ALHAMISI
WIKI YA 5 YA KWAREMA
Somo:
Mwa 17:3-9
Zab:
105:4-5, 6-7, 8-9
Injili:
8:51-59
Nukuu:
“Nawe ulishike agano
langu, wewe na uzao wako kwa vizazi vyao baada yako,” Mwa 17:9
“Amin, amin, nawaambia,
Mtu akilishika neno langu, hataona mauti milele,” Yoh 8:51
TAFAKARI:
“Neno la Mungu ni Uzima wetu; Imani ndiyo msingi wa yote”
Wapendwa wana wa Taifa
la Mungu, “neno la Mungu ni Uzima wetu; Imani ndiyo msingi wa yote.” Kwa
kuamini kwake Ibramu mambo mawili yanamtokea. Kwanza, jina lake lina badilika
na kuwa Ibrahimu, yaani Baba wa mataifa mengi. Pili, Mungu anafanya naye agano
la Milele. “Nawe ulishike agano langu, wewe na uzao wako kwa vizazi vyao baada
yako,” Mwa 17:9
Agano hili, Mungu anahiari mwenyewe kuwa Mungu
wake Ibrahimu, na kumilikisha mambo yote kwa ajili ya kizazi chake Ibrahimu na
kizazi kijacho. Urithi huu na heshima hii kwa Ibrahimu imetokana na kuamini
kwake kusiko na mashaka.
Katika injili ya leo
tunaona mdahalo wa Yesu na Wayahudi, ambao unapelekea Wayahudi kutaka kumpiga
mawe Yesu. Mzozo unazuka pale Yesu anapowashauri kulishika neno lake na
kutokuona umauti. “Amin, amin, nawaambia: Mtu akishika neno langu, hataona
mauti milele.” Yoh 8:5. Kulishika neno la Yesu ni kuamini asemacho na kumwamini
yeye. Neno kwa maana nyingine ni yeye mwenyewe ambaye kwa kupitia neno Yeye
alifanyika mwili, Yoh 1:14.
Ndugu yangu, unamwamini
Yesu? Yesu Kristo ana nafasi gani katika maisha yako? Tulio wengi Yesu wetu ni
Yesu wa historia. Ni yule tunayemtazama kwa mbali na tena tukiwa na shida na
tunafanya hivyo tukiwa na mashaka makubwa kama ataweza kufanya kitu hasa kwa
kile kinachotusibu. Tunapokuwa hatuna nafasi ya Yesu ndani ya Mioyo yetu, basi
ni wazi nafasi hiyo kuna kitu badala yake. Kwa Wayahudi nafasi ya Yesu
haikuwepo na badala yake kulikuwa na nafasi ya Ibrahimu ambaye pia hawakumjua.
“Yesu akawaambia, “Amin, amin, nawaambia: Yeye Ibrahimu asijakuwako, mimi
niko.” Basi wakaokota mawe ili wampupie; lakini Yesu akajificha, akatoka
hekaluni.” Yoh 8:58-59
Tumsifu Yesu Kristo!
“Amin, amin, nawaambia, Mtu
akilishika neno langu, hataona mauti milele,” Yoh 8:51
Karibu moyoni
mwangu Yesu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario