martes, 29 de marzo de 2016

TAFAKARI: JUMATANO YA OKTAVA YA PASAKA

JUMATANO YA OKTAVA YA PASAKA
Somo: Mdo 3:1-10
Zab: 105:1-2, 3-4, 6-7, 8-9
Injili: Lk 24:13-35
Nukuu:                           
Na Petro, akimkazia macho, pamoja na Yohana, akasema, Tutazame sisi. Akawaangalia, akitaraji kupata kitu kwao. Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende,” Mdo 3:4-6

“Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu,” Mdo 3:7

Ikawa katika kuzungumza na kuulizana kwao, Yesu mwenyewe alikaribia, akaandamana nao,” Lk 24:15

Macho yao yakafumbwa wasimtambue,” Lk 24:16

“Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli,” Lk 24:19-21

Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake?” Lk 24:25-26

Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha,” Lk 24:29

TAFAKARI: “Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha; Ndiyo mkao wa Kipasaka, yaani, Ufufuo na Uzima”

Wapendwa wana wa Mungu, ni wakati mwingine tena tunapa fursa ya kuyatafakari Makuu ya Mungu. Kwa namna ya pekee na tulitafakari neno hili, “Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha; ndiyo mkao wetu wa Kipasaka, yaani, Ufufuo na Uzima.” Mkao wa Kipasaka-Ufufuo na Uzima tunauona katika somo letu la leo, ikiwa ndiyo shabaha kubwa ya jumuiya ya kwanza ya Wakristo. Hamu na uhitaji wa kukaa na Kristo Mfufuka, unajitokeza katika Injili yetu ya leo, pale wanafunzi wa Yesu waliokuwa wakielekea Kijiji cha Emau kumtaka akae nao kwani kumekwisha kuchwa, na mchana unakwisha.

Mkao huu wa Kipasaka-Ufufuo na Uzima ndiyo nguvu la Kanisa la Kristo. Mitume hawana cha kutoa zaidi NEEMA na BARAKA za Kristo Mfufuka. Mkao huu unabadilisha tabia na mazoea yetu katika maisha. Kristo anapokuwa kila kitu katika maisha yetu, hubadili maisha yetu na kuwa maisha ya uhai na uzima. Ni katika hali hii tunaopolewa kutoka kwenye kiza na kuingizwa katika mwanga. Tunatolewa katika makaburi yetu na kupelekwa kwenye mwanga na uzima. Tunatolewa katika kufa kufa kwetu kunakotokana na magonjwa na mahangaiko ya maisha na kupelekwa kwenye uzima na faraja.

Ni kwa sababu hii Mtume Petro na Yohana wanamtoa Bwana yule ombaomba katika mlangoni katika kuchoka kwake, na kumwingiza katika uzima na furaha ya kweli. Jambo hili linafanyika ndani na katika jina la Yesu. Na Petro, akimkazia macho, pamoja na Yohana, akasema, Tutazame sisi. Akawaangalia, akitaraji kupata kitu kwao. Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende,” Mdo 3:4-6

Yesu anapokuwa maisha yako ya kila siku unatiwa nguvu na kuondolewa kupooza kwako. Jambo hili hufanyika na uwezekana tu pale unapokubali kuongozwa na kushikwa mkono na Yesu. “Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu,” Mdo 3:7. Hapa ndipo tunapoanza maisha mapya tunapokubali kuongozwa na Kristo Mfufuka.

Injili yetu ya leo inatupa umuhimu wa kukaa muda wote na Kristo Mfufuka. Maisha yetu yanapita kwa kasi sana kama moshi, na wakati mwingine tunaishi tukiwa wakavu sana kiroho. Yesu Kristo kwa walio wengi ni Yesu wa Historia. Kwa walio wengi Yesu huyu hana nguvu tena. Tatizo kubwa tunalokutana nalo katika maisha ni kuyaweka matamanio yetu mbele zaidi ya mafundisho na kweli anayotufundisha Kristo. Sintofahamu hii inawakuta wanafunzi wale ambao wanaona Kifo cha Kristo kama tukio la kudanganywa hivi, na hakuna maana kabisa kwa yule ambaye walimtegemea sana na leo anawaangusha. Kifo hiki cha aibu cha msalaba kwa wanafunzi hawa kimewatoa matumaini yote.

Yesu Kristo hata katika sintofahamu hizi, bado yupo tayari kutusikiliza na kuzidi kutufundisha, licha ya kwamba hatumuoni kwa kuificha taswira yake, ili mradi tu tumpe nafasi. “Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli,” Lk 24:19-21.

Yesu hachoki kutukumbusha yaliyompasa kufanya na yaliyotabiriwa juu yake. Haya yote yapo katika Maandiko Matakatifu. Mt. Jerome anasema hivi kuhusu Yesu Kristo, “tunapokuwa wajinga wa maandiko matakatifu, ni kwa namna hiyo hiyo tu wajinga kuhusu Yesu Kristo.” Kuhusu jambo hili Yesu anatupa sababu ya yale yote yaliyojiri kuhusu Kifo na Ufufuko wake. Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake?” Lk 24:25-26. Ndugu yangu hapa tunakumbushwa pia, kwamba hakuna Utukufu pasipo Msalaba. Penye Msalaba pana Utukufu, na sasa ni rahisi kuupata Utukufu kwa sababa Kristo kesha ushinda Msalaba.

Wapendwa, Kristo anajifunua kwetu leo katika kuumega mkate. Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao,” Lk 24:30-31. Kuumega mkate kunatanguliwa na kulishwa neno lake na kulielewa. Tukio la wanafunzi wa Yesu kukutana naye njiani kuelekea Kijiji cha Emau, ni mtiririko mzima wa adhimisho la Misa Takatifu. Adhimisho hili lina sehemu kuu mbili; Liturjia ya neno na liturjia ya Ekaristi Takatifu. Kwa mantiki hii, uwezekano wa Kristo kujifunua kwetu wakati wa Ekaristi Takatifu, unabebwa kwanza na ufahamu wetu wa kulisikiliza neno lake, kulipokea, kulitafakari, kulishirikisha, na kuliishi. Wanafunzi hawa wa Yesu wanakuwa na hamu ya kukaa naye zaidi baada ya kulishwa neno na Kristo ingawa hawakumfahamu.

Ndugu zangu, wale ambao wamezoea kuchelewa na mara nyingine kushiriki tu liturjia ya Ekaristi Takatifu, ni wavamizi wa Mlo Mtakatifu wasioujua vizuri. Ni sawa na kukishambulia chakula kitamu na kizuri wakati ukiwa na mikono michafu. Ni vizuri kuhudhuria sehemu zote mbili za kiliturjia na ndivyo inavyotakiwa kwa Mkristo na hasa kwetu, ambao Ekaristi Takatifu kicho kiini cha yote. Wapo kati yetu ambao huingia Kanisani na moja kwa moja kujongea Meza ya Bwana. Huu ni uhuni wa hali ya juu kufanywa na Mkristo. Mwisho na muhimu tusichoke kuudhuria mara kwa mara maadhimisho ya Maabudu ya Yesu wa Ekaristo-Sakramenti Kuu. Hapa anakaa kwetu na kujifunua kwetu.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende,” Mdo 3:6


Ee Yesu, Bwana wangu na Mungu wangu, kaa nasi Bwana nyakati zote za maisha yetu hapa nduniani ili tuweze pia kufika kwako mbinguni. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario