viernes, 11 de marzo de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 5 YA KWARESMA YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 5 YA KWARESMA YA MWAKA-C
Somo I: Isa 43:16-21
Zab: 126:1-2, 2-3, 4-5, 6
Somo II: Flp 3:8-14
Injili: Yoh 8:1-11
Nukuu:
Bwana asema hivi, yeye afanyaye njia katika bahari; na mahali pa kupita katika maji yenye nguvu; atoaye gari na farasi, jeshi la askari na uwezo; wamelala, hawataondoka; wametoweka, wamezimwa mfano wa utambi,” Isa 43:16-17

Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani,” Isa 43:19 

 “Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu,” Flp 3:12

 “Lakini Yesu akainama, akaandika kwa kidole chake katika nchi. Nao walipozidi kumhoji, alijiinua, akawaambia, Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe,” Yoh 8:6b-7 

Nao waliposikia, wakashitakiwa na dhamiri zao, wakatoka mmoja mmoja, wakianzia tangu wazee hata wa mwisho wao; akabaki Yesu peke yake, na yule mwanamke amesimama katikati,” Yoh 8:9

TAFAKARI: Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani,” Isa 43:19 

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya tano ya Kwaresma ya Mwaka “C” wa Kanisa. Masomo yetu yote matatu leo yanatuelekeza kwenye  kweli ya ‘Mungu wetu aliye hai.’ Mungu wetu huyu ni Upendo, Haki, Kweli, Huruma, Msamaha na Asiyechoka kwa ajili ya viumbe vyake. Kwa mantiki hii ya Mungu wetu aliye hai, hakuna sababu ya sisi viumbe vyake kukata tamaa na kukosa matumaini. Mambo yote tunayokutana nayo katika maisha tuyaone katika mtazamo wa Mungu wetu huyu aliye hai. Ni katika mtazamo huo wa Kimungu yote hupata maana yake halisi. Hakuna lisilowezekana kwa Mungu wetu aliye hai.

Nabii Isaya katika somo la kwanza anaifunua kweli ya Mungu wetu aliye hai. Nabii Isaya anaamsha tumaini jipya kwa wana wa Israeli waliokwisha anza kulipoteza tumaini hilo. Bwana asema, Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani,” Isa 43:19. Huyu ni Mungu aliye hai na asiyeshindwa kutenda lolote kwa wale wote aliowaridhia na walio mridhia. Tatizo kubwa tulilokuwa nalo wengi ni kukosa subira pale mambo yanapokwenda kombo. Katika hali hii ya sintofahamu Yesu anatukumbusha na kusema, Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu; lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka,” Mt 10:22. Mateso na mahangaiko yako yasiwe ukuta wa kutokuona mbele na kukosa tumaini tena. Kristo aliyeyashinda mateso kwa ajili yako na yangu, awe faraja yetu siku zote. Kwa kuwa kama vile mateso ya Kristo yanavyozidi kwetu, vivyo hivyo faraja yetu inazidi kwa njia ya Kristo,” 2Kor 1:5

Wapendwa wana wa Mungu, ahadi atuhaidiazo Mungu ikiwa ni pamoja na mawazo yake kwetu ni amani na yana umilele ndani yake. Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho,” Yer 29:11. Tumaini katika Mungu ni tumaini hai na yenye mwanga halisi kwa kule tunapokwenda, tusipopajua au kufunuliwa wazi kwetu. Mungu anataka tufahamu ukweli huu: Wanyama wa kondeni wataniheshimu, mbweha pia na mbuni; kwa sababu nimewapa maji jangwani, na mito nyikani, ili kuwanywesha watu wangu, wateule wangu; watu wale niliojiumbia nafsi yangu, ili wazitangaze sifa zangu,” Isa 43:20-21. Wewe unayekata tamaa na kukosa mwelekeo wa maisha, elewa kuwa u mteule wa Mungu, umebeba sura na mfano wa Mungu, na u sifa halisi ya Mungu. Hii ndiyo huruma ya Mungu kwetu isiyokifani.

Tumaini hili la Mungu kwa watu wake na warithi wake limejifunua wazi kwa Mwanaye Mpenzi Yesu Kristo. Huyu ndiye Imanueli, “yaani, Mungu pamoja nasi,” Mt 1:23b. Mungu huyu pamoja nasi, yaani, Yesu Kristo, anajidhihirisha katika Injili ya leo kuwa ni Mungu wa haki, kweli, huruma na Upendo juu ya mwanamke aliyefumaniwa katika uzinzi. Kwa kosa alilofumaniwa mwanamke huyu tulitegemea mbele ya mashtaka yake angekuwepo na aliyeshiriki naye tendo lile. Lakini hilo halionekani. Huu ni uonevu wa kimazingira, kitaratibu na kisheria kwa tuhuma alizobebeshwa mwanamke huyu. Hata hivyo, lengo la Waandishi na Mafarisayo halikuwa tu kumweka mwanamke yule hatiani, bali na Yesu pia katika uamuzi atakao utoa kuhusu shauri lile. Kwa kuwa shauri hili hatma yake ni mauti, yaani muhusika kupigwa mawe hadi kufa, Yesu anazisoma dhamiri zao na kuwaambia, “Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe,” Yoh 8:7. Matokeo ya mtihani huu na zoezi hili la dhamiri ni kwamba,  Nao waliposikia, wakashitakiwa na dhamiri zao, wakatoka mmoja mmoja, wakianzia tangu wazee hata wa mwisho wao; akabaki Yesu peke yake, na yule mwanamke amesimama katikati,” Yoh 8:9. Mungu aliye hai anazifufua dhamiri za Waandishi na Mafarisayo zilizokuwa zimekufa. Swali linabaki kwako na kwangu, Je, hukumu tuzitoazo kila siku twazitoa katika dhamiri iliyo hai? Na kama dhamiri ni hai, Je, hukumu hiyo imejikita katika misingi ya kweli, na haki, huruma na upendo?

Wapendwa katika Kristo, huruma na upendo lazima vitawale kabla na hata baada ya hukumu yoyote ile uitowayo wewe uliye na hofu ya Mungu. Ukweli huu tunauona kwa Kristo Yesu baada ya kubaki na mshtakiwa, yaani mwanamke yule aliyefumaniwa kwa uzinzi. Mambo yalikuwa hivi; Yesu akajiinua asimwone mtu ila yule mwanamke, akamwambia, Mwanamke, wako wapi wale washitaki wako? Je! Hakuna aliyekuhukumu kuwa na hatia? Akamwambia, Hakuna, Bwana. Yesu akamwambia, Wala mimi sikuhukumu. Enenda zako; wala usitende dhambi tena,” Yoh 8:10-11. Ndugu yangu, tazama huruma na upendo wa Mungu ulivyo mkubwa kwetu! Maneno “enenda zako; wala usitende dhambi tena,” kwa namna nyingine yana maanisha hivi: “na sasa uanze upya ndani na katika Kristo Yesu kwa sababu, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,”” Yoh 14:6. Amina!

Wapendwa wana wa Mungu, kielelezo cha Mungu wetu aliye hai ni Kristo mwenyewe kama Mtume Paulo anavyotuwasa katika somo letu la pili. Kristo kwa Mkristo ndiyo kila kitu kwake. Naam, zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo,” Flp 3:8. Ukimpata Kristo na kuishi ndani na katika yeye umeyapata yote yaliyofunuliwa kwake yamuhusuyo Mungu Baba Mwenyezi. Na hayo ndiyo ule uzima wa milele.

Ukiwa ndani na katika Kristo atakayeonekana katika maisha yako si wewe na ubinafsi wako, bali Kristo mwenyewe. Kama binadamu sintakuwa na chochote cha kujivunia zaidi ya Kristo mwenyewe. Tena nionekane katika yeye, nisiwe na haki yangu mwenyewe ipatikanayo kwa sheria, bali ile ipatikanayo kwa imani iliyo katika Kristo, haki ile itokayo kwa Mungu, kwa imani,” Flp 3:9. Mateso na mahangaiko ya Mkristo anayeishi ndani na katika Kristo hupata maana halisi. Huwezi kumjua Kristo kwa kupiga kisogo. Namjua Kristo kwa kuishi ndani na pamoja naye, na kwa kufikiri na kutenda kama yeye. Hivyo, naihitaji neema ili nimjue yeye, na uweza wa kufufuka kwake, na ushirika wa mateso yake, nikifananishwa na kufa kwake; ili nipate kwa njia yo yote kuifikia kiyama ya wafu,” Flp 3:10-11.

Hatua hii ya kukua kiroho ndani na katika Kristo, hutuondolea kiburi na majivuno yote yanayotukwamisha kuuona uzuri wa Kristo ndani yetu. Huku ndiko kupungua ili Kristo aongezeka kila siku ya maisha yetu. Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu,” Flp 3:12. Pasipo kujishusha hatuwezi kufika pale alipo Kristo. Kaa yangu kila siku iniweke karibu na Kristo na kamwe nisichoke kuutafuta uso wake. Mtume Paulo anasema, Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele,” Flp 3:13. Tuliyokwisha yafikia kimaisha leo na sasa hayana umuhimu mkubwa sana tukilinganisha na yale ambayo yapo mbele yetu kuliko na uzima wa milele. Hivyo mara zote nikaze mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu,” Flp 3:14. Na mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu ni huu, kuwa wakamilifu, kama Baba yetu wa mbinguni alivyo mkamilifu, Mt 5:48.’

Ndugu yangu, ni kama wiki tatu zilizopita katika Parokia ya Moyo Safi wa Bikira Maria kulitokea wizi wa tairi la akiba ya gari ya Paroko. Kwa jumapili mbili mfululizo yalitolewa matangazo yakisisitiza aliyechukua tairi hilo arudishe. Matangazo hayo yaliambatana na novena  ya siku 21 kusali kwa nia ya kurejeshwa kwa tairi hilo la akiba la gari ya Baba Paroko.

Basi jumapili ya tatu baada ya tukio hilo kutoke, zilisikia kelele barabarani mara baada ya misa la pili parokiani hapo. Waamini wengi walikimbilia barabarani kujua kulikoni. Na tazama alikuwa Baba mmoja wa umri wa kutosha akiwa amebeba mahindi matatu mabichi akiwa anapata kichapo cha nguvu na kulia kama mtoto. “Jamani nihurumieni ni kwa sababu ya njaa tu nimefanya haya yote,” Baba yule alisikika akisema maneno hayo kwa uchungu.

Kundi lile lililotoka Parokia sauti zilisikika zikisema, “huyu atakuwa ni kibaka yule yule aliyeiba tairi la akiba la Baba Paroko. Dawa ya vibaka kama hawa ni kuwachoma moto. Na tutafute galoni ya kuchukulia petroli hapo sheli.” Mara hara hara watu wawili kutoka kundi lile walijitolea kwenda kufuata mafuta ya Petroli baada ya kupitishwa kwa mchango wa haraka wa fedha za kununulia Petroli ile.

“Jamani msiniue. Nina familia, mke wa watoto ndugu zangu,” Baba yule aliyasema maneno yale kwa msisitizo. Hata hivyo hakuna aliyemsikia. Umati wote kila mtu alikuwa na chochote mkononi kwa kuumaliza uhai wa yule Baba. Mara vijana wale wawili kutoka sheli waliwasili na Petroli yao. Baba yule alimwagiwa Petroli ile na kutiwa kiberiti. Moto ulivyopamba vya kutosha, kila mmoja alisambaa kivyake. Waliokuwa wametoka misa ile ya pili na kushiriki uuaji ule walienda majumbani mwao, na waliokuwa wakienda misa ya tatu walifanya hivyo katika utoshelevu wao kwa tendo lile. Na baada ya saa moja hivi baadaye Baba yule alifariki kwa mateso makubwa sana.

Ndugu yangu, simulizi hili linasema chochote juu ya Ukristo wako?

Tumsifu Yesu Kristo!

“Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe,” Yoh 8:7


Ee Yesu, nijalie utu wema, huruma na upendo wa kweli kwa wema na waovu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario