jueves, 31 de marzo de 2016

TAFAKARI: IJUMAA YA OKTAVA YA PASAKA

IJUMAA YA OKTAVA YA PASAKA
Somo: Mdo 4:1-12
Zab: 118:1-2, 4, 22-24, 25-27a
Injili: Yoh 21:1-14 
Nukuu:
Wakawakamata, wakawaweka gerezani hata asubuhi; kwa kuwa imekwisha kuwa jioni,” Mdo 4:3

Walipowaweka katikati wakawauliza, Kwa nguvu gani na kwa jina la nani ninyi mmefanya,” Mdo 4:7

 “Jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu,” Mdo 4:10

Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 12 

Simoni Petro aliwaambia, Naenda kuvua samaki. Nao wakamwambia, Sisi nasi tutakwenda nawe. Basi wakaondoka, wakapanda chomboni; ila usiku ule hawakupata kitu,” Yoh 21:3

Basi Yesu akawaambia, Wanangu, mna kitoweo? Wakamjibu, La,” Yoh 21:5

Akawaambia, Litupeni jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata. Basi wakatupa; wala sasa hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki,” Yoh 21:6

Basi yule mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda akamwambia Petro, Ndiye Bwana,” Yoh 21:7

“Naye Simoni Petro, aliposikia ya kwamba ni Bwana, akajifunga vazi lake, (maana alikuwa uchi), akajitupa baharini,” Yoh 21:7b

Basi Simoni Petro akapanda chomboni, akalivuta jarife pwani, limejaa samaki wakubwa, mia hamsini na watatu; na ijapokuwa ni wengi namna hiyo, jarife halikupasuka,” Yoh 21:11

TAFAKARI: “Litupeni jarife  upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata.”

Wapendwa wa Mungu, Tumsifuni Yesu Kristo kwa wingi wa neema na baraka zake anazotujalia kila siku tunapo tafakari neno lake. Wapendwa leo kwa namna ya pekee tuyatafakari naneno haya ya Bwana wetu Yesu Kristo, “Litupeni jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata.” Neno hili Yesu anawaambia wanafunzi wake ambao wameshinda usiku kucha wakivua samaki, na kutoka wakavu kabisa. Neno hili la Yesu Kristo limejaa neema na maarifa, limejaa upyaisho na mwelekeo mpya, limejaa nguvu na matumaini, limejaa uthaminishwaji katika kutenda vyema tena. Sababu kubwa na neno hili ni UPANDE WA KUUME liliko elekezwa lile JARIFE. Ni upande walioheri na salama. Ni upande wenye baraka.

Neno hili ndiyo siri kubwa ya uinjilishaji wa kina, chini ya msukumo wa Roho Mtakatifu wa Kanisa la jumuiya ya kwanza ya Wakristo. Roho huyu Mtakatifu, ndiye kichocheo kikubwa cha ushupafu waliokuwa nao Mitume, licha ya kuhujumiwa mara kwa mara kwa sababu la JINA LlLE KUU LA BWANA WETU YESU KRISTO MNAZARETI. Mitume baada ya ufufuko wa Kristo, walisongwa sana, kwa sababu tu walishuhudia ufufuko wa Kristo. Wakawakamata, wakawaweka gerezani hata asubuhi; kwa kuwa imekwisha kuwa jioni,” Mdo 4:3. Misukosuko hii tunayoiona leo katika zama zetu, inakishindo kikuu sana. Leo, Wakristo wengi uharabuni, Iran, na baadhi ya nchi za Afrika kama Nigeria, Somalia, Sudani ya Kaskazini, Tanzania Visiwani yetu ya leo; wanateswa na hata kuuwawa kwa sababu tu wao ni Wakristo.

Pamoja na hali hiyo, Mtume Petro kama kiongozi hakusita kusema iliyo kweli mbele ya macho ya hawa wahujumu wa Kanisa la Kristo. Wanapohojiwa ni kwa mamlaka gani wanafundisha kuhusu JINA LILE-YESU KRISTO, na Imani hiyo, Mitume hawasiti kusimama kwa lililo kweli. Petro bila kupepesa macho anasema,Jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu,” Mdo 4:10. Kiongozi wa dini leo ambaye anapenda kupata sifa na kupendwa na wote, na hasa wanasiasa ambao kwao rushwa ni sifa ya utumishi bora, hakika mbele ya JINA HILI, kiongozi huyu atakuwa na swali kubwa la kujibu.

Petro kama walivyokuwa Mitume wengine hawakuwa na elimu ya ajabu sana zaidi ya stadi za kupambana na maisha ya kila siku. Petro Mtume kama walivyo wengine katika kundi hili la Mitume, walikuwa wavuvi. Watu hawa kwa mang’amuzi yao ya maisha, ilikuwa ni jambo la ajabu kutoa elimu hii ya wokovu juu ya siri ile kubwa ya Ufalme wa Mungu na Uzima wa milele kwa wale waliokuwa wamebobea kwenye uwanja huo kama Waandishi, Mafarisayo na Masadukayo. Jambo hili linatupa ukweli wa nguvu na mwongozo wa Roho Mtakatifu kwa Kanisa hili la Mwanzo. Leo, tunamwitaji sana huyu Roho Mtakatifu katika Kanisa, na siyo majina na vyeo visivyokuwa na uhusiano wa moja kwa moja na maisha yetu ya Imani na ya Kiroho. Wapendwa huu ndio ukweli kwamba, Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 12.

Tunapojaribu kuchenga ukweli huu, tunakuwa nje ya kweli mzima ya mafundisho ya Kristo na lengo zima la umilele wa maisha haya tunayoyaishi. Mara kwa mara kunakuwa na vishawisha vya kurudi nyuma na kufanya yale tuliyoyazoea. Hata Mitume hawakuweza kukwepa hali hiyo, kwani maisha yao na ukuuaji wao wa Imani ulilandana sana na maisha na mazingira yao. Hivyo Mtume Simon Petro anawaambia wenzake, Naenda kuvua samaki. Nao wakamwambia, Sisi nasi tutakwenda nawe. Basi wakaondoka, wakapanda chomboni; ila usiku ule hawakupata kitu,” Yoh 21:3.

Wapendwa wana wa Mungu, tunapokuwa nje ya mpango mzima wa Mungu, na hasa kwa wale tuliopewa thamana hiyo, mafanikio ya yale tuyatamaniyo huwa hewa na kutoweka kabisa. Kumhubiri Kristo na kumshuhudia kwa maneno na matendo ni kazi ya kila  aliyebatizwa na kuimarishwa. Hivyo basi, yatupasa kulifanya tendo hilo pasipo shaka. Kristo hachoki tukumbusha tunapokengeuka kuhusu ukweli huu. Kristo aweza kutumia njia mbalimbali kuwakilisha ujumbe wa kweli hii. Kwa upendo wake, Kristo mara zote anapenda kujua mahangaiko yetu, na kuturudisha katika mstari. Katika hali ya kuchoka na uchovu mwingi kwa kupigika usiku kucha bila kupata samaki, anawaambia wanafunzi wake, Wanangu, mna kitoweo? Wakamjibu, La,” Yoh 21:5. Kwa maana nyingine Yesu anataka kutuambia, Je, mnapozifuata njia zenu na kuacha maagizo yangu mnapata mafanikio?

Kuonyesha ukweli wa jambo hili, Yesu Kristo, anawafundisha njia na maagizo yake yaliyo kweli na sahihi kwa uzima wa mwili na roho. Akawaambia, Litupeni jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata. Basi wakatupa; wala sasa hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki,” Yoh 21:6.

Wapendwa katika Kristo, yawezekana ushapigana sana na maisha kiasi kwamba kila siku ni aheri ya jana. Jambo la kwanza usitafuta mchawi wala kwenda kwa waganga, au kusafisha nyota kama tunavyosikia wengi wakidanganywa. Jambo la kwanza chunguza uhusiano wako na Mungu. Je, umelitupa jarife hilo upande wa kuume wa chombo chako yaani, maisha yake? Je, unaisha kadiri ya matakwa ya Mungu? Kama hapana, Je, unaridhika na hali hiyo? Kama siyo, Je, ni kitu gani kinachokukwamisha kurejesha uhusiano huo? Kama uhusiano wako na Mungu ni mzuri na bado unapigika sana na maisha, jambo hilo unalichukuliaje? Je, walichukulia kama kusahauliwa na Mungu, au kutokutendewa haki na Mungu? Je, unaelewaje subura ya Mungu kwa yale uyaombayo na kuyatamani?

Ndugu yangu, hakuna jambo lolote tuombalo Mungu aache kutupatia. Kama itatokea kwa hapa duniani hatukulipata basi jua umeandaliwa jambo hilo kwa umilele wake, mara baada ya maisha haya ya hapa duniani. Kamwe Mungu hamtupi mja wake. Kwa wale ambao Mungu ametukirimia zaidi na hata kupita mahitaji yetu, tunachukuliaje jambo hilo? Je, tunamtambua Mungu katika mali na utajiri wetu? Ukweli ni kwamba kamwe hatutaweza mtambua Mungu kwa yale tuliyonayo, kama hatuna upendo na Mungu. Yohane Mtume anamtambua Kristo kwa sababu alikuwa na upendo wa dhati kwa Kristo na Kristo alikuwa anampenda kwa namna ya pekee. Na hivi ndiyo Injili inavyotuambia, Basi yule mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda akamwambia Petro, Ndiye Bwana,” Yoh 21:7.

Kumtambua huku Kristo, Yohani habaki na hali hiyo mwenyewe. Anamwambia na Petro pia. Je, tunapoguswa na upendo wa Kristo na Mungu tupo tayari kuushirikisha kwa wenzetu nao wapate wokovu huo? Tunaona baada ya Petro Mtume, kusikia habari hiyo, anajitosa kwenye maji maana alikuwa uchi. “Naye Simoni Petro, aliposikia ya kwamba ni Bwana, akajifunga vazi lake, (maana alikuwa uchi), akajitupa baharini,” Yoh 21:7b. Mpendwa tunayesafari wote katika tafakari hii, Petro kuwa uchi hapa kunamaanisha kwa upande mwingine kwamba anatambua kujikwaa kwake kunakotokana na kutokuyafanya yale aliyopaswa kufanywa kama kiongozi, kama niliyoeleza hapo mwanzo.

Mara baada ya Petro kujitambua, anaingia chomboni na hapa tunaona maajabu haya. Basi Simoni Petro akapanda chomboni, akalivuta jarife pwani, limejaa samaki wakubwa, mia hamsini na watatu; na ijapokuwa ni wengi namna hiyo, jarife halikupasuka,” Yoh 21:11. Ndugu yangu, jarife hili halina tofauti na Kanisa kama chombo cha wokovu ambacho kazi yake kubwa ni kuwavuta watu kwa Kristo na kuwapeleka kwake wakiwa salama. Usalamu huu ni idadi inayotolewa ya samaki hawa. Tutajulikana kwa idadi yetu mbele za Mwanakondoo. Nasi tukifika mbele ya uso wa Mungu tutajulikana kwa idadi, na wale tuliopewa kazi hiyo yatupasa tutoe hesaba ya idadi tulioifikisha mbele ya Mungu na Mwanakondo.

Hata hivyo tunasikia jarife hili-Mtego huu, haukupasuka licha ya wingi wa samaki wale. Jibu ni kwamba mtego haukupasuka kwa sababu u imara. Mtego, yaani Jarife kama Kanisa, na Sakramenti ya wokovu wetu, uimara wake unatokana na uwepo wa nguvu ya Roho Mtakatifu, ambaye uyaratibisha yote kadiri ya mahitaji ya Kanisa lake kwa nyakati zote. Tumruhusu Roho Mtakatifu huyu afanye kazi yake, na siyo Roho Mtakavitu. Roho Mtakavitu atalipasua JARIFE-KANISA. Roho Mtakavitu huyu ni: SIFA, CHEO, KUJULIKANA KULIKO BINAFSI, MAMLAKA MBELE ZA WATU, NA MBAYA ZAIDI KWA VIONGOZI WALA RUSHWA. Tusichoke kuhubiri na kuishi kwa vitendo Huruma ya Mungu kwa sababu hata hawa viongozi wala rushwa,  wote wasio na hofu ya Mungu ndani yao, na sisi sote kwa ujumla wetu kama Kanisa na wabatizwa tunahitaji huruma hiyo na wokovu wa Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 12


Ee Yesu na Mwokozi wetu, tujalie mara zote kuutafuta uso wako wa Huruma ili tuufikie uzima ule wa milele uliyotuhaidia. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario