaye, Niombe nini? Naye akasema, Kichwa cha Yohana Mbatizaji,” Mk 6:24. Na hii ndiyo iliyokuwa nafasi ya Herodia ya kumwangamiza Yohane Mbatizaji ambaye alionekana kero na kiwingu kwa mahusiano yake na Herode. Tuelewe kwamba Herodia alikuwa mke wa Filipo ndugu yake Herode. Yohane Mbatizaji alikemea uovu huu kwa nguvu zake zote kwa Herode kumuoa mke wa ndugu yake. Na sasa Yohane Mbatizaji anakuwa mbuzi wa kafara.

Wapendwa wana wa Mungu, wapo wengi katika jamii yetu wanakutwa na umauti kama Yohane Mbatizaji kwa vile tu wanasimamia kweli na wapo tayari kwa ajili ya kweli. Maisha ya Yohane Mbatizaji hayana ndoa lolote katika jamii. Ukweli huu hata Mfalme Herode anaufahamu. Maana Herode alimwogopa Yohana; akimjua kuwa ni mtu wa haki, mtakatifu, akamlinda; na alipokwisha kumsikiliza alifadhaika sana; naye alikuwa akimsikiliza kwa furaha,” Mk 6:20. Yule binti ya Herode bila kufahamu kilichokuwa nyuma ya pazia anapeleka ujumbe kadiri alivyoambiwa na Mama yake. Binti huyu pia anapenda kwa nafasi hii na umati huu wa watu wengi kumfurahisha Mama yake. Nani kama mama jamani? Mara akaingia kwa haraka mbele ya mfalme, akaomba akisema, “nataka unipe sasa hivi katika kombe kichwa cha Yohana Mbatizaji,” Mk 6:25.

Habari hii inamuhuzunisha sana Mfalme Herode, ila kwa vile iliipenda sifa na umaarufu anashindwa kuizuia nafsi yake iliyoegemea mwili kwa sasa. Mfalme akafanya huzuni sana, lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya hao walioketi karamuni, hakutaka kumkatalia,” Mk 6:26. Hapa ndipo tunapoona matumizi mabaya ya madaraka tuliyonayo na kulevywa nayo kwa ajili ya kujenga majina yetu na kusahau haki na unyenyekevu kama viongozi. Uongozi ni dhamana. Uongozi ni kuwajibika kuliko haki na usawa. Uongozi ni mizania ya haki kwa wote. Mfalme Herode anaisikiliza nafsi yake ambayo kwa sasa inasukumwa na mwili. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21. Maamuzi yoyote uyafanyayo katika hali hii hayana baraka ndani yake. Hivyo, Mara mfalme akatuma askari, akaamuru kuleta kichwa chake. Basi akaenda, akamkata kichwa mle gerezani,” Mk 6:27

Kifo cha ukatili dhidi ya Yohane Mbatizaji mtu mwenye haki kinakuwa furaha ya muda mfupi kwa Herodia.  Naye yule askari mwaminifu akakileta kichwa chake katika kombe, akampa yule kijana, naye yule kijana akampa mamaye,” Mk 6:28. Hata leo watumishi wetu waaminifu, askari polisi na jeshi, huwa wanapewa maagizo na viongozi wetu wenye kutaka sifa na kuyajenga majina yao kwa kumwaga damu za wenye haki kwa kile kisemwacho kama maagizo kutoka juu. Ni mara ngapi tunashuhudia vitendo vya aibu na uvunjifu wa haki za binadamu kwa “maagizo kutoka juu.” Ndugu yangu, aliye juu ni Mungu tu. Wengine wote wanaojiona wapo juu ni kutaka kuchukua nafasi ya Mungu, ambayo hata ibilisi alipenda kufanya hivyo na mwisho wa siku alilaaniwa milele. Je, nawe wapenda laana hiyo?

Ndugu yangu, ni vyema ukajua uongozi ni dhamana na mwisho wa siku itakupasa kutoa hesabu yake. Basi pale tunapokosea kutokana na ubinadamu wetu, tuwe wepesi wa kujirudi na kujirekebisa. Mfano mzuri wa kujirudi na kujirekebisha ni Mfalme Daudi. “Naye Bwana akamwondolea dhambi zake, akaiinua pembe yake hata milele; akampa agano la ufalme, na kiti kitakatifu cha enzi katika Israeli,” YbS 47:11. Leo viongozi wetu walio wengi wamefikia hali ya kuhalalisha maovu yao kwa kile wanachojiita ‘wazalendo na wenye mawazo mapana kwa manufaa ya nchi’ ilhali ni kwa manufaa yao binafsi na familia zao na vyama  vya siasa wanavyoviwakilisha, ambavyo vinaonekana kushika hatamu ya umilele.

Wapendwa wana wa Mungu, bila kujinyenyekeza kuliko kweli na haki kutoka mioyoni mwetu pale tunapopewa dhamana na umma, hata yale mazuri tunayoyafanya hayana thamani yoyote mbele ya Mungu. Mfalme Daudi kwa unyenyekevu wake na kujua nafasi aliyokuwa nayo kama kiongozi wa kutenda haki kwa wote bila kujali maslahi binafsi na marafiki zake, Ufalme wake unabarikiwa hata kwa mrithi wake. Hivyo, “na kwa ajili yake akainuliwa mwanawe, mtu wa ufahamu aliyekaa salama. Sulemani alimiliki katika siku za kufanikiwa, naye Mungu akampa raha kumzunguka pande zote, ili alijengee jina lake nyumba, na kumwekea tayari patakatifu pa milele,” YbS 47:12-13. Jambo la kushangaza leo ni hili; kwa asilimia kubwa viongozi tulionao katika jamii yetu leo ni watoto au familia za viongozi waliokuwapo hapo awali katika uongozi. Kwa jicho la kawaida kabisa waweza kuona mtoto huyu siyo njia yake, bali ni mazoea ya kufaidika na mfumo ambao hauna uwajibikaji. Uongozi umekuwa kama ajira ya kawaida na wala siyo huduma katika maana ya kutumika. Yesu anatuambia, na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mt 20:27-28. Ni wazi kwa mfumo huu wa kutokuwajibika na kutumika ndio unao tugharimu sana katika Taifa letu leo.

Tumsifu Yesu Kristo!


Kalibu ni kwa fedha, na tanuru kwa dhahabu; Na mtu hujaribiwa kwa sifa zake,” Mit 27:21

No hay comentarios:

Publicar un comentario