viernes, 5 de febrero de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 4 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 4 YA MWAKA-C
Somo: 1Fal 3:4-13
Zab: 119:9-14
Injili: Mk 6:30-34
Nukuu:
Basi mfalme akaenda Gibeoni, ili atoe dhabihu huko; kwa kuwa ndipo mahali pa juu palipo pakuu. Sulemani akatoa sadaka elfu za kuteketezwa juu ya madhabahu ile,” 1Fal 3:4 

Na huko Gibeoni Bwana akamtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe,” 1Fal 3:5

Kwa hiyo nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi?” 1Fal 3:9

Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako; bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe, wala baada yako hatainuka mtu kama wewe,” 1Fal 3:11-12 

Na mambo yale usiyoyaomba nimekupa, mali na fahari, hata hapatakuwa na mtu katika wafalme kama wewe, siku zako zote,” 1Fal 3:13

Na mitume wakakusanyika mbele ya Yesu; wakampa habari za mambo yote waliyoyafanya, na mambo yote waliyoyafundisha,” Mk 6:30 

Akawaambia, Njoni ninyi peke yenu kwa faragha, mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo. Kwa sababu walikuwako watu wengi, wakija, wakienda, hata haikuwapo nafasi ya kula,” Mk 6:31

Naye aliposhuka mashuani, akaona mkutano mkuu, akawahurumia; kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji; akaanza kuwafundisha mambo mengi,” Mk 6:34 

TAFAKARI:Omba utakalo nikupe.”

Wapendwa wana wa Mungu, haki huenda wa wajibu. Kumbe utimizapo wajibu wako vyema una haki ya kupata kadiri ya wajibu uliutimiza. Jambo la ajabu wapo kati yetu wengi hupenda kutendewa haki ilhali ni wachengaji wazuri sana katika kutimiza wajibu wao. Mfalme Sulemani anatimiza wajibu wake mbele ya Mungu. Basi mfalme akaenda Gibeoni, ili atoe dhabihu huko; kwa kuwa ndipo mahali pa juu palipo pakuu. Sulemani akatoa sadaka elfu za kuteketezwa juu ya madhabahu ile,” 1Fal 3:4. Kwa kutimiza wajibu huu, Mfalme Sulemani anahesabiwa haki mbele ya Mungu. Na huko Gibeoni Bwana akamtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe,” 1Fal 3:5. Mungu hufurahishwa sana pale unapotimiza wajibu wako vyema na kwa uaminifu kadiri ya nafasi na wito wako.

Wajibu huu muhimu hautegemea uziri wa kile ufanyacho au aina ya kazi ufanyayo, bali ubora katika kufanya na ukamilifu wake. Mtakatifu Theresa wa Yesu, anasema kila mmoja wetu aweza kuwa mtakatifu hasa kwa matendo yale madogo madogo tuyafanyapo kwa ukamilifu wake na uaminifu. Kwa tendo hili la kumtolea Mungu sadaka ya kuteketezwa, Mfalme Sulemani anahesabiwa haki mbele ya Mungu na kupata fursa ya kuomba atakalo. Jambo la kujifunza hapa kutoka kwa Mfalme Sulemani ni kwamba pamoja na fursa hiyo, Mfalme anaomba kitu ambacho kitaweza kumfanya atumike vizuri zaidi na kumpendeza Mungu. Mfalme anaukwepa ubinafsi wake na kujali zaidi wale aliokabidhiwa kuwaongoza. Naye Sulemani anaomba hivi,  nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi?” 1Fal 3:9. Mfalme Sulemani anaomba hekima. Jambo hili pia linamfurahisha Mungu.

Wapendwa wana wa Mungu, sala ya utakatifu kwanza kabisa ni kuwa na imani ya kwamba kile uombacho ushakipata bila kuwa na shaka yoyote juu Mungu. Pili, sala ya utakatifu ni sala ile isiyobeba ubinafsi wako. Ni sala au maombi yanayojali wengine na kwa nafasi ya pekee wale ambao wapo chini yako au unao wajibika kwao moja kwa moja. Ombi la Mfalme Sulemani linathibitisha sala ya utakatifu. Mungu hufurahishwa sana na sala au maombi ya namna hii. Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako; bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe, wala baada yako hatainuka mtu kama wewe,” 1Fal 3:11-12. Ndugu yangu tunayesafiri pamoja katika tafakari hii, yachunguze maombi yako na sala zako mbele ya Mungu.

Mtume Yakobo anatupa angalizo juu ya sala na maombi yetu na kusema, Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu,” Yak 4:3. Kumbe sala ya utakatifu ni kuepuka pia tamaa zako kwa kile uombacho. Ndugu yangu, Mungu anayafahamu mahitaji yako yote na atakupatia kadiri ya mahitaji hayo. Kumbe unapoishinda nafsi yako katika ubinafsi wake kwa maombi na sala zako, Mungu hukupatia hata yale ambayo hukuyaomba kwa sababu anajua unayahitaji katika kweli na haki. Mfalme Sulemani anapewa uhakika huo na Mungu. Na mambo yale usiyoyaomba nimekupa, mali na fahari, hata hapatakuwa na mtu katika wafalme kama wewe, siku zako zote,” 1Fal 3:13. Mungu anayajua mahitaji yako yote. Jambo la muhimu ni hili, ‘timiza wajibu wako kwa uaminifu.’

Wanafunzi wa Yesu wanatimiza wajibu wao kwa uaminifu na wanatoa taarifu ya kile walichokifanya mbele ya Yesu. Na mitume wakakusanyika mbele ya Yesu; wakampa habari za mambo yote waliyoyafanya, na mambo yote waliyoyafundisha,” Mk 6:30. Tendo hili la uaminifu kwa yale waliyoyafanya mitume linamfurahisha Yesu, naye anawaonea huruma. Akawaambia, Njoni ninyi peke yenu kwa faragha, mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo. Kwa sababu walikuwako watu wengi, wakija, wakienda, hata haikuwapo nafasi ya kula,” Mk 6:31. Ni furaha iliyoje tunapohesabiwa haki kwa yale tuyafanyayo kwa uaminifu na yule mwenye Mamlaka na Haki? Ni furaha ya kweli kweli!

Ndugu yangu, kile ufanyacho kwa uaminifu na kuwajibika kuliko tukuka hubarikiwa na wale uliwahudumia hubarikiwa pia. Na ndivyo ilivyokuwa kwa wanafunzi wale wa Yesu. Naye (Yesu) aliposhuka mashuani, akaona mkutano mkuu, akawahurumia; kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji; akaanza kuwafundisha mambo mengi,” Mk 6:34. Hivyo ni vyema kuuthamini wajibu wako na kufanya kwa uaminifu wote. Leo kama tungewajibika kwa asilimia 50 tu kila mmoja wetu kwa nafasi yake na wito wake, ulimwengu huu, na kwa namna ya pekee nchi yetu ingekuwa mahali pazuri zaidi pa kuishi. Basi nikusihi ndugu yangu anza kuwajibika hapo ulipo katika uaminifu wote. Acha mazoea katika utendaji wako wa kila siku. 

Tumsifu Yesu Kristo!


Ili mwenende kama ilivyo wajibu wenu kwa Mungu, mwenye kuwaita ninyi ili mwingie katika ufalme wake na utukufu wake,” 1The 2:12

No hay comentarios:

Publicar un comentario