JUMAPILI
YA MATAWI MWAKA-C
Somo
I: Isa 50:4-7
Somo
II: Flp 2:6-11
Zab:
22:7-8, 16-17a, 18-19, 22-23, (K) 22:1
Injili:
Lk 22:14; 23:56 au Somo fupi Lk 23:1-49
Nukuu:
“Bwana Mungu amenizibua
sikio langu, wala sikuwa mkaidi, wala sikurudi nyuma. Naliwatokea wapigao
mgongo wangu, na wang’oao ndevu mashavu yangu; sikuficha uso wangu usipate
fedheha na kutemewa mate,” Isa 50:5-6
“naye hakuona kule kuwa
sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana
utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu, tena,
alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti,
naam, mauti ya msalaba,” Flp 2:6-8
“Wakati
huo mmoja wa wale Thenashara, jina lake Yuda Iskariote, aliwaendea wakuu wa
makuhani, akasema, Ni nini
mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya fedha. Tokea wakati huo akawa akitafuta
nafasi apate kumsaliti,” Mt 26:14-16
“Yuda Iskariote, yule
mmoja katika wale Thenashara, akaenda zake kwa wakuu wa makuhani, apate
kumsaliti kwao. Nao waliposikia walifurahi, wakaahidi kumpa fedha. Akatafuta
njia ya kumsaliti wakati wa kufaa,” Mk 14:10-11.
“Walakini,
tazama, mkono wake yeye anayenisaliti upo hapa pamoja nami mezani, Kwa kuwa Mwana wa Adamu aenda zake
kama ilivyokusudiwa; lakini, ole wake mtu yule amsalitiye!” Lk 22:21-22
“Yesu
akasema, Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo. Wakagawa mavazi yake,
wakipiga kura,” Lk 23:34
“Hapo
ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, jua limepungua nuru yake; pazia la
hekalu likapasuka katikati,” Lk 23:44-45
“Yesu
akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu,” Lk
23:46
TAFAKARI:
“Yesu Kristo Mfalme Mtaabika na Masikini
ili mimi na wewe tuwe warithi na matajiri, mwili na roho.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha jumapili ya Matawa ya mwaka “C” wa Kanisa, ingawa
tofauti ipo tu kwenye somo la Injili kwa mwaka “A”, “B” na “C”. Somo la Injili
ambalo hubeba simulizi la mateso, kufa, na kufufuka kwake Kristo, kwa Mwaka “A”
tunasoma Injili kama ilivyoandikwa na Mwinjili Mathayo, mwaka “B” Mwinjili
Marko, na Mwaka “C” Injili kama ilivyoandikwa na Mwinjili Luka.
Jumapili hii ya Matawi
kama tulivyoona, sehamu ya kwanza tunaona Bwana wetu Yesu Kristo anavyoingia
Mjini Yerusalemu kwa shangwe na vifijo, huku alaiki ya watu wakiimba Hosana
Mwana wa Daudi. Yesu anaingia Kifalme na kupokelewa kifalme.
Mashangilio haya na
maandamano tuliyokwisha yafanya yana maana kuu tatu: Kwanza, tunamuungama
Kristo kwa tendo hili la umati wa watu. Pili, tunatambua njia yake ni njia yetu
katika maisha yetu yote. Njia hii ni njia ya mateso ambayo ndio mlango wa
Utukufu na Ufufuko. Hivyo nasi tutafufuka naye tukimwamini na kumfuata mpaka
mwisho. Yesu anatuhaidi katika hili kwamba, “mwenye
kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka,” Mt 24:13, Mk 13.13. Na tatu,
tunakubali njia hii na tunamwahidi Kristo kumfuata. Hivyo katika juma hili Mama
Kanisa linatuzamisha katika mateso, kufa na kufufuka kwake Kristo.
Sehemu ya pili tunaona
anavyotaabika na kuhujumiwa na kusalitiwa na zile nderemo na vifijo alivyopewa
awali. Furaha na shangwe inageuka kuwa mateso, na kifo.
Mpendwa katika Kristo,
leo tumtazame Bwana wetu “Yesu Kristo aliye Mtaabika na Maskini ili mimi na
wewe tuwe warithi na matarijiri, mwili na roho.” Mungu aliyeupenda ulimwengu na
viumbe vyake hasa mwanadamu, anamtoa mwanaye mpenzi kuteseka, na kuufia
ulimwengu ili mimi na wewe tuwe warithi wa kweli, matajiri wa kweli, mwili na
roho. “Maana mmejua neema ya Bwana wetu
Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri,
ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9
Kazi na njia ya kufika
hatma hii si rahisi kutokana na hali na uharibifu wa mwanandamu anayetakiwa
kukombolewa. Nabii Isaya anatabiri dhihaka hii ya huyu atakayebeba jukumu hili
na kusema, “Bwana Mungu amenizibua sikio langu, wala sikuwa mkaidi, wala
sikurudi nyuma. Naliwatokea wapigao mgongo wangu, na wang’oao ndevu mashavu
yangu; sikuficha uso wangu usipate fedheha na kutemewa mate,” Isa 50:5-6
Yesu Kristo yupo tayari
kuteseka, na kufa kwa ajili yangu na wewe. Huu ni upendo mkubwa sana kwetu.
Lakini binadamu haachi kuwa kigeugeu. Tunapenda utukufu pasipo mateso.
Tunapenda maisha mazuri pasipo kufanya kazi. Tunapenda kuwa wafalme bila
kutumikia. Tunapenda kuwa na mali bila kujishughulisha. Hii tamaa ya kupenda
kusiko kuwajibika ni mwinamio wa dhambi na mwelekeo wa dhambi. Leo Bwana wetu
Yesu Kristo anakubali kuteseka na kufa ili tuwe hayo tunayotamani katika kweli
na ukamilifu.
Tunakuwa warithi na matajiri
wa kweli, tunapoachilia haya ya ulimwengu
kwa kujisalimisha kila siku mikononi mwa Mungu. Kristo anatufanya
warithi na matajiri mwili na roho kwa kujisalimisha mikononi mwa Mungu bila
kusita na kuwa na mashaka kwa unyenyekevu mkubwa. “Naye hakuona kule kuwa sawa
na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu,
akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu, tena, alipoonekana ana
umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya
msalaba,” Flp 2:6-8. Ndugu yangu kujisalimisha kwa kujinyenyekesha kwa kila
mmoja wetu kupitia wito ulioitiwa na Mungu, (Ndoa, maisha ya wakfu, na ukleri)
ndiyo njia pekee ya kuurithi utajiri anautoa leo Yesu Kristo kwa njia ya mateso
na kifo chake.
Tokeo la kujinyenyekesha ni kukuzwa na
kuhesabiwa haki, siyo kwa mkono wa mwanadamu, bali Mungu mwenyewe. Mtoza ushuru
anahesabiwa haki kwa kujisalimisha kwa kujinyenyekeza. “Lakini yule mtoza
ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni; bali
alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi.
Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule
(Mfarisayo); kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa,”
Lk 18:13-14.
Ndugu yangu, yapo mambo
mengi sana tunayoweza kujifunza katika njili ya leo, ila napenda tujikite sana
katika usaliti wetu, unaotokana na dhambi. Tamaa kubwa ya mwanadamu ni ile ya
kupenda kuwa kitu kingine zaidi na kujikataa kuwa kile alicho. Yesu Kristo
anasalitiwa na wale wanaomjua vizuri na kuonja upendo wake. Leo tuseme hivi;
wanaomsaliti Bwana wetu Yesu Kristo, ni wafuasi wake, yaani mimi na wewe tulio
batizwa. Yuda Iskariote, mfuasi wake wa karibu, na mshika kasma, ndiye
anayemsaliti Kristo. Huku ni kukosa shukrani, fadhila na moyo wa upendo kwa
yule anayekutegemeza kila siku na kwa kila kitu. Ni sawa na kukata tawi la mtu
ulilolikalia. Habari hiyo ilikuwa hivi, kadiri ya Mwinjili Mathayo; “Wakati huo mmoja wa wale Thenashara, jina lake
Yuda Iskariote, aliwaendea wakuu wa makuhani, akasema,
Ni nini mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya
fedha. Tokea wakati huo akawa
akitafuta nafasi apate kumsaliti,” Mt
26:14-16. Yesu anawindwa na yule anayemfahamu vizuri.
Naye Mwinjili Marko anaongelea usaliti huo
hivi; “Yuda Iskariote, yule mmoja katika wale Thenashara, akaenda zake kwa
wakuu wa makuhani, apate kumsaliti kwao. Nao waliposikia walifurahi, wakaahidi
kumpa fedha. Akatafuta njia ya kumsaliti wakati wa kufaa,” Mk 14:10-11. Na
habari hiyo pia ilikuwa hivi, kadiri ya Mwinjili Luka, “Walakini,
tazama, mkono wake yeye anayenisaliti upo hapa pamoja nami mezani, Kwa kuwa Mwana wa Adamu aenda zake
kama ilivyokusudiwa; lakini, ole wake mtu yule amsalitiye!” Lk 22:21-22. Ndugu yangu, ni mara ngapi
unamsaliti Kristo kadiri ya wito wako? Kumsaliti huku Kristo ni pale
tunaposhindwa kuishi ahadi za wito na ubatizo wetu. Kila mmoja wetu ajitazame
na kujipima uaminifu wake katika wito wake.
Mzee Amani katika ndoa
yake alifanikiwa kuwapata mtoto mmoja tu wa kiume ambaye alijulikana kwa jina
la Upendo. Upendo alikuwa ndiye kila kitu kwa Mzee Amani. Upendo alikuwa karibu
sana na watu, alipendwa na kila mtu kwani pamoja na utajiri alikuwa nao baba
yake kamwe hakujigamba nao. Tendo hili lilimpa sana faraja baba yake, na hivyo
hakuona shida kuwaandalia wageni wa Mtoto wake Upendo kila anapokuwa na
marafiki zake nyumbani.
Pamoja na Upendo kuwa
na marafiki wengi, Sikujua Mafikiri alikuwa rafiki yake wa karibu sana, kiasi
kwamba wengi walidhani ni ndugu yake. Ukaribu huu wa Upendo na Sikujua
Mafikiri, ulimfanya Mzee Amani amchukulie Sikujua kama mwanaye pia. Basi Mzee
Amani alimshauri mwanaye Upendo kama inawezekana Sikujua aishi pia nyumbani
kwake.
Upendo alifurahi sana
kusikia jambo hilo la faraja kutoka kwa Baba yake. Hivyo Sikujua aliamia
nyumbani kwa Mzee Amani na kushiriki kila kitu cha nyumba ile bila utofauti
wowote. Basi siku moja Mzee Amani alikuwa akiongelea mali alizokuwa nazo na hata miradi aliyokuwa
akiifanya. Na mwisho ya maongezi haya, Mzee Amani alisema hayo yote ni kwa
ajili ya familia yake kwa sasa, akimaanisha wote, Upendo na Sikujua.
Kusikia vile, Sikujua
aliingiwa na wivu na tamaa, na kuanza kufikiri ingekuwa vyema kama yeye
angeyapata hayo yote. Basi baada ya miezi kama sita hivi, Sikujua aliamua
kuchukuwa sumu na kuwekea Upendo kwenye chai. Upendo alifariki, na kilio kile
kilisikika kila kona ya kijiji, kwani alipendwa na kufahamika na kila mtu wa
kijiji kile.
Baada ya msiba na
matanga kumalizika, ikiwa zishapita wiki kama tatu hivi, Sikujua aliugua sana
rohoni mwake kwa kitendo alichokifanya. Hivyo aliomba kuongea na Mzee Amani.
Mzee Amani alimruhusu. “Baba sidhani kama unanielewa na kuelewa nitakayo
kuambia jioni ya leo. Ukweli ni kwamba, baada ya kuongelea kuhusu mali zako na
miradi yako niliingiliwa na tamaa na kuona ingekuwa vizuri kama mimi ningekuwa
mrithi wa mali zote. Hivyo tamaa hii ilinichukua na kuamua kumuua mwanao
Mpendwa na rafiki yangu Upendo. Nilifanya jambo hilo kwa kumwekea sumu. Hivyo
nakuomba sana msamaha kwa tendo hilo, na ninajuta sana,” Sikujua alilisema neno
lile kwa majuto makubwa. “Mwanangu kuwa na Amani moyoni mwako. Ni jana tu,
nimetoka mahakamani kubadili mrithi wa mirathi ya mali zangu zote. Mwanzoni
kabla la mwangu kufariki, nilizigawa nusu kwa nusu, yaani wewe na yeye. Na sasa
mali zote ni zako, nawe ndiwe mwana wangu Mpendwa. Nimefarijika sana na kuwa
na furaha tena kwa majuto yako, na
kukubali kuwa mwanangu. Hii hapa nakala ya mirathi yako,” Mzee Amani aliyasema
hayo kwa upole na upendo mkubwa huku akamkabidhi hati ile ya mirathi.
Ndugu yangu, huu ndio
upendo wa Mungu Baba kwetu sisi wanadamu. Mwanaye Yesu Kristo na Mfalme, kwenye
milki zote, anakuwa masikini kwa mateso na kifo chake msalabani, ili wewe na
mimi wadhambi tuwe warithi na matajiri mwili na roho. Kibarua chetu ni kimoja
tu; kuupigania ukamilifu kwa kufanya toba na majuto ya kweli ya dhambi zetu, na
kuishi katika hali ya neema. Ukamilifu ndiyo cheo cha kila mbatizwa, na huu
ndiyo wito wa utakatifu tunaoitiwa kila siku. “Basi
ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48
Tumsifu Yesu Kristo!
“Walakini,
tazama, mkono wake yeye anayenisaliti upo hapa pamoja nami mezani, Kwa kuwa Mwana wa Adamu aenda zake
kama ilivyokusudiwa; lakini, ole wake mtu yule amsalitiye!” Lk 22:21-22
Ee Yesu Kristo, kwa kifo chako cha
aibu cha msalaba nijalie neema ya kuona umasikini wako uliopeleka mimi leo kuwa
mrithi na tajiri, mwili na roho. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario